Je! Wakati Ujao ni Wenye Kuhuzunisha kwa Watu Wazee-Wazee?
“NALIKUWA kijana,” akasema Mfalme Daudi. “Nami sasa ni mzee.” (Zaburi 37:25) Katika nyakati za Biblia watu wazee walikuwa wachache lakini waliheshimiwa. Hata hivyo, mielekeo ya kisasa ikiendelea, huenda watu wazee wakawa si wachache wala wenye kuheshimiwa.
Katika United States peke yake, inakadiriwa kwamba kuna watu milioni 26 walio na umri wa miaka zaidi ya 65. Kufikia mwaka 2040 hesabu hii ingeweza kuongezeka karibu mara tatu! Kulingana na gazeti Asiaweek, mataifa fulani ya Kiesia ‘yanatazamia hesabu za watu wao wazee-wazee ziwe maradufu katika mwongo unaokuja.’ Hata hivyo, tazamio la wazee wenye umri kuwapita vijana katika hesabu halionyeshi mambo mazuri yajayo kwa watu wazee-wazee. Tayari hesabu yenye kutisha wanajikuta wakiwa maskini na bila makao. Wengine wanaachwa wadhoofike katika mahospitali na makao ya kuwatunza wazee—wakiwa pekee yao, bila kutembelewa, na bila kutunzwa. Visa vyenye kushtusha vya kutotunzwa na kutendwa vibaya vinaripotiwa hata katika nchi ambako kumekuwa na desturi ya kuheshimu wazazi.
Aliandika hivi G. M. Ssenkoloto kwa ajili ya gazeti World Health: “Katika nyingi za nchi za Kiafrika na kwa kweli katika nyingi za nchi zinazositawi, kulingana na mapokeo kila jamaa iliwatunza wanawake wao wazee. Mwanamke ambaye hakuwa na watoto wa kumtunza alitunzwa na majirani au na kijiji kwa ujumla.” Hata hivyo, yeye anaripoti hivi: “Kanuni ambazo zimekuwapo kwa muda mrefu zinabadilika. Nguvu zenye kuharibu uchumi, ugawaji mbaya wa mali, tamaa nyingi ya vitu vya kimwili, watu kujikaza sana ili wajipatie umashuhuri na cheo—mambo yote hayo yanatangulizwa mbele ya kanuni njema za mapokeo ya kuwategemeza watu wazee-wazee.”
Maneno ya mwandikaji wa Biblia Aguri yanathibitika kuwa kweli kwa sehemu kubwa: “Kuna kizazi cha watu wamlaanio baba yao; wala hawambariki mama yao.” (Mithali 30:11) Ndiyo, watu wazee-wazee wanapinduliwa kutoka kwenye cheo cha heshima walichofurahia nyakati zilizopita. Wengi wanawaona kama mzigo katika jamii badala ya kuwaona kama mali yenye thamani. Kwa sehemu kubwa, matarajio yao ya wakati ujao yanaonekana kuwa yenye kuhuzunisha.
Ingawa hivyo, Wakristo wa kweli wanawaonaje watu wazee? Je! wao wangali wanazifuata “kanuni njema za mapokeo” kuhusiana na wazee hao?