Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Mithali 27:23 inatoa shauri gani la msingi kwa wachungaji wa kiroho na pia kwa Wakristo kwa ujumla?
Mstari huo unasomwa hivi: “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako; na kuwaangalia sana ng’ombe zako.” (Mithali 27:23) Andiko hilo limetumiwa mara nyingi kuwatia moyo wachungaji wa kiroho waonyeshe upendezi katika na kuzijua sana hali na matatizo ya Wakristo kundini. Kitia-moyo kama hicho kinafaa, kwa kuwa Biblia inawafananisha wazee kuwa wachungaji na kundi kuwa kondoo. (Matendo 20:28, 29; 1 Petro 5:2-4) Hata hivyo, ingawa kanuni iliyo juu inatumika, mstari huo hauhusu kwa msingi wachungaji wa kiroho.
Kitabu cha Mithali kina mistari mingi ambayo peke yayo ni taarifa za shauri zenye maana, lakini Mithali 27:23 ni sehemu ya kikundi cha mistari: “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako; na kuwaangalia sana ng’ombe zako. Kwa maana mali haziwi za milele; na taji je! yadumu tangu kizazi hata kizazi? Manyasi huchukuliwa, na majani mabichi huonekana, na maboga ya milimani hukusanyika. Wana-kondoo hufaa kwa mavazi yako; na mbuzi ni thamani ya shamba: Tena yatakuwapo maziwa ya mbuzi, ya kukutosha kwa chakula chako, na chakula cha watu wa nyumbani mwako, na posho la vijakazi vyako.”—Mithali 27:23-27.
Fungu hilo la maneno lililopuliziwa roho linasifu kuwa na mtindo-maisha wenye alama ya bidii-nyendelevu, bidii ya kazi, usahili, na utambuzi wa kutegemea kwetu Yehova. Linafanya hivyo kwa kutokeza maisha ya uchungaji-kondoo ya mchungaji Mwisraeli, labda kwa kutofautisha hayo na maisha ya madoido yenye msingi wa shughuli za kibiashara na mali zenye kuchumwa kwa haraka.
“Mali,” au utajiri upatwao katika shughuli za biashara za haraka-haraka, zikitokeza umashuhuri (“taji”), zaweza kutokomea kwa urahisi, kama vile wengi waweza kushuhudia. Kwa hiyo, kuna mengi ya kusema kwa maisha rahisi, kama yale yaliyofuatwa na wachungaji wa zamani katika kutunza wanyama. Njia hiyo ya maisha haikuwa rahisi katika maana ya kuwa bila daraka lolote. Mchungaji alihitaji kuwa na ufikirio kwa kundi lake, akihakikisha kwamba kondoo walilindwa. (Zaburi 23:4) Ikiwa, alipokuwa akiwachunguza, angepata kondoo aliyekuwa mgonjwa au aliyejeruhiwa, angeweza kumpaka mafuta yenye kutuliza. (Zaburi 23:5; Ezekieli 34:4; Zekaria 11:16) Katika hali zilizo nyingi mchungaji mwenye bidii-nyendelevu aliyehangaikia makundi yake kwa moyo angeona jitihada zake zikiwa na matokeo—ongezeko la polepole la kundi lake.
Mchungaji mwenye bidii na aliye mwangalifu alikuwa na chanzo cha msaada chenye kutegemeka—Yehova. Jinsi gani? Mungu huandaa majira na mirudio ambayo hutokeza kwa kawaida manyasi ya kutosha ambayo yangeweza kulisha kundi. (Zaburi 145:16) Wakati, kwa mabadiliko ya majira, manyasi mabichi hutoweka katika mikoa ya chini, yanaweza kuwa tele kwenye sehemu zilizoinuka zaidi, ambapo mchungaji mwenye uangalifu angeweza kuhamisha wanyama wake.
Mithali 27:26, 27 inataja tokeo moja la kazi ngumu kama hiyo—chakula na mavazi. Ni kweli, maelezo hayahusu vyakula vya raha vyenye gharama nyingi au aina za kipekee, wala hazimpi mfanyakazi sababu ya kutazamia mavazi ya karibuni yenye kutungwa na mbuni mwenye kujulikana sana au ya nguo ya hali bora kabisa. Lakini ikiwa ana nia ya kujitahidi, mchungaji na familia yake wangeweza kupata maziwa kutoka kwa kundi (na hivyo kupata jibini), na pia kupata sufu ili wafume mavazi mazito na imara.
Kwa hiyo shauri: “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako” haliwahusu hasa waangalizi wa kiroho; lahusu Wakristo wote. Lakazia thamani ya kutosheka kwetu na riziki na mavazi yanayopatwa kwa kazi ya ukawaida yenye bidii-nyendelevu, tukiamini kwamba Mungu hatatuacha. (Zaburi 37:25; 2 Wathesalonike 3:8, 12; Waebrania 13:5) Kwa kulinganisha Mithali 27:23-27 na shauri kwenye Luka 12:15-21 na 1 Timotheo 6:6-11, tunaona jinsi shauri la Mungu juu ya jambo hilo limekuwa lenye kupatana. Kwa hiyo kila mmoja wetu aweza kusoma tena Mithali 27:23-27, akijiuliza, ‘Je! ninatia maneno hayo moyoni na kuyatumia katika maisha yangu ya kila siku?’
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.