Ni Nini Kisababishi cha Uhalifu wa Vijana?
JE, WEWE una maoni ya kawaida kwamba watoto wahalifu hutoka katika familia zilizo maskini na kwamba watoto kutoka familia zenye “kuheshimiwa” ni vigumu wajihusishe na uhalifu? Katika Asia mambo ya hakika yalionekana yakiunga mkono maoni hayo. “Jambo hili si kweli tena,” laripoti Asia Magazine. “Takwimu za polisi na kesi katika Asia kote zaonyesha kwamba vijana wengi zaidi na zaidi kutoka familia zenye kuheshimiwa huiba, huharibu vitu, hutumia dawa za kulevya na hugeukia ukahaba.”
Kwa kielelezo, katika Japani nusu ya vijana wote walioshtakiwa kosa la jinai wanatoka katika familia tajiri. Ndivyo hali ilivyo katika Bangkok pia. “Zamani,” asema Adisai Ahapanun, mkuu wa Chuo cha Muhita, “uhalifu wa vijana ulichochewa zaidi na ukosefu wa pesa. Leo, zaidi ya asilimia 50 ya vijana hapa wanatoka katika familia tajiri zisizokuwa na magumu yoyote ya kiuchumi.”
Wengine wanasema hali hii imesababishwa na wanawake wanaofanya kazi, ongezeko la talaka, kupenda vitu vya kimwili maishani. Asema Eddie Jacob, naibu-mkurugenzi wa mahali pa kupumzikia safarini kwa vijana katika Singapore: “Msingi ni familia zenye shida—ambapo wazazi waweza kuwa wametalikiana, au kuna mzazi mmoja, au wazazi wote wawili wanafanya kazi na watoto wanapuuzwa. Watoto hujifunza maadili nyumbani.”
Biblia ilitabiri kwamba nyakati zetu zingetiwa alama na uasi miongoni mwa vijana. (2 Timotheo 3:1, 2) Na bado, kitabu hichohicho chaweza kuzipa familia kanuni zinazohitaji ili ziwe pamoja, bila kujali hali yao ya kiuchumi. Inastahili kuichunguza Biblia, kwani “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Timotheo 3:16) Mashahidi wa Yehova katika Asia—kwa kweli, ulimwenguni pote—wanapata thawabu ya kujifunza Biblia wakiwa familia. Watafurahi kukusaidia ufanye vivyo hivyo.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Chaguo ni lako—uhalifu au kibali cha Mungu