Kizazi Changu—cha Pekee Sana na Chenye Kupendelewa Sana Sana!
Kama ilivyosimuliwa na Melvin Sargent
VIJANA wengi leo wamezaliwa katika jamaa ya Mashahidi wa Yehova. Lakini katika 1896 hilo lilikuwa pendeleo lililotukia mara chache sana sana. Tangu utotoni nilifundishwa na Mama yangu kumwogopa Yehova ifaavyo na kuthamini dhabihu ya ukombozi iliyofanywa na Mwanaye. Kwa hiyo mimi ni wa kizazi cha pekee sana na chenye kupendelewa sana sana—mwenye umri wa kutosha kuona mwanzo wa ishara ya kuwapo kwa Kristo katika 1914 na hata hivyo pengine mchanga kutosha kuishi nikaone mwisho wacho kwenye Har–Magedoni.—Mathayo 24:3, 33, 34.
Mwanzo Mwanzo kwa UMU
Nikiwa mtoto, nilipewa kile kinachoitwa kutendewa kwa UMU, Utunzaji Mwororo wa Upendo. Hata hivyo nyakati nyingine utunzaji huo ungeweza kuonyeshwa katika njia ambazo wengine leo wangezifikiria kuwa kali. Mimi nakumbuka kwamba wakati mmoja Mama alinisikia bila kukusudiwa nikicheza na mvulana mwenye umri mkubwa zaidi yangu ambaye kwa ghafula alianza kutumia maneno mapya kabisa kwangu. “Hayo ni maneno mabaya ambayo ni lazima usiyatumie kamwe,” Mama akaniambia, akikazia jambo hilo juu yangu kwa kutumia zaidi ya maneno matupu! Lakini mimi nilitambua kwamba nidhamu yake ilikuwa wonyesho wa utunzaji mwororo wa upendo, nami nakumbuka nikijiuliza ni kwa sababu gani mama ya Jimmie hakuwa amemtia nidhamu. Je! yeye kweli hakumpenda vya kutosha?
Sisi tulikuwa ndiyo jamaa ya Mashahidi pekee katika Jewell County, Kansas. Baba hakuwa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu, lakini kwa kutaka kusaidia yeye aliongoza funzo la Biblia pamoja na sisi watoto. Dada yangu, Eva, ndiye aliyekuwa na umri mkubwa zaidi, na Walter alinipita kwa umri wa miezi 16. Kila jioni tulitazamiwa tushiriki katika kuosha vyombo. Lakini Walter mara nyingi alipata visababu vya kuomba ruhusa asishiriki. Eva na mimi, hata hivyo, tulitumia kazi hiyo ya nyumbani kuwa nafasi ya kila siku ya kuzungumzia kweli za Biblia, hivyo ilikuwa baraka isiyoonekana wazi. Baadaye nilikuja kuthamini kwamba watu wanaopuuza madaraka maishani wanapoteza baraka nyingi. Hilo lilimpata Walter, ambaye baadaye aligeukia mbali akaacha ukweli.
Kutendewa kwetu kwa UMU kuliongoza kwenye matokeo mazuri Agosti 4, 1912. Eva na mimi tuliamka kabla ya mapambazuko na kusafiri kilometa 16 kwa gari lenye kukokotwa na farasi tukaliwahi gari-moshi la mapema la kwenda Jamestown, Kansas. Pilgrimu mmoja, jina waliloitwa Wanafunzi wa Biblia wasafirio, alikuwa akizuru huko, na huu ndio ungekuwa mkutano wetu wa kwanza pamoja na Wanafunzi wa Biblia nje ya jamaa yetu. Ilikuwa pia siku yetu ya ubatizo.
Ijapokuwa nilikuwa na umri wa miaka 16 tu, nilimuuliza ndugu pilgrimu kama ningeweza kuchukua huduma ya wakati wote, iliyoitwa wakati huo kazi ya kolporta. Yeye alinitia moyo niandikie Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi. Hata hivyo, kwa kuwa nilikuwa ningali ninahitajiwa nyumbani, jambo hilo lililazimika kukawizwa. Kwa wakati uo huo, nilitumia wakati wangu wa ziada kusaidia kwa ukawaida wanafunzi wa Biblia wa Jamestown kugawa trakti kote kote katika miji na majiji yapatao 75 yaliyotuzunguka.
Pia nilitoa ushuhuda nyakati nyingine. Pindi moja wakati bibi mwenye nyumba tulimoishi alipokuja mjini kwa shughuli ya kibiashara na akakaa pamoja nasi kwa siku chache, nilimpa trakti. Lazima jambo hilo liwe lilimvutia. Lakini baada ya kurudi nyumbani Iowa, ilipita miaka 30 kabla sijamwona tena. Alikuwa amekuwa mfuasi wa Adventisti naye hakupendezwa na ‘dini yangu.’ Hata hivyo, yeye alikuwa na shamba kubwa lililotaka kutunzwa, na kwa kuwa hakujua “mwanamume Mkristo kikweli” katika dini yake aliyekuwa na utumainifu naye, alinijia mimi. Yale malipo aliyonilipa yalinisaidia kuniweka katika huduma ya wakati wote kwa miaka kadha. Ulikuwa uthibitisho kama nini wa Mhubiri 11:1: “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi.” Au wa aliyosema Yesu wakati mmoja: “Basi, endeleeni, kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na mambo yote hayo mengine mtaongezewa.”—Mathayo 6:33, NW.
Maono Yasiyoweza Kusahauliwa
Nilihudhuria mkusanyiko wangu wa kwanza katika 1913. Nilivutiwa kuona wapya 41 wakibatizwa, na nikatiwa moyo kufikiri kwamba kwa kuwa nilikuwa nimewatangulia (mimi nilikuwa nimebatizwa kwa miezi kumi), huenda nikawa na tumaini fulani la kuweza kusitawisha “sifa kama ya Kristo” kufikia 1914, ili kuhakikisha ‘kuitwa na kuchaguliwa’ kwangu. Nilivutiwa pia kuona tepe nyingi sana nyekundu na za manjano. Makolporta waliokuwa wakitafuta wenzi walivalia tepe nyekundu, na ye yote aliyetaka kujiunga pamoja nao alivalia utepe wa manjano.
Kwangu mimi jambo moja kuu la mkusanyiko wangu wa 1914 lilikuwa kuona sinema ya Mchezo wa Kuigizwa Wenye Picha za Uumbaji na kupata kumwona Ndugu Russell akiwa karibu. Alikuwa mchangamfu na alionyesha tamaa halisi ya kutoa habari yenye kutia-moyo kwa wasikilizaji wake. Alikuwa mwenye kusikitikia na moyo wa kupenda kusikiliza waliomjia wakiwa na matatizo. Wala hakuwa mashuhuri mno asiweze kupata nafasi ya kushiriki mchezo wenye makelele ya furaha wa matineja pindi kwa pindi. Jioni moja nilipokuwa nikipatia watu maandishi ya programu ya Mchezo wa Kuigizwa Wenye Picha, alinipita kwa haraka. Nilimtolea nakala moja, nikijifanya kuwa sikutambua yeye ni nani. Kwanza yeye alipita, kisha akageuka na kunishukuru kwa kicheko, akinijulisha kwamba alikuwa amefahamu ucheshi wangu.
Mwishowe katika 1917, nikiwa na umri wa miaka 21, niliweza kuingia katika kazi ya kolporta. Vita ya Ulimwengu ya Kwanza tayari ilikuwa imeendelea kwa muda wa karibu miaka mitatu. Sanduku la mavazi yangu likiwa mkononi, vitabu vingi, na dola 30 mfukoni mwangu, nilishika njia kuelekea Nebraska pamoja na mwenzangu, Ernest Leuba, kolporta mwenye umri mkubwa na ujuzi zaidi. Tulikuwa na mambo yaliyoonwa yalikuwa yenye kufaa na yasiyofaa pia. Nakumbuka, kwa mfano, wakati mmoja, tulipoamua kutumia njia ya kuharakisha ya kuangusha vitabu, tulichapisha kadi zilizotolea watu nafasi ya siku mbili za kuchunguza bure kile kitabu The Finished Mystery, wakiwa na pendeleo la kukipata kwa senti 60 (U.S.) turudipo. Asubuhi moja kila mmoja wetu aliazima vitabu kumi katika mtindo huo. Siku mbili baadaye, mimi niliweza kuangusha saba za zile zangu, hali Ndugu Leuba, ambaye alikuwa amefanya kazi katika ujirani wenye idadi kubwa sana ya Wakatoliki, aliangusha kimoja tu. Ili akipate tena kitabu kimoja cha vile alivyokuwa ameazima, alilazimika kwenda kwa kasisi Mkatoliki wa mahali pale aliyekuwa amepelekewa kitabu hicho. Kwa hiyo tuliamua upesi kwamba njia yetu ya kuharakisha kwa kweli haikuwa bora kama ile ya kutumia wakati zaidi tukiongea na watu.
Bila shaka, tulikuwa na pesa kidogo sana, kumaanisha kwamba nyakati nyingine tulikuwa wastadi sana katika kufikiria njia za kuwa waekevu. Kwa hiyo baadaye wakati tulipohamia kwenye mgawo mpya katika Boulder, Colorado, tulinunua tikiti ya kutufikisha kwenye stesheni iliyo karibu zaidi na mpaka wa mkoa. Halafu tulishuka kutoka kwenye gari-moshi na kununua tikiti nyingine katika gari-moshi lililofuata kwa ajili ya sehemu iliyobaki ya safari yetu. Kwa sababu gani? Kwa sababu nauli ndani ya mkoa zilikuwa senti mbili kwa kila maili, lakini bei za kuvuka kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine zilikuwa juu zaidi. Licha ya kuokoa pesa, tuliweza kutumia wakati wetu wa kutua tukitoa ushuhuda wa vivi hivi.
Matatizo ya Wakati wa Vita na Mwanzo Mpya
Kufikia sasa ilikuwa 1918, na United States ilikuwa imejiingiza sana katika vita. Dhoruba ya upinzani ilianza waziwazi dhidi ya Wanafunzi wa Biblia, ikitambulisha wale waliokuwa waoga-waoga na wale ambao hawakuwa waoga. Baadhi ya akina ndugu wenye umri wa kuandikishwa jeshini, ijapokuwa walikataa kuingia jeshini kwa sababu ya dhamiri, walikubali kufanya utumishi wa kijeshi usio wa kupigana.
Nilipojiandikisha, nilidai niachiliwe nikiwa mhudumu. Nilidhani, hoja zangu, zilikuwa na msingi mzuri, na kuingizwa kwanza jeshini kulikawizwa wakati kesi yangu ilipopelekwa kwenye baraza la rufani. Wao walifikiria vingine na kukataa dai langu. Kukawizwa huku, hata hivyo, kulinisaidia nisitiwe gerezani kwa sababu kufikia sasa ulikuwa wakati wa mavuno, nami niliahirishwa mpaka kazi hii ya maana kwenye shamba la wazazi wangu iwe imemalizika. Mwishowe kuingizwa kwangu jeshini kuliwekwa kuwe Novemba 15. Vita ile ilimalizika Novemba 11. Nilikuwa nimenusurika kwenda gerezani kwa siku nne tu.
Wengine ambao walijitokeza bila woga kuunga mkono kutokuwamo kwa Kikristo hawakuwa na hali nzuri kama mimi. Kwenye mkusanyiko katika Denver, nilikutana na mmoja wao. Akieleza ni kwa sababu gani alikuwa na upara, ndugu huyo alisimulia jinsi alivyofungwa kwenye mti na kundi lenye ghasia lenye kushikilia mambo bila akili ambalo lilimwaga lami moto juu ya mwili wake wote. “Wanawake waliokuwa katika kikundi hicho,” akasema, “walikuwa ndio wabaya zaidi.” Alikuwa amenyoa nywele yake yote kuondoa lami hiyo. Ndipo akatoa tabasamu kubwa na kusema kuhusu ono lake: “Singaliweza kulikosa kwa vyo vyote.”
Kwa sababu ya msimamo wao Wasiowacha, baadhi ya maafisa wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi walitiwa gerezani kwa makosa. Lakini katika 1919, walipokuwa wangali gerezani, walichaguliwa tena kwenye vyeo vyao katika Sosaiti, ingawa waasi-imani walijaribu kuchukua vyeo vyao. Ndugu waaminifu walikubali huo kuwa wonyesho wa kibali cha Yehova. Wakiwa wamejaa furaha, wakitiwa moyo na mtiririko mpya wa roho takatifu, walikuwa sasa wameazimia zaidi kuliko wakati mwingine wo wote uliotangulia kuchukua kazi ya kuhubiri Ufalme upya na kufunua viongozi wa kidini kwa sababu ya kushindwa kwao kwa unafiki kuunga mkono Ufalme wa Mungu. Kuvunja kabisa uhusiano na Babuloni kulikuwa kumeanza.
Katika Februari 24, 1918, katika Los Angeles, Kalifornia, baada ya United States kujitia katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza Aprili 6, 1917, Ndugu Rutherford alitoa kwa mara ya kwanza ile hotuba yenye kusisimua “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.”
Mabadiliko Yenye Maana Katika Muda wa Miaka Iliyopita
Kwa muda wa miaka saba Lydia Tannahill nami tulikuwa tumedumisha urafiki hasa kwa njia ya kuandikiana barua. Baada ya kufikiria kwa sala, tuliamua katika 1921 ingetufaa sisi tutumie kwa faida kukubali kwa Paulo alipokuwa akipendekeza useja, yaani, kwamba yeye ambaye “atoa ubikira wake katika ndoa afanya vema.” (1 Wakorintho 7:38, NW) Ndoa yetu ilikuwa zawadi kutoka kwa Yehova na ilifanya mioyo yetu kushangilia. Kabla ya muda mrefu, hata hivyo, tulikabiliwa na hatari kubwa. Kusafiri kulikuwa kumefanya umizo la mgongoni la zamani la Lydia kuwa mbaya sana, na moyo wangu, ujapokuwa mshikamanifu na wenye kupenda, ulikuwa na mwendo wa polepole, “moyo uliochoka” ndivyo walivyouita madaktari. Hilo lilitokeza ugonjwa wa kupungukiwa damu. Sisi wawili tulikuwa tunaishiwa nguvu. Tulishauriwa twende mahali ambako hali ya hewa ilikuwa tofauti na tupunguze safari zetu za kila siku. Makao yetu yanayoweza kuhamishwa kwa urahisi yalifaa sana kutusaidia sisi kufuata shauri hili, na hivyo tulitumia Septemba 1923 tukiwa barabarani kwenda Kalifornia.
Nikiwa kama nilivyo wa kile kizazi chenye kupendelewa sana, nimeruhusiwa kuona jinsi tengenezo lionekanalo la Yehova limesitawi katika muda wa miaka iliyopita. Nilikuwapo kule wakati Los Angeles ilipogawanywa katika maeneo moja moja ya kuhubiri, wakati kutoa ushuhuda Jumapili kulipoanza, na wakati tulipopokea jina letu jipya, Mashahidi wa Yehova, katika 1931. Ni sisimuko kama nini kuona marekebisho yakifanywa katika 1932 na 1938 yaliyohakikisha kuwekwa rasmi kwa wazee kwa njia ya kitheokrasi badala ya njia ya kidemokrasi. Na imekuwa furaha yangu kuona masuala na maswali yasiyo wazi, kama yale ya kutokuwamo na utakatifu wa damu, yakielezwa wazi.
Ingawa niliacha kazi ya kolporta katika 1923, sikuzote nilidumisha roho ya upainia. Hivyo katika 1943 niliweza kujiunga tena na hesabu zenye kuongezeka haraka za mapainia. Katika 1945 hata nilipendelewa kuwa painia wa pekee, nikatumikia miaka tisa katika cheo hicho mpaka “moyo uliochoka” wangu kwa mara nyingine tena uliponikatiza. Tangu 1954 nimetumika nikiwa painia wa kawaida.
Ndoa yangu pamoja na Lydia ilidumu kwa miaka 48 mpaka 1969 alipoondoka kwenda kwenye mgawo mpya, urithi wake “uliotunzwa mbinguni,” mgawo ambao, mimi, pia natumaini kuupokea wakati ufikapo. (1 Petro 1:4) Ingawa hatukubarikiwa kamwe kuwa na watoto, tulibarikiwa kuwa na ndoa ambayo wengi wanaiona kuwa yenye kufaa sana. Ingawa hasara yangu ilikuwa kubwa, kuendelea kujishughulisha na faida za kitheokrasi kulinisaidia niishinde. Baadaye nilioa painia mwenye ujuzi niliyekuwa nimemjua kwa miaka mingi, Evamae Bell, tulifurahia miaka 13 ya ushirikiano wa uaminifu mpaka yeye, pia, alipokufa.
Kizazi Changu—cha Pekee Sana Katika Njia ya Pekee
Nyakati nyingine nimepata kuulizwa: “Ni nini limekuwa ono lako bora zaidi katika ukweli?” Bila kusita ninajibu: “Kuona yakitimizwa katika kizazi changu maunabii ya Biblia yaliyoandikwa na wanaume walioongozwa kwa roho na walio wakfu karne nyingi zilizopita.”
Washiriki wa kizazi changu nje ya tengenezo la kitheokrasi, bila shaka, wamekuwa sawa-sawa kama vile Mchezo wa Kuigizwa wa Uumbaji wa 1914 ulivyosema wangekuwa: wenye kichaa cha pesa, kichaa cha anasa, na kichaa cha umashuhuri. Wale wetu tuliomo ndani ya tengenezo la Bwana tumejaribu, katika kila njia iwezekanayo, kuelekeza fikira zao kwenye ujumbe wa uzima. Tumetumia maneno ya shime, matangazo ya ukurasa mzima, redio, magari yenye kutoa sauti, vinanda vya kuchezea sahani za santuri, mikusanyiko mikubwa, maandamano ya watu wanaotembea wakibeba ishara, na jeshi linaloendelea kuongezeka la wahudumu wa nyumba kwa nyumba na wahubiri penye pembe za barabara za mji. Utendaji huu umetumika kugawanya watu wale wanaopendelea Ufalme wa Mungu uliosimamishwa wakiwa upande mmoja, na wale wanopinga wakiwa upande mwingine. Hii ndiyo kazi aliyotabiri Yesu kwa kizazi changu!—Mathayo 25:31-46.
Mpaka huu “moyo uliochoka” wangu upige pigo lao la mwisho, utaendelea kupiga katika uthamini wa pendeleo ambalo nimefurahia la kuwa wa kizazi cha pekee sana. Utaendelea kupiga kwa msisimuko juu ya pendeleo ninalo sasa la kuona mamilioni ya nyuso zenye kutabasamu ambazo zimekusudiwa ziendelee kutabasamu milele.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Melvin na Lydia Sargent, makolporta, 1921
[Picha katika ukurasa wa 24]
Melvin na Evamae Sargent, 1976