Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kuwahubiri “Wafungwa Kufunguliwa Kwao” Katika Brazili
ROHO ya Yehova inafanya kazi kwa uwezo juu ya watu wake katika Brazili wakiwa wanahubiri habari njema ya kufunguliwa kwa wale walio katika utumwa wa dini bandia. (Isaiah 61:1, 2; Luka 4:18) Katika 1947 kulikuwako Mashahidi 648 tu katika nchi hiyo. Katika 1967 idadi hiyo iliongezeka kufikia 41,548. Kwa baraka ya Yehova, mapema katika 1991 imefikia kilele cha zaidi ya 302,000! Kwa kweli, ‘Mungu aliikuza.’ (1 Wakorintho 3:7) Katika mwaka wa utumishi wa 1990 peke yao, 27,068 walibatizwa.
Ukuzi kama huo ulilazimisha kufanywa kwa mzunguko mpya mmoja kila mwezi, na Majumba ya Ufalme mapya 150 yalizinduliwa katika mwaka mmoja tu. Tena, ofisi ya tawi ilinunua hektari 180 za ardhi ili kupanua vifaa vyao vya kuchapia, ambapo sasa wanachapa Biblia kwenye matbaa zao wenyewe. Hivyo Mashahidi katika Brazili wanafanya bidii ili kusaidia walio na mioyo mipole kutoka katika “Babuloni Mkubwa” kabla ya “dhiki ile iliyo kuu.”—Ufunuo 7:9, 10, 14; 18:2, 4, NW.
◻ Mhubiri wa umri wa miaka nane aliangushia mke wa mkuu wa polisi kitabu halafu, akiwa peke yake, akafanya ziara ya kurudia. Kusudi lake lilikuwa kumfanya mwanamke huyo amsomee baadhi ya hadithi kisha amwombe asimulie yale aliyoelewa kutokana na kila hadithi. Mwanamke huyo alipokuwa akimsimulia mhubiri huyo hadithi, yeye mwenyewe alianza kuthamini kitabu hicho akamwomba kijana huyo amjulishe kwa mamake. Alifanya hivyo, na sasa mwanamke huyo anaonea shangwe funzo la Biblia nyumbani kwa ukawaida.
◻ Katika 1984, Maria alichoka na unafiki alioona katika jamii, naye alikata tamaa kwa sababu ya misiba aliyosoma juu yayo iliyokuwa ikitukia ulimwenguni. Kwa hiyo alichagua mtindo-maisha wa kuonyesha mwenendo wa uasi. Ataarifu hivi: “Mradi wetu ulikuwa dhidi ya kila jambo na kila mtu. Sura yangu ilibuniwa ili kuwashtua watu tu—nguo za kiajabu-ajabu zenye rangi nyeusi-nyeusi, nywele zangu zilikuwa zimenyolewa kwa sehemu. Sikujali mume wangu, watoto wangu, wala nyumba yangu nikaanza kuvuta marijuana na kutumia kokeni ili kuepuka matatizo. Lakini hilo lilinifanya nihisi vibaya zaidi. Nililia. Niliposoma Biblia, sikuelewa. Basi nikamwomba Mungu msaada.
“Siku moja Mashahidi wawili walizuru nyumba yangu, na baada ya mazungumzo mafupi, walinitolea magazeti mawili. Nilipokuwa nikipitia moja yayo, niliona makala yenye kichwa ‘Kutokumtegemea Mungu—Sababu Gani Hakufai?’a Makala hiyo iligusa moyo wangu. Niliona kwamba Mungu alikuwa amejibu sala zangu, na siku iyo hiyo, Mashahidi walianza kujifunza Biblia pamoja na mimi. Kutoka wakati huo na kuendelea nilifanya mabadiliko yaliyonifanya niwe mtu bora zaidi. Mume wangu na familia yangu mwanzoni walipinga kujifunza kwangu Biblia, lakini walipoona mabadiliko niliyokuwa nikifanya, walianza kunitia moyo. Sasa mimi ni mtumishi wa Mungu aliyebatizwa.”
Mashahidi wa Yehova katika Brazili, kama vile katika sehemu nyingine zote za dunia, wana bidii katika kuwahubiri “wafungwa kufunguliwa kwao.” Wengi wanaitikia, wakipata uhuru na furaha ya kweli katika kumtumikia Yehova.
[Maelezo ya Chini]
a Toleo la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1985.
[Sanduku katika ukurasa wa 30]
BRAZIL
Idadi ya Watu -150,367,800
Kilele cha Wahubiri cha 1990 -293,466
Uwiano, Mhubiri 1 kwa Watu -512
Waliobatizwa 1990 -27,068
Wastani ya Wahubiri Mapainia -30,115
Idadi ya Makundi - 4,625
Wastani ya Mafunzo ya Biblia -341,305
Hudhurio la Ukumbusho -790,926