Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 5/15 kur. 22-24
  • Jilishe kwa Ukawaida Kweli za Biblia!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jilishe kwa Ukawaida Kweli za Biblia!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUIFAHAMU DHAMIRI VIZURI ZAIDI
  • KUENDELEA KUWA KATIKA HALI YA KUWEZA KUPIGANA
  • NAMNA GANI WAKATI WA KUFANYA HIVYO?
  • Sauti ya Dhamiri Iliyomo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Je! Wewe Unaongozwa na Dhamiri Nyepesi ya Kikristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Kuendelea Kuwa na Dhamiri Njema
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Dhamiri Njema Mbele za Mungu
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 5/15 kur. 22-24

Jilishe kwa Ukawaida Kweli za Biblia!

MWALIMU mkuu aliyepata kuishi wakati mmoja alisema kwamba mtu haishi kwa mkate tu, bali pia anahitaji chakula cha kiroho, Neno la Mungu. Kutokana na hayo, kwa kufaa tunaweza kukata maneno kwamba Wakristo wanapaswa kujilisha kwa ukawaida chakula cha kiroho, kama wanavyojilisha kwa ukawaida mkate wa halisi. (Mathayo 4:4) Chakula hicho cha kiroho ni kutia Biblia na pia vitabu vinavyotusaidia kuifahamu Biblia. Ndiyo sababu shirika lenye kuchapisha na kusimamia la Mashahidi wa Yehova, Watch Tower Society, haliridhiki na kuchapa Biblia peke yake. Vilevile linachapisha vifaa vya Biblia kwa ukawaida ili kuwasaidia wasomaji wapate ufahamu kamili zaidi wa Biblia.

Suala la thamani ya kujifunza kwa ukawaida vichapo hivyo limetokezwa, kwa kuwa nyakati nyingine habari ile ile huenda ikatokea tena ili irudiwe kuzungumzwa. Walakini je! hatuli mkate, viazi au mchele kwa ukawaida? Vilevile, mtume Petro aliandika hivi: “Kwa sababu hiyo sikuzote nitakuwa na maelekeo ya kuwakumbusha mambo hayo, ingawa mnayajua na mmeimarishwa katika kweli iliyomo ndani yenu.” (2 Petro 1:12, NW) Vilevile na iangaliwe kwamba wakati habari fulani inazungumzwa zaidi ya mara moja, mara nyingi kuna njia tofauti ya kuliangalia jambo hilo, mambo makuu mapya ya maoni, ufahamu zaidi, habari zaidi na yenye kutokeza zaidi. Ni kama Mithali 4:18 inavyosema: “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.”

KUIFAHAMU DHAMIRI VIZURI ZAIDI

Kwa kutaja mfano mmoja, ebu lifikirie jambo la dhamiri. Katika Machi 1973, Mnara wa Mlinzi ulichapisha makala kadha juu ya dhamiri ya kibinadamu kama “mshuhudiaji.” Zilionyesha kwamba dhamiri yetu ni shahidi tunayezaliwa naye, ikitutetea au ikitushtaki, na kwamba ilifanya kazi hata kabla Yehova Mungu hajawapa wanadamu orodha za sheria iliyoandikwa. Makala hizo pia zilionyesha uhitaji wa kuheshimu dhamiri za wengine na sehemu ambayo dhamiri inatimiza katika mambo yanayohusu kazi ya kuajiriwa. Kabla ya hapo mambo hayo hayakuwa yamepata kufafanuliwa wazi sana hivyo.

Kisha katika Oktoba 1975, makala mbili zaidi zilitokea juu ya dhamiri. Kati ya mambo makuu kadha wa kadha yaliyotolewa katika makala hizo, lilikuwa jambo la kwamba kuna sehemu mbili za msingi zinazofanywa na dhamiri. Moja ni ile inayoweza kuonwa kuwa ya kuhukumu. Hiyo ni sehemu inayofanywa na dhamiri “baada ya uhakika kutolewa,” inapotuhukumu kuwa wenye hatia kwa sababu tumekosa katika njia fulani. (2 Samweli 24:10) Hata hivyo, kwa Wakristo, dhamiri inapasa kufanya mara nyingi zaidi ile inayoweza kuitwa kutunga sheria. Bila shaka hiyo haimaanishi kwamba kwa hakika inatungia Mkristo sheria mpya. Walakini, kwa kutegemea sheria na kanuni za Biblia dhamiri yenye nguvu ya Mkristo itamwongoza. Ni kama kwamba inatangulia kumtungia sheria kwamba mwendo fulani ni kosa. Mfano wa Kimaandiko unaojulikana vizuri ni ule wa mwana wa Yakobo, Yusufu, alipokataa vishawishi vya mke wa Potifa.​—Mwanzo 39:9.

Halafu karibuni zaidi, Mnara wa Mlinzi (wa Januari 15, 1977) ulikuwa na makala zaidi juu ya dhamiri iliyokuwa na kichwa “Kuzoeza Dhamiri Zetu Zitusaidie Zaidi.” Kwa ujumla, wakati wa kuchunguza mambo yanayohusu dhamiri ulizo ni kama jambo fulani ni zuri au baya, linafaa au halifai. Walakini katika makala hiyo mkazo uliwekwa juu ya namna Biblia inavyoshirikisha dhamiri nzuri na imani na upendo (1 Timotheo 1:5) Ndiyo, dhamiri zetu zinapsa kutuepusha tusivunje sheria za Yehova Mungu na pia zinapasa kuhusika inapokuwa ni kutumia vizuri nafasi za kufanya mambo yasiyo ya kichoyo, yaliyo mazuri, ya fadhili, ya upendo.​—Linganisha Luka 10:29-37.

Kwa hiyo, wakati wo wote usione kamwe kwamba ati kwa sababu makala fulani iliyomo ndani ya Mnara wa Mlinzi inazungumza juu ya habari fulani iliyotangulia kuzungumzwa ni kurudia-rudia tu. Ni kweli kwamba nyakati nyingine marekebisho yanayofanywa si makubwa mno, walakini yote yanaongeza jambo fulani kufunua wazi kweli ya Biblia kuwa yenye kupendeza zaidi, yenye maana zaidi, ndiyo, yenye kutusaidia zaidi.

Hayo yote yanakumbusha juu ya kisa kimoja kinachosimuliwa juu ya Michelangelo. Rafiki mmoja alikuwa amevutiwa na sanamu nzuri sana ambayo Michelangelo alikuwa amechonga. Alipomjia tena wakati fulani baadaye, rafiki huyo alishangaa kumwona akiwa bado anatengeneza sanamu iyo hiyo. Michelangelo alimwonyesha marekebisho aliyokuwa ameyafanya katika wakati huo, na rafiki huyo wake akajibu hivi, ‘Lakini hayo ni mambo madogo-madogo tu.’ Katika kumjibu, Michelangelo alisema: ‘Ndiyo, hiyo ni kweli. Walakini mambo madogo-madogo ndiyo yanayoleta ukamilisho na ukamilisho si jambo dogo!’ Kwa hiyo ingawa nyakati nyingine marekebisho yanayofanywa huenda yasionekane kuwa ya umaana mwingi, yanasaidia kufanya ufahamu wetu wa habari fulani ukaribie zaidi kukamilika.

KUENDELEA KUWA KATIKA HALI YA KUWEZA KUPIGANA

Wala si hayo tu. Biblia na vichapo vinavyotusaidia tuifahamu Biblia vizuri zaidi havishughuliki na maarifa ya akili peke yake. Neno la Mungu ni ‘taa ya miguu yetu, na mwanga wa njia yetu.’ (Zaburi 119:105) Vilevile, tunaambiwa kwamba Neno la Mungu “lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Lakini linaweza kutimiza makusudi hayo kwa kadiri ile tu ambayo tunaitumia maishani mwetu. Na tunawezaje kuitumia ikiwa tumesahau yale ambayo tumesoma?

Ni jambo la maana sana kwamba tuendelee kukumbushwa juu ya mashauri yaliyomo ndani ya Neno la Mungu kwa sababu ya maadui watatu ambao lazima tushindane nao. Kuna ulimwengu; urafiki nao unamaanisha uadui na Yehova Mungu. (Yakobo 4:4) Kuhusu pambano letu na ulimwengu, mtume Yohana aliandika hivi: “Huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu.” (1 Yohana 5:4) Imani inategemea maarifa​—maarifa ambayo yanakumbukwa kwa urahisi na akili, si habari ambayo imesahauliwa kwa muda mrefu. Kwa sababu ulimwengu unatusonga kwa nguvu sana siku baada ya siku, tunapaswa kukumbushwa wakati wote tusiwe tukiupenda ulimwengu wala vitu vilivyomo ndani yake; kwa maana ulimwengu na vyote vilivyomo ndani yake utapita, bali yeye anayefanya mapenzi ya Mungu atabaki milele.​—1 Yohana 2:15-17, NW.

Vilevile Ibilisi na mashetani wake ni maadui wetu. “Adui yenu, Ibilisi, anatembea-tembea uku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8, NW) Yeye pamoja na mashetani wake wanafanya vita juu yetu na kwa hiyo tunahitaji kuvaa silaha zote za kiroho za Mungu, ambazo mtume Paulo anasimulia katika Waefeso 6:11-17. Kwa mara nyingine kuvaa kwetu silaha hizo na kuzitumia kunategemea kwetu kujilisha Neno la Mungu. Bila shaka, ili kuweza kupunga ‘upanga wa roho, neno la Mungu,’ kwa njia inayofaa, tunahitaji kulikumbuka neno hilo akilini na mioyoni mwetu.

Adui wetu wa tatu ni maelekeo yetu wenyewe yenye dhambi tuliyorithi ambayo ni lazima tung’ang’ane nayo kwa bidii na kwa kuendelea. Kwa kuwa mama zetu ‘walituchukua mimba katika dhambi na wakatuzaa katika kosa,’ tangu ujana kuendelea maelekeo yetu ni mabaya. (Mwanzo 8:21; Zaburi 51:5, NW) Kwa sababu hivyo ndivyo ilivyo, sote tunaweza kuomboleza, kama mtume Paulo: “Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.” (Warumi 7:19) Kwa sababu ya urithi huo, tunaona kwamba moyo wa kibinadamu ni mpotovu, wenye hila, mdanganyifu. Walakini kwa msaada wa Neno la Mungu na wa vifaa vya Biblia vinavyotusaidia tufahamu na kutumia kanuni za Biblia, tunaweza kukabili adui huyo aliye ndani yetu. Hata hivyo, kama mtume Paulo, ni lazima tuipige-pige miili yetu na kuiongoza kama watumwa.​—Mithali 3:32; Yeremia 17:9; 1 Wakorintho 9:27.

NAMNA GANI WAKATI WA KUFANYA HIVYO?

Maisha ya Mkristo yamejawa na mambo ya kufanya. Kuna Biblia ya kusoma, pamoja na gazeti jipya kila juma, matayarisho ya kufanywa kwa ajili ya mikutano na kuihudhuria, na kushiriki katika kazi kuu ya kufanya wanafunzi wale wanaosikiliza kwa furaha. Vilevile, kuna madaraka ya kila siku ya kilimwengu ya kujitunza wenyewe na jamaa zetu. Kila mmoja anaweza kujiuliza hivi: Ninatumia wakati mwingi kadiri gani nikisoma vitabu, magazeti na jarida za kilimwengu?Ninatumia wakati mwingi kadiri gani nikitazama au kusikiliza muziki unaopendwa na watu wengi? Ni kweli kwamba hizo ni namna za kujitumbuiza na ni tafrija, ambapo wengi huenda wakaona kufanya matayarisho ya mikutano ya Kikristo na kusoma vitabu vya Kikristo kuwa ‘kazi nyingi mno.’ Lakini je! matayarisho na usomaji huo unapasa kuonwa kwa njia hiyo? Mtunga zaburi alisema: “Ninashangilia usemi wako kama anavyofanya mtu anapopata nyara nyingi.” (Zaburi 119:162, NW) Kwa hiyo tunahitaji kuchunguza kwa uangalifu kama mwendo wetu wa maisha unatutambulisha kuwa watu wa kiroho bali si watu wa kimwili.​—1 Wakorintho 2:14-16.

Hayo yote yanakumbusha maneno ya Yesu juu ya furaha ya wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho. (Mathayo 5:3) Viumbe wa hali ya chini​—ndege, wadudu wanyama, samaki, na kadhalika​—hawana mahitaji ya kiroho. Walakini wanadamu wanayo. Kwa sababu ameyapuza ametokeza mvurugo wenye kusikitisha katika ulimwengu leo. Falsafa (filosofia) na maongozi ya kisiasa ya kutafuta mali yanawasukuma wanadamu mbali zaidi na Mungu. Mahitaji yao ya kimwili​—chakula, mavazi na nyumba​—na ngono, pamoja na anasa, au tamaa nyingi ya mamlaka, yanakuwa mambo makuu zaidi maishani mwao. Walakini ikiwa kweli kweli tunatambua mahitaji yetu ya kiroho, kwa ukawaida tutajilisha kweli za Biblia, na kutafuta wakati wa kufanya hivyo na kuzithamini kikamilifu. Thawabu itakuwa nini? Tutasaidiwa tufuatie mwendo wa utawa, ambao “hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.”​—1 Timotheo 4:8.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki