Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 8/1 kur. 23-24
  • Jinsi ya Kupainia—Mambo Yaliyoonwa Yenye Kufaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kupainia—Mambo Yaliyoonwa Yenye Kufaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUFANYA MAREKEBISHO KATIKA WAKATI NA FEDHA
  • USHIRIKIANO WA JAMAA
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Yehova Ategemeza Jeshi Lake la Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Utumishi wa Painia—Je, Wakufaa Wewe?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 8/1 kur. 23-24

Jinsi ya Kupainia—Mambo Yaliyoonwa Yenye Kufaa

“NI NINI kinachonizuia . . .” ilikuwa sehemu ya ulizo juu ya ubatizo ambalo Mwethiopia mmoja alimwuliza Filipo mweneza Injili.​— Matendo 8:36.

Lakini huenda tukauliza ulizo la maana kama hilo linalowahusu Wakristo wengi leo. Pengine tayari umekwisha kulifikiria ulizo hilo. Ulizo hilo ni: ‘Ni nini kinachonizuia’ nisipainie?

Kwa habari yako huenda mkazo wa ulizo hilo ukawa huu: ‘Ni nini kinachonizuia nisiingie katika utumishi wa painia?’ Au huenda ukahisi kwamba suala hasa ni: ‘Ningewezaje kuendelea nikiwa painia?’ Kuhusu maoni hayo yote mambo ya kweli yaliyoonwa maishani mwa Wakristo fulani yanaweza kutusaidia. Basi, na tusikilize wanavyosema mapainia wengine wenye kufanikiwa na wenye furaha.

KUFANYA MAREKEBISHO KATIKA WAKATI NA FEDHA

Ili kuwa painia na kuendelea kuwa mmoja lazima uwe na tamaa ya kupenda kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote, nafsi, akili na nguvu. (Mathayo 22:37-39, NW) Lazima uuone sana umaana wa kueneza ujumbe wa onyo la Mungu leo na kusaidia watu waingie kwenye barabara inayoongoza kwenye uzima maadamu kungali na wakati. Na kwa hakika unahitaji roho takatifu ya Mungu na baraka zake. Hata hivyo huenda mahangaiko fulani yakaja akilini mwako, kama jinsi ya kuwa na wakati na fedha za kutosha. Wengi wamelazimika kurekebisha maisha na orodha yao ili watafutie wakati upainia. Jambo linalohusiana na hilo ni kwamba huenda ukahitaji kurekebisha kazi yako ya kuajiriwa ili uweze kujiruzuku na wakati huo upainie. Je! hiyo inawezekana?

Wenzi fulani wa ndoa katika Pomona, California, walikabili ulizo hilo. Ndugu huyo anaeleza kwamba yeye hakuwa anachukua kweli kwa uzito na “alikuwa anajishughulisha na muziki wenye mdundo wa sauti kubwa na kunywa pombe sana.” Walakini hotuba fulani katika kusanyiko la mzunguko mwaka 1979 ilimfanya ajiulize hivi kwa uzito: ‘Je! maisha yangu yanaonyesha tamaa ya kweli ya kutaka taratibu ya mambo machafu iliyopo iondolewe na mahali pake pachukuliwe na nyingine?’ Baada ya yeye na mkewe kulizungumza jambo hilo, walitambua kwamba katika sehemu mbalimbali hawakuwa wanafuata mashauri ya kimungu, kwa hiyo wakaazimia kurekebisha namna yao ya kuishi na kujitahidi kufikia upainia. Yeye anaandika hivi: “Ni vigumu kuamini marekebisho yote tuliyolazimika kufanya. Tuliiuza nyumba yetu tukahamia kwenye nyumba inayokokotwa na motokaa. Tukaacha tafrija zetu za usiku zenye kutapanya fedha. Niliuza biashara yangu, iliyokuwa ikikusanya dola zaidi ya 2,000 kila mwezi, na nikatafuta kazi ya kuajiriwa ambayo ingeniruhusu nifanye kazi siku mbili tu kwa juma.” Sasa wakiwa wamekuwa wanapainia kwa karibu miaka miwili, yeye anasema hivi: “Ninahisi ni kama uzito mkubwa sana umeondolewa katika mabega yangu; ni kama tumetolewa katika mtego uliokuwa umetufyatukia.”

Ndugu mmoja kipofu katika Yucatan, Mexico, ni mwenye umri wa miaka 56 na ana mke na watoto wa kuruzuku. Yeye anafanya kazi gani? Eleuterio Pinto anaamka saa 11 asubuhi ili atengeneze nazi. Anaondoa ganda la nje kwa upanga na kwa kutumia msumari mkubwa anatoboa nazi ili wanunuzi waweze kunywa maziwa (maji ya dafu) yenye kuburudisha yaliyomo ndani. Ndugu Pinto anauza bidhaa zake tangu saa 2 asubuhi mpaka baada ya saa za chakula cha mchana halafu anashiriki katika huduma ya painia, ambayo amekuwa akiifurahia kwa miaka mitano.

Katika Afrika ya Kusini, V. Standley alikuwa amepanga kupata masomo ya chuo kikuu ya kufunza kazi ya ukulima. Walakini baada ya kuwa Shahidi alitumikia kwa miaka mingi kwenye kiwanda cha uchapaji cha Sosaiti na baadaye yeye na mkewe walikuwa mapainia wa pekee. Kisha mimba ikawataka wafanye marekebisho. Walipata nyumba isiyogharimu sana na Ndugu Standley akapata kazi ya kufanya muda-muda na kampuni ndogo yenye kusafisha afisi. Hivi karibuni walihamia kwenye eneo ambalo mapainia walihitajiwa zaidi, na aliweza kufungua tawi la kampuni ndogo hiyo hiyo, bado akiwa anafanya kazi ya muda-muda. Yeye anaripoti hivi: “Leo tuna makao yenye kupendeza sana, mahitaji yetu ya kimwili yanatoshelezwa vya kutosha na tungali na pendeleo la utumishi wa wakati wote. Nimethibitisha tena na tena kufaa kwa maneno ya Daudi juu ya kuwa kijana na kuwa mzee na kutokuona kamwe ‘mtu ye yote mwenye haki akiwa ameachwa kabisa.’”​—Zaburi 37:25.

Je! ukiisha kujiuzulu kazi, huo unaweza kuwa wakati mzuri kupainia? Kwa wengi imekuwa hivyo. Lakini hata hapa jitihada ya pekee na marekebisho huenda yakahitajiwa. Kwa mfano, Ndugu Balmaceda alijiuzulu kazi ya serikali katika Visiwa vya Filipino na akatazamia kupainia. Hata hivyo, angeweza kufanya nini ili kuangalia mahitaji yake ya kifedha? Aliona kwamba kufuga nguruwe kungemletea fedha na bado awe na orodha yenye kumpa wakati. Painia huyo mwenye umri wa miaka 70 anasema kwamba ‘anajiona kuwa karibu na Yehova kuliko hapo mbele,’ naye ameona roho yake ya upainia ikichochea watatu wa jamaa yake wauchukue utumishi huo ulio pendeleo.

Huenda ukahitajiwa kufanya marekebisho hata kama wewe ni ofisa wa kampuni mwenye ‘mshahara mnono.’ Hiyo ndiyo iliyokuwa hali ya Shozo Mima, msimamizi wa kampuni ya Kijapan yenye kufanikiwa ya kusafirisha bidhaa. Akiwa na roho ya painia, Ndugu Mima alianza kupainia alipokuwa angali msimamizi wa kampuni hiyo. Hata hivyo, akaanza “kuhisi kwamba akiwa katika cheo chake cha msimamizi wa kampuni na akiwa painia alikuwa akitumikia utajiri na Yehova.” (Mathayo 6:24) Kwa hiyo polepole aliwapa wengine kazi yake na akapata kazi ya kuajiriwa ambayo haikuhitaji wakati mwingi sana wala kukaziwa fikira. Kutokana na fedha alizolipwa na zile alizokuwa ameweka akiba aliweza kuitunza jamaa yake na kupainia. Ndiyo, alihisi kwamba alipaswa kujibidiisha katika kumtumikia Yehova kikamilifu zaidi wala si katika kufanya kampuni ifanikiwe.

USHIRIKIANO WA JAMAA

Huenda ukahisi kwamba kuwa painia au kuendelea kuwa painia ni kazi kubwa sana kwako ukiwa peke yako. Basi, huenda ukafaulu kwa ushirikiano wa jamaa yako, kutia na watoto wako. Mambo mengi yaliyoonwa yanaonyesha kwamba jitihada ya pamoja ya jamaa ya kumsaidia mmoja au zaidi wapainie inaleta mafanikio, na inatokeza pia jamaa zenye furaha ‘ sana.

Ndugu Kozo Sato katika Japan ana mke, na watoto wawili katika shule kuu. Yeye alizungumza pamoja nao juu ya tamaa yake nyingi ya kuweka mfano mwema akiwa mzee. Uamuzi ulikuwa nini? Yeye aliacha kazi ya kuajiriwa na kampuni moja iliyotaka kazi ya kufanywa kila siku kwa saa nane. Kisha akaanzisha biashara yake mwenyewe. Biashara ya kufanya nini? Siku nne katika juma kwa saa chache yeye anakusanya magazeti yaliyotumiwa na karatasi nyingine auze kwa wenye kuyatumia tena. Na kila asubuhi wote wanne katika jamaa hiyo wanatumia saa moja hivi wakipelekea watu magazeti. Kwa kufanya hivyo, pamoja na kupunguza gharama, Ndugu Sato anaweza kupainia kwa ukawaida, na watoto wake wawili pia wana mradi huo.

Katika nchi iyo hiyo Dada Toshiko Zenko hakuwa tena na mume lakini alipaswa kuruzuku watoto watatu wanaokua. Yeye alipokea fedha chache kutokana na kisehemu cha ardhi, na hizo zililipia kodi yake ya nyumba. Ili kulipia chakula na gharama nyingine, yeye anafanya kazi siku mbili katika juma na bado anaweza kupainia. ‘Ushirikiano wa jamaa unahusikaje hapo?’ huenda ukataka kujua. Yeye anaeleza kwamba wavulana wake wawili “wanashirikiana vizuri sana katika kununua vitu dukani kufanya kazi nyumbani na hata wanaweza kubadili utambi katika stovu ya mafuta ya taa na mipira katika mifereji ya maji.” Vilevile binti yake anasaidia kupika na kusafisha. Msichana huyo alifanya kazi za muda-muda baada ya saa za shule, lakini kwa kuwa sasa amekwisha kufuzu (kumaliza shule), yeye ameanza kupainia, akiwa anabadilishana siku za kufanya kazi pamoja na mamaye. Kwa kweli, wote wanne katika jamaa hiyo wanapanga kupainia pamoja hivi karibuni.

Ndiyo, ukiwa na jamaa, kupainia kutataka ushirikiano na utegemezo wa wote. Lakini kunaweza kuleta furaha na uradhi kama nini! Na kunaweza kutokeza wahudumu mapainia wengine.

Kama ilivyo, hali zako zinatofautiana na za mtu yule mwingine. Hata hivyo ukichochewa na upendo na kujitoa kutaka kupainia, huenda mradi huo ukawezekana hata kukiwa na vizuizi vya kushinda. Zungumza na Wakristo wengine juu ya jambo hilo, sana-sana na wale ambao ni mapainia wenye kufanikiwa, au ambao wamepata kuwa mapainia wenye kufanikiwa. Huenda wakawa na mapendekezo ya ziada yanayofaa juu ya namna ya kuwa painia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki