“Mwanga Katika Enzi Yenye Giza”
Na mleta-habari wa Amkeni! katika Ujerumani
HIVYO ndivyo mwanahistoria mmoja alivyofafanua historia ya Mashahidi wa Yehova wakati wa enzi ya Nazi. Pindi hiyo ilikuwa sherehe ya wonyesho wa kwanza wa vidio ya masimulizi iitwayo Jehovah’s Witnesses Stand Firm Against Nazi Assault, iliyofanywa katika Ravensbrück Memorial, nchini Ujerumani. Vidio hii inasimulia masimulizi yenye kusikitisha ya moyo mkuu na imani kama yalivyosimuliwa na waokokaji 24 wa enzi ya Nazi, pamoja na wasomi 10 wa historia na dini.
Kambi ya mateso ya Ravensbrück pindi moja ilikuwa na mamia ya Mashahidi wa Yehova. Mashahidi fulani waliookoka, ambao walifungwa na Nazi zaidi ya miaka 50 iliyopita, walikuwa katika wonyesho huo. Wao, na vilevile wanahistoria na maofisa wa serikali, walikumbuka zile siku zenye huzuni ambapo utawala wa Nazi uliteka Ulaya katika utawala wenye kuogofya. Wahudhuriaji wapatao 350 walisikiliza masimulizi yenye kuvuvia ya uaminifu-maadili wa Kikristo wa mamia ya Mashahidi ambao walikabili vifo kishujaa badala ya kukana imani yao.
Vyombo vya Habari Vyatazama
Mkutano wa waandishi wa habari ulifanywa kwenye hoteli moja ya Berlin asubuhi ya siku ya wonyesho, Novemba 6, 1996. Waandishi wa habari walitazama sehemu fupi-fupi za vidio hiyo kisha wakasikiliza hotuba za wasomi ambao walitaja umuhimu wa vidio hiyo mpya katika kujulisha historia hiyo isiyojulikana sana lakini iliyo muhimu. Dakt. Detlef Garbe, mkurugenzi wa Neuengamme Memorial, alieleza: “Sisi—Mashahidi wa Yehova na wale wasio Mashahidi—hatupaswi kusahau historia ya wafungwa wenye pembetatu za zambarau [ishara iliyovaliwa na wafungwa Mashahidi]. Huo ulikuwa mwanga katika enzi yenye giza.”
Mashahidi kadhaa waliookoka na ambao walitokea katika Stand Firm walikuwapo ili kusimulia mambo waliyojionea. Je, walikuwa na kinyongo kwa jinsi walivyoteswa? Nyuso zao zenye utulivu na wangavu zilionyesha kwamba hawakufungia kinyongo.
Baada ya kipindi cha maswali kwa majibu, waandishi wa habari walialikwa kwenye wonyesho wa kwanza wa vidio Stand Firm katika Ravensbrück Memorial, umbali wa kilometa 60 hivi. Karibu wote walikubali mwaliko huo.
Huo Wonyesho
Anga yenye rangi ya kijivu na manyunyu katika siku hiyo yenye baridi katika msimu wa vuli iliondolewa na hali ya uchangamfu iliyokuwa ndani ya ukumbi uliotoka kurekebishwa upya kando ya Ravensbrück Memorial. Profesa Jürgen Dittberner, ambaye wakati huo alikuwa mkurugenzi wa Wakfu wa ukumbusho wa Ravensbrück, Sachsenhausen, na Brandenburg, alisema: “Moyo mkuu wa kiadili ulioonyeshwa na Mashahidi wa Yehova waliokuwa chini ya usoshalisti wa kitaifa ni lazima ustahiwe. . . . Tunawakumbuka kwa staha sana watu hawa ambao hawakukana imani yao na ambao walilazimika kuteseka au hata kufa kwa sababu ya imani yao.”
Angelika Peter, waziri wa elimu, vijana, na mchezo wa Brandenburg, Ujerumani, alipeleka ujumbe ambao ulisomwa. Ujumbe huo ulisema: “Ni muhimu kwamba leo twakumbuka ushikamanifu wenye mfano mzuri wa Mashahidi wa Yehova.” Dakt. Sigrid Jacobeit, mkurugenzi wa Ravensbrück Memorial, alisema: “Natazamia wonyesho huo wa kwanza kwa hamu na shangwe. Nafikiri hii ni siku ya pekee kwetu sote.”
Ndipo taa zikapunguzwa mwanga ili vidio ianze. Kwa dakika 78 si waokokaji pekee kutoka nchi nane bali pia wote waliohudhuria walikumbuka msiba na ushindi wa kipindi hicho chenye uchungu katika historia ya Ujerumani. Wengi walishindwa kuzuia machozi wakati watu hao wa kawaida walipoeleza matendo yasiyo ya kawaida ya upendo na imani wakiwa chini ya hali mbaya kabisa.
Baada ya makofi makubwa kupoa, mwanahistoria Joachim Görlitz alisoma maneno ya mwisho ya Shahidi mmoja ambaye alikuwa amefishwa katika Brandenburg. Görlitz alikuwa amepata karatasi hiyo majuma mawili tu awali alipokuwa akifanya utafiti katika Brandenburg Memorial and Archive, ambalo yeye ndiye mkurugenzi walo. Sauti yake ilitetemeka kwa hisia alipokuwa akisoma maneno ya Mkristo huyo mwaminifu yenye kutia moyo waamini wenzake kushikilia Bwana wao. Kisha Görlitz akamalizia: “Mabibi na Mabwana, naamini kwamba sinema juu ya Mashahidi wa Yehova itachangia sana kazi yetu ya kielimu.”
Mwanahistoria Wulff Brebeck alitangaza kwamba “kupitia sinema hii kitu fulani chenye thamani kimeongezwa—maneno ya waokokaji ambao hawajasikiwa sana, na . . . maneno ya wale ambao hawakuokoka.” Dakt. Garbe aliongezea: “Haya ni mambo muhimu yaliyoonwa na wanadamu ambao imani yao kwa Mungu na itibari zao katika ahadi za Biblia ziliwapa nguvu za kusimama imara katika pindi hiyo yenye kuogofya.”
Ukiwa mwisho ufaao wa programu hiyo, kwa mara nyingine tena waokokaji kadhaa walio Mashahidi walitoa hotuba. Ilikuwa wazi kwa wote kwamba Wakristo hao walio imara bado wana imani ileile yenye nguvu ambayo iliwategemeza katika majaribu yao mengi.
Tangu wonyesho huo, zaidi ya makala 340 kuhusu Mashahidi wa Yehova na vidio ya Stand Firm zimetokea katika magazeti ya habari kote Ujerumani. Programu kadhaa za redio, moja ikiwa katika redio ya kitaifa, zilikuwa na ripoti nzuri vilevile.
Hii vidio ya Stand Firm hatimaye itapatikana katika angalau lugha 24. Vidio iliyohaririwa ya kutumiwa darasani pia itapatikana hatimaye. Tangu kutolewa kwa vidio hiyo, idadi inayozidi kuongezeka ya waelimishaji imeanza kutumia vidio ya Stand Firm ikiwa sehemu ya mafundisho yao ili kusaidia vijana kufikiria masuala muhimu, kama vile ubaguzi, msongo wa marika, na kukataa kidhamiri.
Katika ulimwengu huu ambao umegawanyika sana kwa chuki na usaliti, yafaa kama nini kwamba masimulizi haya ya uaminifu-maadili yajulishwe umma! Kwa kweli mateseko ya Wakristo hao waaminifu hayajakuwa ya bure.—Waebrania 6:10.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Mkutano wa waandishi wa habari uliofanywa Berlin. Kutoka kushoto: Dakt. Detlef Garbe, waokokaji wa Maangamizi Simone Liebster na Franz Wohlfahrt, na mwanahistoria Wulff Brebeck