Watu Wanaojali
MASHAHIDI WA YEHOVA ni tengenezo la kimataifa la wanafunzi wa Biblia zaidi ya milioni nne ambao wamepangwa kitengenezo katika makutaniko zaidi ya 69,000 ulimwenguni pote. Mashahidi wamejitoa kusaidia watu wajifunze zaidi juu ya makusudi ya Mungu na pia wao hupendana kama Yesu Kristo alivyoamuru. (Yohana 13:34, 35) Upendo huo unadhihirishwa katika njia zenye kutumika.
Kwa mfano, wakati fulani uliopita Mashahidi karibu 30 kutoka Kutaniko la East San Marcos, Kalifornia, walikusanyika kwa ajili ya kiamshakinywa saa kumi na mbili asubuhi moja ya Jumamosi. Walikuwa na mradi wa pekee akilini—kusaidia wale kutanikoni waliohitaji usaidizi katika kutunza makao yao.
Baadhi ya hao wenye uhitaji walikuwa wazazi wasio na wenzi, wajane, na waume na wake wenye umri mkubwa zaidi. Mahitaji yao yalitia ndani kurekebisha paa ya nyumba zao, kuziba mashimo katika vijia vya uani, kutia taa za usalama, kuangika milango ya gereji, kupaka rangi, kuchenga miti, na kazi nyinginezo. Kujitayarishia kazi kulianza zaidi ya mwezi mmoja mbele wakati mahitaji yalipotambuliwa na vifaa kupatwa.
Katika Jumamosi iliyowekwa, matayarisho ya mwisho yalifanywa wakati wa kiamshakinywa. Vikundi vya kazi vilipangwa, na kila kimoja kilipokea migawo hususa. Wanawake waliandaa viburudisho, kutia na mlo wa mchana. Utendaji wa siku ulikuwa na matokeo mema sana juu ya wale ambao makao yao yalirekebishwa na pia kila mtu kutanikoni.