Je, Kweli Ni Lazima Kutiwa Damu Mishipani?
SWALI hilo lilizushwa katika makala moja ya gazeti la habari mwezi wa Novemba mwaka jana iliyoandikwa na Dakt. Ciril Godec, mwenyekiti wa urolojia katika Long Island College Hospital, huko Brooklyn, New York. Aliandika hivi: “Leo huenda damu isikubaliwe kuwa dawa, kwa kuwa haitatimiza viwango vya usalama vya Shirika Linaloshughulikia Chakula na Dawa. Damu ni kiungo cha mwili, na utiaji-damu mishipani kwa kweli ni kupandikiza kiungo.”
Dakt. Godec alisema: “Kupandikizwa kiungo ni uamuzi wa mwisho kabisa wa matibabu wanaopata wagonjwa. Kwa sababu ya uwezekano wa kupata athari mbaya sana, wagonjwa huarifiwa kikamili kuhusu matibabu yote ya badala kabla ya kupandikizwa kiungo.” Kuhusu utiaji-damu mishipani, yeye alikata kauli hivi: “Manufaa yake ni yenye kutiliwa shaka sana hivi kwamba madaktari wapasuaji wengi wanafuata falsafa ya ‘kuepuka utiaji-damu mishipani’ si kwa sababu za kitiba tu bali pia kwa sababu za kisheria.”
Tatizo kubwa la utiaji-damu mishipani ni kuwa maelfu ya watu wameambukizwa maradhi ya kufisha, kutia ndani UKIMWI. Ijapokuwa njia za kupima damu zimeboreshwa katika sehemu nyingi, Dakt. Godec alisema: “Hatari kubwa hutokana na damu iliyotolewa na watu walioambukizwa ambao bado hawaonyeshi zindiko zinazoweza kugunduliwa kupitia upimaji.”
Akimalizia makala yake, Dakt. Godec alizungumzia swali lililozushwa hapo juu: “Matabibu na madaktari wapasuaji waelewapo zaidi uwasilishaji wa oksijeni na kutambua kwamba kiasi cha hemoglobini hakihitaji kuwa juu jinsi ilivyofikiriwa hapo awali, sikuzote inakuwa kwamba wanaweza kupata matibabu badala yasiyohusisha utiaji-damu mishipani. Hivi karibuni, yapata mwaka mmoja uliopita upasuaji mgumu wa kupandikiza moyo na ini ulihusisha kupoteza damu nyingi sana hivi kwamba upasuaji wa aina hiyo sikuzote ulionwa kuwa unahitaji kiasi kikubwa sana cha damu ili kurudishwa mwilini. Sasa, upasuaji wote huo umeweza kufanywa bila uhitaji wa kutia damu mishipani.
“Ni jambo linalowezekana kwamba hivi karibuni utiaji-damu mishipani utakomeshwa kabisa. . . . Licha ya utiaji-damu mishipani kugharimu fedha nyingi na kuwa hatari; huo si utunzaji bora ambao wagonjwa wanastahili kupata.”