Jinsi Ulimwengu Utakavyoungana
JITIHADA za wanadamu za kujitawala wenyewe kwa mafanikio zimeshindwa sikuzote. Bila shaka utakubaliana na kadirio hili lililopuliziwa: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Mhubiri 8:9) Ni kwa nini wanadamu wameshindwa vibaya sana kujitawala wenyewe?
Biblia hutoa sababu, ikieleza hivi: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) La, mwanadamu hana uwezo, au haki, ya kujitawala yeye mwenyewe wala kutawala wanadamu wenzake. Hiyo ni haki ya pekee ya Yehova Mungu, Muumba wetu, ambaye juu yake twaambiwa: “BWANA [Yehova, New World Translation] ndiye mwamuzi wetu; BWANA [Yehova, NW] ndiye mfanya sheria wetu; BWANA [Yehova, NW] ndiye mfalme wetu.”—Isaya 33:22.
Ni wakati tu wanadamu wote watakapomkubali Yehova kuwa Mtawala wao ndipo ulimwengu utaunganika. Lakini je, hilo litatukia kweli? Zamani za kale nabii wa Mungu aliongea juu ya “siku za mwisho,” wakati watu watakapoanza kumtafuta Yehova awafundishe.
Amani ya Ulimwenguni Pote Iliyotabiriwa
“Na itakuwa katika siku za mwisho,” akaandika nabii Isaya, kwamba “mlima wa nyumba ya BWANA [Yehova, NW] utawekwa imara juu ya milima . . . na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA [Yehova, NW], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake.” Tunaposoma zaidi, twaona matokeo ya kutafuta mafundisho ya Yehova. “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu,” unabii waendelea. “Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:2-4.
Ndiyo, matokeo ya kutii ufundishaji huu wa kimungu ni kubwa hakungekuwa kupigana tena, wala hakungekuwa jeuri ya kikabila tena, wala hakungekuwa vita. Watawala wa kibinadamu walidhania kwamba wangeweza kutimiza unabii wa Biblia na hata wameandika sehemu ya mwisho kwenye ukuta wa Jengo la Umoja wa Mataifa katika Jiji la New York. Hata hivyo, vita na chuki miongoni mwa mataifa na vikundi vya kikabila vimeongezeka tu hadi mwisho wa 1993. Kwa hiyo je, utasema kwamba unabii wa Mungu umeshindwa?
La, haujashindwa—kwa kuwa watu miongoni mwa mataifa yote hivi sasa wanaiendea nyumba ya Yehova kwa wingi ili kupata ufundishaji wa kimungu. Naam, Mikusanyiko ya “Ufundishaji Kimungu” ya Mashahidi wa Yehova ya kiangazi hiki imekuwa ushuhuda mkubwa kama nini kwa utimizo wa unabii huu! Udugu wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova hauruhusu chochote—wala rangi, taifa, wala malezi ya kikabila—kuwafanya wachukiane au wauane. Wao wamefua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu kitamathali.
‘Lakini,’ mtu fulani aweza kupinga, ‘huwezi kutazamia kila mtu atii agizo la Mungu la kupendana.’ Ijapokuwa hilo ni kweli, Mungu ana uwezo wa kuondoa wapinzani wote wa penzi lake la kimungu.
Atakayofanya Mungu
Je! wewe husali kama vile Yesu alivyofundisha wanafunzi wake, yaani: “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni”? (Mathayo 6:9, 10) Ikiwa unafanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo atajibu sala hiyo. Yeye atafanyaje hivyo?
Mungu tayari amemweka Mwana wake, ‘Mwana-Mfalme wa Amani,’ akiwa mtawala mchaguliwa wa “serikali” yake, Ufalme ambao tulifundishwa kusali kwa ajili yao. (Isaya 9:6) Twahitaji mtawala wa aina hiyo mwenye uwezo kuliko wa mwanadamu, kwani ndiye pekee atakayeweza kuondolea ainabinadamu uvutano mwovu wa Shetani na roho wake waovu. Watawala wa kibinadamu, hata wawe wenye nia nzuri vipi, hawawezi kufanya hivyo.—1 Yohana 3:8; Ufunuo 12:7-12.
Lakini, nini kitakachozipata serikali za ki-siku hizi zinazoshindwa kujitiisha kwa utawala wa kimungu? Unabii mwingine wa Biblia unaoeleza Ufalme ambao Yesu alitufundisha kusali juu yake husema: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, . . . [Ufalme wa kimbingu wa Mungu] utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Hivyo, kusali Ufalme wa Mungu uje kwamaanisha kwamba twasali juu ya serikali moja ya ulimwenguni pote chini ya utawala wa ‘Mwana-Mfalme wa Amani.’—Danieli 2:44; Isaya 9:6.
Kisha, wakati familia ya kibinadamu itakapokuwa imeunganishwa kwa amani chini ya Ufalme wa Mungu, wote watapendana bila kujali rangi au malezi ya kikabila. Utakuwa wakati mtukufu kama nini! (Ufunuo 21:3, 4) Twakukaribisha ufurahie mwono wa kimbele wa hali hiyo yenye amani hata sasa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova kisha utazamie pamoja nao wakati ambao ulimwengu wote utaunganika kwa amani.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Ufalme wa Mungu utaunganisha watu wote kwa amani