Vijana Je! Mtaupita Mtihani wa Uaminifu-Mshikamanifu wa Kikristo?
“HUFIKIRII mwenendo usio wa adili kuwa ni kukosa uaminifu-mshikamanifu. Unaona raha tu. Ni kweli kwamba wajua ya kuwa kama wazazi wako au wazee wangegundua, jambo hilo lingeleta mvunjiko wa moyo na matatizo chungu nzima. Lakini unapokuwa ukiona raha, unafungia kabisa mawazo yote hayo.”
Kijana mwanamume aliyenukuliwa sasa hivi alikuwa amefanya zoea la siri la uasherati. Alikuwa ameishi maisha maradufu, akidanganya wazazi wake na kundi la Kikristo. Wakati huo hakung’amua kwamba alikuwa akishindwa mtihani fulani wa uaminifu-mshikamanifu wa Kikristo.
Maelfu ya vijana Wakristo wameshindwa mitihani kama hiyo ya uaminifu-mshikamanifu. Na si ajabu! Kwani, Shetani Ibilisi ‘anafanya vita’ pamoja na watu wa Mungu, akifanya yote awezayo kuvunja uaminifu-mshikamanifu wao. (Ufunuo 12:17) Hasa amefanya vijana wawe shabaha ya ‘vitendo vyake vya kiufundi.’ (Waefeso 6:11, Kingdom Interlinear) Hivyo huwa inahitaji jitihada halisi na kupiga moyo konde ili kubaki mwaminifu-mshikamanifu.
Uaminifu-mshikamanifu ni nini hasa? Katika Maandiko ya Kiebrania, neno la lugha ya awali kwa “uaminifu-mshikamanifu” laonyesha ushikamano wenye upendo kwa mtu fulani kwa kutazamia kusudi fulani. (Zaburi 18:25) Halielezi juu ya kifungo fulani dhaifu kiwezacho kuvunjwa kwa urahisi bali ushikamano ubakio thabiti mpaka kusudi lao kuhusiana na mtu huyo litimizwe. Katika Maandiko ya Kigiriki, neno la lugha ya awali kwa “uaminifu-mshikamanifu” lina wazo la utakatifu, uadilifu, au kicho.
Hivyo uaminifu-mshikamanifu wahusisha uhusiano ufaao pamoja na Mungu. Waefeso 4:24, NW, watuambia ‘tuvae utu mpya ulioumbwa katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’ Je! wewe wataka kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova? Basi ni lazima usitawishe ushikamano wenye uaminifu kwake, kifungo kisichovunjika, kupiga moyo konde kumfurahisha katika njia zako zote. Ni lazima ushikamane na viwango vya uadilifu vya Yehova—hata kama kufanya vinginevyo ni jambo lenye ushawishi kadiri gani!
Misongo ya Kukosa Uaminifu-Mshikamanifu
Kwa kupongezeka, vijana walio wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kubaki wakiwa waaminifu-washikamanifu, na tokeo huwa kuonea shangwe dhamiri safi. Hata hivyo mtume Paulo alitoa unabii wa kwamba wakati wa “siku za mwisho,” kukosa uaminifu-mshikamanifu kungekuwa kitabia cha watu kwa ujumla. (2 Timotheo 3:1, 2, NW) Jambo la msiba ni kwamba, vijana fulani Wakristo wameruhusu ulimwengu huu usio na uaminifu-mshikamanifu ‘uwasonge ndani ya mfinyango wao wenyewe.’ (Warumi 12:2, Phillips) Shetani ametimizaje jambo hilo?
Msongo wa marika ni chombo kimoja chenye matokeo cha Shetani. Watu walio wengi hutaka kufikiriwa vema na wengine, na Shetani ajua jinsi ya kutumia vibaya tamaa hiyo ya kiasili. Wakitaka kuonwa kuwa watu wasio na kasoro, vijana fulani Wakristo wamejitia katika maongezi yasiyofaa, mwenendo wa kukosa adili, kuvuta sigareti, ulevi—hata utumizi mbaya wa dawa za kulevya—yote hayo ili tu wakubaliwe na marika wao.
Shetani atutaka ‘tuenende katika tamaa za miili yetu, tukiyatimiza mapenzi ya mwili.’ (Waefeso 2:3) Ajua vema jinsi mvuto wa tamaa ya ngono uwezavyo kuwa na nguvu wakati wa “uzuri wa ujana.” (1 Wakorintho 7:36) Naye ataka wewe ujiachilie kushindwa na tamaa hizo. Vijana fulani Wakristo hucheza-cheza katika mikono yake bila kujua kwa kutazama fasihi za umalaya, sinema, na video au kuzoea kupiga punyeto. Mambo hayo, nayo, huongoza mara nyingi kwenye vitendo vizito vya kukosa uaminifu-mshikamanifu. Je! ulimwengu wa Shetani ‘umekusonga wewe ndani ya mfinyango wao’ katika mengine ya maeneo hayo?
Kuendesha Maisha Maradufu
Ingawa kutenda kosa zito kama uasherati ni jambo zito sana lenyewe, vijana fulani huongezea magumu yao. Wao ni kama “watu wasio wa ukweli,” wasemwao kwenye Zaburi 26:4, NW, “wafichao kile walicho.” Vijana wa jinsi hiyo huendesha maisha maradufu, wakitenda kwa njia moja wakiwa katika uandamani wa wazazi wao au Wakristo wengine wakomavu na kwa njia nyingine wawapo katika uandamani wa marika wao.
Hata hivyo, kuendesha maisha maradufu ni kujishinda na ni hatari. Vitendo vyenye makosa visivyozuiwa huwa karibu sikuzote vyaongoza kwenye vitendo vingine vyenye makosa. Na ingawa huenda dhamiri ya mtu ikasumbuka mara ya kwanza, kadiri mtu azidivyo kuwa katika kosa, ndivyo dhamiri yake ipunguzavyo kusumbuliwa na kosa. Mtu aweza kwa uhalisi ‘kuacha kuhisi maumivu’ juu ya kufanya kosa.—Waefeso 4:19, Kingdom Interlinear.
Kwenye hatua hii huwa ni vigumu kabisa mtu kuungama kosa lake na kupata msaada. Huwa hivyo hasa ikiwa vijana wengine Wakristo wanahusika katika kosa hilo. Hisia yenye kuongozwa vibaya ya uaminifu-mshikamanifu mara nyingi huwa na nguvu nyingi zaidi. Yule kijana aliyenukuliwa mwanzoni alieleza hivi: “Unang’amua unalofanya, nawe wajua kwamba ni kosa. Ili watu wale wengine mmoja mmoja wahusikao wasiingie katika matata, wewe wakubali kutoambia mtu yeyote.”
Ingawa huenda mtu ‘akaficha kile alicho’ kutoka kwa wazazi wake au kundi, hawezi kujificha kutoka kwa Yehova. “Hakuna kiumbe cho chote kilichofichika mbele ya Mungu; kila kitu kimefunuliwa wazi mbele ya macho yake. Kwake, sisi sote tutapaswa kutoa hoja ya matendo yetu.” (Waebrania 4:13, HNWW) Biblia yatuhakikishia hivi: “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa.” (Mithali 28:13) Baada ya muda kosa hilo litafichuliwa. Mtu hawezi kamwe kumzidi Yehova akili. Mithali 3:7 yasema: “Usiwe mwenye hekima machoni pako; mche BWANA [Yehova, NW], ukajiepushe na uovu.” Kumbuka, pia, kwamba “macho ya BWANA [Yehova, NW] yako kila mahali; yakimchunguza mbaya na mwema.”—Mithali 15:3.
Hivyo kijana aliyetangulia kutajwa, pamoja na wengine kadhaa waliohusika katika kosa la siri, aligunduliwa, na yeye na waandamani wake wakalazimika kuondoshwa katika kundi la Kikristo. Baadaye walipona kiroho na kurudishwa. Na bado, hiyo ni njia ngumu kama nini ya kujifunza maana ya uaminifu-mshikamanifu!
‘Kunyoosha Mambo’ Pamoja na Mungu
Namna gani ikiwa tayari mtu amethibitika kuwa mkosa uaminifu-mshikamanifu kwa njia fulani, labda kwa kufanya kitendo fulani chenye kosa? Ni rahisi kujipumbaza na kukana uhitaji wa kusahihisha mambo. Kijana mmoja aliyehusika katika uasherati kwa siri alisema hivi: “Niliongezea huduma yangu ya shambani, nikifikiri kwamba jambo hilo lingefunika kosa hilo kwa njia fulani.” Vivyo hivyo taifa la Israeli lenye kupotoka lilijaribu kumtuliza Yehova kwa dhabihu. Lakini Yehova alikataa ujitoaji huo wa kinafiki. Aliwahimiza hivi: “Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya.” Yehova angekubali dhabihu zao baada tu ya wao ‘kusemezana naye’ (‘kunyoosha mambo naye,’ NW). Hivyo ndivyo ilivyo leo kwa yeyote ambaye huenda akahusika katika kosa.—Isaya 1:11, 15-18.
Mtu hawezi kunyoosha mambo pamoja na Yehova kwa kutolea kijana wa rika lake tu usiri wake. Kwanza, si sikuzote ambapo marika hutoa msaada ulio bora kabisa, kwa kuwa mara nyingi wao huwa wamepungukiwa jinsi ile ile katika ujuzi maishani. La maana zaidi, wao hawawezi kusamehe dhambi yako. Ni Mungu peke yake awezaye kufanya hivyo. Hivyo basi ‘funua [mwaga, NW] moyo wako’ kwake katika ungamo. (Zaburi 62:8) Ingawa huenda wewe ukaaibika kwa kina kirefu juu ya mwenendo wako, uwe na uhakikisho wa kwamba Yehova ‘husamehe kabisa.’—Isaya 55:7.
Utahitaji msaada wa ziada. “Wajulishe wazazi wako, wajulishe wazee moja kwa moja—pale pale mwanzoni,” ahimiza Mkristo kijana mmoja aliyenufaika kutokana na msaada wa jinsi hiyo. Ndiyo, wazazi wako labda wamo katika hali nzuri ya kuweza kukusaidia. ‘Wape moyo wako,’ ukiwajulisha kadiri kamili ya matatizo yako. (Mithali 23:26) Wao waweza kukupangia upokee usaidizi zaidi kutoka kwa wazee wa kundi wakati uhitajiwapo kabisa.—Yakobo 5:14, 15.
Kudhihirisha Uaminifu-Mshikamanifu wa Kweli—Jinsi Gani?
Bila shaka, ingekuwa afadhali kabisa kutoanguka katika mwenendo wa kukosa uaminifu-mshikamanifu pale mwanzoni. Zaburi 18:25 yatuambia hivi: “Kwa mtu mwenye fadhili [uaminifu-mshikamanifu, NW] utakuwa mwenye fadhili [uaminifu-mshikamanifu, NW]; kwa mkamilifu utajionyesha kuwa mkamilifu.” Yehova huwabariki sana wale wadumishao viwango vya juu vya mwenendo kwa uaminifu-mshikamanifu.
Ingawa hivyo, kuna njia nyinginezo ambazo katika hizo uaminifu-mshikamanifu wako waweza kutiwa katika mtihani. Kwa kielelezo, tuseme rafiki yako ameanza kutembea katika mwendo mpotovu. Je! wewe utaacha uaminifu-mshikamanifu wenye kuongozwa vibaya kwa rafiki huyo ufunike uaminifu-mshikamanifu wako kwa Yehova? Jambo la upendo kufanya lingekuwa kumwendea rafiki huyo na kumhimiza aripoti jambo hilo kwa wazazi wake au kwa wazee. Mwambie rafiki yako kwamba ikiwa yeye hatafanya hivyo katika kipindi fulani cha kadiri inayofaa, wewe mwenyewe utalazimika kufanya hivyo. Mithali 27:5 yasema hivi: “Lawama ya wazi ni heri, kuliko upendo uliositirika.” Kwa kusaidia rafiki yako kwa njia hiyo, wadhihirisha si unyoofu tu wa urafiki wako kwake bali pia kina cha uaminifu-mshikamanifu wako kwa Yehova.
Hata kuwe na mtihani gani, imara ya kuonyesha uaminifu-mshikamanifu hutokana na kuwa na uhusiano imara wa kibinafsi pamoja na Yehova. Sala yenye maana na funzo la kibinafsi la bidii nyendelevu ni mambo ya maana sana ikiwa sisi tutaonea shangwe uhusiano wa jinsi hiyo. Kwa kupendeza, vijana wote wenye kukosa waliotajwa mapema kidogo walikiri kwamba sala zao na tabia za funzo la kibinafsi zilikuwa zimekuwa kawaida tu—na baada ya muda zikawa hazipo. Yehova alikoma kuwa mtu halisi kwao, na muda si muda mwenendo usio safi ukafuata. Je! wewe unaimarisha uhusiano wako pamoja na Yehova kwa sala na funzo la kibinafsi ili ubaki ukiwa mwaminifu-mshikamanifu?
Ni kweli kwamba nyakati fulani huenda ukashangaa kama unakosa starehe fulani. “Nyakati fulani huonekana kama kwamba walimwengu wanaona raha,” akasema kijana mwanamke mmoja. “Lakini unaswapo katika hali fulani, waweza kuona kwamba si raha hata kidogo.” Yeye alisema kutokana na aliyojionea mwenyewe, akiisha kuhusika katika ukosefu wa adili kingono, tokeo likiwa ni mimba na utoaji mimba. “Kuwa katika ukweli ni ulinzi,” sasa yeye asema hivyo—somo ambalo alijifunza kwa magumu. Zaburi 119:165 yatukumbusha kwamba “wana amani nyingi waipendao sheria [ya Mungu].”
Kwa hiyo, fanya yote uwezayo ubaki ukiwa mwaminifu-mshikamanifu. Jitahidi kujenga uhusiano wenye kudumu pamoja na Yehova. Chukia lililo baya na ushikamane sana na lililo jema. (Warumi 12:9) Zaburi 97:10 yatuambia hivi: “Enyi mmpendao BWANA [Yehova, NW], uchukieni uovu; huwalinda nafsi zao watauwa wake, na kuwaokoa na mkono wa wasio haki.” Ndiyo, wewe uliye kijana Mkristo, utanufaika kutokana na ulinzi wa Yehova na kuonea shangwe uhai wa milele ikiwa utaupita mtihani wa uaminifu-mshikamanifu wa Kikristo.