Biblia Inasaidia Kuendeleza Umoja wa Jamaa
KWA SABABU ya kutokutumia shauri la Biblia katika maisha zao, leo jamaa nyingi zinapata matatizo mazito. Walakini, mara wanapoanza kufuata shauri hilo, kunatokea mabadiliko ya ajabu ya kuwa na maisha bora ya jamaa.
Mwanamume anayeishi katika nchi ya Spania anasimulia hivi: “Hali yangu ya uchumi katika ulimwengu ilikuwa yenye kufanikiwa sana. Nilikuwa na idara yangu ya uenezaji wa habari iliyofanikiwa sana. Walakini, ndoa yangu ilivunjwa na uzinzi. Kila mmoja wetu aliishi maisha yaliyo tofauti hata kuwa na siku iliyowekwa ya kufanya uzinzi. Siku iliyokuwa zamu ya mke wangu mimi nilibaki nyumbani na kuangalia watoto wawili na mambo mengine. Ingawaje, nilifahamu kwamba hali haiwezi kuendelea namna hiyo. Nikataka nitengeneze maisha yangu. Nilimwomba Mungu anisaidie, na msaada huo ukaja kwa njia isiyotazamiwa.
“Nilikuwa katika chumba cha mchoraji picha pamoja na rafiki wengine wakati mmoja wao, alipotazama saa yake, alisema: ‘Ninakwenda. Nina Shahidi anayeningojea nyumbani.’ Nikamwuliza, ‘Hicho ni nini?’ Jibu lake liliamsha kupendezwa kwangu nikaenda naye nikasikilize. Nilionyeshwa Mashahidi wa Yehova waliko katika mtaa wangu, kisha mke wangu na mimi tukaanza kujifunza. Kidogo kidogo tulifanya mabadiliko katika maisha yetu wenyewe, si katika maisha mema tu, bali hata kwa kadiri ya kuacha kampuni yangu ya uenezaji wa habari ili kuepuka kushirikiana na watu wasiofaa. Asante kwa Yehova, sasa jamaa ina umoja.”