Wakati Ujao Mwangavu kwa Watoto
‹c g92 12/8 8›
KATIKA Mkutano wa Ulimwenguni Pote Kwa Ajili ya Watoto, viongozi wengi wa ulimwengu walizungumza kwa uthabiti juu ya wakati ujao. Walitabiri “enzi mpya” kwa watoto, “ujitoaji mpya kwa mahitaji ya mtoto.” Waliongea juu ya “‘ushirikiano mpya,’ kutoa ‘uhai kwa mapatano ya ulimwengu ya muungano na yaliyoazimiwa’” ya kuwasaidia watoto.
Hayo ni maneno mazuri. Lakini kadiri mataifa yatakavyofikia miradi yao bado twangoja kuona. Ni jambo la kustahili kutambua kwamba kati ya miezi mitano ya mkutano huo, mataifa yalipigana katika Ghuba la Uajemi vita iliyothibitika kuwa ghali zaidi—dola bilioni 61—na yenye maangamizi ya mazingira kwelikweli. Baada ya vita maelfu ya mamia ya watu katika Iraki na Kuwait waliondoshwa kwenye makao yao. Maelfu waliangamia—katika kipindi kimoja mamia ya watu kila siku—kutokana na njaa, kutupwa, utapiamlo, na magonjwa. Wapatao 8 kati ya 10 walikuwa wanawake na watoto.
Taabu Zatabiriwa
Wanafunzi wa Neno la Mungu wanajua kwamba matatizo yanayowapata watoto wa ulimwenguni yalikuwa yametabiriwa karibu miaka elfu mbili iliyopita. Biblia ilitabiri juu ya hizi “siku za mwisho” hivi:
◻ “Kutakuwa na . . . tauni.” —Luka 21:11.
◻ “Kutakuwa na njaa.” —Mathayo 24:7.
◻ ‘[Watu watakuwa] wakiiharibu nchi.’ —Ufunuo 11:18.
◻ “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme.” —Marko 13:8.
◻ “Siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasiowapenda wa kwao.” —2 Timotheo 3:1-3.
Biblia pia ilitabiri kwamba wakati unakuja upesi wakati mataifa watafikiria kwamba wanafanya mambo ili kurekebisha matatizo ya wanadamu nao watatangaza: “Amani na salama!”—1 Wathesalonike 5:3.
Wakati Ujao Mwangavu
Hata hivyo, tangazo hilo kwa hakika litatoa dalili ya Mungu kuingilia mambo ya wanadamu. Kupitia Ufalme wake wa kimbingu, Mungu ataondoa mfumo wa mambo wa sasa na kuleta ulimwengu mpya wa amani ya kweli na usalama wenye kudumu, kwa watoto na pia kwa watu wazima.—Mithali 2:21, 22; Danieli 2:44; Mathayo 6:10.
Chini ya mpango mtukufu wa Ufalme wa Mungu, “hakuna mwenyeji atakayesema: Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Utapiamlo utakuwa jambo la zamani: ‘Kutakuwa na wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.’ (Zaburi 72:16) Hata vita haitakuwapo tena, kwa kuwa Biblia yaahidi hivi: “[Yehova] avikomesha vita hata mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:9.
Lakini vipi juu ya watoto wote—na wengine—ambao wamekufa kutokana na utapiamlo, ugonjwa, au visababishi vingine? Neno la Mungu lililopuliziwa lasema hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.”—Matendo 24:15.
Yesu Kristo alipokuwa duniani, alionyesha kwamba ufufuo wa uhai duniani katika ulimwengu mpya wa Mungu ungetia ndani wachanga. Kwa mfano, wakati msichana mmoja wa karibu miaka 12 alipokufa, “watu wote walikuwa wakilia na kumwomboleza.” Lakini kisha, akichukua mkono wa kijana huyo, Yesu alimwambia: “Kijana, inuka.” Habari ya historia hiyo yaeleza: “Naye mara hiyo akasimama. Akaamuru apewe chakula.” Biblia yaripoti: “Mara wakashangaa mshangao mkuu.”—Luka 8:40-42, 49-56; Marko 5:42.
Katika pindi nyingine, Yesu alikutana na maandamano ya mazishi yaliyohusu mjane ambaye mwanawe pekee alikuwa amekufa. Yesu “akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka. Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. [Yesu] akampa mama yake.” Wale waliokuwa karibu ‘walianza kumtukuza Mungu.’—Luka 7:11-16.
Hivyo, chini ya utawala mwadilifu wa serikali ya Ufalme wa Mungu, watoto, kutia ndani wale waliofufuliwa, watakuwa na wakati ujao mwangavu kwelikweli. Wataweza kukua katika ulimwengu wa uadilifu na amani wenye kupendeza sana, wenye usalama, wenye kudumu, ambao Yesu aliuita kwa namna ifaayo “Paradiso.”—Luka 23:43, NW.
[Picha katika ukurasa wa 32]
Katika ulimwengu mpya wa Mungu, watoto watakua wakiwa salama, wenye afya, na furaha