Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 5/15 kur. 8-11
  • Katika Ujeremani Uliofuata baada ya Vita Vijana Wamsifu Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Katika Ujeremani Uliofuata baada ya Vita Vijana Wamsifu Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WALIOLELEWA NA WAZAZI WAAMINI
  • TATIZO LA JAMAA ZILIZOGAWANYIKA
  • KUSHINDA MATATIZO, MAKUBWA NA MADOGO
  • WALE AMBAO HAWAKULELEWA NA WAZAZI WAAMINI
  • UTUMISHI WA WAKATI WOTE
  • KUMSIFU YEHOVA KATIKA LUGHA NYINGI
  • ULE UPANDE MWINGINE
  • Tunawafurahia Vijana Wanaotembea Katika Njia ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • “Kutoka Kinywani mwa Watoto Wachanga”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 5/15 kur. 8-11

Katika Ujeremani Uliofuata baada ya Vita Vijana Wamsifu Yehova

UJEREMANI (Allemagne) 1978. Nyanda tambarare za kaskazini zivumiwazo na upepo mwingi na zilizofunikwa kwa mimea iotayo nyikani inayovutia macho; makao makuu ya viwanda ya Ruhr yenye shughuli (kazi) nyingi mno yakiwa yamefunikwa karibu yasionekane kwa mchanganyiko wa moshi na ukungu; milima yenye fahari ya Alps ya Bavaria iliyofunikwa kwa theluji nyingi inayoanguka wakati wote, na watalii wakiikumba nchi wakitafuta suruali fupi zilizotengenezwa kwa ngozi, dirndls (mavazi ya kike yenye rangi nyingi) makopo ya bia (kileo) pamoja na saa zenye kutoa sauti kama ile ya mlembe​—huo ndio Ujeremani unaojulikana na watu wote. Inaelekea umebadilika kidogo sana.

Lakini kumbe! ulimwengu, kutia na Ujeremani, umepata kubadilika, pengine haraka zaidi baada ya kumalizika Vita ya Pili ya Ulimwengu kuliko wakati mwingine wo wote. Umepatwa na hatari mpya, maoni mapya na kanuni mpya za tabia. Kikitoka katika maangamizi ya vita, kizazi kilichotangulia kingekipa kizazi cha baada ya vita urithi gani?

Hakungalikuwako urithi bora zaidi wa kuwezesha hicho kizazi kipya kutatua matatizo (magumu) yao kuliko maarifa sahihi ya Mungu wa kweli Yehova na makusudi yake. Wakati wa utawala wa Hitler kulikuwako Wakristo waliokuwa na maarifa hayo na ambao uaminifu wao chini ya mateso unajulikana sana. Wakikumbuka maneno ya Daudi kwamba “kizazi kwa kizazi kitayasifu matendo yako, kitayatangaza matendo yako makuu,” kimeazimia kupitisha urithi huu ulio bora kwa kizazi kilichofuata baada ya vita’. (Zab. 145:4) Je! kimefaulu kufanya hivyo? Na tuchunguze.

WALIOLELEWA NA WAZAZI WAAMINI

Wengi wa Mashahidi wa Yehova wa kizazi kilichopo (tangu 1945) wamepata pendeleo la kulelewa na wazazi na hata babu na nyanya waliokuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, Elke na dada yake Heidi, wote wawili wakiwa wanatumikia Mungu wakati wote, wana furaha ya kuwa wa kizazi cha tano cha Mashahidi katika jamaa yao. Lo! namna inavyopendeza kuona jamaa nzima zikitumikia Yehova kwa umoja!

Fikiria, vilevile jamaa fulani katika Westphalia yenye watoto 15. Gerhard, ambaye sasa anatumikia wakati wote katika afisi ya tawi ya Sosaiti katika Wiesbaden, anakumbuka mazoezi mazuri waliyopata kutoka kwa wazazi walipokuwa bado nyumbani. Mafunzo matatu ya jamaa yalihitajiwa ili kuangalia mahitaji ya kila mmoja wao: moja kwa ajili ya watoto wale wakubwa zaidi, moja kwa ajili ya wale wadogo kabisa, na moja kwa ajili ya wale wa umri wa katikati. Kabla na baada ya mikutano, baba alikuwa akitumia saa moja na nusu kuendesha gari kwenda na kurudi ili apeleke jamaa Yote kwenye Jumba la Ufalme. Jamaa zenye nguvu za Kikristo hazifanywi pasipo jitihada!

TATIZO LA JAMAA ZILIZOGAWANYIKA

Wengine hawakubarikiwa kuwa na msingi wa jamaa yenye umoja, kwa kuwa wamelelewa katika jamaa zilizogawanyika kidini.

Friedhelm anakumbuka kwamba baba yake alichoma Biblia yake, vitabu vyake na magazeti yake mara nyingi. Ijapokuwa mipango ya kujitafutia makuu aliyokuwa amefanyiwa na baba yake, akiwa ndiye mtoto wa pekee, aliamua kutumikia akiwa mtangazaji wa wakati wote wa habari njema za ufalme wa Mungu.

Vivyo hivyo, Wilfred anaeleza namna yeye na mamaye walivyofungiwa nje mara nyingi waliporudi nyumbani kutoka mikutano ya Kikristo. Safari moja walilazimika kulala garini usiku kucha. Pindi nyingine baba yake alimburuta kutoka kitandani akaanza kumpiga kwa taa. Lakini kwa kuendelea kuwa mwaminifu, alipata, si heshima kutoka kwa baba yake tu, bali, lililo la maana zaidi, kibali ya Yehova. “Wakati wote ndugu walinifanya nijisikie ninakaribishwa kundini, hata ingawa nilikuwa na miaka 11 au 12 tu wakati huo na upendo huu ndio ulioniwezesha kuendelea,” ndivyo anavyoeleza.

Uwe, akiwa tineja (miaka 13-19) alipopata kuwa Shahidi mara ya kwanza, alipata upinzani kazini na nyumbani pia.

Yeye anakumbuka wakati mmoja alipotumia vizuri nafasi fulani kuzungumza na wengine kweli wakati wa kunywa kahawa akathawabishwa, si kwa masikio yenye kusikiliza, bali kwa kumwagiwa ndoo ya maji kichwani. Hata hivyo, yeye na nduguye, ambaye sasa ni mmisionari katika Spania, waliendelea kusonga mbele kwenye kukomaa kwa Kikristo.

Rolf-Dieter alikuwa na umri wa miaka 5 au 6 hivi wakati mamake alipopendezwa na kweli ya Biblia. Yeye na nduguye mchanga hawakuruhusiwa na baba yao mwenye kupinga wahudhurie mikutano ya Kikristo, ingawa mama yao aliwazungumzia nyumbani na kwenda pamoja nao ilipowezekana.

“Ninakumbuka pindi moja wakati baba yangu aliponilazimisha nihudhurie mikutano ya kanisa mojawapo ya madhehebu ya Jumuiya ya Wakristo,” yeye anasimulia. “Lakini mama alikuwa ametangulia kunieleza kila kitu. Nilienda nikasikiliza, walakini dhamiri yangu haikuniruhusu nishiriki katika sherehe, ambazo nilifahamu hazikupatana na maandiko, ingawa wengine waliokuwa wamekaa karibu nami walinipiga-piga na kuninong’onezea lile nililopaswa kufanya.” Hata hivyo, Rolf alitumia kujiweza kuelekea wale waliohudhuria mikutano hiyo, akifahamu kwamba Maandiko yanaamuru wengine waonyeshwe heshima.

KUSHINDA MATATIZO, MAKUBWA NA MADOGO

Wakristo vijana wanapata matatizo (magumu). Kudhihakiwa na kuchekelewa kunaweza kuwa jaribu kweli kweli la ukamilifu wa mtu. Baada ya kumaliza masomo ya juu wanafunzi wa kiume wanakabiliwa (wanaelekewa) na ulizo la kutokuwamo. Nao, Mashahidi wa kike pia, wamelazimika kushindana na matatizo yote yanayopata vijana leo: dawa za kulevya, vileo, uasherati na mengine, mengi sana.

Ala! hata kumpata mwenzi wa ndoa linaweza kuwa tatizo. Ndivyo ilivyokuwa kwa Ute. Yeye anaeleza hivi:

“Ningepata wapi mwenzi anayefaa? Vijana wote kundini walikuwa wameoa tayari. Labda haingedhuru kutafuta kidogo huku na huku ulimwenguni. Lakini, sivyo, nisingaliweza, nikiwa nafahamu shauri la Maandiko, yaani, kuolewa ‘katika Bwana tu.’ Katika jambo hili, pia, niliweka tumaini langu katika Yehova. Kisha wakati wa kazi ya kujenga Jumba letu jipya la makusanyiko katika Trappenkamp nilimpata mchumba wangu. Tutaoana Juni.”

Namna gani watoto wetu wachanga na matatizo yao “madogo”? Ebu na tumsikilize Eric:

“Mimi nina umri wa miaka 10 na katika darasa la nne. Wazazi wangu wamekuwa Mashahidi kwa muda mrefu, kwa hiyo kabla sijaanza shule nilikuwa nikishirikiana na waamini wenzangu peke yao. Mambo yote yaliendelea vema mpaka siku ile darasa letu lilipoondoka kwenda huko mashambani kukaa kwa juma moja katika jumba la shule la kukaa wanafunzi. Kabla ya hapo sikuwa nimepata kukaa mbali na nyumbani. Mwalimu wetu akawa mgonjwa ghafula na mwalimu mwingine akaja badala yake. Sikumjua. Jumapili asubuhi akasema: ‘Sote tutakwenda kanisani asubuhi hii.’ Nilifahamu kwamba ningelazimika kumweleza kwamba sikubaliani na mafundisho yanayotolewa huko, na kwa sababu hiyo ingekuwa afadhali nisiende. Wakati wa kiamsha kinywa nilifikiria yale ningemwambia. Baada ya kiamsha kinywa, nilizungumza naye, lakini akasema: ‘Utakwenda, kwa hiyo hakuna kubishana!’ Nilienda chumbani mwangu, na, nilipokuwa peke yangu, nikakumbuka aliyoniambia mama asubuhi ile niliyoondoka: ‘Ukiingia katika shida, Yehova aujua moyo wako. Unaweza kumwambia tatizo lako.’ Nililia nilipokuwa nikiomba. Sikutaka jambo lo lote linalohusiana na dini ya uongo! Muda mdogo baadaye niliporudi nje nilimkuta mwalimu mwingine akaniuliza kuna nini, kwa kuwa aliona kwamba nilikuwa nimelia. Nikamwambia. Akasema: ‘Nitakutengenezea jambo hilo.’ Nilifurahi weee! Nilimshukuru Yehova kwamba alikuwa amesikia sala yangu. Mkono Wake haukuwa mfupi.”

Tatizo “dogo”? Huenda wengine wakadhani hivyo, walakini kizazi chetu kilichofuta baada ya vita kimefahamu kwamba Yehova halioni tatizo lo lote kuwa dogo sana au lisilo la kuhangaikiwa. Wala hatuachi tunapopatwa na yale makubwa. Chukua mfano wa Marion:

Yeye alikuwa mfano mwema wa kijana Mkristo, akitenda kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Marion alikuwa na miaka 17 tu na mwenye juhudi sana. Walakini kivimbe katika uti wake wa mgongo kikafanya mkono wake upooze polepole. Ikawa lazima afanyiwe upasuaji, walakini kwa sababu ya hali yake ya hatari hakuna daktari (mganga) ye yote aliyekubali kuufanya pasipo kutumia damu. Marion na wazazi wake waliendelea kuwa imara. Hawangekosa kumtii Yehova! Ingawa alikuwa akipata uchungu mwingi sana, uchangamfu wake haukukoma hata kidogo. Mwishowe alipatikana daktari fulani wa kupasua ambaye alikubali kuheshimu imani ya kidini ya msichana huyo. Upasuaji ulifanywa bila kutumia damu ukafaulu! Hata hivyo, faraja ikawa ya kitambo tu; upasuaji wa pili ukawa lazima kisha wa tatu. Kupooza kulipoendelea kuenea, akapata uchungu mwingi zaidi. Ulimi wake ukapooza, walakini matendo yake hospitalini yakaendelea kutoa ushuhuda wa imani yake. Kwa upendo mwingi na kwa jitihada nyingi sana, akamshonea mwuguzi wake wa kike fulana. Wakati kifo kilipokuwa hakiwezi kuepukika, wazazi wake wakamchukua nyumbani. Ijapokuwa sauti yake ilikuwa inasikika kidogo tu na aliweza kuinua kichwa chake kidogo tu bado waliendelea kumchukua mikutanoni ya Kikristo kwa machela (kitanda cha kubebea mgonjwa). Kama vile Ayubu alipopatwa na ugonjwa, msichana huyu aliendelea kushikilia uhakika thabiti kwamba yeye, vilevile, atakuja kubarikiwa na Mungu siku moja apate kuwa mwenye shauku milele. Alikufa Desemba 28, 1977, akiwa na umri wa miaka 18. Kwa kukataa kuacha imani yake katika Yehova, alitiwa nguvu Naye akajiunga na Wakristo wengine waliokuwa waaminifu mpaka kufa, kutia na wengine wa kizazi chetu kilichofuata baada ya vita, ambao sala zao za kutaka uzima zitajibiwa katika ufufuo.​—Matendo 24:15.

WALE AMBAO HAWAKULELEWA NA WAZAZI WAAMINI

Bila shaka, wengi wa vijana wetu walio Mashahidi hawakulelewa na wazazi waamini. Wao, pia, iliwalazimu kushinda matatizo, nyakati nyingine yakiwa magumu sana, kabla ya kuwa watumishi wa Yehova.

Kwa mfano, yuko Christa, mwenye umri wa miaka 22, ambaye alipendezwa na kweli wakati Mashahidi wa Yehova walipoanzisha funzo la Biblia na nduguye. Alikuwa mwenye bidii katika kazi ya vijana Wakatoliki, lakini vilevile, alikuwa akihudhuria mikutano ya Wabaptisti kila juma. Anaeleza sababu gani yeye mwenyewe alianza kujifunza na Mashahidi:

“Siku wa na wazo hata kidogo la kuwa mmoja wao. Lengo langu lilikuwa kumrudisha ndugu yangu katika Ukatoliki. Kwa hiyo nilitaka kujifunza mengi iwezekanavyo juu ya Biblia kisha niitumie kupigana na ‘adui’ hawa.” Lakini kadiri alivyojifunza, ndivyo alivyosadikishwa kwamba Mashahidi ndio waliokuwa na kweli, kama vile asemavyo, “Ukawa woga wangu!” Anaendelea hivi “Nilipaswa kuamua kati ya rafiki zangu Wakatoliki, na rafiki zangu wapya Wabaptisti na Mashahidi wa Yehova, ambao nilijua machache sana juu yao ila tu kwamba waliweza kujibu maulizo yangu yote ya Biblia.”

Tatizo la Christa lililofuata lilikuwa muziki. Tangu umri wa miaka 15 alikuwa anaimba hadharani na alitarajia kuwa bingwa siku moja. Alipata sifa nzuri katika maonyesho ya ujuzi na alipata kucheza katika Uingereza na vilevile katika Ujeremani. Alipaswa kufanya jambo gani? Anaendelea kusema hivi:

“Nilifanya uamuzi wangu baada ya kumtembelea rafiki yangu Janet, niliyejuana naye kwa kuandikiana barua, katika Uingereza. Aliniambia kwamba alikuwa amelazimika kuondoka nyumbani kwa sababu ya kweli. Hili lilinifanya niwaze, kwa kuwa Janet alikuwa amefahamu kweli kwa muda wa miezi minne tu, tangu wakati ndugu yangu nami tulipomtolea ushuhuda wakati wa matembezi yake Ujeremani. Sasa mambo yakaanza kutendeka upesi-upesi. Kabla ya kuondoka Uingereza nikaacha kuvuta sigara. Muda mfupi baada ya kufika nyumbani nilivunja urafiki wangu na walimwengu wote na kurarua picha zote za mabingwa zilizokuwa kwenye kuta zangu. Sasa nilikuwa huru kuhudhuria mikutano yote. Karibuni nilipata rafiki wengi wapya wa kweli. Nilibatizwa katika mwaka 1974. Miezi saba baadaye niliruka kwa ndege mpaka Uingereza ili nimwone rafiki yangu Janet akibatizwa. Tulimshukuru Yehova sana kwa kuwa alitukomboa na dini ya uongo akatutia nguvu ili tushinde matatizo yetu mengi.”

UTUMISHI WA WAKATI WOTE

Kwa kuwa wao ni vijana na kwa kawaida hawana madaraka ya jamaa, wengi wa kizazi hiki kilichofuata baada ya vita katika Mwungano wa Jamhuri ya Ujeremani wamepata kutoa nguvu zao wakati wote katika kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu. Mara tu baada ya kuonja baraka za utumishi wa wakati wote au “upainia,” wengi wametaka kuendelea kuzifurahia wakati mrefu iwezekanavyo. Kwa kweli, Karl-Hienz aliazimia kufanya hivyo sana hata akamtafuta mwenzi wa ndoa ambaye akikuwa na maoni kama yake kuhusu utumishi huu. Anasema hivi:

“Mpaka sasa tumefurahia pamoja miaka minane ya utumishi wa ‘painia’ na tumebarikiwa sana. Tuna ndoa yenye furaha na tumesaidia watu kadha waikubali kweli, kutia na jamaa nzima, ambayo sasa kichwa chake ni mzee kundini.”

Wengine wamekuwa na nia ya kufanya mabadiliko fulani katika kazi zao za kimwili ili kuwawezesha kutoa wakati mwingi zaidi kwa utangazaji wa “habari njema.” “Kufanya kazi ya kibarua halikuwa jambo la chini sana nisiweze kulifanya ili ‘nipainie,’” asema Wolfang, fundi wa upambaji. Carola mwenye umri wa miaka 18 anafanya kazi ya muda ya nyumbani na anasema ni “kazi nzuri ajabu!” Helmut aliyezoezwa katika afisi ya uchoraji wa ramani za majengo, alitumia sehemu ya wakati wake katika kazi ya kupiga lipu katika kuta za nyumba kisha akabadilisha akawa akigawa magazeti asubuhi sana ili awe “painia.”

Kabla ya kujifunza kweli, Ulrich alikuwa mpishi mkuu akifanya kazi katika mahoteli (mikahawa) yale mazuri sana, yanayotoa utumishi kwa wanasiasa wenye sifa na wacheza sinema wanaojulikana sana. Aliiacha apate kuwa na wakati mwingi zaidi kwa ajili ya kazi ya Kimaandiko Anasema hivi:

“Rafiki zangu walinishauri nisifanye hivyo, wakisema kwamba ningeendelea ‘kushuka.’ Taraja langu la kuwa mpishi mkuu maarufu likamalizika, vilevile na ndoto yangu ya kupata fedha nyingi. Walakini siwezi hata kidogo kubadilisha hayo yote kwa yale niliyo nayo leo. Nikiwa ‘painia’ nina furaha ajabu​—bila shaka ni mwenye furaha zaidi kuliko wakati nilipokuwa ‘sijashuka’ sana kama nilivyo.”

KUMSIFU YEHOVA KATIKA LUGHA NYINGI

Vilevile, kizazi kilichofuata baada ya vita kimefanya kazi nzuri sana katika vikundi vya lugha za kigeni katika Ujeremani. Wengi wamejifunza lugha geni ili watumikie katika mojawapo ya makundi 167 ya Kiingereza, Kigiriki, Kiitaliano, Kireno, Kispania, Kituruki, na Kiyugoslavia yaliyomo Ujeremani.

ULE UPANDE MWINGINE

Walakini kama ilivyo kawaida ya mambo kuna pande mbili katika kila hadithi na ungekuwa udanganyifu kufikiri kwamba vijana wote kati ya Mashahidi wa Yehova katika Ujeremani ni wa namna ile iliyotajwa hapo juu. Ubaridi wa watu, uvutano wa kilimwengu, kupenda mali za kimwili​—ni mambo ambayo yameangusha wengi na yangali yakifanya hivyo. Vijana wengi wamekuwa dhaifu kiroho kwa sababu ya kutojifunza Biblia kwa bidii na kwa kutomwomba Mungu awape “hekima itokayo juu.” Mwangalizi mwenye kusafiri aliandika karibuni kwamba alifadhaika sana kuona namna wengine wanavyofanya machache sana katika kazi ya kuhubiri:

“Katika makundi matatu ya mwisho niliyotembelea, wao ni sehemu ya 23 kwa mia ya Mashahidi, lakini kwa habari ya muda wanaotumia katika kuhubiri, wao ndio dhaifu zaidi. Inaumiza sana kuona kwamba wengine wao wana uhusiano mdogo sana na Yehova na kundi. Wao ni ‘washiriki’ tu wa dini! Inawaletea wazazi uchungu wanapogundua jambo hilo, lakini nyakati nyingi wao wenyewe wana lawama. Wengine ni kwa sababu wazazi hawakujali hali njema ya kiroho ya watoto wao.”

Taratibu hii mbovu ya mambo inapojiharakisha kuelekea uharibifu wake, huu ndio wakati wa vijana kama hao kuamka na kuona hatari ya hali hiyo, na kutenda kama iwapasavyo. Yehova atawabariki wakifanya hivyo.​—Rum. 13:11; Luka 21:34-36.

Enyi mlio wa kizazi chetu kilichofuata baada ya vita mnaomtumikia Yehova kwa uaminifu na kuyasema matendo yake makuu ENDELEENI NA KAZI HIYO ILIYO NZURI! (Zab. 145:4, 12) Mfano wao na uwatie moyo wengine wa rika yao wapigane kweli kweli wasinaswe na taratibu mbovu ya Shetani. Wao wenyewe wakiwa wamepokea urithi bora, na walione daraka lao la kuupitisha kwa kizazi kinachofuata. Lakini kuna kingine zaidi kinachowafanya watumikie kwa uaminifu sasa. Ikiwa watafanya hivyo, huenda wakapendelewa, kwa sababu ya mwujiza ujao wa ufufuo, wapate kupitisha urithi huu ulio bora kwa vizazi na vizazi vilivyotangulia! Lo! namna lilivyo taraja la kusisimua! Ni nani asingetaka kuwa kati ya wanaopendelewa hivyo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki