-
Mathayo 20:29-34Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
29 Walipokuwa wakitoka Yeriko umati mkubwa ukamfuata. 30 Na tazama! wanaume wawili vipofu waliokuwa wameketi kando ya barabara waliposikia kwamba Yesu anapitia hapo, wakapaza sauti: “Bwana, Mwana wa Daudi, tuhurumie!”*+ 31 Hata hivyo, umati ukawakemea na kuwaambia wanyamaze; lakini wakapaza sauti hata zaidi, wakisema: “Bwana, Mwana wa Daudi, tuhurumie!”* 32 Basi Yesu akasimama, akawaita na kuwauliza: “Mnataka niwafanyie nini?” 33 Wakamjibu: “Bwana, tunaomba macho yetu yafunguliwe.” 34 Yesu akawasikitikia, akayagusa macho yao,+ na mara moja wakaanza kuona, nao wakamfuata.
-
-
Marko 10:46-52Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
46 Kisha wakafika Yeriko. Lakini yeye na wanafunzi wake na umati mkubwa walipokuwa wakitoka Yeriko, Bartimayo (mwana wa Timayo), kipofu aliyekuwa akiombaomba, alikuwa ameketi kando ya barabara.+ 47 Aliposikia kwamba ni Yesu Mnazareti, akaanza kusema kwa sauti kubwa: “Mwana wa Daudi,+ Yesu, nihurumie!”*+ 48 Ndipo wengi wakaanza kumkemea, wakimwambia anyamaze, lakini akazidi kusema kwa sauti kubwa: “Mwana wa Daudi, nihurumie!”* 49 Basi Yesu akasimama na kusema: “Mwiteni.” Nao wakamwita yule kipofu, wakamwambia: “Jipe moyo! Simama; anakuita.” 50 Akatupa vazi lake la nje, akasimama haraka na kumwendea Yesu. 51 Kisha Yesu akamwuliza: “Unataka nikufanyie nini?” Yule kipofu akamwambia: “Raboni,* naomba niweze kuona tena.” 52 Yesu akamwambia: “Nenda, imani yako imekuponya.”+ Na mara moja akaanza kuona,+ naye akaanza kumfuata barabarani.
-