Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 8/15 uku. 3
  • Unachagua Kuishi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unachagua Kuishi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Habari Zinazolingana
  • Unaweza Kushindana na Matatizo ya Maisha
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Jinsi ya Kudhibiti Mfadhaiko
    Amkeni!—2010
  • Mkazo Mzuri, Mkazo Mbaya
    Amkeni!—1998
  • Jinsi Mfadhaiko Unavyotuathiri
    Amkeni!—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 8/15 uku. 3

Unachagua Kuishi

KWA sababu gani wewe unapumua sasa? Ni kwa sababu unachagua kuishi. Leo utakunywa maji, kwa sababu unachagua kuishi. Leo utakula, kwa sababu unachagua kuishi. Kwa sababu iyo hiyo utalala leo, urudiwe na nguvu mpya ili uweze kuishi kesho. Na ukiisha kuamka, utakwenda kazini, uipende usiipende kazi yako. Utakwenda ukajitafutie mahitaji ya maisha.

Walakini, yaangalie kidogo maisha haya ya sasa unayoyachagua. Iangalie kidogo migawanyiko ya kikabila inayofanya watu wengine wajione kuwa wakubwa kuliko wenzao na kuwaonea kwa kuwahesabu kuwa watu ovyo tu. Uangalie udhalimu na jeuri na hata vita vinavyotokea kwa sababu ngozi za watu zina rangi tofauti.

Uangalie utaifa unaogawanya makundi ya watu duniani, mapinduzi yanayofanya mataifa yagawanyikane na kufanya watu wengi wawe watoro, vyama vya kisiasa vinavyogombania mambo madogo na kupigana, ufisadi wa mambo ya fedha unaomalizia watu vitu wanavyohitaji na kuifanya mifuko ya wanasiasa iwe mizito kwa kujaa fedha.

Usisahau kwamba dini zinazojulikana zaidi zinahusika pia. Zinagawanya watu, zinajiingiza katika siasa, mara kwa mara zinachochea vita na mara nyingi zinawatesa waabudu wa kweli wa Yehova Mungu. Ndiyo, “Wakristo” wengi ati, lakini Ukristo mchache sana!

Usikomee hapo, bali yaangalie mambo makubwa ambayo yameshindikana katika ulimwengu. Ebu viangalie vitongoji vyenye makao machafu-machafu katika kila jiji kubwa, umaskini, uchafu mwingi lo, magonjwa ambayo ukiyatazama yanataka kukutapisha, wakaaji wasio na tumaini wanaofinyana-finyana katika vijumba vyenye giza-giza, majira ya baridi wakipatwa na baridi kali kweli kweli au kutoa jasho kama maji wakati wa kiangazi. Barabara zenye uhalifu mwingi, wilaya zenye umalaya mwingi lo, mazoea ya kuvuta bangi, makao ya kutunzia waliorukwa na akili yakiwa yamejaa pomoni kwa sababu watu wengi ni wagonjwa sana.

Ulimwenguni pote tabia za upotovu zimewakumba wanadamu kwa njia mbaya sana. Kila mahali uangaliapo unaweza kuona nyuso za mamilioni ya watu zikiwa zimekunjamana kwa sababu ya kufa moyo na kukata tumaini. Hayo yote yanatokeza jambo lenye kuonekana ulimwenguni pote liitwalo mikazo ya moyoni. Mikazo hiyo imeitwa yule Mwuaji wa Karne ya Ishirini. Jarida moja liitwalo Wall Street Journal lilitoa ripoti yenye kudai kwamba: “Mkazo wa moyoni ulio mkali au wa muda mrefu unaweza kulegeza mwili uwe mwepesi zaidi kupatwa na magonjwa, kuanzia vipele vya ngozi na mafua yale ya kawaida mpaka kuugua-ugua moyo kwa ghafula na kupatwa na kansa.” Ripoti moja iliyokuwa katika gazeti To the Point ilisema kwamba: “Magonjwa ya kimwili [ambayo mikazo ya moyoni] inatokeza yanafanya sasa watu wengi sana wapelekwe hospitalini na kuleta vifo vingi kila mwaka—visivyopungua makumi ya mamilioni.”

Ongezeko hili la sasa la mikazo linatimiza utabiri uliotolewa karne nyingi zilizopita. “Juu ya dunia,” Yesu alisema kutakuwa na “taabu nyingi ya moyoni ya mataifa, bila kuwa yanajua ile njia ya kutokea.” Ndipo alipoongeza kusema, “Wanadamu [watazimia] kwa sababu ya hofu na tazamio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.”​—Luka 21:25, 26, NW.

Kurasa mbili zinazofuata zinakaza fikira zako kwa urefu zaidi juu ya mambo ya waziwazi yanayopatikana katika maisha haya yenye mikazo ambayo watu wengi wanayachagua kwa kula, kulala na kufanya kazi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki