Kutumia Mashauri ya Biblia Kunaendeleza Umoja wa Jamaa
JE! NYUMBA yenye hali ya amani kwa kweli haitamaniki? Lo! ni vizuri kama nini watoto wanapozungumza na wazazi wao kwa uhuru, wakizishiriki furaha zao na magumu yao na machungu yao! Na inafurahisha kweli kweli wakati roho iliyomo nyumbani inapokuwa ya upendo na upendano pahali pa kugombana, kuzozana na kubishana.
Lakini maisha ya jamaa yawezaje kugeuzwa kuwa bora? Jamaa nyingi zimeona kwamba kutumia kwao mambo waliyojifunzwa kupitia kwa funzo la Biblia kumekuwa msaada mkubwa sana.
● Jamaa moja katika Okinawa iliingia katika hali mbaya sana ya kukosa fedha. Kusudi aipatie jamaa chakula mke aliokota chupa tupu akaziuze. Mumewe alipokuwa nyumbani, mke huyu alilalamika wakati wote. Kwa hiyo mumewe alikaa mbali kama ilivyowezekana. Mwishowe mmoja wa mashahidi wa Yehova akatembelea nyumba hii, na, kutoka kwa Biblia, akamweleza mke chanzo cha taabu na shida duniani. Alikubali kuwa na funzo la nyumbani la Biblia. Nyuma ya mafunzo machache alifahamu kwamba alichokuwa anajifunza kilikuwa kweli kabisa. Karibuni akaanza kuhudhuria mikutano iliyofanywa na mashahidi wa Yehova na kuanza kushiriki na wengine mambo mazuri aliyokuwa amejifunza. Vile vile aliyajua makosa yake katika kushughulika na mumewe, akilikumbuka andiko la Biblia linalomfananisha mke mgomvi na “kutona-tona daima siku ya mvua nyingi [kunakomfukuza mtu].” (Mit. 27:15) Kwa hivyo, aliugeuza mwendo wake wa kutenda. Mahali pa kulalamika wakati wote, aliuzuia ulimi wake na kutafuta amani.
Kama matokeo mumewe hakukaa mbali na nyumbani tena, lakini alianza kujifunza Biblia na Shahidi mmoja. Leo jamaa hii inafurahi katika hali yenye kupendeza ya nyumbani, kwa maana wote wameungana wakijitahidi kuzitumia kanuni za Biblia katika ujamaa wao kwa mmoja na mwenzake.
● Vivyo hivyo, matumizi ya kanuni za Biblia yaliukomesha ugomvi wa sikuzote wa mume na mke katika Surinam. Mke huyo alianza kujifunza Biblia na mashahidi wa Yehova. Lakini ulikuwako ugomvi mara kwa mara nyumbani, zaidi wakati ulipokuwa ni wakati wa funzo hilo la Biblia au wakati ambao mke alijitayarisha akahudhurie mikutano ya mashahidi wa Yehova.
Upeo ulikuja wakati mke alipoamua kuhudhuria kipindi kila siku penye kusanyiko la mzunguko la mashahidi wa Yehova. Mumewe alimfungia nje, bila ya kufungua mlango mpaka wakati mwingi ulipokuwa umepita. Hata wakati mwishowe alipomfungulia alizungumza kwa hasira. Lakini, mke huyu alitaka kuzizoea kanuni nzuri alizokuwa amejifunza kutokana na funzo lake la nyumbani la Biblia. Aliponyamaa, ndipo mumewe alipokasirika hata zaidi. Kisha mkewe akasema kwa utulivu: ‘Tafadhali usikilize kwa dakika moja. Unajua namna nilivyotenda hapo kwanza, sivyo? Wakati wo wote tulipogombana, sikuzote ndimi niliyetaka nikate shauri na kuzungumza zaidi. Lakini kwa maana sasa najifunza Biblia na kusoma Mnara wa Mlinzi na Awake! kwa kawaida sitaki nigombane nawe tena. Ukitaka kugombana nami wewe, waweza. Lakini sitaujibu ugomvi wako tena.’
Mara moja mtu huyo akatulia. Hakuamini alichosikia. Ikiwa kile ambacho mkewe alikuwa anajifunza kilitokeza matokeo mema kama hayo, kilistahili kichunguzwe. Halafu akasema: ‘Hata na mimi nitaanza kuyasoma magazeti hayo na vitabu hivyo vyako, kwa maana vimekufundisha jambo lenye faida.’
● Jamaa moja katika Jamaica vile vile ilivutwa karibu karibu kupitia kwa funzo la Biblia. Ijapokuwa waliishi katika nyumba moja, kila mshiriki wa jamaa alifuata njia yake mwenyewe. Halafu kijana mwanamke katika jamaa hii akaanza kujifunza na mashahidi wa Yehova. Lililompendeza zaidi ni unabii wa Yesu katika Mathayo 24 (NW) juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo.” Kwa shauku alimkaribisha mamaye ashiriki katika funzo.
Mama yake alikubali, lakini ili kwamba aone tu alilokuwa anajifunza kijana wake wa kike. Kwa sababu kupendezwa kuliongezeka kidogo kidogo kupitia kwa funzo lao, wote wawili waligundua kwamba kutoshirikiana kwa wazazi na watoto wa jamaa hiyo kulikuwa kunakwisha. Vile vile kijana huyu wa kike alisema na dada yake. Lakini nyumaye dada huyu alisihiwa na kiongozi wa dini ajiepushe na Mashahidi kwa maana, huyo alisema, ‘dini yao inazitenganisha jamaa.’ Lakini, dada huyu aliona kwamba kilichokuwa kinatukia katika jamaa yake ni tofauti tu ya alichosema. Mwishowe yeye na washiriki wengine wa jamaa wakaanza kujifunza Biblia na mashahidi wa Yehova. Hivyo watu sita waliokuwa wameishi kwa kutotegemeana waliunganishwa na ujumbe wa Neno la Mungu.
Bila shaka matumizi ya mashauri ya Biblia yanaweza kuleta umoja kwa jamaa. Je! hiyo si sababu ya kutosha kuyafikiria kwa uzito yaliyomo katika Neno la Mungu?