‘Wanawake Wenye Bidii Katika Bwana’
“Nisalimieni Trifaina na Trifosa, wenye bidii katika Bwana.”—WARUMI 16:12.
1. Huduma ya Yesu ya kidunia ilithibitikaje kuwa baraka kwa wanawake?
HUDUMA ya kidunia ya Yesu kwa kweli ilikuwa baraka kwa wanawake Wayahudi. Kazi ambayo alianzisha ingeleta faraja, tumaini, na fahari mpya kwa wanawake wa jamii zote. Yeye hakufuata hata kidogo mapokeo ya dini ya Kiyahudi ‘yaliyotangua neno la Mungu.’ (Mathayo 15:6) Mengi ya mapokeo hayo yalidharau haki za msingi za wanawake zilizotolewa na Mungu.
Mtazamo wa Yesu Kuelekea Wanawake
2. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba mfikio wa Yesu kuelekea wanawake ulikuwa ugeuzi mkubwa kwa nyakati hizo?
2 Kulikuwako tofauti kubwa kama nini kati ya mtazamo wa Yesu kuelekea wanawake na ule wa viongozi wa kidini Wayahudi! Kunukuu ile Encyclopaedia Judaica, hao viongozi wa kidini Wayahudi waliona wanawake kuwa “wenye pupa, wenye kunyemelea maongezi ya siri, wavivu, na wenye wivu.” Maongezi pamoja na mwanamke yalichukiza, na “ilikuwa fedheha kwa mwanachuo kuongea na mwanamke barabarani.” (Jerusalem in the Time of Jesus, ya Joachim Jeremias; linganisha Yohana 4:27.) Mengi zaidi yangeweza kusemwa juu ya mtazamo huo wenye kudharau wa viongozi wa dini ya Kiyahudi kuelekea wanawake. Lakini mambo yaliyo juu yatatosha kuonyesha jinsi njia ya Yesu kuelekea wanawake ilikuwa ugeuzi mkubwa kwa nyakati hizo.
3. Ni matukio gani wakati wa huduma ya Yesu yanaonyesha kwamba alikuwa mwenye nia ya kufunza wanawake kweli za kiroho zenye kina kirefu?
3 Yesu aandaa mfano mkamilifu wa jinsi wanaume wanaweza kuwa na uhusiano mchangamfu lakini ulio safi pamoja na wanawake. Hakuongea tu pamoja nao bali pia aliwafunza kweli za kiroho zenye kina kirefu. Kwa uhakika, mtu wa kwanza kabisa aliyemfunulia waziwazi Umesiya wake alikuwa mwanamke, na isitoshe alikuwa mwanamke Msamaria. (Yohana 4:7, 25, 26) Zaidi ya hayo, tukio linalohusu Martha na Mariamu linaonyesha kwa wazi kwamba tofauti na viongozi wa kidini Wayahudi, Yesu hakuhisi kwamba mwanamke hakuwa na haki ya kuacha masufuria na vyungu vyake kwa muda tu ili kuongeza maarifa yake ya kiroho. Pindi hiyo, Mariamu ‘alilichagua fungu lililo jema,’ kwa kuweka mambo ya kiroho kwanza. (Luka 10:38-42) Lakini miezi michache baadaye, ndugu yao akiisha kufa, ni Martha, wala si Mariamu, aliyeonyesha tamaa kubwa zaidi ya kukutana na Bwana Mkubwa. Tunasisimukaje hata leo tusomapo mazungumzo hayo yenye umaana mkubwa wa kiroho kati ya Yesu na Martha juu ya tumaini la ufufuo! (Yohana 11:20-27) Jinsi hilo lilivyokuwa pendeleo kwa Martha!
Wanawake Waliomhudumia Yesu
4, 5. Zaidi ya mitume, ni nani waliomfuata Yesu wakati wa huduma yake ya Kigalilaya, nao walimhudumiaje?
4 Yesu alikubali pia kuhudumiwa na wanawake alipokuwa akisafiri kotekote nchini. Katika usimulizi wake wa Gospeli, Marko ataja “wanawake . . . waliofuatana naye [Yesu] huko Galilaya.” (Marko 15:40, 41) Wanawake hao walikuwa nani, nao walimtumikiaje Yesu? Hatuyajui majina yao wote, lakini Luka atambulisha machache na kueleza njia ambayo walimhudumia Yesu.
5 Luka aandika hivi: “Ikawa baada ya hayo alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye, na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, na Yoana mkewe Kuza, wakili wake Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao.” (Luka 8:1-3) Yesu alikubali kuwa na wanawake hao wakimfuata na kutumia mali zao kuhudumia mahitaji ya kimwili yake na yale ya mitume wake.
6. (a) Ni nani waliofuatana na Yesu wakati wa safari yake ya mwisho kwenda Yerusalemu? (b) Ni nani walioendelea kumtegemeza Yesu wakiwa kando yake hadi kifo chake, na wengine wao walipewa thawabu jinsi gani? (c) Kulingana na mapokeo ya dini ya Kiyahudi, ni jambo gani linalotokeza kuhusu usimulizi kwenye Yohana 20:11-18?
6 Yesu alipouawa, “Palikuwa na wanawake wengi pale wakitazama kwa mbali, hao ndio waliomfuata Yesu toka Galilaya, na kumtumikia. Miongoni mwao alikuwamo Mariamu Magdalene, na Mariamu mama yao Yakobo na Yusufu.” (Mathayo 27:55, 56) Hivyo, wanawake wengi waliendelea kumtegemeza Yesu wakiwa kando yake wakati wa kifo chake. Pia yastahili kuangaliwa kwamba wanawake ndio waliokuwa mashahidi wa kwanza wa ufufuo wake. (Mathayo 28:1-10) Hilo lenyewe lilikuwa pigo kwa mapokeo ya Kiyahudi, kwa maana katika dini ya Kiyahudi wanawake walionwa kutostahili kuwa mashahidi kisheria. Ukiwa na hilo akilini, soma Yohana 20:11-18, na ujaribu kuona ile hisia-moyo ya ndani sana ambayo ni lazima Mariamu Magdalene awe alihisi wakati Bwana Mkubwa aliyefufuka alipomtokea, akamwita kwa jina lake, na kumtumia kuwa shahidi wake kuwajulisha wanafunzi wake kwamba kwa kweli alikuwa hai!
Wanawake Waaminifu Wakristo Baada ya Pentekoste
7, 8. (a) Tunajuaje kwamba wanawake walikuwako wakati roho ilipomwagwa siku ya Pentekoste? (b) Wanawake Wakristo walishirikije katika mweneo wa mapema wa Ukristo?
7 Baada ya kupaa kwa Yesu mbinguni, wanawake wenye kutii Mungu walikuwako pamoja na mitume waaminifu katika chumba cha orofani Yerusalemu. (Matendo 1:12-14) Ni wazi kwamba kulikuwamo wanawake miongoni mwa wale ambao juu yao roho takatifu ilimwagwa siku ya Pentekoste. Kwa nini? Kwa sababu Petro alipoeleza yale yaliyotukia, alinukuu Yoeli 2:28-30, NW, ambayo inataja mahususi “binti” na ‘watumishi wanawake,’ au ‘watumwa wa kike.’ (Matendo 2:1, 4, 14-18) Kwa hiyo wanawake Wakristo waliozaliwa kwa roho na kutiwa mafuta walikuwa sehemu ya kundi la Kikristo kutoka palepale penye msingi walo.
8 Wanawake walikuwa na daraka la maana, ingawa halikuwa kuu, la mweneo wa Ukristo. Mariamu, mama ya Marko na shangazi ya Barnaba, alitoa nyumba yake ambayo yaonekana ilikuwa kubwa itumiwe na kundi la Yerusalemu. (Matendo 12:12) Naye alikuwa na nia ya kufanya hivyo kulipokuwako kishindo kipya cha mnyanyaso dhidi ya Wakristo. (Matendo 12:1-5) Binti wanne wa mwevanjeli Filipo walikuwa na pendeleo la kuwa manabii wa kike Wakristo.—Matendo 21:9; 1 Wakorintho 12:4, 10.
Mtazamo wa Paulo Kuelekea Wanawake
9. Paulo alitoa shauri gani kuhusu wanawake Wakristo katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, naye alikuwa akiwatia moyo wanawake waheshimu kanuni gani ya kimungu?
9 Nyakati nyingine mtume Paulo analaumiwa kuwa mchukia wanawake asiye na imani kwao. Ni kweli Paulo ndiye aliyesisitiza kwamba wanawake wadumishe mahali pao pawafaapo ndani ya kundi la Kikristo. Katika utaratibu wa mambo ya kawaida, hawakutakiwa kufundisha kwenye mikutano ya kundi. (1 Wakorintho 14:33-35) Ikiwa mwanamke Mkristo alisema kwenye mkutano, kwa sababu hakukuwako mwanamume Mkristo yeyote au kwa sababu alitoa unabii chini ya uvutano wa roho takatifu, alihitajiwa avae kifuniko cha kichwa. Kifuniko hicho kilikuwa “ishara ya mamlaka,” uthibitisho wenye kuonekana kwamba mwanamke alitambua mpango wa Mungu wa ukichwa.—1 Wakorintho 11:3-6, 10, NW.
10. Wengine wamemlaumu mtume Paulo kwa jambo gani, lakini ni nini kinachothibitisha kwamba lawama hiyo ni ya uwongo?
10 Ni wazi kwamba Paulo aliona uhitaji wa kukumbusha Wakristo wa mapema juu ya kanuni hizi za kitheokrasi ili ‘mambo yote yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu’ kwenye mikutano ya kundi. (1 Wakorintho 14:40) Lakini je, hiyo inamaanisha kwamba Paulo alikuwa mpinga-wanawake, kama wengine wanavyodai? La, haimaanishi hivyo. Je! haikuwa Paulo ambaye katika sura ya kufunga ya barua yake kwa Warumi alipeleka salamu zenye uchangamfu kwa wanawake Wakristo tisa? Je! hakuonyesha uthamini wenye kina kirefu kwa Fibi, Priska (Prisila), Trifaina, na Trifosa, akiwaita hao wa mwisho wawili ‘wanawake wenye bidii katika Bwana’? (Warumi 16:1-4, 6, 12, 13, 15) Na ilikuwa Paulo ambaye chini ya mpulizio wa roho aliandika hivi: “Ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu.” (Wagalatia 3:27, 28) Paulo kwa wazi alipenda na kuthamini dada zake Wakristo, kutia na Lidia, ambaye alionyesha ukaribishaji-wageni unaostahili kufuatwa wakati wa kipindi cha jaribu.—Matendo 16:12-15, 40; Wafilipi 4:2, 3.
Wanawake Wenye Bidii Leo
11, 12. (a) Zaburi 68:11 inatimizwaje kwa uhalisi leo? (b) Wengi wa dada zetu hujipata katika hali gani, na kwa nini wanahitaji shauku na sala zetu?
11 Ndani ya kundi la Kikristo leo, mna wanawake Wakristo wengi ambao ni “wenye bidii katika Bwana.” Kwa hakika, takwimu huonyesha kwamba “wanawake watangazao habari [njema, NW] ni jeshi kubwa,” wakifanyiza sehemu iliyo kubwa ya jeshi la Mashahidi ambalo Yehova anatumia katika wakati huu wa mwisho. (Zaburi 68:11) Wanawake hao Wakristo wenye bidii wamejipatia sifa nzuri wengi wao wanapojitahidi kutimiza daraka lao la wake, akina mama, wapambaji-nyumba, waleta-riziki, na pia wahudumu Wakristo.
12 Idadi fulani ya dada hao wazuri wana waume wasioamini. Inawabidi kukabiliana na hali hiyo saa 24 kila siku. Wengine wamekuwa wakijitahidi kwa miaka mingi kuwa wake wazuri huku wakipatana na matakwa ya watumishi washikamanifu wa Yehova. Imekuwa si rahisi, lakini wamevumilia, sikuzote wakitumaini kwamba waume zao ‘wavutwe pasipo lile Neno’ kupitia mwenendo wao mzuri wa Kikristo. Na ni shangwe iliyoje inayoshirikiwa na familia nzima wakati mume kama huyo aitikiapo! (1 Petro 3:1, 2) Kwa sasa, dada waaminifu hao wanahitaji kwa uhakika shauku ya kidugu na sala za washiriki wale wengine wa kundi. Kama vile “roho ya upole na utulivu” ambayo wanajaribu kuonyesha ni “ya thamani kuu mbele za Mungu,” ndivyo ushikamanifu wao wa maadili ulio imara ulivyo wa thamani machoni mwetu.—1 Petro 3:3-6.
13. Kwa nini inaweza kusemwa kuhusu dada zetu mapainia kwamba wao ni ‘wanawake wenye bidii katika Bwana,’ nao wapaswa waonweje katika makundi yao mbalimbali?
13 Akina dada wanaotumikia wakiwa mapainia wanaweza kwa uhakika kusemwa kuwa “wenye bidii katika Bwana.” Wengi wao wana makao, mume, na watoto wa kutunza, kuongezea kazi yao ya kuhubiri. Wengine hufanya kazi ya nusu-wakati ili kuweza kulipia mahitaji yao ya kimwili. Yote hayo huhitaji kupanga mambo vizuri, kupiga moyo konde, kuvumilia, na kazi nyingi ya bidii. Wanawake Wakristo hao wanapaswa kuhisi upendo na tegemezo la wale ambao hali yao haiwaruhusu watoe saa za upainia kwa kazi ya kutoa ushuhuda.
14. (a) Ni mfano gani mzuri wa uvumilivu unaotajwa? (b) Ni wanawake gani wengine Wakristo wanaostahili sifa, na kwa nini? Taja mifano yoyote ya kwenu.
14 Wanawake wengine Wakristo wameonyesha uthabiti usio wa kawaida katika utumishi wa upainia. Katika Kanada, Grace Lounsbury alikuwa na mwonjo wake wa kwanza wa upainia katika 1914. Alilazimika kutoka kwenye orodha ya mapainia katika 1918 kwa sababu ya ugonjwa, lakini kufikia 1924 alirudi katika utumishi wa wakati wote. Kufikia wakati huu wa kuandika, yeye bado yuko kwenye orodha ya mapainia, ingawa ni mwenye umri wa miaka 104! Akina dada wengi wamisionari ambao katika miaka ya 1940 walikuwa wamezoezwa katika madarasa ya mapema ya Watchtower School of Gilead bado wanatumikia kwa uaminifu, ama katika eneo la umisionari ama wakiwa washiriki wa familia ya Betheli katika Brooklyn au mojawapo la matawi ya Watch Tower Society. Wanawake Wakristo wote hao, na kwa kweli akina dada wote wanaojitia katika utumishi wa Betheli, huonyesha roho ya kujidhabihu nao ni mifano mizuri. Je! sisi huwajulisha wakati wowote kwamba wanathaminiwa?
Wake za Waangalizi Wasafirio
15, 16. Ni kikundi gani cha wanawake Wakristo kinachostahili hasa sifa yetu yenye uchangamfu, na kwa nini?
15 Wake za waangalizi wasafirio hufanyiza kikundi kingine cha wanawake Wakristo ambao hustahili sifa na kitia-moyo chenye uchangamfu. Akina dada hao wapendwa wako tayari kufuata waume zao wanapoenda kutoka kundi hadi kundi, au kutoka mzunguko hadi mzunguko, ili waweze kujenga ndugu zao kiroho. Wengi wao wamejinyima raha za makao; wanalala katika kitanda tofauti kila juma, na si kitanda kizuri sikuzote. Walakini wanafurahi kukubali chochote ambacho akina ndugu wanaweza kutoa. Wao ni mfano mzuri kwa dada zao wa kiroho.
16 Pia wanawake Wakristo hao huandalia waume zao tegemezo la thamani kubwa sana kwa kadiri kubwa kama wanawake ‘waliofuatana na Yesu kumtumikia.’ (Marko 15:41) Hawawezi kutumia wakati mwingi wakiwa pamoja na waume zao, ambao sikuzote huwa “na bidii katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 15:58, HNWW) Wengine wao, kama Rosa Szumiga katika Ufaransa, ambaye aliingia utumishi wa wakati wote katika 1948, wamekuwa wakifungia mzigo waume zao na kusafiri nao kwa miaka 30 au 40. Wanakubali kujinyima kwa ajili ya Yehova na kwa ajili ya ndugu na dada zao. Wanastahili uthamini, upendo na sala zetu.
Wake za Wazee
17, 18. (a) Ni sifa gani zinazohitajiwa kwa wake za ndugu waliowekwa kwenye vyeo vya utumishi? (b) Ni kujinyima kupi ambako wake za wazee hukubali kwa ajili ya Yehova na ndugu zao, na wake wengine wanaweza kusaidiaje waume zao?
17 Alipokuwa akitaja sifa moja moja za ndugu ambao huenda wakawekwa kuwa wazee na watumishi wa huduma, mtume Paulo alitaja pia wanawake, akiandika hivi: “Vivyo hivyo wake zao na wawe wastahivu [wenye uzito, NW]; si wasingiziaji; watu wa kiasi, waaminifu katika mambo yote.” (1 Timotheo 3:11) Ni kweli, shauri hilo la ujumla linatumika kwa wanawake Wakristo wote. Lakini kulingana na muktadha, kwa wazi linapasa lifuatwe katika njia bora na wake za wazee waliowekwa katika vyeo vya utumishi.
18 Kwa furaha, hiyo ndiyo hali ya maelfu mengi ya wake za waangalizi Wakristo. Wao ni wenye kiasi katika tabia na nguo zao, wenye uzito juu ya mwendo wa Kikristo, waangalifu juu ya yale wanayosema, nao hujitahidi kwa moyo mweupe kuwa waaminifu kwa mambo yote. Wao pia hukubali kujinyima, wakikubali kwamba waume zao watumie katika mambo ya kundi wakati ambao huenda ikawa ungetumiwa pamoja nao. Wanawake Wakristo waaminifu hao hustahili upendo na kitia-moyo chetu chenye uchangamfu. Labda ndugu wengine zaidi wangeweza kufikia mapendeleo ndani ya makundi yetu mengi ikiwa wake zao wangekubali kwa unyenyekevu kujinyima jinsi hiyo kwa ajili ya hali njema ya wote.
“Wazee wa Kike” Waaminifu
19. Kwa nini “wazee wa kike” wengi huthaminiwa sana katika makundi yao, na maoni yetu kuwaelekea yapasa kuwa gani?
19 Pitio letu la habari za wanawake wanaotajwa katika Biblia limetuwezesha kuona kwamba umri wa miaka hauzuii wanawake wa imani kumtumikia Yehova. Uhakika huo ulitolewa kielezi katika visa vya Sara, Elisabeti, na Ana. Leo, kuna wanawake Wakristo wengi wenye umri wa miaka mingi ambao ni mifano mizuri ya imani na uvumilivu. Kuongezea hayo, wao wanaweza kwa busara kuwaunga mkono wazee kwa kusaidia akina dada wachanga. Wakitwaa katika maarifa yao ya muda mrefu, wanaweza kutoa shauri lenye hekima kwa wanawake wachanga, sawasawa na vile Maandiko huwaamuru wafanye. (Tito 2:3-5) Huenda ikawa nyakati nyingine kwamba dada mzee ahitaji kushauriwa mwenyewe. Ikiwa ndivyo, mzee afanyaye hivyo apaswa ‘amwonye kama mama.’ Wazee wapaswa ‘kuwaheshimu wajane’ na, ikihitajiwa, wapange msaada wa kimwili kwa ajili yao. (1 Timotheo 5:1-3, 5, 9, 10) Dada zetu wazee wapendwa wapaswa kuhisi kwa uhakika kuwa wanatakwa na kuthaminiwa.
Watawala Pamoja na Yesu
20. Ni pendeleo gani kuu ambalo limetolewa kwa wanawake Wakristo wengi, na kwa nini kondoo wengine wanaweza kufurahi kuhusu jambo hilo?
20 Ni wazi kabisa kutokana na Maandiko kwamba “hakuna upendeleo kwa Mungu” kuhusu rangi ya ngozi au hali ya kuwa kiume au kike. (Warumi 2:10, 11; Wagalatia 3:28) Na hilo ni jambo la ukweli pia katika njia ambayo Yehova achagua wale ambao watashiriki pamoja na Mwana wake katika serikali ya Ufalme. (Yohana 6:44) Kondoo wengine wa umati mkubwa wanaweza kushukuru kama nini kwamba wanawake waaminifu, kama vile Mariamu mama ya Yesu, Mariamu Magdalene, Prisila, Trifaina, Trifosa, na wengine wengi katika kundi la mapema la Kikristo, sasa wanashiriki katika utawala wa Ufalme, wakitajirisha serikali hiyo kwa ufahamu wao wa kindani juu ya hisia na maono ya wanawake! Ni mwono-mbele na hekima yenye upendo kama nini kwa upande wa Yehova!—Warumi 11:33-36.
21. Maoni yetu leo kuelekea ‘wanawake wenye bidii katika Bwana’ ni gani?
21 Sisi leo tunaweza kushiriki hisia za mtume Paulo aliposema kwa upendo na uthamini juu ya ‘wanawake walioishindania Injili pamoja nami.’ (Wafilipi 4:3) Mashahidi wa Yehova wote, wanaume na wanawake, huihesabu kuwa shangwe na pendeleo kufanya kazi pamoja na ‘jeshi kubwa la wanawake watangazao habari njema,’ naam, ‘wanawake wenye bidii katika Bwana.’—Zaburi 68:11; Warumi 16:12.
Maswali ya Kupitia
◻ Yesu alionyeshaje kwamba hakushiriki ubaguzi mbalimbali wa viongozi wa kidini Wayahudi dhidi ya wanawake?
◻ Wanawake wenye kumhofu Mungu walimhudumiaje Yesu, na wengine wao walipokea pendeleo gani kubwa?
◻ Paulo alitoa shauri gani kuhusu wanawake katika mikutano ya Kikristo?
◻ Ni aina zipi za akina dada wanaostahili shauku na tegemezo letu la pekee, na kwa nini?
◻ Tunapaswa kuwa na maoni gani kuelekea wale wote leo ambao ni ‘wanawake wenye bidii katika Bwana’?
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
Wanawake walimhudumia Yesu na mitume wake
[Picha katika ukurasa wa 18]
Wake wenye kujidhabihu wa waangalizi wasafirio na wa wazee wengine hutoa mchango wenye thamani kwa kazi ya Mungu