‘Thabiti Mpaka Mwisho’
TUNASIKITIKA sana kutangaza kwamba mtumishi mwaminifu wa Yehova, Ndugu Nathan H. Knorr alikufa usiku wa Juni 8, 1977 baada ya kuwa mgonjwa sana miezi mingi. Aliweka mfano mwema wa ‘kutazama mbele sawasawa’ akiwa na juhudi na uthabiti muda wa miaka mingi. Njia zake zilikuwa ‘zimethibitika,’ naye ‘hakugeuka kwa kuume wala kwa kushoto.’ (Mit. 4:25-27) Sikuzote alikuwa akitia watu alioshirikiana nao moyo wa ‘kushikamana sana na ujasiri wetu na fahari ya taraja letu mpaka mwisho.’—Ebr. 3:6.
Ndugu Knorr alizaliwa Aprili 23, 1905. Alibatizwa Julai 4, 1923, akaingia utumishi wa Betheli mwaka uo huo. Kuanzia mwaka 1932 alikuwa na vyeo mbalimbali vya madaraka ya kuongoza utendaji wa Mashahidi wa Yehova, halafu mwaka 1942 akawa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Alimwoa Audrey Mock, Januari 31, 1953. Majaliwa yake ya kuweza kusimamia kazi na kuipanua yalitumiwa sana kuangalia matawi ya Sosaiti ulimwenguni pote, akawa akisafiri sana na kutoa hotuba. Elimu ya kazi yetu ya Kikristo iliongezeka sana miaka aliyotumikia kama msimamizi. Mwaka 1943 alitumiwa kuanza Watchtower School of Gilead ya kuzoezea wamisionari. Alipata pendeleo la kuona hesabu ya Mashahidi ikiongezeka kutoka 115,240 mwaka 1942 kufika 2,248,390 mwaka 1976.
Ingawa kifo kinaleta masikitiko, sisi tunamfurahia Ndugu Knorr, hasa kwa sababu alipenda watu na kazi ya Mungu muda mrefu, akaonyesha hivyo kwa kuwa na juhudi isiyotikisika na moyo wa kujitoa mpaka mwisho. Tunafurahi hata zaidi kwa sababu tunaishi siku ambazo wale wenye tumaini la kuishi mbinguni ‘wanabadilika dakika moja, kufumba na kufumbua,’ wanapomaliza mwendo wao duniani, halafu ‘wanafufuliwa, wasiwe na uharibifu.’ (1 Kor. 15:51, 52) Tumaini la kupata uzima wa milele katika ufalme wa Mungu na litufanye sisi pia ‘tushikamane na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho.’—Ebr. 3:14.