Sala za Amani Katikati ya Kumbukumbu za Vita
KATIKA Novemba 1994, Papa John Paul wa 2 aliandaa kusanyiko la mchanganyiko wa dini mbalimbali katika Vatikani. Sala kwa ajili ya amani ya ulimwenguni zilikuwa jambo kuu la hiyo pindi. “Haidhuru hata migongano ya wakati uliopita au uliopo iwe nini,” akasema papa katika hotuba yake ya kufungua, “ni kazi na wajibu wetu sote kufanya uhusiano kati ya dini na amani ujulikane vyema zaidi.”
Kwa kinyume, dini za ulimwengu huu zina sifa mbaya kwa habari hii. William Vendley, katibu-mkuu wa kongamano hilo, alikubali kwamba “dini zinahusika kwa kina katika migongano katika sehemu mbalimbali za ulimwengu.” Fikiria yale machinjo katika Rwanda, bara lenye uvutano wa Katoliki ya Kiroma.
Katika Mei 1994, Papa John Paul wa 2 alikiri kwamba msiba wa Rwanda ulikuwa “maangamizi ya jamii nzima-nzima ambayo kwayo, inasikitisha, hata Wakatoliki walihusika.” Je, kujiunga kwa Katoliki kumeathiri itikadi ya watu katika hilo kanisa? “Machinjo hayo yametikisa imani za watu wengi,” akasema André Bouillot, Myesuiti Mbelgiji. Na kukiwa na sababu nzuri.
Kulingana na ripoti ya shirika la habari la Reuters iliyochapishwa katika gazeti Herald la Miami, “makasisi, mapadre na watawa wa kike wako miongoni mwa wafungwa Wahutu 40,000 wanaongojea kuhukumiwa kwa ajili ya matendo ya maangamizi ya jamii nzima-nzima.” The New York Times liliripoti hivi: “Warwanda wengi wanasema kwamba maaskofu na maaskofu wao wakuu hawakushutumu hayo machinjo haraka au kwa uthabiti vya kutosha na kwamba walikuwa na uhusiano wa karibu sana na Serikali ya Habyarimana, ambayo ilisaidia kuzoeza vikundi vya kuua. Angalau kasisi mmoja amefungwa na Serikali mpya inayoongozwa na Watutsi kwa mashtaka ya kushiriki katika machinjo.” Haishangazi, “Serikali mpya,” laongeza Times, “yasema kwamba haitaki Kanisa Katoliki liwe na uwezo mwingi kama lilivyokuwa awali, na majeshi yamesumbua na hata kutisha kuwafunga makasisi ambao wana uhuru sana wa kuongea na wenye ushupavu.”
Je, Yehova Mungu anaonaje sala za amani zinazotolewa na wanadini wenye hatia ya damu? Isaya 1:15 lajibu hivi: “Nanyi mkunjuapo mikono yenu, nitaficha macho yangu nisiwaone; naam, mwombapo maombi mengi, sitasikia; mikono yenu imejaa damu.”
Wakati huohuo, watumishi wa kweli wa Yehova wanabaki wakiwa ‘si sehemu ya ulimwengu’ na migongano yao. Wakati wa hayo machinjo katika Rwanda, Mashahidi wa Yehova wa kila kabila waliandaa makao ya kujificha katika nyumba zao kwa Mashahidi waliotishwa wa kabila jingine, hivyo wakiwalinda kwa kuhatarisha uhai wao wenyewe. Ule “umati mkubwa” wa Mashahidi, unaotolewa ulimwenguni pote kutoka kila kabila, husali kwa ajili ya Ufalme wa Mungu na kuuunga mkono kuwa tumaini pekee la amani na usalama wa kweli.—Yohana 17:14; Ufunuo 7:9; Mathayo 6:9, 10; 24:14.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 24]
Luc Delahaye/Sipa Press