Zawadi ya Pekee Sana ya Watoto
SEMI za unyofu za watoto mara nyingi hufanya watu wazima kutua na kufikiri. Katika pindi moja, baada ya kuona Yesu akifanya baadhi ya miujiza yake, wavulana walianza kupaaza sauti hivi: “Hosana, Mwana wa Daudi!” Viongozi wa kidini walipinga hilo. Kwa kupofushwa na wivu, hawangeweza kutambua kwamba Yesu alikuwa yule mzao wa Kimasihi wa Mfalme Daudi. Lakini Yesu aliwajibu akasema: “Hamkupata kusoma, Kwa vinywa vya watoto wachanga na wanyonyao [Mungu] umekamilisha sifa?” (Mathayo 21:15, 16) Leo, Mungu angali anatumia “vinywa vya watoto wachanga” kusaidia wale ambao akili zao zimepofushwa na fundisho la uwongo.—2 Wakorintho 4:4.
◻ Daleen, mwenye umri wa miaka 12, alijithibitisha mwenyewe kuwa msichana mwenye kukubali daraka shuleni. Siku moja alipewa mgawo wa kulipa darasa kazi ya kufanya wakati mwalimu wake alipokuwa akifanya kazi nyingine. Angefanya nini? “Niliamua kuwaeleza wanadarasa wenzangu kwamba wenye uadilifu wataishi milele juu ya dunia na kwamba si watu wote wataenda mbinguni,” akasema Daleen. Kwa ruhusa ya mwalimu, Daleen alitoa habari yake kwa darasa kwa namna ya mazungumzo pamoja na mwanadarasa mwenye nia ya kushiriki katika mazungumzo. Yeye alisoma maandiko kadha, kutia na Zaburi 37:29, NW; “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yayo.” Itikio lilikuwaje? “Mwalimu aliacha kazi yake na kusikiliza kwa makini kama walivyofanya watoto,” asema Daleen. “Baadaye yeye alishukuru mimi, na wachache wa watoto hao wakauliza maswali.”
◻ Lillian, wa umri wa miaka 5, na wazazi wake waliishi kilometa 19 kutoka mji mdogo wa Afrika Kusini ambako mara nyingi walihudhuria mikutano na kushiriki katika kuhubiri nyumba kwa nyumba. Jumapili moja, kwa sababu ya gari lao kuwa na tatizo fulani, wazazi wake waliamua kukaa nyumbani. “Ni kwa sababu hatuendi nje kuhubiri?” akauliza Lillian. Kwa kukosa kuridhishwa na sababu, yeye alisema: “Mimi sitaruhusu hilo linizuie.” Baadaye mama akagundua kwamba Lillian hakuwapo na mkoba wake wa kutolea ushuhuda pia. Kile kisichana kilikuwa kikishughulika na kutembelea nyumba zilizokuwa karibu, kikigawa kwa ukarimu vitabu vya Biblia—kutia na Biblia ya kibinafsi ya mama yake! Bibi mmoja mzee-mzee alivutiwa sana na elezo la Lillian la Paradiso inayokuja hivi kwamba baadaye alikubali toleo la funzo la Biblia kutoka kwa mama wa Lillian. Baada ya muda mwanamke huyo akawa mwabudu wa Yehova aliye wakfu.
Ndiyo, Mungu angali anatumia “vinywa vya watoto wachanga” kutoa sifa. Unyofu wao unaweza kugusa sana mioyo ya watu wazima. Kwa kufaa, basi, watoto pamoja na watu wazima wanatiwa ndani katika mwaliko huu mzuri sana: “Msifuni [Yehova, NW] kutoka nchi, . . . vijana waume, na wanawali, wazee, na watoto; na walisifu jina la [Yehova, NW], maana jina lake peke yake limetukuka.”—Zaburi 148:7, 12, 13.