‘Mlinunuliwa kwa Bei’
“Mulinunuliwa kwa bei; basi tukuzeni Mungu katika mwili wenu.”—1 WAKORINTHO 6:20, ZSB.
1, 2. (a) Nini ilifungua “njia za kutoka mautini”? (b) Nini ilipaswa kufanywa ili dhabihu ya Kristo ihalalishwe kisheria, kama ilivyoonyeshwa na nini kimbele?
“MUNGU kwetu sisi ni Mungu wa kuokoa,” alisema mtunga zaburi, “na njia za kutoka mautini zina YEHOVA Bwana.” (Zaburi 68:20) Dhabihu ya Yesu Kristo ilifungua njia hiyo. Lakini ili dhabihu hiyo ihalalishwe kisheria, Kristo alipaswa yeye binafsi kuonekana mbele ya Mungu mwenyewe.
2 Hili lilionyeshwa kimbele katika Siku ya Upatanisho wakati kuhani mkuu alipoingia Patakatifu Zaidi. (Walawi 16:12-15) “Lakini,” akaandika mtume Paulo, “Kristo akiisha kuja, aliye kuhani mkuu . . . , wala si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele. Kwa sababu Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu.”—Waebrania 9:11, 12, 24.
Uwezo wa Damu
3. (a) Damu inaonwaje na waabudu wa Yehova, na kwa nini? (b) Nini inaonyesha kwamba damu ina uwezo wa halali kisheria kufanya upatanisho wa dhambi?
3 Damu ya Kristo ina daraka gani katika wokovu wetu? Tangu siku ya Noa, waabudu wa kweli wameona damu kuwa takatifu. (Mwanzo 9:4-6) Damu ina sehemu ya maana sana katika kuendelea kwa uhai, kwa kuwa Biblia yasema kwamba “uhai wa mwili u katika hiyo damu.” (Walawi 17:11) Kwa hiyo Sheria ya Kimusa ilitaka kwamba wakati mnyama alipodhabihiwa, damu yake imwagwe mbele ya Yehova. Nyakati nyingine damu iliwekwa pia juu ya pembe za madhabahu. Kwa wazi, uwezo wa dhabihu wa kufanya upatanisho wa dhambi ulikuwa katika damu yayo. (Walawi 8:15; 9:9) “Katika Torati karibu vitu vyote husafishwa kwa damu, na pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo.”—Waebrania 9:22.
4. (a) Kusudi gani lilitimizwa katika kuzuia kwa Mungu utumizi wa damu? (b) Nini kilikuwa cha maana kuhusu njia ambayo Yesu aliuawa?
4 Haishangazi, basi, kwamba chini ya Sheria, utumizi wowote mbaya wa damu uliadhibishwa kwa kifo! (Walawi 17:10) Sisi sote tunajua kwamba wakati kitu kinafanywa kisipatikane kwa urahisi, au utumizi wacho unazuiwa sana, thamani yacho inaongezeka. Kuweka kwa Yehova kizuizi juu ya utumizi wayo kulihakikisha kwamba damu ingeonwa, si kuwa kitu cha thamani ya kawaida, bali kuwa cha hali ya juu sana, chenye thamani. (Matendo 15:29; Waebrania 10:29) Hii ilipatana na kusudi tukufu ambalo damu ya Kristo ingetimiza. Kwa kufaa, yeye alikufa katika njia ambayo ilifanya damu yake imwagike. Kwa hiyo, ilikuwa wazi kwamba Kristo hakudhabihu mwili wake wa kibinadamu tu bali alimwaga nafsi yake, alidhabihu uhai wake wenyewe akiwa binadamu mkamilifu! (Isaya 53:12) Kristo hakupoteza haki yake iliyo halali kisheria kwa uhai huo kwa sababu ya kutokamilika, kwa hiyo damu yake iliyomwagwa ilikuwa na thamani kubwa na ingeweza kutolewa mbele ya Mungu kwa ajili ya kulipia dhambi za ainabinadamu.
5. (a) Yesu alipeleka nini mbinguni, na kwa nini? (b) Ilionekanaje wazi kwamba Mungu alikubali dhabihu ya Yesu?
5 Kristo hangeweza kuchukua damu yake ya halisi mbinguni. (1 Wakorintho 15:50) Badala yake, alichukua kile ambacho damu hiyo ilikifananisha: thamani iliyo halali kisheria ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu. Usoni pa Mungu, angeweza kufanya toleo la kirasmi la uhai huo ukiwa ukombozi badala ya ainabinadamu wenye dhambi. Kibali cha Mungu kwa dhabihu hiyo kikawa wazi katika Pentekoste ya 33 W.K., wakati roho takatifu ilikuja juu ya wanafunzi 120 katika Yerusalemu. (Matendo 2:1-4) Sasa ni kama Kristo alikuwa mwenye jamii ya binadamu kwa kuwanunua. (Wagalatia 3:13; 4:5; 2 Petro 2:1) Kwa sababu hiyo, manufaa za ukombozi zingeweza kumiminikia ainabinadamu.
Wa Kwanza Wanaonufaika na Ukombozi
6. Mungu amefanya mipango gani ili manufaa za ukombozi wa Yesu zitumike?
6 Hata hivyo, hiyo haikumaanisha kwamba ainabinadamu wangepewa ukamilifu wa kimwili mara moja, kwa sababu kama asili yenye dhambi ya mwanadamu haingeshindwa, ukamilifu wa kimwili haungewezekana. (Warumi 7:18-24) Hali yenye dhambi ingeshindwaje na lini? Mungu alipanga kwanza ili 144,000 walio ‘makuhani wa kimbingu kwa Mungu wetu watawale wakiwa wafalme juu ya dunia’ pamoja na Kristo Yesu. (Ufunuo 5:9, 10, NW; 7:4; 14:1-3) Kupitia hao manufaa za ukombozi zitatumika hatua kwa hatua kwa ainabinadamu kwa kipindi cha miaka elfu.—1 Wakorintho 15:24-26; Ufunuo 21:3, 4.
7. (a) Agano jipya ni nini, nani ni washirika walo, na linatumikia kusudi gani? (b) Kwa nini kifo kilipasa kutukia ili agano jipya liwezekane, na damu ya Yesu inatimiza sehemu gani?
7 Kuongoza kwenye hilo, wale wafalme-kuhani 144,000 ‘wananunuliwa katika wanadamu.’ (Ufunuo 14:4) Hilo linatimizwa kwa njia ya “agano jipya.” Agano hili ni mkataba kati ya Yehova Mungu na Israeli ya kiroho ya Mungu ili washirika walo watumike wakiwa wafalme na makuhani. (Yeremia 31:31-34; Wagalatia 6:16; Waebrania 8:6-13; 1 Petro 2:9) Lakini, je! agano kati ya Mungu na mwanadamu asiyekamilika lawezekanaje? Paulo aeleza hivi: “Maana agano la urithi [kati ya Mungu na wanadamu wasiokamilika] lilipo, lazima iwepo mauti yake aliyelifanya. Kwa maana agano la urithi lina nguvu palipotukia kufa kwa mtu; kwa kuwa halina nguvu kabisa, akiwa yu hai yeye aliyelifanya.”—Waebrania 9:16, 17.
8, 9. Ukombozi unahusianaje na agano jipya?
8 Kwa sababu hiyo, dhabihu ya ukombozi ni msingi wa agano jipya, ambalo kwalo Yesu ndiye mpatanishi. Paulo aliandika hivi: “Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake.” (1 Timotheo 2:5, 6) Maneno hayo yanatumika hasa kwa wale 144,000, ambao agano jipya limefanywa pamoja nao.
9 Mungu alipofanya agano pamoja na Waisraeli wa kimnofu, halikuhalalishwa mpaka damu ya mnyama ilipotolewa katika dhabihu. (Waebrania 9:18-21) Vivyo hivyo, ili agano jipya liwe lenye kutenda kazi, Kristo alipaswa kutoa ‘damu ya agano.’ (Mathayo 26:28; Luka 22:20) Huku Kristo akitenda akiwa Kuhani Mkuu na pia “mjumbe [mpatanishi, NW] wa agano jipya”, Mungu anatumia thamani ya damu ya Yesu kwa wale wanaoletwa ndani ya agano jipya, akiwahesabia kihalali uadilifu wa kibinadamu. (Waebrania 9:15; Warumi 3:24; 8:1, 2) Mungu basi aweza kuwaingiza katika agano jipya ili wawe wafalme-kuhani wa kimbingu! Akiwa Mpatanishi na Kuhani Mkuu wao, Yesu anawasaidia kudumisha msimamo safi mbele ya Mungu.—Waebrania 2:16; 1 Yohana 2:1, 2.
Kukusanya Vitu Vilivyopo Duniani
10, 11. (a) Ukombozi unapanukaje kuwapita Wakristo wapakwa mafuta? (b) Umati mkubwa ni akina nani, nao wana msimamo gani pamoja na Mungu?
10 Je! ni Wakristo wapakwa mafuta tu ambao wanaweza kupata kufunguliwa kwa ukombozi, msamaha wa dhambi zao? La, Mungu anapatanisha kwake vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu iliyotoka juu ya mti wa mateso, kama vile Wakolosai 1:14, 20 yaonyesha. Hilo linatia ndani vitu vilivyomo mbinguni (wale 144,000) na pia vitu vilivyopo duniani. Hivi vya pili ni wale watakaopata uhai wa kidunia, wanadamu watakaoonea shangwe uhai mkamilifu katika Paradiso duniani. Kumekuwa bidii nyingi sana hasa tangu 1935 ili kukusanya watu hao. Ufunuo 7:9-17, NW wawaeleza kuwa “umati mkubwa” ambao una deni kwa Yehova na Mwana-Kondoo kwa wokovu wao. Wao bado wanahitaji kuokoka “dhiki kubwa” na ‘kuongozwa kwenye chemchemi za maji yenye uhai,’ kwa kuwa Ufunuo 20:5 waonyesha kwamba watu hao watakuja kuwa hai kikamili, wawe na uhai mkamilifu wa kibinadamu, mwishoni mwa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu. Wale ambao kisha wanapita mtihani wa mwisho katika hali yao kamilifu ya kibinadamu watajulishwa rasmi kuwa waadilifu kwa ajili ya uhai wa milele duniani.—Ufunuo 20:7, 8.
11 Hata hivyo, kwa njia ya utangulizi, umati mkubwa tayari “wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:14) Kristo hatendi akiwa Mpatanishi wa agano jipya kuwaelekea, hata hivyo wao hufaidika kutokana na agano hili kupitia kazi ya Ufalme wa Mungu. Hata hivyo, Kristo hutenda kuwaelekea, akiwa Kuhani Mkuu, ambaye kupitia yeye Yehova aweza kutumia na atumia ukombozi kwa kadiri ambayo wanajulishwa rasmi sasa kuwa rafiki za Mungu. (Linganisha Yakobo 2:23.) Wakati wa Mileani, wao kwa taratibu ‘watawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu [mpaka hatimaye wao] hata waingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.’—Warumi 8:21.
12. Mungu alishughulikaje na wanaume waaminifu kabla ya nyakati za Ukristo?
12 Kuhusu msimamo wao pamoja na Mungu, ingeweza kuonekana ni kama wale wa umati mkubwa wanatofautiana kidogo na waabudu wa kabla ya Ukristo. Hata hivyo, Mungu alishughulika na hao wa pili akitazamia uandalizi wa ukombozi wa wakati ujao. (Warumi 3:25, 26) Wao walionea shangwe msamaha wa dhambi zao kwa muda tu. (Zaburi 32:1, 2) Badala ya kuwaondolea kabisa ‘kutokujiona tena kuwa na dhambi,’ dhabihu za wanyama zilitokeza “kumbukumbu la dhambi.”—Waebrania 10:1-3.
13. Sisi tuna faida gani kuzidi watumishi wa Mungu wa kabla ya Ukristo?
13 Ni tofauti na Wakristo wa kweli leo. Wao huabudu kwa msingi wa ukombozi ambao umelipwa! Kupitia Kuhani Mkuu wao, wao ‘hukaribia kiti cha neema [fadhili zisizostahiliwa, NW] kwa ujasiri.’ (Waebrania 4:14-16) Kupatanishwa na Mungu si jambo linalotumainiwa kuja kusitawishwa lakini ni uhalisi wa kisasa! (2 Wakorintho 5:20) Wanapokosea, wanaweza kupokea msamaha wa kweli. (Waefeso 1:7) Wao huonea shangwe dhamiri ambayo imesafishwa kikweli. (Waebrania 9:9; 10:22; 1 Petro 3:21) Baraka hizi ni kitangulizi cha uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu ambao watumishi wa Yehova wataonea shangwe wakati ujao.
Kina cha Hekima na Upendo wa Mungu
14, 15. Ukombozi unakaziaje hekima ya Yehova isiyochunguzika, na hata pia uadilifu na upendo wake?
14 Ukombozi ni zawadi iliyo ajabu kama nini kutoka kwa Yehova! Unaeleweka kwa urahisi, hata hivyo ni wa maana inayotosha kuwasha kicho katika akili yenye kusababu. Pitio letu la vitendo vya ukombozi limegusa mambo ya juu juu tu. Hata hivyo, tunapaaza sauti pamoja na mtume Paulo hivi: “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani!” (Warumi 11:33) Hekima ya Yehova inaonyeshwa kwa vile aliweza kuokoa ainabinadamu na kutetea enzi kuu yake pia. Kwa njia ya ukombozi, “haki [uadilifu, NW] ya Mungu imedhihirika . . . Mungu amekwisha kumweka [Kristo] awe upatanisho kwa njia ya imani katika damu yake.”—Warumi 3:21-26.
15 Hakuna uchambuzi wowote unaoweza kuwekwa dhidi ya Mungu kwa ajili ya kusamehe dhambi zilizotendwa wakati uliopita na waabudu wa kabla ya Ukristo. Zaidi ya hayo, hakuna uchambuzi wowote unaoweza kuwekwa dhidi ya Yehova kwa ajili ya kuwajulisha rasmi wapakwa mafuta kuwa waadilifu wakiwa wana wake au umati mkubwa kuwa rafiki zake. (Warumi 8:33) Kwa gharama kubwa kwake mwenyewe, Mungu amekuwa halali, au mnyofu, kikamilifu katika shughuli zake, akikanusha kabisa dai la uongo la Shetani kwamba Yehova ni mtawala asiye haki! Vilevile upendo wa Mungu usio wa ubinafsi kwa ajili ya viumbe vyake umeonyeshwa kwa kadiri isiyoweza kutiliwa shaka.—Warumi 5:8-11.
16. (a) Ukombozi huandaaje kujibiwa kwa suala la ukamilifu wa watumishi wa Mungu? (b) Ukombozi unatupa nini kuwa msingi wa imani katika ulimwengu mpya unaokuja wenye uadilifu?
16 Njia ambayo kwayo ukombozi uliandaliwa ilijibu pia masuala yaliyotia ndani ukamilifu wa watumishi wa Mungu. Utiifu wa Yesu pekee ulitimiza hilo. (Mithali 27:11; Warumi 5:18, 19) Lakini ongeza kwa hilo mwendo wa maisha ya Wakristo 144,000 ambao, ijapokuwa upinzani wa Shetani, wanabaki waaminifu mpaka kifo! (Ufunuo 2:10) Ukombozi unafanya iwezekane kwa hawa kupokea kama thawabu yao kutokufa—uhai usioweza kuharibiwa! (1 Wakorintho 15:53; Waebrania 7:16) Hilo linafanya dai la Shetani kwamba watumishi wa Mungu si wenye kuaminika liwe la upuzi! Pia ukombozi umetupa sisi msingi thabiti kwa ajili ya imani katika ahadi za Mungu. Tunaweza kuona mjengo wa wokovu ‘ulioimarishwa kihalali’ kupitia dhabihu ya ukombozi. (Waebrania 8:6, NW) Kwa hiyo ulimwengu mpya wa uadilifu umehakikishwa!—Waebrania 6:16-19.
Usikose Kusudi Lake
17. (a) Wengine huonyeshaje kwamba wamekosa kusudi la ukombozi? (b) Nini yaweza kutuchochea kubaki safi kiadili?
17 Ili kunufaika kutokana na ukombozi, inahitajiwa kabisa kwamba mtu atwae maarifa, azoee imani, na aishi kulingana na viwango vya Biblia. (Yohana 3:16; 17:3) Ingawaje, kwa kulinganisha ni wachache ambao wana nia ya kufanya hivyo. (Mathayo 7:13, 14) Hata miongoni mwa Wakristo wa kweli, huenda wengine ‘wakapokea fadhili zisizostahiliwa za Mungu na kukosa kusudi lazo.’ (2 Wakorintho 6:1, NW) Kwa mfano, miaka iliyopita maelfu wametengwa na ushirika kwa mwenendo mbaya wa ngono. Ni aibu kama nini kulingana na yale Yehova na Kristo wametufanyia! Je! uthamini kwa ajili ya ukombozi haupasi kusukuma mtu aepuke ‘kusahau kule kutakaswa dhambi zake za zamani’? (2 Petro 1:9) Kwa kufaa, basi, Paulo akumbusha Wakristo hivi: “Mulinunuliwa kwa bei; basi tukuzeni Mungu katika mwili wenu.” (1 Wakorintho 6:20, ZSB) Kukumbuka hilo kutatupa kichocheo chenye nguvu kubaki safi kiadili!—1 Petro 1:14-19.
18. Mkristo anayeanguka katika dhambi nzito anawezaje bado kujifaidi na ukombozi?
18 Vipi ikiwa mtu amekwisha anguka katika dhambi nzito? Yeye anapaswa kufaidika na msamaha unaofanywa uwezekane na ukombozi, akipokea msaada kutoka kwa waangalizi wenye upendo. (Yakobo 5:14, 15) Hata ikiwa nidhamu thabiti inahitajiwa, Mkristo aliyetubu hapaswi kulegea chini ya usahihisho kama huo. (Waebrania 12:5) Sisi tuna ahadi hii ya ajabu ya Kibiblia: “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”—1 Yohana 1:9.
19. Mkristo anaweza kuonaje matendo yake mabaya yaliyotendeka kabla ya kujifunza ukweli?
19 Nyakati nyingine Wakristo wanavunjika moyo isivyohitajika kwa sababu ya mwenendo mbaya wa zamani. “Kabla ya kuja ndani ya ukweli,” aliandika ndugu mmoja aliyevunjika moyo, “mke wangu nami tuliambukizwa na uvimbe mwingi wenye majimaji katika viungo vya uzazi. Nyakati nyingine tunajiona kuwa wachafu, kama kwamba ‘hatufai’ kuwa katika tengenezo safi la Yehova.” Ni kweli, hata baada ya kuwa Wakristo, wengine wangeweza kuvuna kadiri fulani ya mateso kwa sababu ya makosa ya zamani. (Wagalatia 6:7) Hata hivyo, hakuna sababu yoyote kujiona kuwa si safi machoni pa Yehova ikiwa mtu ametubu. “Damu yake Kristo” inaweza ‘kusafisha dhamiri zetu na matendo mafu.’—Waebrania 9:14.
20. Imani katika ukombozi inawezaje kumwondolea Mkristo hatia isiyohitajiwa?
20 Ndiyo, imani katika ukombozi yaweza kusaidia kutuondolea mizigo isiyohitajiwa ya hatia. Dada mmoja kijana alikiri hivi: “Nimekuwa nikishindana kwa miaka 11 sasa na tabia mbaya ya kupiga punyeto. Karibu niache kundi wakati mmoja, nikiona kwamba Yehova hangetaka kamwe mtu aliyechukiza sana kunajisi kundi lake.” Ingawaje, ni lazima tukumbuke, Yehova ni ‘mwema na tayari kusamehe’ ikiwa tunashindana kwa bidii dhidi ya uovu, bila kujiachilia utushinde!—Zaburi 86:5.
21. Ukombozi unapasa kuathirije maoni yetu juu ya wale wanaotuudhi?
21 Ukombozi pia wapasa kuwa na uvutano juu ya jinsi tunavyoshughulika na wengine. Kwa mfano, unaitikiaje Mkristo mwenzi anapokuudhi? Je! unanyosha msamaha kama wa Kristo kwa hiari? (Luka 17:3, 4) Je! wewe ni ‘mwenye huruma, ukisamehe wengine kama na Mungu katika Kristo alivyokusamehe wewe’? (Waefeso 4:32) Au una mwelekeo wa kuweka kinyongo moyoni au kulea chuki? Hakika hiyo ingekuwa ni kukosa kusudi la ukombozi.—Mathayo 6:15.
22, 23. (a) Ukombozi unapasa kuwa na matokeo gani juu ya miradi yetu na mtindo-maisha? (b) Wakristo wote wapaswa kufanya azimio gani kuhusu ukombozi?
22 Mwisho, uthamini wa ukombozi unapasa kuwa na matokeo ya kina kirefu kuhusu miradi yetu na mtindo-maisha. Paulo alisema hivi: “Mulinunuliwa kwa bei; musiwe watumwa wa watu.” (1 Wakorintho 7:23, ZSB) Je! mahitaji ya kiuchumi—nyumba, kazi, chakula, nguo—bado ndiyo kitovu cha maisha yako? Au unatafuta Ufalme kwanza, ukiweka imani katika ahadi ya Mungu ya kukuandalia? (Mathayo 6:25-33) Je! ungeweza kumtumikia mwajiri wako lakini ukose kuwa na wakati wa kutosha kwa ajili ya utendaji wa kitheokrasi? Kumbuka, Kristo “alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu ili . . . kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema.”—Tito 2:14; 2 Wakorintho 5:15.
23 ‘Shukrani kwa Mungu kwa njia ya Yesu Kristo’ kwa ajili ya zawadi hii iliyo bora mno—ukombozi! (Warumi 7:25, HNWW) Tusikose kamwe kusudi la ukombozi bali tuukubali uwe nguvu ya kweli katika maisha zetu. Katika mawazo, katika maneno, na katika matendo, na tumtukuze Mungu sikuzote, kwa shukrani tukikumbuka kwamba tumenunuliwa kwa bei.
Maswali ya Kupitia
◻ Kwa nini damu inaonwa kuwa takatifu, na damu ya Kristo ilitolewaje mbele ya Yehova mbinguni?
◻ Damu ya Yesu ilitimiza sehemu gani katika kuthibitisha agano jipya?
◻ Wapakwa mafuta na umati mkubwa wanafaidikaje na ukombozi?
◻ Tunaweza kuonyeshaje kwamba hatujakosa kusudi la ukombozi?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Uwezo wa dhabihu wa kufanya upatanisho wa dhambi umo katika damu ya uhai wayo
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mtu anayethamini msamaha wa Mungu ana nia ya kunyoshea wengine msamaha