Mwana wa Miaka Tisa Azuia Ndoa Isivunjike
JE! KITENDO kimoja cha mume cha uzinzi kinataka kabisa mke amtaliki, hata anapotubu kikweli? Mke mmoja alifikiri hivyo, walakini mwana wake wa miaka tisa hakufikiri hivyo.
Mwanamume mmoja aliyebatizwa mwenye mke aliyejiweka wakf na watoto watatu wachanga alifanya uzinzi hivi karibuni. Lilikuwa kosa moja na mara moja aliwaarifu wazee wa kundi waliowekwa. Yeye alisihiwa na wazee hao amwombe mkewe msamaha kwa kukiri kosa hilo kwake pia. Mke huyo alikasirika sana na akaazimia kukomesha ndoa yao. Yeye aliwaambia wazee waliokuwa wakishughulikia kesi hiyo kwamba alikuwa ameamua kabisa na kwamba tayari alikuwa amemfikia mwanasheria. Wazee hao walizungumza naye, wakataja kwamba watoto hao watatu walikuwa wachanga mno, yule mkubwa zaidi akiwa mwenye umri wa miaka tisa. Lakini yajapokuwa hayo yote, yeye alikuwa ameamua kabisa. Kwa hiyo, mume huyo alihuzunika sana asiweze hata kula. Wakati mwingi alikuwa akilia.
Ndipo watoto wao walipojua yaliyokuwa yakitokea, na yule mvulana mkubwa zaidi akaamua kufanya jambo fulani. Yeye aliketi atayarishe hotuba au mambo ambayo angemwambia mamaye. Kwa sababu ya kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, yeye alikumbuka maandiko fulani na vilevile habari katika kitabu “Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha.’’ Sasa akawa tayari kushughulika na mamaye. Akamwita kwenye chumba cha kulala na akaketi chini naye. Maelezo yake ya kwanza yalikuwa kwamba yeye alikuwa amehuzunika sana na hakutaka jamaa yao ivunjike. Kisha akasema: “Mama, angalia, yale ambayo Biblia inasema katika Nehemia 9:17.” Mama yake alipokwisha kulisoma andiko hilo, yeye (mwanawe) alisema: “Je! unaona namna Yehova alivyo Mungu anayetenda kwa njia ya kusamehe. Mama, je! hufikiri kwamba wewe pia unapaswa kumsamehe Baba?” Mama yake akajibu “pengine.” Yeye alikuwa amekaza fikira sana amsaidie mamaye aone umaana wa kuwa mwenye kusamehe.
Vilevile mvulana huyo alitaja Waefeso 5:22, 33 akatoa hoja ya kwamba kwa kuwa babaye ndiye kichwa cha nyumba, mamaye (mvulana) alipaswa kumsikiliza. Halafu, mvulana huyo akataja Mathayo 6:11, 12. Baada ya kusoma mistari hiyo miwili, yeye alimwuliza mamaye maana ya “deni” ni nini. Mamaye alimpa jibu na mvulana huyo akamsihi amsamehe “Baba deni zake.” Alitumia maandiko mengi zaidi na katika kumalizia akamwuliza mamaye hivi: “Je! hufikiri kwamba unapaswa kumsamehe Baba?” Kwa furaha, jibu lilikuwa, “Ndiyo, nitamsamehe.”
Sasa jamaa hiyo imeungana kwa furaha tena. Baadaye mwanamke huyo alisema kwamba yeye alifurahia jinsi mambo yalivyokuwa na akasema kwamba yeye aliona kwamba mumewe alitubu kikweli na alikuwa akijaribu sana kufanya marekebisho katika uhusiano wa jamaa. Kwa hiyo, yale ambayo maelezo ya wengine yalishindwa kufanya, maelezo ya mvulana wa miaka tisa yalifaulu, kwa kutumia Neno la Mungu. Kweli kweli, “vinywani mwa watoto wachanga . . . [wewe Yehova] umeiweka misingi ya nguvu.”—Zaburi 8:2.