Sura ya 26
Watoto Wamsifuo Mungu
IMEPATA kusimama kidogo kufikiri ni kwa sababu gani unacho kinywa? Unakitumiaje?—
Kwa hakika ni kweli kwamba tunataka kinywa kwa kula. Lakini kinywa kazi yake si kula tu. Karibu wote wa sisi tunakula mara chache tu kila siku. Lakini je! si kweli kwamba unakitumia kinywa chako zaidi sana kwa kusema? Midomo yako, ulimi wako, meno, ndani ya kinywa chako, na zaidi sana, vyote vinafanya kazi kila wakati unaposema.
Ebu fikiri ingekuwaje ikiwa usingeweza kuse-ma. Ingekuwa huzuni kama nini ikiwa usingeweza kumsimulia mwingine uliyokuwa ukifikiria! Hufurahi kwa vile Yehova alitupa kinywa?— Na kwa kuwa alitupa kinywa chetu, hukubali kinapaswa kitumiwe katika njia itakayomheshimu yeye?—
Ndivyo Mfalme Daudi alivyoona. Yeye alikuwa mtumishi wa Mungu. Na, akasema: “Kinywa changu kitazinena sifa za [Yehova].” Unakubali kwamba hili ni jambo zuri kufanya kwa vinywa vyetu? Basi, na turudie kusema pamoja aliyosema: “Kinywa changu kitazinena sifa za [Yehova].”—Zaburi 145:21.
Palikuwa na mwanamke mdogo Mwisraeli aliyetumia kinywa chake katika njia hiyo. Alipokuwa hai, taifa la Shamu na taifa Ia Israeli wali-kuwa adui. Siku moja Washami wakapigana na Israeli na kumchukua mwanamke mdogo huyo kama mtumwa. Alipelekwa nyumbani kwa mkuu wa jeshi, aliyeitwa Naamani. Ndiko akawa mtumishi wa mke wa Naamani.
Sasa, Naamani akapata ugonjwa unaoitwa ukoma. Hakuna mmoja wa madaktari aliyeweza kumsaidia. Lakini mwanamke mdogo kutoka Israeli alikuwa na imani kuu katika Yehova. Alijua kwamba yeye angeweza kufanya maajabu. Naye aliamini mmoja wa watumishi wa pekee wa Mungu, nabii, angeweza kumsaidia Naamani. Bila shaka, Naamani na mke wake hawakumwamini Yehova. Walikuwa na dini nyingine. Je! mwanamke mdogo awaambie alichojua? Pengine hata wasingetaka kusikia. Wewe ungalifanyaje?—
Akajua imempasa aseme. Ingekuwa wema kufanya hivyo. Na ingeonyesha upendo wake kwa Mungu. Basi akasema: ‘Kama Naamani angeweza kumwendea nabii wa Yehova katika Israeli. Maana angeweza kumponya ukoma wake.’
Naamani alitaka sana sana aponywe. Basi akamsikiliza mwanamke mdogo. Alimwendea nabii wa Yehova. Alipofanya alivyoambiwa na nabii kufanya, aliponywa. Jambo hili lilimfanya Naamani awe mwabudu wa Mungu wa kweli. Lo! namna alivyofurahi kwa vile mwanamke mdogo kutoka Israeli hakuogopa kumsifu Yehova!— 2 Wafalme 5:1-15.
Ungependa umsaidie mtu fulani ajifunze juu ya Yehova kama alivyofanya mwanamke yule mdogo?— Ni nani ungeweza kusaidia?—
Ndiyo, huenda kwanza wakafikiri hawataki msaada. Lakini ungeweza kusema kwao juu ya mambo mazuri ambayo Yehova anafanya. Na huenda watasikiliza. Je! isingekuwa ajabu ikiwa wangempenda Yehova kama wewe?— Mambo kama hayo yanatukia wakati unapotumia kinywa chako kumsifu Yehova.
Tena Biblia inasema juu ya kijana mwanamume jina lake Timotheo. Baba yake hakumwamini Yehova. Lakini mama yake alimwamini, na vile vile bibi yake. Timotheo aliwasikiliza. Na tangu alipokuwa mdogo sana alijua Biblia. Yatupasa tujue Biblia ili tumsifu Yehova. Ni Biblia inayotuambia juu yake.
Wakati Timotheo alipokua, akawa kijana mwanamume mzuri. Siku moja Paulo, mtume wa Yesu Kristo, alitembelea mji alikoishi Timotheo. Aliona namna Timotheo alivyotaka sana kumtumikia Yehova. Basi alimkaribisha kijana huyu aende naye kumtumikia Mungu katika njia iliyo kubwa hata zaidi. Walisafiri pamoja mahali pengine. Kila mahali waliwaambia watu juu ya ufalme wa Mungu na juu ya Yesu.— Matendo 16:1-5.
Timotheo alijifunza mengi juu ya kumsifu Mungu kutoka kwa mtume Paulo. Alimwona Paulo akihubiria vikundi vikubwa vya watu. Alio-na namna Paulo alivyokwenda nyumbani kwa watu kuwafundisha vile vile. Lakini Timotheo hakutazama tu. Alishiriki katika kazi. Kama alivyosema Paulo, ‘Timotheo anafanya kazi ya Yehova vile vile kama mimi mwenyewe.’— 1 Wakorintho 16:10.
Si kila mtu alipenda wakati Timotheo alipozungumza juu ya Mungu. Lakini hakuacha. Hakusema alitaka kurudi nyumbani. Alifurahi kwa vile alikitumia kinywa chake kusema sifa ya Yehova.
Sasa, huenda watu wengine wakasema hii ni kazi ya watu wazima peke yao kufanya. Lakini unasadiki hilo? Mwalimu Mkuu alijua haikuwa hivyo. Siku moja wakati watu wengine walipojaribu kuwazuia vijana wadogo, wasimsifu Mungu, Yesu alisema: ‘Hamkupata kusoma, Kwa vinywa vya watoto wachanga na wanyonyao umekamilisha sifa?’—Mathayo 21:16.
Sisi sote twaweza kumsifu Yehova ikiwa kweli tunataka. Si vigumu. Mungu alitupa kinywa cha kusema. Si lazima tujue kila kitu juu ya Biblia mbele ya kuanza. Twaweza kuwaambia wengine mambo ambayo tumekwisha jifunza. Utapenda kufanya hivyo?
(Maandiko mengine yanayotia moyo vijana wadogo kumtumikia Mungu ni Zaburi 148:12, 13; Mhubiri 12:1; 1 Timotheo 4:12.)