Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati
14 Mfalme Hiramu+ wa Tiro aliwatuma wajumbe kwa Daudi, pamoja na mbao za mierezi, waashi,* na maseremala ili wamjengee Daudi nyumba.*+ 2 Na Daudi alijua kwamba Yehova alikuwa amemwimarisha kabisa kuwa mfalme wa Israeli,+ kwa maana ufalme wake ulikuwa umekwezwa sana kwa ajili ya watu Wake Waisraeli.+
3 Daudi alichukua wake+ zaidi huko Yerusalemu, na Daudi akazaa wana na mabinti zaidi.+ 4 Haya ndiyo majina ya watoto wake waliozaliwa Yerusalemu:+ Shamua, Shobabu, Nathani,+ Sulemani,+ 5 Ibhari, Elishua, Elpeleti, 6 Noga, Nefegi, Yafia, 7 Elishama, Beeliada, na Elifeleti.
8 Wafilisti waliposikia kwamba Daudi alikuwa ametiwa mafuta kuwa mfalme wa Waisraeli wote,+ Wafilisti wote wakapanda kuja kumtafuta Daudi.+ Daudi aliposikia jambo hilo, akaenda kukabiliana nao. 9 Kisha Wafilisti wakaja na kuvamia tena na tena katika Bonde la* Refaimu.+ 10 Daudi akamuuliza Mungu: “Je, nipande kwenda kuwashambulia Wafilisti? Je, utawatia mikononi mwangu?” Ndipo Yehova akamwambia: “Panda uende, nami hakika nitawatia mikononi mwako.”+ 11 Basi Daudi akapanda kwenda Baal-perasimu,+ naye akawaua huko. Ndipo Daudi akasema: “Mungu wa kweli amewapasua na kuwapita maadui wangu kwa mkono wangu, kama ufa uliopasuliwa na maji.” Ndiyo sababu walipaita mahali hapo Baal-perasimu.* 12 Wafilisti wakaacha miungu yao hapo, na Daudi alipotoa amri, miungu hiyo iliteketezwa motoni.+
13 Baadaye Wafilisti wakaja tena na kuvamia bondeni.*+ 14 Daudi akamwomba Mungu ushauri tena, lakini Mungu wa kweli akamwambia: “Usipande moja kwa moja na kuwafuatia. Badala yake, zunguka nyuma yao, uwashambulie mbele ya vichaka vya mibaka.+ 15 Na utakaposikia sauti ya watu wakipiga mwendo juu ya vichaka vya mibaka, washambulie, kwa sababu mimi Mungu wa kweli nitakuwa nimetangulia mbele yako ili kuliua jeshi la Wafilisti.”+ 16 Basi Daudi akafanya kama Mungu wa kweli alivyomwamuru,+ wakaliua jeshi la Wafilisti kuanzia Gibeoni mpaka Gezeri.+ 17 Umaarufu wa Daudi ukaenea katika nchi zote, na Yehova akayafanya mataifa yote yamwogope Daudi.+