Kitabu Cha Biblia Namba 46—1 Wakorintho
Mwandikaji: Paulo
Mahali Kilipoandikiwa: Efeso
Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 55 W.K.
1. Korintho lilikuwa jiji la aina gani katika siku za Paulo?
KORINTHO “lilikuwa jiji maarufu lenye anasa za kimwili, ambapo maovu ya Mashariki na Magharibi yalikutania.”a Likiwa katika isthmasi (shingo-ardhi) yenye kuunganisha Peloponnesus na Ugiriki ya kontinenti, Korintho lilikuwa ndipo mahali pakuu pa kupitia nchi kavu wakati wa kuendea sehemu ile kubwa zaidi ya bara. Katika siku za mtume Paulo, idadi yalo ya watu waliokadiriwa kuwa 400,000 hivi ilipitwa tu na Rumi, Aleksandria, na Antiokia ya Shamu. Upande wa mashariki wa Korintho ilikuwako Bahari ya Aegea, na upande wa magharibi, Ghuba ya Korintho na Bahari Ionia. Kwa hiyo Korintho, likiwa ndilo jiji kuu la mkoa wa Akaya, wenye bandari mbili za Kenkrea na Lekayo, lilikuwa mahali palipofaa sana kwa biashara. Lilikuwa pia kitovu cha kusomea mafunzo ya Kigiriki. “Utajiri walo,” imesemwa, “uliadhimishwa sana hata ukawa ukisifiwa kila mahali; ndivyo na maovu na upotovu wa wakaaji walo.”b Miongoni mwa mazoea yalo ya dini ya kipagani ilikuwamo ibada ya Afrodite (mlingani wa Venasi Mroma). Tamaa za mwili zilikuwa ni zao la ibada ya Korintho.
2. Kundi la Korintho lilianzishwaje, na kwa sababu hiyo lilikuwa na kifungo gani pamoja na Paulo?
2 Mji mkuu huo wenye kusitawi sana lakini wenye kuchakaa kiadili wa ulimwengu wa Kirumi ndio mtume Paulo alisafiri kuuendea katika 50 W.K. hivi. Wakati wa kukaa kwake huko miezi 18, kundi la Kikristo lilianzishwa. (Mdo. 18:1-11) Ni upendo ulioje ambao Paulo alihisi kuelekea waamini hawa aliokuwa amewapelekea kwanza habari njema juu ya Kristo! Kwa kutumia barua aliwakumbusha kifungo cha kiroho kilichokuwako, akisema: “Ijapokuwa mna waalimu kumi elfu katika Kristo, walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili.”—1 Kor. 4:15.
3. Ni nini kilichosukuma Paulo kuandika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho?
3 Hangaiko la kina kirefu kuhusu hali njema yao ya kiroho lilisukuma Paulo kuandika barua yake ya kwanza kwa Wakristo Wakorintho akiwa katika safari yake ya tatu ya umisionari. Miaka michache ilikuwa imepita tangu alipokuwa amekaa katika Korintho. Sasa ilikuwa 55 W.K. hivi, na Paulo alikuwa katika Efeso. Yaonekana alikuwa amepokea barua kutoka kundi hilo la Korintho lililokuwa jipya kwa kulinganisha, na barua hiyo ilitaka jibu. Zaidi ya hilo, ripoti za kusumbua zilikuwa zimefikia Paulo. (7:1; 1:11; 5:1; 11:18) Zilikuwa za kutaabisha fikira sana hivi kwamba mtume hata hakurejezea barua yao ya kuulizia mambo mpaka kwenye mstari wa kufungua sura ya 7 ya barua yake. Paulo aliona lazima ya kuandikia Wakristo wenzake katika Korintho hasa kwa sababu ya ripoti alizokuwa amepokea.
4. Ni nini kinachothibitisha kwamba Paulo aliandika Wakorintho wa kwanza akiwa Efeso?
4 Lakini sisi twajuaje kwamba Paulo aliandika Wakorintho wa Kwanza kutoka Efeso? Kwanza, katika kumalizia barua hiyo kwa salamu, mtume atia ndani zile za Akila na Priska (Prisila). (16:19) Matendo 18:18, 19 yaonyesha kwamba wao walikuwa wamehama Korintho wakaenda Efeso. Kwa kuwa Akila na Prisila walikuwa wakikaa huko na Paulo aliwatia katika salamu za mwisho-mwisho za Wakorintho wa Kwanza, lazima awe alikuwa katika Efeso alipoandika barua hiyo. Hata hivyo, jambo moja lisiloacha shaka ni taarifa ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 16:8: “Lakini nitakaa Efeso hata Pentekoste.” Kwa hiyo Wakorintho wa Kwanza kiliandikwa na Paulo kule Efeso, yaonekana karibu na mwisho wa kukaa kwake huko.
5. Ni nini kinachothibitisha uasilia wa barua hizi kwa Wakorintho?
5 Uasilia wa Wakorintho wa Kwanza, na pia Wakorintho wa Pili, hauwezi kutiliwa shaka. Barua hizo zilihesabiwa kuwa za Paulo na kuonwa na Wakristo wa mapema kuwa zenye kukubalika, nao walizitia miongoni mwa mikusanyo yao. Kwa uhakika, yasemwa kwamba Wakorintho wa Kwanza chagusiwa na kunukuliwa angalau mara sita katika barua moja ya kutoka Rumi kwenda Korintho ya tarehe ya 95 W.K. hivi ambayo yaitwa Clement wa Kwanza. Kwa wazi akirejezea Wakorintho wa Kwanza, mwandikaji alihimiza wapokeaji wa barua hiyo “wakubali waraka huu wa Paulo mbarikiwa aliye mtume.”c Pia Wakorintho wa Kwanza chanukuliwa moja kwa moja na Justin Martyr, Athenagoras, Irenaeus, na Tertullian. Kuna uthibitisho wenye nguvu kwamba mkusanyo wa barua za Paulo, kutia na Wakorintho wa Kwanza na wa Pili, “ulifanyizwa na kutangazwa katika miaka kumi ya mwisho ya karne ya kwanza.”d
6. Ni matatizo gani yaliyokuwa katika kundi la Korintho, na Paulo alipendezwa na nini hasa?
6 Barua ya kwanza ya Paulo kwa Wakorintho yatupa nafasi ya kutazama ndani ya kundi lenyewe la Korintho. Wakristo hao walikuwa na matatizo ya kupambana nayo, nao walikuwa na masuala ya kutatuliwa. Kulikuwa na vikundi vyenye kuzozana katika kundi, kwa maana wengine walikuwa wakifuata wanadamu. Kisa fulani chenye kuhuzunisha cha ukosefu wa adili za kingono kilikuwa kimetokea. Watu fulani walikuwa wakiishi katika nyumba zilizogawanyika kidini. Je! wabaki pamoja na wenzi wao wa ndoa wasioamini au watengane? Namna gani juu ya kula nyama iliyotolewa sadaka kwa sanamu? Je! waishiriki? Wakorintho walihitaji ushauri kuhusu uongozaji wa mikutano yao, kutia na mwadhimisho wa Chakula cha Jioni cha Bwana. Msimamo wa wanawake katika kundi ulipasa kuwa nini? Halafu, pia, kati yao walikuwako wale waliokana ufufuo. Matatizo yalikuwa mengi. Ingawa hivyo, mtume alipendezwa hasa na kurudisha Wakorintho kwenye hali ya kiroho inayofaa.
7. Twapaswa kufikiria Wakorintho wa Kwanza tukiwa na mwelekeo gani wa akilini, na kwa nini?
7 Kwa sababu hali iliyokuwa ndani ya kundi na mazingira yaliyokuwa nje katika Korintho la kale, pamoja na usitawi na upotovu mwingi wa jiji hilo, havikosi ulinganifu wa ki-siku-hizi, shauri thabiti la Paulo lililoandikwa chini ya upulizio wa kimungu lastahili fikira zetu. Aliyosema Paulo yamejaa maana sana kwa siku yetu wenyewe hivi kwamba tutapata mafaa kweli kweli tukifikiria kwa uangalifu barua yake ya kwanza kwa ndugu na dada zake Wakorintho. Sasa kumbuka roho ya wakati wenyewe na mahali penyewe. Fikiri kwa kupekua-pekua, kama vile ambavyo ni lazima Wakristo Wakorintho wawe walifanya, wakati tunapoyapitia maneno yaliyopuliziwa na Mungu, yenye kupenya moyoni, yenye kuchochea, ambayo Paulo alisema kwa waamini wenzake katika Korintho la kale.
YALIYOMO KATIKA WAKORINTHO WA KWANZA
8. (a) Paulo anafunuaje upumbavu wa kuwa na hali ya mfarakano katika kundi? (b) Paulo aonyesha ni nini kinachohitajiwa kabisa ili kuelewa mambo ya Mungu?
8 Paulo afichua hali ya mfarakano, ahimiza umoja (1:1–4:21). Paulo awatakia mema Wakorintho. Lakini namna gani juu ya vile vikundi vyenye kuzozana, ile migawanyiko, miongoni mwao? “Kristo amegawanyika.” (1:13) Mtume ashukuru kwamba amebatiza wachache sana kati yao, hivyo hawawezi kusema wamebatizwa kwa jina lake. Paulo ahubiri Kristo mtundikwa. Hicho ni kisababishi cha kukwaza Wayahudi na ni upumbavu kwa mataifa. Lakini Mungu alichagua vitu vilivyo vipumbavu na dhaifu vya ulimwengu ili kuaibisha walio na hekima na wenye nguvu. Kwa hiyo Paulo hatumii uneni wa kupita kiasi bali awaacha akina ndugu waone roho na nguvu ya Mungu kupitia maneno yake, ili imani yao isiwe katika hekima ya wanadamu bali katika nguvu ya Mungu. Sisi twanena mambo yaliyofunuliwa na roho ya Mungu, asema Paulo, ‘maana roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu.’ Hayo hayawezi kueleweka na mwanadamu wa kimwili isipokuwa tu na mtu wa kiroho.—2:10.
9. Paulo aonyesha kwa hoja gani kwamba hakuna mmoja anayepaswa kujisifu katika wanadamu?
9 Wao wafuata wanadamu—wengine wao Apolo, wengine wao Paulo. Lakini hao ni akina nani? Ni wahudumu tu ambao kupitia kwao Wakorintho walikuja kuwa waamini. Wenye kupanda na kutia maji si kitu, kwa maana “mwenye kukuza ni Mungu,” nao ni “wafanya kazi pamoja na” yeye. Mtihani wa moto utathibitisha ni kazi za nani zilizo za kudumu. Paulo awaambia, “Ninyi mmekuwa hekalu la Mungu,” ambamo roho Yake yakaa. “Hekima ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu.” Kwa sababu hiyo, mtu yeyote asijisifu katika wanadamu, kwa maana kweli kweli vitu vyote ni vya Mungu.—3:6, 9, 16, 19.
10. Kwa nini kujisifu kwa Wakorintho hakufai, na ni hatua gani ambazo Paulo achukua aondoe hali ile?
10 Paulo na Apolo ni mawakili wanyenyekevu wa siri takatifu za Mungu, na mawakili wapaswa kupatikana wakiwa waaminifu. Hao ndugu wa Korintho ni akina nani hata wajisifu, nao wana kitu gani ambacho hawakupokea? Je! wao wamekuwa matajiri, wakaanza kutawala wakiwa wafalme, na kuwa wenye akili na nguvu sana, huku mitume, ambao wamekuwa tamasha kwa malaika na hata wanadamu, wakiwa wangali ni wapumbavu na dhaifu, takataka za vitu vyote? Paulo atuma Timotheo kuwasaidia kukumbuka njia alizotumia yeye kuhusiana na Kristo kisha wawe waigaji wake. Yehova akipenda, Paulo mwenyewe atakuja baada ya muda mfupi na kupata kujua, si uneni tu wa wale waliojivimbisha kwa kiburi, bali pia nguvu yao.
11. Ni ukosefu gani wa adili umetokea miongoni mwao, ni jambo gani lazima lifanywe kuhusu hilo, na kwa nini?
11 Kuhusu kuweka kundi likiwa safi (5:1–6:20). Kisa cha kuhuzunisha juu ya ukosefu wa adili kimeripotiwa miongoni mwa Wakorintho! Mwanamume mmoja amechukua mke wa baba yake. Lazima apewe kwa Shetani kwa sababu chachu kidogo huchachusha donge zima. Lazima waache kuchangamana katika uandamani pamoja na yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwovu.
12. (a) Paulo atoa hoja gani juu ya kupelekana mahakamani? (b) Kwa nini Paulo asema, “Ikimbieni zinaa”?
12 Naam, Wakorintho wamekuwa hata wakipelekana mahakamani! Je! isingekuwa afadhali wakubali kupunjwa? Kwa kuwa wao watahukumu ulimwengu na malaika, je! hawawezi kupata mmoja miongoni mwao wa kuhukumu kati ya akina ndugu? Zaidi ya hilo, wapaswa kuwa safi, kwa maana waasherati, waabudu-sanamu, na watu kama hao hawatarithi Ufalme wa Mungu. Hivyo ndivyo baadhi yao walivyokuwa, lakini wameoshwa wakawa safi na kutakaswa. “Ikimbieni zinaa,” asema Paulo. “Maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.”—6:18, 20.
13. (a) Kwa nini Paulo ashauri wengine wafunge ndoa? Lakini wakiisha kufunga ndoa, wapaswa kufanya nini? (b) Ni jinsi gani asiyefunga ndoa ‘afanya vizuri zaidi’?
13 Shauri juu ya useja na ndoa (7:1-40). Paulo ajibu swali moja juu ya ndoa. Kwa sababu ya kuwako sana kwa uasherati, huenda ikafaa mwanamume au mwanamke afunge ndoa, na wale waliofunga ndoa hawapaswi kuwa wakinyimana haki za ndoa. Ni vizuri wasiooa na wajane wabaki bila kufunga ndoa, kama Paulo; lakini ikiwa hawana kujiweza, acheni wafunge ndoa. Wakiisha kufunga ndoa, wapaswa kubaki pamoja. Hata ikiwa mwenzi wa mtu si mwamini, aliye mwamini hapaswi kuondoka, kwa maana kwa njia hiyo aliye mwamini huenda akaokoa mwenzi asiyeamini. Kwa habari ya kutahiriwa na utumwa, kila mmoja aridhike kubaki katika hali ambayo alikuwa nayo alipoitwa. Kwa habari ya mtu aliyefunga ndoa, yeye amegawanyika kwa sababu ataka kupata kibali cha mwenzi wake wa ndoa, hali asiyefunga ndoa ahangaikia mambo ya Bwana tu. Wale wanaofunga ndoa hawafanyi dhambi, lakini wale wasiofunga ndoa ‘wanafanya vizuri zaidi.’—7:38, NW.
14. Paulo asema nini juu ya “miungu” na “mabwana,” hata hivyo ni wakati gani ambapo ni jambo la hekima kujiepusha na chakula kilichotolewa sadaka kwa sanamu?
14 Kufanya mambo yote kwa ajili ya habari njema (8:1–9:27). Namna gani juu ya chakula kilichotolewa kwa sanamu? Sanamu si kitu! Kuna “miungu” mingi na “mabwana” wengi ulimwenguni, lakini kwa Mkristo “Mungu ni mmoja tu, aliye Baba,” na “Bwana mmoja Yesu Kristo.” (8:5, 6) Hata hivyo huenda mtu fulani akaudhika akikuona ukila nyama iliyotolewa sadaka kwa sanamu. Chini ya hali hizo, Paulo ashauri, jiepushe nayo ili usisababishe ndugu yako ajikwae.
15. Paulo ajiendeshaje katika huduma?
15 Paulo ajinyima mwenyewe mambo mengi kwa ajili ya huduma. Akiwa mtume, ana haki ya ‘kupata riziki kwa hiyo Injili,’ lakini amejiepusha kufanya hivyo. Hata hivyo, uhitaji wa lazima umewekwa juu yake ahubiri; kwa uhakika, yeye asema, “Ole wangu nisipoihubiri Injili!” Kwa hiyo amejifanya mtumwa kwa wote, akiwa “hali zote kwa watu wote,” ili kwamba ‘kwa njia zote apate kuwaokoa watu’ kwa kadiri fulani, akifanya mambo yote “kwa ajili ya Injili.” Ili ashinde shindano na taji lisiloharibika, autenda vikali mwili wake ili kwamba baada ya kuhubiria wengine yeye mwenyewe ‘asiwe mtu wa kukataliwa’ kwa njia fulani.—9:14, 16, 19, 22, 23, 27.
16. (a) Ni onyo gani ambalo Wakristo wapaswa kuchukua kutokana na “baba” waliotangulia? (b) Wakristo wawezaje kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu kuhusu ibada ya sanamu?
16 Onyo juu ya mambo yenye madhara (10:1–33). Namna gani juu ya “baba” waliotangulia? Wao walikuwa chini ya lile wingu na walibatizwa katika Musa. Walio wengi kati yao hawakupata kibali cha Mungu bali waliuawa jangwani. Kwa nini? Wao walitamani mambo yenye madhara. Wakristo wapaswa kuchukua onyo kutokana na jambo hilo na kujiepusha na ibada ya sanamu na uasherati, na kutomtia Yehova kwenye mtihani, na kunung’unika. Anayefikiri amesimama apaswa kuwa mwangalifu asije akaanguka. Kishawishi kitakuja, lakini Mungu hataacha watumishi wake wajaribiwe kadiri wasivyoweza kuvumilia; yeye atatoa njia ya kutokea ili waweze kuvumilia. “Kwa ajili ya hayo,” aandika Paulo, “ikimbieni ibada ya sanamu.” (10:1, 14) Hatuwezi kuwa washiriki wa meza ya Yehova na meza ya roho waovu. Hata hivyo, iwapo wala katika nyumba fulani, usiulizie-ulizie chanzo cha nyama ile. Ingawa hivyo, ikiwa mtu fulani akushauri kwamba imetolewa sadaka kwa sanamu, jiepushe kuila kwa sababu ya dhamiri yake. “Fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu,” aandika Paulo.—10:31.
17. (a) Ni kanuni gani ambayo Paulo aweka wazi kuhusu ukichwa? (b) Yeye aunganishaje suala la mgawanyiko kundini pamoja na mazungumzo ya Chakula cha Jioni cha Bwana?
17 Ukichwa; Chakula cha Jioni cha Bwana (11:1-34). “Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo,” ajulisha rasmi Paulo, na kisha aweka wazi kanuni ya kimungu ya ukichwa: Kichwa cha mwanamke ni mwanamume, kichwa cha mwanamume ni Kristo, kichwa cha Kristo ni Mungu. Kwa hiyo, mwanamke apaswa kuwa na “dalili ya kumilikiwa” juu ya kichwa chake wakati anaposali au anapotoa unabii katika kundi. Paulo hawezi kuwapongeza Wakorintho, kwa maana migawanyiko imo miongoni mwao wakati wanapokutana pamoja. Wakiwa katika hali hiyo, wawezaje kushiriki ifaavyo Chakula cha Jioni cha Bwana? Yeye apitia jambo lililotukia wakati Yesu alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake. Lazima kila mmoja ajichunguze sana mwenyewe kabla ya kushiriki, asije akajiletea hukumu mwenyewe kwa kutoupambanua “ule mwili.”—11:1, 10, 29.
18. (a) Ingawa kuna zawadi na huduma za namna mbalimbali, kwa nini hakupasi kuwa na mgawanyiko wowote katika mwili? (b) Kwa nini upendo ndilo jambo kubwa kuliko yote?
18 Zawadi za kiroho; upendo na kuufuatia (12:1–14:40). Kuna namna mbalimbali za zawadi za kiroho, hata hivyo roho ni ile ile moja; namna mbalimbali za huduma na utendaji, hata hivyo kuna Bwana na Mungu yule yule mmoja. Vilevile kuna washiriki wengi katika mwili ule mmoja tu wa Kristo ulio na muungamano, kila mshiriki akihitaji yule mwingine, kama ilivyo katika mwili wa kibinadamu. Mungu ameweka kila mshiriki katika mwili kama impendezavyo Yeye, na kila mmoja ana kazi yake, kwa hiyo “kusiwe na faraka katika mwili.” (12:25) Watumizi wa zawadi za kiroho si kitu ikiwa hawana upendo. Upendo ni mstahimilivu na mfadhili, si wenye wivu, haujivimbishi kwa kiburi. Washangilia pamoja na ukweli tu. “Upendo haupungui neno wakati wo wote.” (13:8) Zawadi za kiroho, kama vile kutoa unabii na kusema ndimi mbalimbali, zitaondolewa mbali, lakini imani, tumaini, na upendo vyabaki. Kati yavyo, kilicho kikubwa zaidi ni upendo.
19. Paulo atoa shauri gani ili kundi lijengwe, na mambo kupangwa kwa utaratibu?
19 “Ufuateni upendo,” Paulo aonya kwa upole. Zawadi za kiroho ni za kutumiwa kwa upendo ili kujenga kundi. Kwa sababu hiyo, kutoa unabii kwaonwa kuwa afadhali kuliko kunena kwa ndimi. Afadhali anene maneno matano yenye kueleweka ili afundishe wengine kuliko maneno elfu kumi kwa lugha isiyojulikana. Kusema ndimi mbalimbali kwafanywa ili kuwe ishara kwa wasioamini, lakini kutoa unabii ni kwa ajili ya waamini. Wao hawapaswi kuwa “watoto” katika kuelewa kwao mambo haya. Kwa habari ya wanawake, wapaswa kuwa katika ujitiisho kundini. “Mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.”—14:1, 20, 40.
20. (a) Paulo atoa uthibitisho gani juu ya ufufuo wa Kristo? (b) Ufufuo watokea kwa kufuata utaratibu gani, na ni adui gani ambao wataangushwa?
20 Uhakika wa tumaini la ufufuo (15:1–16:24). Kristo mfufuliwa alitokea Kefa, wale 12, hata wengi zaidi kufikia ndugu 500 wakati mmoja, Yakobo, mitume wote, na mwisho kabisa akamtokea Paulo. “Kama Kristo hakufufuka,” aandika Paulo, ‘kuhubiri kwetu na imani yetu ni bure.’ (15:14) Kila mmoja ainuliwa kwa kufuata utaratibu wake mwenyewe, Kristo matunda ya kwanza, halafu baadaye wale walio wake wakati wa kuwapo kwake. Mwishowe ampa Baba yake Ufalme baada ya maadui wote kuwa wamewekwa chini ya nyayo zake. Hata kifo, ambacho ndicho adui wa mwisho, chabatilishwa kabisa. Kuna faida gani Paulo kupambana na hatari za kifo kwa uendelevu ikiwa hakuna ufufuo?
21. (a) Wale watakaorithi ufalme wa Mungu wainuliwaje? (b) Paulo afunua siri gani takatifu, na asema nini kwa habari ya ushindi juu ya kifo?
21 Lakini wafu watainuliwaje? Ili mwili wa mmea ukue, ni lazima mbegu iliyopandwa ife. Ndivyo ulivyo ufufuo wa wafu. “Hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili wa roho. . . . Nyama na damu haziwezi kuurithi ufalme wa Mungu.” (15:44, 50) Paulo asimulia siri takatifu: Si wote ambao watalala usingizi katika kifo, bali wakati wa tarumbeta ya mwisho, watabadilishwa kwa kufumba na kufumbua jicho. Wakati hiki chenye kufa kivaapo kutokufa, kifo kitamezwa kabisa milele. “Ku wapi, Ewe mauti, kushinda kwako? U wapi, Ewe mauti, uchungu wako?” Paulo apaaza mshangao huu: “Lakini Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda [kupitia, NW] kwa Bwana wetu Yesu Kristo”!—15:55, 57.
22. Paulo atoa shauri na himizo gani la kumalizia?
22 Kwa kumalizia Paulo atoa shauri juu ya kuwa na utaratibu katika kukusanya michango ya kupelekwa Yerusalemu ili kusaidia ndugu wahitaji. Aeleza juu ya ziara yake inayokuja ya kupitia Makedonia na kuonyesha kwamba huenda pia Timotheo na Apolo wakawatembelea. “Kesheni,” Paulo ahimiza. “Simameni imara katika Imani, fanyeni kiume, mkawe hodari. Mambo yenu yote na yatendeke katika upendo.” (16:13, 14) Paulo apeleka salamu kutoka makundi katika Asia, halafu aandika salamu ya mwisho kwa mkono wake mwenyewe, akiwapitishia upendo wake.
KWA NINI NI CHENYE MAFAA
23. (a) Paulo atoaje kielezi cha matokeo yenye maafa ya tamaa mbaya na kujitegemea? (b) Paulo arejezea mamlaka gani anaposhauri juu ya Chakula cha Jioni cha Bwana na vyakula vinavyofaa?
23 Barua hii ya mtume Paulo ni yenye mafaa sana katika kukuza kuelewa kwetu na Maandiko ya Kiebrania, ambamo yatoa mengi ya manukuu yayo. Katika sura ya kumi, Paulo ataja kwamba Waisraeli chini ya Musa walikunywa kutoka kwa tungamo-mwamba wa kiroho, uliomaanisha Kristo. (1 Kor. 10:4; Hes. 20:11) Kisha aendelea kurejezea kwenye matokeo yenye maafa ya kutamani vitu vyenye kudhuru, kama ilivyotolewa kielezi na Waisraeli chini ya Musa, na kuongeza hivi: “Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani.” Tusijitegemee kamwe, tukiwaza kwamba hatuwezi kuanguka! (1 Kor. 10:11, 12; Hes. 14:2; 21:5; 25:9) Kwa mara nyingine, yeye atoa kielezi kutoka kwa Sheria. Arejezea dhabihu za shirika katika Israeli ili kuonyesha jinsi washiriki wa Chakula cha Jioni cha Bwana wapaswa kushiriki inavyostahili meza ya Yehova. Kisha, ili kutegemeza hoja yake kwamba yafaa kula kila kitu kinachouzwa katika soko la nyama, yeye anukuu kutoka Zaburi 24:1, akisema, “Dunia ni mali ya Bwana [Yehova, NW] na vyote viijazavyo.”—1 Kor. 10:18, 21, 26; Kut. 32:6; Law. 7:11-15.
24. Ni marejezeo gani mengine anayofanya Paulo kwa Maandiko ya Kiebrania ili kuunga mkono hoja zake?
24 Katika kuonyesha ubora wa “mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao” na ubatili wa “mawazo ya wenye hekima” wa ulimwengu huu, Paulo anukuu tena Maandiko ya Kiebrania. (1 Kor. 2:9; 3:20; Isa. 64:4; Zab. 94:11) Yakiwa mamlaka ya maagizo yake katika sura ya 5 juu ya kutenga na ushirika mkosaji, yeye anukuu sheria ya Yehova juu ya ‘kuondoa uovu katikati yako.’ (Kum. 17:7) Katika kuzungumza juu ya haki yake ya kupata riziki kutokana na huduma yake, kwa mara nyingine Paulo arejezea Sheria ya Musa, ambayo ilisema kwamba wanyama wenye kufanya kazi hawapaswi kufumbwa kinywa ili kuwazuia wasile na kwamba Walawi katika utumishi wa hekalu walipaswa kupokea fungu lao kutoka kwa madhabahu.—1 Kor. 9:8-14; Kum. 25:4; 18:1.
25. Ni yapi baadhi ya mambo yenye kutokeza ya maagizo yenye mafaa yaliyomo katika Wakorintho wa Kwanza?
25 Jinsi tumepokea mafaa ya maagizo yaliyopuliziwa na Mungu kutokana na barua ya kwanza ya Paulo kwa Wakristo Wakorintho! Tafakari juu ya shauri lililotolewa juu ya migawanyiko na kufuata watu. (Sura 1-4) Kumbuka kisa cha ukosefu wa adili na jinsi Paulo alivyokazia uhitaji wa wema na usafi ndani ya kundi. (Sura 5, 6) Fikiria ushauri wake uliopuliziwa na Mungu kuhusu kutofunga ndoa, ndoa, na mtengano. (Sura 7) Fikiria mazungumzo ya mtume juu ya vyakula vilivyotolewa sadaka kwa sanamu na pia jinsi ambavyo lazima ya kujilinda na kukwaza wengine na kuangukia ibada ya sanamu ilivyotokezwa kwa mkazo. (Sura 8-10) Onyo la upole kuhusu ujitiisho unaofaa, ufikirio wa zawadi za kiroho, yale mazungumzo yenye kutumika kabisa juu ya ubora wa kuvumilia, sifa ya upendo isiyoshindwa—mambo hayo pia yamepitiwa. Na jinsi mtume alivyokazia vizuri uhitaji wa utaratibu katika mikutano ya Kikristo! (Sura 11-14) Jinsi alivyoandika chini ya upulizio wa Mungu akitetea ufufuo vizuri! (Sura 15) Yote hayo na zaidi yamepita mbele ya jicho la akili—na ni yenye thamani sana kwa Wakristo katika siku yetu!
26. (a) Ni kazi gani iliyotabiriwa zamani anayotimiza Kristo aliyefufuliwa atawalapo akiwa Mfalme? (b) Kwa msingi wa tumaini la ufufuo, ni kitia-moyo gani chenye nguvu anachotoa Paulo?
26 Barua hii yaongezea sana uelewevu wetu wa habari kuu tukufu ya Biblia ya Ufalme wa Mungu. Yatoa onyo kali kwamba watu wasio waadilifu hawataingia katika Ufalme, na yaorodhesha mengi ya maovu yanayoweza kumfanya mtu asistahili. (1 Kor. 6:9, 10) Lakini la maana zaidi, yaeleza uhusiano kati ya ufufuo na Ufalme wa Mungu. Yaonyesha kwamba Kristo, “malimbuko” ya ufufuo, “sharti amiliki yeye, hata [Mungu] awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake.” Kisha, akiisha kuweka chini maadui wote, kutia na kifo, ndipo “atakapompa Mungu Baba ufalme wake; . . . ili kwamba Mungu awe yote katika wote.” Hatimaye, kwa utimizo wa ahadi ya Ufalme iliyofanywa katika Edeni, kutiwa jeraha kamili kwa kichwa cha Nyoka kwatimizwa na Kristo, pamoja na ndugu Zake wa kiroho waliofufuliwa. Hakika, taraja la ufufuo ni tukufu kwa wale watakaoshiriki kutokuharibika pamoja na Kristo Yesu katika Ufalme wa kimbingu. Ni kwa msingi wa tumaini la ufufuo kwamba Paulo aonya hivi kwa upole: “Basi, ndugu zangu wapendwa, mwimarike, msitikisike mkazidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika Bwana.”—1 Kor. 15:20-28, 58; Mwa. 3:15; Rum. 16:20.
[Maelezo ya Chini]
a Halley’s Bible Handbook, 1988, H. H. Halley, ukurasa 593.
b Dictionary of the Bible ya Smith, 1863, Buku 1, ukurasa 353.
c The Interpreter’s Bible, Buku 10, 1953, ukurasa 13.
d The Interpreter’s Bible, Buku 9, 1954, ukurasa 356.