Vijana Huuliza...
Kwa Nini Kila Mtu Anafunga Ndoa ila Mimi?
“Natamani ningekuwa ninafunga ndoa. Kisha ningekuwa na furaha.”—Cheryl.a
NI JAMBO la asili tu kutaka kufunga ndoa. Mungu aliwapa mwanamume na mwanamke uvutio wa asili kati ya jinsia tofauti. Na akaanzisha ndoa ikiwa muungano wa kudumu kati ya mwanamume na mwanamke.—Mwanzo 1:27, 28; 2:21-24.
Kwa kueleweka basi, huenda ukahisi kuvunjika moyo hivi au hata kuhisi kutengwa ikiwa hujafunga ndoa bado—hasa ikiwa wengi wa marika wako tayari wamefunga ndoa. Marafiki wenye nia njema wanaweza kuongezea huo msongo. “Nina umri wa miaka 24 na ni mseja, sina miadi ya kijinsia na yeyote kwa wakati huu,” asema Tina. “Yaonekana kwamba kila mtu anahangaika sana kwamba sijafunga ndoa hivi kwamba naanza kupatwa na wasiwasi sana juu ya jambo hilo. Wananifanya nijihisi kama mwanamke asiyeelekea kufunga ndoa au kama kwamba nina kasoro fulani.”
Kwa watu fulani useja waweza kuanza kuonekana kama ukuta, kizuizi kisichoweza kushindwa, ambacho kinawatenganisha na furaha. Kila mwaka upitapo, huenda ikaonekana kama kwamba tabaka jingine la matofali laongezwa kwenye ukuta huo. Kijana anaweza kuanza kuhisi kwamba ni lazima iwe havutii au hatamaniki. Asema mwanamke kijana katika Italia anayeitwa Rosanna: “Mara nyingi nahisi upweke na kuwa bure; yaonekana kwamba sina fursa za kuolewa.” Wanaume vijana wanaweza kuwa na hisia sawa na hizo. Kwa kielelezo, Frank alianza kuhisi kwamba rafiki zake walikuwa wenye kupendeza zaidi na wenye ujuzi baada ya wao kufunga ndoa. Yeye alianza kujiuliza kama ndoa ingemfanyia jambo lilo hilo.
Je, wewe hujipata ukiwaza hivyo? Ikiwa wewe ni mseja, je, nyakati fulani wewe hujiuliza ikiwa una kasoro au ikiwa umeamuliwa kuwa na maisha ya useja milele?
Ndoa—Ngano Dhidi ya Uhakika
Kwanza kabisa, ebu tuchunguze itikadi maarufu sana kwamba ndoa hufungua bila kupingwa mlango kuelekea furaha. Ni kweli kwamba ndoa yaweza kuchangia na huchangia furaha ya mtu. Hata hivyo, kuwa tu katika kifungo cha ndoa hakumfanyi mtu awe na furaha. Hata ndoa bora kuliko zote huleta kiwango fulani cha “dhiki katika mwili.” (1 Wakorintho 7:28) Furaha ya ndoa yapatikana tu kupitia kujidhabihu kwenye kuendelea na jitihada nyingi. Kwa kupendeza, yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, Yesu Kristo, alikuwa mseja. Kuna yeyote ambaye angemtaja kuwa asiye na furaha? Kwa hakika sivyo! Shangwe yake ilitokana na kufanya mapenzi ya Yehova.—Yohana 4:34.
Ngano nyingine ni kwamba ndoa ni tiba iliyohakikishwa ya upweke. Sivyo ilivyo! Mwanamume mmoja Mkristo aliomboleza hivi: “Mke wangu hajapata kamwe kunieleza yaliyo moyoni mwake au kuwa na mazungumzo ya maana nami, hajapata kamwe!” Baadhi ya wake Wakristo wamelalamika vivyo hivyo kwamba waume wao hukosa kuwasiliana, au kwamba huonekana wakipendezwa zaidi na kazi yao au marafiki kuliko wao. Kwa kusikitisha, kuwa katika ndoa na kubaki ukiwa mpweke ni jambo la kawaida sana.
Kisha kuna wale wanaoona ndoa kuwa njia ya kuhepa matatizo ya familia. Asema mwanamke mmoja kijana aliyeolewa: “Nafikiri wazazi wangu walipaswa kunipa fursa ya kukua. Lakini hawakuniruhusu niwe na rafiki-mvulana au kwenda na marafiki . . . Kama wazazi wangu wangalinipa fursa, nafikiri singeolewa nikiwa na umri wa miaka 16. Lakini nilitaka kuwaonyesha kwamba nilikuwa mtu mzima.”
Huenda ukahisi kwamba maisha nyumbani ni yenye kuzuia uhuru sana. Lakini ndoa huleta madaraka ambayo yaweza kuzuia kwa njia kubwa mno uhuru wa kibinafsi. Fikiria kile kihusikacho katika kufanya kazi ya kujiruzuku, kulipa bili, kufanya marekebisho ya nyumbani au ya gari, kupika, kusafisha, kuosha nguo, na labda hata kulea watoto! (Mithali 31:10-31; Waefeso 6:4; 1 Timotheo 5:8) Vijana wengi huvurugika kiakili wanapokabiliwa na madaraka haya ya watu wazima.
Wengine pia wanaamini kwamba ndoa ndio ufunguo wa kupata umashuhuri. Lakini hakuna uhakikisho kwamba wengine watatamani sana uandamani wako—au ule wa mwenzi wako—eti kwa sababu mmefunga ndoa. Watu watakupenda ikiwa wewe ni mwenye fadhili, mkarimu, asiye na ubinafsi, uwe umefunga ndoa au uwe mseja. (Mithali 11:25) Na ikiwa kuwa mume na mke kwafanya iwe rahisi kidogo kufaa miongoni mwa marafiki waliofunga ndoa, ni lazima mume na mke wakumbuke kwamba wao ni “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Hangaiko lao kuu lazima liwe jinsi ya kuwa na uhusiano mzuri na mmoja na mwenzake—si na marafiki wao.
Uko Tayari kwa Ndoa?
Bila shaka, hata ikiwa waona busara iliyo katika hoja hizi, huenda bado ukahisi kuvunjika moyo nyakati fulani. Methali ya kale ilisema hivi: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.” (Mithali 13:12) Kwa kielelezo, kijana Tony alijikuta katika hali ya utamausho kwa sababu alikuwa mseja. Yeye alianza kuhisi kwamba alikuwa tayari kuoa mtu yeyote. Msichana mchanga aitwaye Sandra vivyo hivyo alivunjika moyo kila wakati alipojua kuhusu mahaba yaliyositawi; yeye alikuwa akijiuliza ni wakati gani zamu yake ingefika.
Kabla ya kujiachilia kuanguka katika hali ya kujihisi kukataliwa, jiulize hivi, ‘Je, niko tayari kweli kwa ndoa?’ Kwa kusema wazi, ikiwa wewe ni tineja, jibu laweza kuwa la! yenye mkazo. Katika Marekani, ndoa nyingi za wakati wa utineja hukosa kufaulu mnamo miaka mitano.b Bila shaka, vijana fulani huenda wakawa wamekomaa isivyo kawaida kwa umri wao na kuweza kuwa na mafanikio ya ndoa. Lakini hilo halimaanishi kwamba wewe unapaswa kufunga ndoa. Je, umefikiria kwa weupe wa moyo kama uko tayari kuchukua madaraka ya ndoa?
Kujichunguza kwa weupe wa moyo kwaweza kufunua mengi. Kwa kielelezo, Je, umekomaa na ni mwenye uwezo wa kuchukua daraka kwa kadiri gani? Je, unaweza kuweka pesa akiba, au wewe huzitumia mara tu uzipatapo? Je, wewe hulipa bili zako kwa wakati? Je, una uwezo wa kudumisha kazi au kusimamia nyumba? Je, wewe huwa na uhusiano mzuri na wengine, kama vile wafanyakazi wenzako na wazazi, au unakorofishana nao daima? Ikiwa ndivyo, huenda ukapata kwamba kuwa na uhusiano mzuri na mwenzi wa ndoa kutakuwa jambo gumu sana.
Ikiwa bado wewe ni tineja, huenda ukagundua kwamba unahitaji miaka michache zaidi ya uzoefu ili kupata ukomavu na uthabiti unaohitajika ili kuwa mume au mke mwema. Kutambua uhakika huu kwaweza kukusaidia kurekebisha upya mataraja yako na kuona ndoa kuwa uwezekano wa wakati ujao. Hili laweza kukusaidia ‘kutulia moyoni’ kuhusu hali yako ya useja, angalau kwa wakati uliopo.—1 Wakorintho 7:37.
Kujitayarisha Kufaako
Ingawa hivyo, namna gani ikiwa unaamini kwamba umepita “uzuri wa ujana” na wahisi kwamba uko tayari kufunga ndoa? Inaweza kuvunja moyo ikiwa wenzi wa ndoa ni wachache au ikiwa unakataliwa kila wakati unapoonyesha upendezi kwa mtu fulani. Lakini je, hili lamaanisha kwamba wewe si mwenye kutamanika? Sivyo hata kidogo. Mfalme Sulemani hakufaulu hata chembe katika kumbembeleza msichana aliyekuwa amempenda—ilhali alikuwa mmoja wa watu tajiri na wenye hekima kuliko wote waliopata kuishi! Tatizo lilikuwa nini? Moyo wa huyo msichana haukuelekea kuhisi mahaba kumwelekea. (Wimbo Ulio Bora 2:7) Vivyo hivyo, huenda ikawa kwamba hujakutana na mtu ambaye mnafaana kikweli.
Je, wewe huhisi ukiwa mwenye sura mbaya mno kuweza kuvutia mtu? Ni kweli, sura nzuri zina faida zazo, lakini hizo si kila kitu. Unapofikiria waume na wake unaowajua, si kweli kwamba miongoni mwao mna watu wa vimo vyote, maumbo, na viwango vya uvutio? Isitoshe, mtu anayemhofu Mungu kikweli atahangaikia kwa msingi kile ulicho katika “utu wa rohoni.”—1 Petro 3:4.
Bila shaka, hupaswi hata kidogo kupuuza sura yako ya kimwili; angalau ni jambo la kiakili kujaribu kuonekana vyema kadiri uwezavyo. Mavazi na kujipamba kizembe kwaweza kuwapatia watu maoni mabaya kukuhusu.c Pia, stadi mbaya za mazungumzo au kasoro katika utu wako huenda zikafanya wengine wakuchukie kabla ya kupata kukujua. Rafiki aliyekomaa au mzazi anaweza kukueleza ikiwa marekebisho machache katika sehemu hizi yanahitajiwa. Huenda ukweli uumize, lakini kuukubali labda kwaweza kukusaidia kufanya marekebisho na hivyo kuwa mwenye kuvutia wengine.—Mithali 27:6.
Hata hivyo, katika uchanganuzi wa mwisho, ustahiki, au thamani yako ukiwa mtu haitegemei ikiwa umefunga ndoa au hujafunga. Jambo la thamani ni jinsi Mungu anavyokuona, naye “huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Kwa hivyo jambo kuu la hangaiko lako lapasa kuwa kupata ukubali wa Yehova na si kufunga ndoa. Jaribu kutoruhusu ndoa itawale mawazo na mazungumzo yako. Angalia kwa uangalifu mashirika yako, uchaguzi wako wa muziki, na vitumbuizo.
Ni kweli, tamaa ya kufunga ndoa huenda isitoweke, lakini usiwe na wasiwasi. Uwe na subira. (Mhubiri 7:8) Badala ya kuona useja wako kuwa laana, tumia kikamili faida ya uhuru ambao useja hutoa na fursa unazotoa za kumtumikia Mungu bila kukengeushwa. (1 Wakorintho 7:33-35, 38) Huenda ndoa itokee kwa wakati ufaao—labda hata karibuni zaidi ya unavyofikiri.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Ona makala “Vijana Huuliza . . . Tumeoana Mapema Mno—Je, Tunaweza Kufaulu?” katika toleo letu la Aprili 22, 1995.
c Kwa madokezo hususa kuhusu mambo haya, ona sura za 10 na 11 za kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Ni rahisi kwa mtu kuhisi ameachwa kando wakati marika wake wanafunga ndoa