Sababu Inayofanya Makanisa Yafungwe
MAJUZI sana kama miaka 50 iliyopita, makanisa, kwaya, na makaa-mawe, yalikuwa ishara hakika kwamba ulikuwa katika mabonde ya machimbo ya South Wales. Ilionekana kwamba kwa kila meta mia moja, ungepata ama kanisa la lugha ya Wales ama kanisa la Baptisti la lugha ya Kiingereza au makanisa kama hayo kwa ajili ya Wamethodisti, Wamethodisti wa Kikalvini, Wakongrigeshenali, Wapresbiteri, na kadhalika. Kwa kuwa watu wengi wa Wales walisema lugha yao ya kitaifa, karibu kila dini ilikuwa na makanisa tofauti kwa kila lugha. Uvutano wa televisheni wa miongo mitano na viwango vinavyobadilika vimebadili sana yote hayo.
Islwyn Jones ambaye ni mwenyeji wa Wales, anayeishi katika Blaenclydach katika Bonde la Rhondda, ametumia miaka mingi akitarihi mambo yaliyopata makumi ya makanisa ya Rhondda. Gazeti la huko, Rhondda Leader, lilitangaza orodha ya makanisa karibu mia moja, mengi yakianzia tangu karne ya 19, ikionyesha hali yayo ya wakati huu. Ripoti hiyo ilitaarifu: “Majengo haya makuu yalikuwa sehemu muhimu sana ya Rhondda lilipokuwa likipata ongezeko kubwa katika miaka ya uchimbaji wa makaa-mawe hadi kwenye kuanguka hatimaye kwa maegemeo haya mawili [dini na makaa-mawe] ya maisha ya bondeni.”
Orodha hiyo hutumika ikiwa mfano bora zaidi wa kushindwa kwa uvutano wa dini, si katika Wales tu bali pia katika sehemu nyingi za Ulaya. Makanisa 68 yaliorodheshwa kuwa “sasa yamebomolewa.” Kumi na tisa yalikuwa yamegeuzwa kwa matumizi mengineyo. Baadhi ya vielelezo: “limegeuzwa kuwa klabu cha Aikido cha mbinu za kupigana,” “limegeuzwa kuwa nyumba za kuishi,” “limegeuzwa kuwa bohari,” “limegeuzwa kuwa maduka” “limegeuzwa kuwa duka la dawa.” Moja ambalo halikuorodheshwa, katika Penygraig, liligeuzwa miaka mingi iliyopita kuwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova kwa Kutaniko la Rhondda lenye kusitawi sana.
Kama ilivyotabiri Biblia kuhusu “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, maji yayo ya ufananisho, utegemezo wa watu, yanakauka katika sehemu nyingi za ulimwengu. Karibuni sehemu za kisiasa za ulimwengu zitageukia dini zitakapokuwa ‘zikitekeleza fikira ya [Mungu]’ ya kuharibu dini isiyo ya kweli, ambayo imekufuru katika ulimwengu wote mzima jina na kusudi la Yehova Mungu.—Ufunuo 17:5, 15-17, NW.a
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari ya ndani zaidi kuhusu mambo yatakayopata Babiloni Mkubwa, ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kurasa 258-266, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.