Kujua Yaliyo Katika Habari
Gharika Haikutiliwa Chumvi
Ule usimulizi wa Kibiblia juu ya gharika ya duniani pote umechambuliwa kwa muda mrefu kuwa pokeo linalotegemea ngano ya kubuniwa tu badala ya kutegemea uhakika. New Catholic Encyclopedia inashikilia hivi: “Sasa inaafikiwa kwa ujumla kwamba lile tukio la Noa na safina si kipande cha ripoti ya kihistoria bali ni ubuni wa maandishi yaliyowaziwa tu yaliyo ya namna nyingine kabisa.” Watu fulani wenye kutia-tia mashaka wamebishania kwamba unyevunyevu wote ulio katika anga ungesababisha inchi chache tu za mvua ya duniani pote. Wao wanasema lile wazo la dunia kugharikishwa kabisa katika maji si halisi.
Lakini je! ndivyo? Kulingana na usimulizi wa Mwanzo, chanzo cha maji ya gharika hakikuwa ule unyevunyevu tu ulio katika anga. Kwenye Mwanzo 1:6, NW, tunaambiwa kwamba Muumba aliamrisha uamuzi huu: “Acha mtandao [wa kianga] uje kuwa kati ya yale mafungu ya maji na mgawanyo utukie kati ya yale mafungu ya maji [ya zile bahari] na yale mafungu ya maji [yaliyo juu ya mtandao huo].” Inaonekana wazi kuwa yale mafungu ya maji yenye kuning’inia juu ya mtandao-anga yalibaki hapo mpaka wakati wa Gharika. Kulingana na mtume Petro, “mbingu” ambazo ni anga na mafungu ya maji yaliyokuwa juu yazo na chini yazo ndiyo ambayo kwayo “ulimwengu wa wakati wa [Noa] ulipatwa na uharibifu wakati ulipogharikishwa kwa maji.”—2 Petro 3:5, 6; Mwanzo 1:7, NW.
Athari zenye uharibifu mkuu za gharika ya maji zilihisiwa hivi majuzi katika Afrika Kusini wakati furiko moja lilipopiga mkoa wa Natal na kuchukua uhai wa watu zaidi ya 300. Akieleza juu ya msiba huo, mhifadhi-mazingira K. H. Cooper alionelea hivi: “Mimi nimejiuliza mara nyingi ni jambo gani lingetukia katika siku na muda huu kama mvua ingekunya kwa michana 40 na masiku 40 bila kuacha. . . . Je! mvua kama hiyo ingaliweza kufutilia mbali karibu uhai wote duniani? Nikiisha kuwa nimeona hivi majuzi lililotukia baada ya siku nne tu za mvua katika Natal,” Cooper anaendelea, “sasa mimi nasadiki juu ya unyoofu wa ile hadithi ya Agano la Kale.”
Je! Ni Hangaikio kwa Walio Maskini?
Lile pengo linalotenganisha maskini kutoka kwa matajiri linaweza kuzibwa jinsi gani? Hilo ndilo suala lililofikiriwa na papa John Paul wa 2 katika barua ya kipapa ya hivi majuzi yenye kuenezwa sana yenye kichwa Sollicitudo rei socialis (Hangaikio kwa Jamii ya Watu.) Kwa kutiwa wasiwasi na hali za ulimwengu, hasa kulingana na rai ya mambo ya uchumi, papa alishikilia kwamba kanisa linapaswa kuhisi wajibu wa kuwaondolea umaskini wale wanaoteseka. Jinsi gani? “Kwa kukabiliwa na visa vya uhitaji,” papa akatangaza, “mmoja hawezi kuvipuuza kwa kupendelea madoido mengi mno ya kanisa na vifaa vya bei kubwa kwa ajili ya ibada ya kimungu; bali ingeweza kuwa kuna wajibu wa kuuza bidhaa hizo ili kuwaandalia chakula, kinywaji, nguo na mahali pa kuishi wale wasio na vitu hivyo.”
Hata hivyo, akitoa maelezo juu ya barua ya papa, mstadi wa Vatikani Domenico Del Rio, alionelea hivi katika La Repubblica: “Ni wazi kwamba sasa watu watakuwa wakingoja kuona . . . papa mwenyewe, na wale wanaomzunguka, wakiweka kielelezo. Basilika ya Vatikani na mabasilika ya Roma yamejaa ‘vifaa vya bei kubwa,’ labda pia yamejaa ‘madoido ya kanisa yaliyo mengi mno.”’ Hata hivyo, kulingana na gazeti Fortune, “maafisa wa Vatikani wanachukizwa sana na lile wazo la kukubali kuachilia hata vitu vilivyo na thamani inayolingana na chungu kimoja cha muundo wa Kigiriki ili wachange pesa.”
Wakati Yesu alipoagiza mtawala mmoja tajiri ‘auze mali zake zote na kugawanya pesa hizo kwa maskini,’ mwanamume huyo tajiri hakuwa na nia ya kufanya hivyo. Bali, yeye ‘alienda akiwa na kihoro, kwa maana yeye alikuwa na mali nyingi.’ Kwa kufaa, Yesu alionya hivi: “Hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.”—Marko 10:21, 22, NW; Mathayo 6:21, UV.