Kanisa Anglikana la Australia—Nyumba Iliyogawanyika
Na mleta habari za Amkeni! katika Australia
ULE mjadala wa kama wanawake wapaswa kuwekwa rasmi kuwa makasisi katika Kanisa Anglikana si jambo jipya hata kidogo. Lakini jambo hilo limekuwa suala kubwa katika Australia hivi karibuni.
Katika Januari 1992 askofu wa Canberra na Goulburn alitangaza mipango ya kuweka rasmi wanawake mashemasi kadhaa kuwa makasisi wa Kanisa Anglikana. Alikataa kungojea sinodi (mkutano wa wakuu wa kanisa) ambayo ingekuja. Kwa kweli, sinodi hiyo tayari ilikuwa imeamua mara tatu dhidi ya kuweka rasmi wanawake kuwa makasisi.
Na hatimaye jambo hilo lilipotendeka, wanawake kumi waliwekwa rasmi kuwa makasisi wa Kianglikana mapema katika mwezi wa Machi mjini Perth, Australia, ujapokuwapo upinzani. Basi, si ajabu kwamba uangalifu mwingi uliwekwa kwenye sinodi ya kanisa iliyokuwa ikija. Mkutano wa Julai haukutoa uamuzi wa mwisho, na hivyo “mkutano usio wa kawaida” ulipangwa ufanywe Novemba 21, 1992.
Muda wa juma moja tu uliokuwa umepita, Sinodi Kuu ya Kanisa la Uingereza ilipiga kura kwa kupendelea kuweka rasmi wanawake kuwa makasisi. Wengi walitazamia kwamba uamuzi huo ungekuwa na ushawishi katika Australia. Sinodi ya kanisa la Australia ilipofanywa, gazeti moja lilieleza hivi: “Mijadala na mabishano yalipamba moto katika siku yenye kujaa mikazo.” Kabla ya kufunua matokeo ya kura, msimamizi wa sinodi hiyo aliomba kwamba tokeo la tangazo hilo lipokewe kwa unyamavu. Ilipofunuliwa kwamba kuwekwa rasmi kwa wanawake kulikuwa kumekubaliwa, baadhi ya wahudhuriaji walijikaza kuzuia hisia zao. Mara habari hiyo ilipoenea nje, vifijo vilitokea, na mabango yakarushwa hewani.
Furaha hiyo haikushirikiwa na wote. Gazeti The Sydney Morning Herald lilimnukuu askofu mkuu wa Sydney akisema hivi: “Hatutaweza kuishi pamoja kwa furaha . . . Kutakuwa na madhehebu mawili katika Kanisa moja la Anglikana.” Kasisi mwingine hata alifikia hatua ya kusema kwamba kuweka rasmi wanawake kuwa makasisi kulionyesha kwamba “Kanisa Anglikana la Australia linaanza kuvunjika.”
Biblia hutoa msingi mkubwa wa mahangaiko hayo. Yesu Kristo mwenyewe alisema hivi: “Kila ufalme ambao umejigawanya utaharibika; hakuna mji, hakuna nyumba, ambayo inajigawanya inayoweza kusimama.”—Mathayo 12:25, The New English Bible.
Jambo hilo latokeza swali ambalo laonekana lilipotea katika mabishano ya kanisa, Biblia inasema nini juu ya daraka la wanawake katika kutaniko? Ingawa yasema kwamba Yehova Mungu anathamini wanaume na wanawake waliojitoa wakfu kwa usawa, hata hivyo, inawapa wanaume na wanawake migawo tofauti katika kutaniko. (Wagalatia 3:28) Inaelezwa hivi na 1 Wakorintho 11:3: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu.” Hivyo, kuhusu mafundisho rasmi katika kutaniko, Paulo alipuliziwa na Mungu aandike hivi: “Mwanamke na ajifunze katika utulivu, akitii kwa kila namna. Simpi mwanamke ruhusa ya kufundisha, wala kumtawala mwanamume.”—1 Timotheo 2:11, 12.
Hata hivyo, jambo hilo halihitaji kufadhaisha wanawake Wakristo kwa sababu wako huru kufundisha katika huduma ya peupe kama walivyofanya wanawake kama Loisi, Eunike, Euodia, na Sintike katika nyakati za mapema za Kikristo.—Wafilipi 4:2, 3; 2 Timotheo 1:5.