Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 12/15 kur. 563-568
  • Endelea Kumtumaini Yehova Uipate Thawabu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Endelea Kumtumaini Yehova Uipate Thawabu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTUMAINIKA NYAKATI ZOTE
  • KUMTUMAINI YEHOVA SIKU ZETU
  • Mtumaini Yehova kwa Moyo Wako Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Yehova Hutimiza Ahadi Zake kwa Waaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • “Mtegemee Yehova na Ufanye Mema”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Mtumaini Yehova Atimize Kusudi Lake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 12/15 kur. 563-568

Endelea Kumtumaini Yehova Uipate Thawabu

“Kila amwaminiye [Yehova] ana heri.”​—Mit. 16:20.

1, 2. Kwa sababu gani inatupasa tumtumaini Yehova atatue matatizo ya wanadamu?

MAELFU ya miaka iliyopita, imeonekana kwamba wanadamu hawawezi kujiondolea matatizo yao makubwa, hata wawe na makusudi mazuri na maendeleo mengi sana ya kisayansi. Muumba wa ulimwengu mzima, na uhai ulio juu ya dunia hii, ndiye peke yake anayeweza kutumainiwa afanye hivyo. Yeye peke yake ndiye mwenye hekima, uwezo na mapenzi yanayotakiwa. Mtunga zaburi alifahamu jambo hilo, akasema hivi: “Ndiwe taraja langu, Ee Bwana [Yehova], tumaini langu tokea ujana wangu.” (Zab. 71:5) Tumaini hilo linafaa, kwa maana Neno la Mungu linaahidi hivi: “Tumaini halitahayarishi.” (Rum. 5:5) Basi, Biblia inafanya vizuri kutushauri hivi: “Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe.”​—Mit. 3:5.

2 Sababu inayotulazimisha sana tumtumaini Yehova ni kwamba, yeye ndiye atakayeamua jinsi hali ya wanadamu itakavyokuwa wakati ujao, wala sio watakaojiamulia wenyewe. Wala hali yao’ haitaamuliwa na wazo la kihadithi kama lile la “mageuzi,” wala na yale yanayoitwa “maendeleo.” Hasa, Yehova amekwisha amua jinsi wakati ujao utakavyokuwa. Nasi tunaweza kumtumaini atimize mambo anayokusudia kufanya wakati ujao, kwa maana “Mungu hawezi kusema uongo.” (Ebr. 6:18) Tena, Yehova anatufariji kwa kutuambia hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isa. 55:11) Hakuna mwanadamu anayeweza kutumainika hivyo.

3. Yehova anafariji watumishi wake namna gani?

3 Tena, Yehova anaonyesha anapenda watumishi wake kwa kuwajulisha makusudi yake nyakati zote: “Hakika Bwana [Yehova] hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.” (Amosi 3:7) Yehova anasema: “Nayahubiri mambo mapya; kabla hayajatokea nawapasheni habari zake.” (Isa. 42:9) Mungu anafariji sana watumishi wake wanaomtumaini kwa kuwaeleza mapema mambo atakayofanya wakati ujao. Naye anapotimiza ahadi zake, wanazidi sana kumtumaini. Yesu alisema: “Sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini.”​—Yohana 14:29.

KUTUMAINIKA NYAKATI ZOTE

4, 5. (a) Maneno ambayo Yehova aliwaambia wazazi wetu wa kwanza yalitimiaje? (b) Viumbe vingine vya Mungu vimeumiaje duniani?

4 Tangu pale pale mwanzoni katika historia, Yehova ameonyesha kwamba ahadi zake zinatumainika na kwamba yapasa watu watii maonyo yake. Mfano wa kuonyesha hivyo ni yale yaliyowapata wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. Walitumia vibaya zawadi nzuri ya uhuru wa hiari ambao Mungu aliwapa. Hawa alidhani kwamba kuacha kutegemea utawala wa Mungu kungeleta hali bora, kumwezeshe ‘awe kama Mungu.’ (Mwa. 3:5) Je! ndivyo ilivyokuwa? Hapana, kwa maana Yehova alikuwa amekwisha waonya kwamba wangepatwa na msiba na kifo wakiuacha utawala wake. Yehova alijua kwamba wanadamu hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kufanikiwa bila ya kumtegemea Muumba wao.​—Mwa. 2:17; 3:17-19.

5 Hakika maneno ambayo Yehova aliwaambia wazazi wetu wa kwanza yalitimia. Walipojiondoa chini ya uongozi wa Mungu, walijiondoa pia katika Chanzo cha uzima. Baadaye, walizeeka wakafa, sawa-sawa na vile Mungu alivyokuwa amewaonya. Vilevile waliwapa wazao wao hali ya kutokamilika. Basi wanadamu wote wamepatwa na mabaya ya dhambi na kifo yaliyoletwa na wazazi wetu wa kwanza, walioutumaini utawala wa mwanadamu, badala ya utawala wa Mungu. (Rum. 5:12) Wanyama pia wamepatwa na mabaya. Mwanadamu hatawali wanyama kwa upendo kama hapo kwanza. (Mwa. 1:26) Mwanadamu ametumia wanyama vibaya ili kujifaidi, akafanya namna mbalimbali za wanyama zimalizike kabisa, hasa miaka ya majuzi. Vilevile mwanadamu ametumia dunia vibaya ili kujifaidi, akainyang’anya vitu na kuichafua hata ikawa shaghala baghala mahali pengi. “Viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa” kwa sababu mwanadamu hakumtumaini Yehova.​—Rum. 8:22.

6. Matokeo ya kumtumaini Yehova au kutomtumaini siku za Nuhu yalikuwa nini?

6 Siku za Nuhu wanadamu walikuwa wamepotoka sana na kuwa na jeuri nyingi, kame nyingi baada ya uasi wa Edeni. Mungu alimwambia Nuhu kwamba ulimwengu wa kale ungeharibiwa kwa gharika ambayo ingeenea duniani pote. Nuhu na jamaa yake walimtumaini Yehova, kwa hiyo wakaanza kujitayarisha: “Ndivyo alivyofanya Nuhu, sawasawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwa. 6:22) Lakini Nuhu alilazimika kuendelea kumtumaini Yehova miaka mingi, kwa maana alielezwa habari za gharika miaka mingi kabla haijatokea. Namna gani watu wale wengine katika ulimwengu huo wa kale? Yesu alisema, ‘Hawakutambua.’ Lakini, katika wakati ule ule uliowekwa “Gharika ikaja, ikawachukua wote.” (Mt. 24:39) Maneno ya Yehova yalikuwa yenye kutumainika kwa sababu sisi tupo leo. Tena kuwapo kwetu kunahakikisha kwamba njia inayowafaa sana wanadamu ni kuendelea kumtumaini Yehova. Kwa sababu gani? Kwa sababu sisi sote ni wazao wa Nuhu. Wale ambao hawakumtumaini Yehova siku za Nuhu hawakuzaa watoto wengine. Wote walizama katika gharika, ukoo wao ukaishia hapo.​—Mwa. 7:22, 23.

7. Ahadi ya Yehova ilitumainikaje wakati wa Ibrahimu?

7 Siku za Ibrahimu ilionekana tena kwamba Yehova anatumainika. Yehova alikuwa ameeleza Ibrahimu na Sara mkewe kwamba wangezaa mtoto. Lakini, Sara alikuwa ameupita sana ule umri wa kuweza kuzaa. Alipopata habari hizo, alicheka. Yehova alimwona akicheka, basi akamwambia Ibrahimu: “Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda [Yehova]? Kwa muhula wake nitakurudia, wakati uu huu mwakani, na Sara atapata mwana wa kiume.” Sara alipata mwanawe Isaka katika wakati ule ule uliowekwa na Yehova. Yehova alimrudishia Sara nguvu za uzazi kwa mwujiza ili kutimiza kusudi lake la kumtokeza Masihi kupitia ukoo wa Ibrahimu.​—Mwa. 18:9-14; 21:2.

8. Taifa zima lilitimiziwaje ahadi za Yehova?

8 Siku za Musa, watumishi wa Mungu walionewa sana na mamlaka katili ya ulimwengu wa wakati huo, yaani. Misri. Lakini Yehova alisema hivi: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri. niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema. kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali.” (Kut. 3:7, 8) Ahadi hizo zilitimizwa, kwa maana Mungu alikomboa watumishi wake Misri, kisha akawaondolea mataifa mengine hodari yenye uadui. Mwishowe mamilioni ya watumishi wake waliingia “nchi njema, kisha pana,” “ijaayo maziwa na asali.” Kwa hiyo ahadi ambazo Yehova alilipa taifa zima hilo zilikuwa zenye kutumainika, zikatimizwa kwa upana na urefu.​—Yos. 21:43-45.

9. Israeli na Yuda walipatwa na nini kwa sababu ya kutomtumaini Yehova?

9 Kama Waisraeli wa kale wangaliendelea kumtumaini Yehova, wangaliendelea kupata ufanisi katika nchi yao mpya. Lakini, walianza kuitumaini hekima yao wenyewe ya kibinadamu. Mwishowe walizoea kuasi imani na kupotoka wajapoonyeshwa fadhili wasizostahili na Yehova. Ahiya mnenaji wa Mungu alitabiri yafuatayo kuhusu ufalme wa kaskazini wa Israeli wenye makabila kumi: “[Yehova] atawapiga Israeli . . . naye atawang’oa Israeli katika nchi hii njema, aliyowapa baba zao.” (1 Fal. 14:15) Maneno ya Yehova yalitimia tena: “Mfalme wa Ashuru akautwaa Samaria, akawahamisha Israeli mpaka Ashuru.” “[Yehova] akawaondoa Waisraeli wasiwe mbele zake, kama vile alivyosema kwa kinywa cha watumishi wake wote, manabii. Basi Waisraeli walichukuliwa mateka kutoka nchi yao wenyewe, waende nchi ya Ashuru.” (2 Fal. 17:6, 23) Baadaye, maneno ya Yehova yalitimia tena, wakati ufalme wa kusini wa Yuda ulipochukuliwa mateka na Wababeli.​—2 Nya. 36:15-21.

KUMTUMAINI YEHOVA SIKU ZETU

10. Katika siku zetu, inapasa watumishi wa Yehova waonyeshe tumaini la namna gani?

10 Leo watumishi wa Mungu wamezungukwa na ulimwengu wenye upotovu na jeuri nyingi, kama ule wa siku za Nuhu. Tunahitaji sana kuendelea kumtumaini Yehova kabisa ili kuepuka kuingizwa katika uovu, kuvunjika moyo au kukosa imani. Inatupasa tuwe na nia kama ile ambayo Yoshua, mtumishi mwaminifu wa Yehova, alikuwa nayo. Alisema: “Mnajua mioyoni mwenu, na [nafsini] mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu, hapana neno lo lote mlilopungukiwa.” “Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo [Yehova] alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.”​—Yos. 23:14; 21:45.

11. Maneno ambayo Yehova alisema juu ya kizazi chetu yametimizwaje?

11 Lakini, si nyakati za kale tu ambapo watumishi wa Mungu wameona maneno na ahadi zake zikitimia. Mambo mengine kama hayo yametimia siku zetu. Mfano mmoja ni mambo yaliyoupata ulimwengu katika kizazi hiki. Ingawa viongozi wengi wa kibinadamu walitabiri kwamba karne hii ingetokeza kizazi kipya cha kisayansi chenye mambo matukufu, na kutatulia wanadamu matatizo yao, Neno la Mungu lilitabiri kwa usahihi likasema: “Ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.” Mambo yote yaliyotabiriwa kwamba yangetukia wakati wetu, kama pupa, chuki, kuasi sheria, vita vya ulimwengu, uasi wa watoto, kuvunjika kwa jamaa, unafiki wa dini na kutomwamini Mungu, yametimia. Yametokea katika wakati ule ule uliowekwa na Yehova, kuanzia mwaka 1914 ulioleta kipindi chenye mambo mapya.​—Mt. 24:3-14; 2 Tim. 3:1-5, 13.

12. Yehova amefanikisha watumishi wake leo kwa njia gani?

12 Lakini, katika kipindi kiki hiki chenye magumu, yaani, hizi “siku za mwisho” za taratibu iliyopo, Yehova amelinda watumishi wake wanaomtumaini, akawafanikisha sana. Ingawa waabudu hao wametendwa ukatili mwingi na watesi, wameongezeka wakazidi milioni. Ni kama vile Neno la Yehova lilivyotabiri: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, [Yehova], nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isa. 60:22) Tena, watumishi wake wanajifunza jinsi ya kuzaa matunda ya roho ya Mungu yenye kuwaongoza, kwa maana wanasitawisha “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Gal. 5:22, 23, tafsiri ya Kiingereza ya New World) Watumishi wa Mungu wanatimiziwa maneno ya Zaburi 29:11: “[Yehova] atawapa watu wake nguvu; [Yehova] atawabariki watu wake kwa amani.” Anafanya hivyo huku ulimwengu ukizidi kuzoea “uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo.”​—Gal. 5:19-21.

13, 14. Ingawa wakuu wa ulimwengu wanajua kwamba mwanadamu anapatwa na matatizo makubwa sana, wangali wakisema yataondolewaje?

13 Wakuu wa ulimwengu wanakubali kwamba hali za ulimwengu ni zenye hatari. Lakini hawamtegemei Yehova awaondolee hali hizo. Wangali wakitegemea hekima ya kibinadamu iwaonyeshe njia ya kuziepuka. Mfano mmoja unaonekana katika kitabu Environmental Ethics, kinachosema hivi: “Mwanadamu anapochunguzwa vizuri leo duniani, inaonekana kwamba anaelekea kwenye misiba mikubwa ya njaa, magonjwa ya kipuku, na vita.” Lakini kinapendekeza hali hizo ziondolewe na nini? Waandikaji wanasema:

“Lazima serikali ya namna fulani kama Umoja wa Mataifa ianzishwe katika ulimwengu mzima ili mwanadamu aweze kujichukua kuwa kiumbe cha namna yake na kujiongoza.

“Mpango wa elimu unahitajiwa kufanywa ulimwenguni pote ili kusadikisha walimwengu uhitaji mkubwa wa kupanga mipango ya kufanya hesabu ya watu ilingane na mali zinazopatikana katika mazingira yao, nalo jambo hilo linawezekana mataifa yote tu yakikubaliana. . . .

“Tunaweza kutumaini kwamba watu walio wakubwa zaidi katika ulimwengu, yaani, viongozi wa serikali, wa biashara, wa viwanda, na wa jeshi, watauona uhitaji wa kupanga ulimwengu ukubaliane kwa faida ya ukoo wa kibinadamu, halafu waanzishe serikali ya ulimwengu.”

Lakini, baada ya waandikaji hao kuonyesha kwamba kuna uhitaji wa serikali ya ulimwengu, walihofu “kwamba hatua hazitachukuliwa kutimiza uhitaji huo . . . mpaka njaa, magonjwa ya kipuku, na vita viue hesabu kubwa ya watu wa ulimwengu.”

14 Vivyo hivyo, katika kitabu kinachoitwa Ark II, wanasayansi D. Pirages na P. Ehrlich wanasema:

“Nuhu alipata onyo la kutosha kutoka kwa mkuu mheshimiwa ajenge Safina yake, naye alitumia wakati wake vizuri. Wenye mashaka walicheka, wakadhihaki, kisha wakafa maji​—lakini Nuhu . . . aliokoka.

“Sisi pia tumeonywa kwamba matatizo mengi sana yanaelekea kupata wafanya kazi, lakini safina ya sasa haiwezi kujengwa kwa mbao wala kwa vifaa vya kuzuia maji yasipenye.

“Lazima tuhakikishe kwamba tutaokoka kwa kutengeneza upya vyama vya kisiasa, vya uchumi na vya wafanya kazi. Safina ya vyama vipya isipoweza kufanywa kwa vifaa visivyopenywa na maji, wafanya kazi watakufa maji.”

15. (a) Kwa sababu gani haifai kutumaini wanadamu wajitatulie matatizo yao nyakati hizi za mwisho? (b) Ni nani peke yao wanaokubaliana na njia ya pekee ya kuondoa matatizo ya mwanadamu?

15 Je! mambo ambayo yamekwisha tukia katika historia ya kibinadamu yanatupa sababu nzuri ya kuamini kwamba taratibu hii potovu inaweza ‘kutengenezwa upya’? Je! kuna msingi wa kutumaini kwamba mataifa yatajikuta ghafula yakikubaliana ulimwenguni pote, bila uchoyo, katika kila upande wa mambo ya kibinadamu? Je! wanaendesha mpango wa elimu ulimwenguni pote ili kuunganisha wanadamu wote chini ya serikali moja, na kuongoza watu wote wajaribu kutimiza kusudi moja? Hawafanyi hata mojawapo mambo hayo. Katika mataifa yote watumishi wa Yehova peke yao ndio wanaoshirikiana kwa amani na umoja wafundishe watu habari za serikali moja inayokuja ambayo Yehova amekusudia itawale wanadamu wote, yaani, ufalme wake wa mbinguni unaosimamiwa na Kristo. Wao hawasaidii kutengeneza upya taratibu hii ya mambo isiyotengenezeka, kwa sababu Mungu hakusudii wafanye hivyo. Yeye hataitengeneza upya, bali ataibomoa. Tunaweza kuitumaini ahadi yake ya kufanya hivyo.​—Dan. 2:44; Mt. 6:9, 10.

16. Inatupasa tutumaini kabisa ahadi gani?

16 Haiwapasi watumishi wa Yehova wadanganywe na mipango yo yote ya kuendeleza milele taratibu hii potovu. Bali, imewapasa waendelee kumtumaini Yehova wakiwa na hakika kabisa kwamba atakomesha taratibu hii mbovu alete taratibu yake mpya yenye haki. (2 Pet. 3:10-13) Lazima tuwe na hakika kwamba Yehova peke yake ndiye atakayeweza kuondolea watumishi wake wanaomtumaini “kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufu. 21:4) Katika wakati ule ule alioweka, Yehova atatimiza ahadi hizo, kwa maana “maneno hayo ni amini na kweli.”​—Ufu. 21:5.

17. Ni jambo gani linalotutia moyo?

17 Tena, Yehova anatia watumishi wake moyo wa kuendelea kumtumaini kwa kuwaagiza wakaze macho yao juu ya thawabu atakazowapa. “Mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao” kwa bidii. (Ebr. 11:6) Tumaini la kuipata thawabu liliwachochea Wakristo wa karne ya kwanza. Mtume Paulo alisema: “Ndugu zangu wapendwa, mwimarike, msitikisike, mkazidi sana kutenda kazi ya Bwana siku-zote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika Bwana.” “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.”​—1 Kor. 15:58; Ebr. 6:10.

18. Je! inatupasa tuache kumtumaini Yehova tukilazimika kufa?

18 Haitupasi tuache kumtumaini Yehova hata tukilazimika kufa kabla taratibu mpya ya Mungu haijaingia. Tunaweza kuwa na tumaini lile lile ambalo Ibrahimu alikuwa nalo alipoagizwa amtoe Isaka kama dhabihu. ‘Alihesabu ya kuwa Mungu awe-za kumfufua hata kutoka kuzimu.’ Wakati Yehova alipomzuia Ibrahimu, Isaka alikuwa karibu sana kumalizwa, na hiyo ndiyo sababu Biblia inasema kwamba Ibrahimu ‘alimpata Isaka tena toka huko kuzimu, kwa mfano.’ (Ebr. 11:19) Je! mwanadamu ye yote anaweza kufufua wafu? Wapi. Yehova peke yake ndiye anayeweza kuwafufua kwa kutumia mipango yake.​—Matendo 24:15.

19. Ni baadhi ya thawabu gani ambazo watumishi wanaomtumaini Yehova watapokea katika Taratibu Mpya?

19 Katika taratibu mpya ya Mungu, watumishi wake wanaomtumaini watapokea thawabu kamili ya kuwa waaminifu kwake. Wataachishwa milele na taratibu potovu ya mambo inayowaonea sasa. Wataachishwa milele na laana za dhambi na kifo. Wakiwa chini ya uongozi wa ufalme wa Mungu, wataanza upesi kuifanya dunia iwe paradiso kwa kutumia mazoezi ambayo wanapokea sasa kuwafanya washirikiane katika kazi na kuishi pamoja kulingana na kanuni za Mungu. Weee! ni furaha gani watakayoona wale wote walioendelea kumtumaini Yehova! Lo! jinsi watakavyomshukuru Yehova waonapo baraka zikiwamiminikia chungu chungu! Hakika, “wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”​—Zab. 37:11.

20. Tunaweza kuwa na hakika kwamba mali za dunia zitatumiwa kwa njia gani chini ya ufalme wa Mungu?

20 Katika taratibu mpya ya Mungu, watu hawataona wasiwasi tena kwa sababu ya mabaya yanayotokana na uvumbuzi wa sayansi na mashine zake. Yehova, aliyeumba vitu vyote, pamoja na nguvu, anajua vifaa ambavyo inapasa watumishi wake watumie kuifanya dunia iwe paradiso. Watu hawataiharibu dunia wala hawataichafua kwa sababu ya kupata maarifa zaidi na kanuni bora za maisha. Muumba na Mwendeshaji wa mabilioni ya galaksi zilizo katika ulimwengu anajua kuongoza watu wake watumie daima na kwa manufaa vitu ambavyo amefanya ili kuwafurahisha. Basi, tunapotazama mambo ya zamani na ya sasa, inatupasa sana tuendelee kumtumaini Yehova, kama linavyoshauri Neno lake: “Umtumaini [Yehova] ukatende mema, ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu. Nawe utajifurahisha kwa [Yehova], naye atakupa haja za moyo wako. Umkabidhi [Yehova] njia yako, pia umtumaini, naye atafanya.”​—Zab. 37:3-5.

​—Kutoka The Watchtower, July 15, 1977.

[Picha katika ukurasa wa 566]

Watumishi wa Yehova peke yao ndio wameungana ulimwenguni pote kufundisha watu habari za serikali moja ambayo Mungu amekusudia kuletea wanadamu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki