Maoni ya Biblia
Unayopaswa Kujua Juu ya Malaika
Karibu wasomi 3,000 wa kidini walikusanyika kwa siku nne katika New York juma lililopita ili wasikie ripoti zaidi ya 500 juu ya habari za kuanzia sehemu ya ucheshi katika mahubiri hadi umaana wa sherehe kwa Wapentekoste. Hakuna aliyetaja malaika.”—Daily News, Desemba 26, 1982.
LEO miaka nane baadaye, makasisi wangali husema machache kuhusu malaika. Kwa nini? Je! yaweza ikawa wajumbe hao wa kimbingu huonwa tu kuwa sehemu ya hadithi za kale? Au je! kweli wao wapo? Ikiwa ndivyo, unapaswa kujua nini kuwahusu?
Je! Wao Wapo?
Malaika si “uwezo” fulani tu au “miendo ya ulimwengu mzima wote,” kama wanafalsafa fulani wanavyodai. Lazima wao wawe ni halisi kabisa ndio waweze kutajwa mara mamia katika Neno la Mungu, Biblia. Katika lugha za awali za Biblia, maneno yanayotafsiriwa “malaika” (Kiebrania, mal·’akhʹ; Kigiriki agʹge·los) humaanisha kwa halisi “mmoja anayeleta ujumbe fulani” au kwa neno rahisi “mjumbe.” Maneno hayo huonekana mara karibu 400 katika Biblia yote, nyakati nyingine yakirejezea binadamu, lakini kwa kawaida hurejezea wajumbe wa kiroho.
Malaika aliyemtokea mke tasa wa Manoa akatangaza kutungwa mimba ya mwanae, Samsoni, alikuwa halisi kwake. Ndivyo walivyokuwa wale malaika watatu waliotokea Abrahamu na Sara, mke wake, na wale wawili waliomtafuta Loti, na yule mmoja aliyeketi chini ya mti mkubwa na kuongea na Gideoni. (Mwanzo 18:1-15; 19:1-5; Waamuzi 6:11-22; 13:3-21) Wakati wa kuzaliwa kwa Yesu, malaika alitokea ghafula kikundi cha wachungaji katikati ya nuru nyangavu, yenye kumeta.—Luka 2:8, 9.
Malaika hao walikuwa ni halisi. Wao hawakuwa wa kuwaziwa au uwezo fulani usio na utu. Wao walitimiza kusudi walilopewa wakiwa wajumbe kutoka kwa Mungu, na kwa kufaa masimulizi hayo yamerekodiwa katika Biblia yawe kwa manufaa yetu leo. (2 Timotheo 3:16) Hivyo, Biblia hufunua mambo yenye umaana juu ya malaika ambayo wewe wahitaji kujua, baadhi yayo yakiwa yanapingana na mawazo ya kimapokeo.
Wao Wanafananaje?
Huenda ukawazia malaika kuwa wanawake wazuri au viumbe vinono vyenye mabawa, vifananavyo na watoto, vikiwa vinatabasamu kwa kupendeza na vikiwa vimevaa kanzu nyeupe, huku vikicharaza vinubi vidogo sana, na kuruka-ruka hewani. Ikiwa ndivyo, wapaswa kujua kwamba hizo ni dhana zenye kosa zilizotokana na mawazo ya kipagani, kama vile hadithi za Kigiriki. Au mawazo hayo yalitokezwa baada ya Biblia kukamilika kuandikwa. Katika njozi za mfano za Kibiblia, viumbe wa kiroho kama vile maserafi na makerubi wana mabawa.—Isaya 6:2; Ezekieli 10:5; Ufunuo 14:6.
Neno la Mungu huwaeleza malaika kuwa roho wenye uwezo mwingi sana, na roho haionekani kwa macho ya binadamu. (1 Wafalme 22:21; Zaburi 34:7; 91:11) ‘Malaika wa Yehova’ ndiye aliyeua Waashuri 185,000 katika kambi ya adui wa Israeli kwa usiku mmoja tu! (Isaya 37:36) Malaika walipojionyesha kwa binadamu, sikuzote walitokea kama wanaume waliovishwa nguo kabisa, si kama wanawake au watoto na hawakutokea kamwe kama binadamu nusu.
Viumbe hao wenye uwezo wa kiroho walitoka wapi? Biblia husema kwamba “katika yeye [Yesu] vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana.” (Wakolosai 1:16) Yehova Mungu, kupitia Mwanae mzaliwa wa kwanza, si kwamba tu aliumba malaika muda mrefu kabla ya mwanadamu bali pia aliwafanya wenye umbo la uhai wa juu zaidi kushinda mwanadamu.—Ayubu 38:4, 7; 2 Petro 2:11.
Je! Wao Wana Nyutu?
Malaika, kama vile binadamu, wana maono ya moyoni. Baada ya kushuhudia uumbaji wa dunia, twaambiwa kwamba malaika ‘waliimba pamoja,’ hata ‘walipiga kelele kwa furaha.’ (Ayubu 38:7) Pia Biblia hufunua kwamba “kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.” (Luka 15:10) Bila shaka, hakuna “uwezo” wowote usio na utu ungeweza kuona shangwe kubwa inayosimuliwa katika mistari hiyo.
Malaika wana mipaka pia. Mambo fulani ya hakika juu ya Kristo na wakati ujao yalifunuliwa kwa manabii wanadamu wala si kwa malaika. Neno la Mungu hutuambia kwamba ni katika “mambo hayo malaika wanatamani kuyachungulia.”(1 Petro 1:10-12, NW) Kwa habari ya tarehe barabara iliyochaguliwa na Mungu ya kuja kwa Bwana, Yesu alisema: “Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake.”—Mathayo 24:36.
Kisha, pia, majina ya malaika wawili, Mikaeli na Gabrieli, huonekana katika Biblia. (Danieli 12:1; Luka 1:26) Je! hilo haliongezei uthibitisho wa kwamba wao ni tofauti mmoja na mwenzake? Wakiwa mmoja mmoja, wao hawakufanywa wafuate programu fulani, kama vile kompyuta au mashine fulani, ili watende kwa njia fulani. Badala yake, malaika wamepewa zawadi ya uwezo wa kutumia akili kufikiri na wana uhuru wa kufanya maamuzi ya kibinafsi ya adili. Kwa hiyo, wakiwa wana uhuru wa adili, malaika fulani walichagua kumwasi Mungu na wakawa Shetani na roho waovu wake.—Mwanzo 6:1-4; Yuda 6; Ufunuo 12:7-9.
Je! Wanapaswa Kuabudiwa?
Ingawa twaweza kutambua kuwapo kwa malaika kuwa uhakika, si hekaya, ni lazima tuepuke kukosa kiasi. Matengenezo fulani ya kidini yamewapa malaika umaarufu usiofaa, ijapokuwa ibada ya malaika imelaaniwa vikali katika Biblia. (Wakolosai 2:18; Ufunuo 22:8, 9) Kanisa Katoliki limefanya Mikaeli na Gabrieli wakawa vitu vya kuabudiwa. Na katika makanisa ya Orthodoksi ya Mashariki, malaika ni wa maana sana sana katika kuomba dua. Ni kinyume kama nini na onyo lililotolewa na malaika wa Yehova wakati mtume Yohana aliposujudu penye miguu yake: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! Mimi ni mtumwa mwenzako tu.”—Ufunuo 19:10, NW.
Kwa nini kuna vurugu nyingi sana juu ya malaika? Shetani, ambaye hujifanya mwenyewe kuwa “malaika wa nuru,” “amepofusha akili zao wasioamini.” (2 Wakorintho 4:4; 11:14) Kwa hiyo, je! halingekuwa jambo la akili kutazamia kwamba wengi leo wangeshikilia maoni yao wenyewe kuhusu kuwapo na asili ya malaika badala ya kukubali yale ambayo Neno la Mungu linasema? Ndiyo, ingawa huenda makasisi leo wakasema machache juu ya malaika, tuna uhakikisho wa Mungu kupitia rekodi ya Biblia kwamba wao wapo kikweli na hufanya utumishi wenye heshima wakiwa wajumbe wa Yehova.—Waebrania 1:7, 14; 6:18.
[Picha katika ukurasa wa 14]
Kuonyeshwa kwa malaika wakiwa viumbe vinavyofanana na watoto wadogo wenye mabawa hutokana na mawazo ya kipagani
[Hisani]
Cupid a Captive by François Boucher, c. 1754