Muziki wa Daudi.
24 Dunia na vyote vilivyomo ni vya Yehova,+
Nchi inayozaa na wale wanaokaa ndani yake.
 2 Kwa maana ameiweka imara kabisa juu ya bahari+
Na kuiweka imara kabisa juu ya mito.
 3 Ni nani anayeweza kuupanda mlima wa Yehova,+
Na ni nani anayeweza kusimama mahali pake patakatifu?
 4 Yeyote mwenye mikono isiyo na hatia na mwenye moyo safi,+
Ambaye hajaapa kwa uwongo kwa uhai Wangu,
Wala kuapa kwa udanganyifu.+
 5 Atapokea baraka kutoka kwa Yehova+
Na uadilifu kutoka kwa Mungu wa wokovu wake.+
 6 Hiki ndicho kizazi cha wale wanaomtafuta,
Cha wale wanaoutafuta uso wako, Ee Mungu wa Yakobo. (Sela)
 7 Inueni vichwa vyenu, enyi malango;+
Fungukeni, enyi milango ya kale,
Ili Mfalme mtukufu aingie!+
 8 Mfalme huyu mtukufu ni nani?
Yehova, mwenye nguvu na hodari,+
Yehova, hodari katika vita.+
 9 Inueni vichwa vyenu, enyi malango;+
Fungukeni, enyi milango ya kale,
Ili Mfalme mtukufu aingie!
10 Mfalme huyu mtukufu ni nani?
Yehova wa majeshi—yeye ndiye Mfalme mtukufu.+ (Sela)