Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 8/1 kur. 25-29
  • Ni Shangwe Kama Nini Kuketi Kwenye Meza Ya Yehova!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Shangwe Kama Nini Kuketi Kwenye Meza Ya Yehova!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupatwa na Majaribu
  • Chakula cha Kiroho Kambini
  • Mwaminifu Hadi Kifo
  • Maandalizi ya Kiroho Katika Neuengamme
  • Mibaraka ya Kiroho Kwa Wingi
  • Imani Katika Mungu Ilinitegemeza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kuendeleza Imani Pamoja na Mume Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kushika Ukamilifu-Maadili Katika Ujerumani ya Nazi
    Amkeni!—1993
  • Kwa Msaada wa Yehova, Tuliokoka Serikali za Kimabavu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 8/1 kur. 25-29

Ni Shangwe Kama Nini Kuketi Kwenye Meza Ya Yehova!

Kama ilivyosimuliwa na Ernst Wauer (Ernist Vaua)

LEO ni rahisi kwangu kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, kujifunza Biblia, na kuhubiri habari njema za Ufalme. Hata hivyo, hali haikupata kuwa hivyo sikuzote huku Ujerumani. Wakati Adolfu Hitla alipokuwa dikteta (mtawala wa mabavu), tangu 1933 hadi 1945, kushiriki katika utendaji wa Kikristo kama huo kulitia ndani kuhatarisha uhai.

MWAKA kabla ya Hitla kupata mamlaka, nilipokuwa mwenye umri wa miaka 30, nilikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza katika Dresden. Katika Januari 1935, nilijiweka wakfu kwa Yehova nikaonyesha tamaa yangu kubatizwa. Kazi yetu ilikuwa tayari imepigwa marufuku katika 1933, kwa hiyo niliulizwa hivi: “Je! unang’amua uamuzi wako unachomaanisha? Unahatarisha familia yako, afya yako, kazi yako, uhuru wako, na hata uhai wako!”

“Nimehesabu gharama, nami nina nia ya kufanya penzi la Mungu na kufa kwa ajili yalo,” nikajibu.

Hata kabla ya ubatizo wangu, nilikuwa nimeanza kuhubiri kutoka nyumba kwa nyumba. Kwenye mlango mmoja, nilikutana na kiongozi wa vijana wa SS (Kikosi cha Hitla wenye shati nyeusi/Walinzi Bora kabisa) aliyenipazia sauti hivi: “Je! hujui kuwa jambo hili limekatazwa? Mimi nitawaita polisi!”

“Haya basi waite. Mimi ninasema tu juu ya Biblia, na hakuna sheria yoyote dhidi ya hiyo,” nikajibu kwa upole. Kisha nikageukia mlango uliofuata na upesi nikakaribishwa ndani na mwanamume mwenye urafiki. Hakuna jambo lililotendeka kwangu.

Upesi nilikabidhiwa kutunza kikundi cha funzo chenye Mashahidi karibu watano hadi saba wakikutana kila juma. Tulijifunza nakala za Mnara wa Mlinzi zilizokuwa zimeingizwa nchini Ujerumani kwa siri kutoka nchi jirani. Kwa hiyo, kujapokuwa kupigwa marufuku, tuliketi kwa ukawaida kwenye “meza ya Bwana [Yehova, NW]” ili kuimarishwa kiroho.—1 Wakorintho 10:21.

Kupatwa na Majaribu

Katika 1936, J. F. Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Society, alizuru kusanyiko katika Lucerne, Switzerland, akawakaribisha akina ndugu waliokuwa katika vyeo vya uangalizi wa kitheokrasi katika Ujerumani wawepo. Kwa kuwa pasipoti za ndugu wengi zilikuwa zimetwaliwa na serikali na idadi kubwa ya ndugu walikuwa wakichunguzwa kwa ukaribu na polisi, ni wachache tu wangeweza kuhudhuria. Ndugu aliyekuwa akisimamia kazi katika Dresden aliniomba nimwakilishe katika Lucerne.

“Lakini je, mimi si mchanga mno na mwenye kukosa ujuzi?” nikauliza.

“Lenye umaana sasa,” akanihakikishia, “ni kuwa mwaminifu. Hilo ndilo jambo kuu.”

Muda mfupi baada ya kurudi kutoka Lucerne, nilikamatwa na kutenganishwa ghafula na mke wangu, Eva, na watoto wetu wawili. Nilipokuwa njiani kwenda kwenye makao makuu ya polisi katika Dresden, nilijitahidi sana kukumbuka andiko lenye kuniongoza. Nilikumbuka Mithali 3:5, 6: “Mtumaini BWANA [Yehova, NW] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” Kukumbuka andiko hilo kuliniimarisha kwa ajili ya mahoji ya mwanzo. Baadaye nilifungiwa katika seli iliyosongamana, na kwa muda mfupi nilikuwa na maoni ya kukata tamaa ya kuwa nimeachwa. Lakini sala ya bidii kwa Yehova ilinijaza amani.

Mahakama ilinipa hukumu ya miezi 27 gerezani. Niliwekwa katika kifungo cha kukaa peke yangu kwa mwaka mmoja kwenye gereza katika Bautzen. Wakati mmoja, ofisa wa kihakimu aliyestaafu—alikuwa akifanya kazi badala ya mtu mwingine—alifungua mlango wa seli yangu akasema kwa huruma: “Najua hauruhusiwi kusoma chochote, lakini labda utahitaji kitu fulani ili kupumzisha akili yako usifikirie hali yako.” Kisha akanipitishia kisiri magazeti machache ya zamani ya familia akasema: “Nitayachukua leo usiku.”

Kwa kweli sikuhitaji chochote ‘ili kupumzisha akili yangu nisifikirie hali yangu.’ Nilipokuwa katika kifungo cha kukaa peke yangu, nilikumbuka maandiko ya Biblia kutoka moyoni na kukuza hotuba na kuzitoa kwa sauti. Lakini nilitupia jicho magazeti kuona kama yalikuwa na Maandiko yoyote—nami nikapata kadhaa! Mojawapo lilikuwa Wafilipi 1:6, linalosomwa kwa sehemu: “Niliaminilo ndilo hili . . . yeye aliyeanza kazi njema mioyoni mwenu ataimaliza.” Nilimshukuru Yehova kwa kitia-moyo hicho.

Baadaye nilihamishwa kwenye kambi ya kazi ngumu. Halafu, katika masika ya 1939, kifungo changu kilipokuwa karibu kuisha, msimamizi wa kambi aliuliza kama maoni yangu yalikuwa yamebadilika. “Mimi nina nia ya kubaki mshikamanifu kwa imani yangu” likawa jibu langu. Kisha akanijulisha kwamba ningehamishwa kwenye kambi ya mateso ya Sachsenhausen (Saksenhauzeni).

Huko nilisalimisha nguo zangu za kibinafsi, nikaoga, nikanyolewa nywele zote za mwilini, nikapewa nguo za gereza. Halafu nikawekwa majini tena, wakati huu nikiwa na nguo—tendo ambalo askari wa SS waliita “ubatizo.” Baadaye nililazimishwa nisimame nje mpaka jioni, nikiwa nimelowa maji.

Katika kambi Mashahidi wa Yehova waliwekwa chini ya ukatili wa pekee na askari wa SS. Pindi nyingi tulipaswa kusimama kwenye uwanja wa maonyesho saa nyingi mfululizo. Nyakati nyingine mmoja wetu aliweza kuhema akisema: “Je! haingekuwa vizuri kuwa na mlo mzuri kweli kweli? Mwingine aliweza kujibu: “Usikazie akili yako juu ya mambo kama hayo. Fikiria tu jinsi ilivyo staha kutetea jina na Ufalme wa Yehova.” Na mtu mwingine aliweza kuongeza hivi: “Yehova atatuimarisha!” Tulitiana moyo kwa njia hiyo. Nyakati nyingine mwinamo wa kichwa tu wenye urafiki ulikuwa wa kutosha kusema: “Nataka kuwa mshikamanifu; wewe na uwe pia!”

Chakula cha Kiroho Kambini

Watu fulani waliongoza katika kulisha akina ndugu kiroho, na mimi nilichaguliwa kuwasaidia. Tulikuwa tu na Biblia nene ya tafsiri ya Lutheri. Kuwa nayo bila shaka, kulikatazwa. Kwa hiyo hazina hiyo ilifichwa, na katika kila kikundi cha seli ni ndugu mmoja tu aliyechaguliwa ndiye aliyekuwa na ruhusa ya kuiona kwa muda mfupi. Ilipokuwa wakati wangu, niliweza kutambaa chini ya kitanda nikiwa na mwenge na kusoma kwa karibu dakika 15. Nilijifunza kwa moyo maandiko ambayo ningeweza kuzungumzia pamoja na akina ndugu katika kikundi chetu cha seli. Hivyo, ugawanyaji wa chakula cha kiroho ulipangwa kitengenezo kwa kadiri fulani.

Ndugu wote walitiwa moyo kumwomba Yehova katika sala kwa ajili ya chakula zaidi cha kiroho, naye alisikia maombi yetu. Katika kipupwe cha 1939/40 ndugu aliyetiwa gerezani karibuni aliweza kuingiza kwa siri matoleo mapya machache ya Mnara wa Mlinzi kambini ndani ya mguu wake wa mbao. Huo ulionekana kuwa muujiza, kwa kuwa watu wote walichunguzwa kwa uangalifu.

Magazeti hayo yalifanywa yapatikane kwa ndugu waliochaguliwa kwa muda wa siku moja moja, kwa sababu za usalama. Wakati mmoja, banda la kuwekea motokaa lilipokuwa likijengwa, nilijikunyata katika handaki na kusoma huku ndugu mmoja akiwa macho nje. Pindi nyingine niliweka Mnara wa Mlinzi pajani pangu wakati wa “saa [yetu] ya kushona” (nyakati za jioni tulikuwa tukiketi katika jumba letu la kukaa tukitia viraka mifuko ya mikono na vitu vinginevyo), huku akina ndugu wakiwa wameketi kila upande wakiwa macho. Askari wa SS alipokuja, nilificha mbali Mnara wa Mlinzi upesi. Kushikwa kungemaanisha kifo changu!

Yehova alitusaidia katika njia ya ajabu kukumbuka moyoni mawazo yenye kuimarisha katika makala hizo. Kwa ukawaida uchovu tu ndio ulinifanya nilale usingizi mzito sana usiku. Lakini masiku ambayo nilikuwa nimekwisha kusoma Mnara wa Mlinzi, ningeamka mara kadhaa na kukumbuka mawazo kwa uwazi sana. Ndugu waliochaguliwa katika seli nyingine walikuwa na maono ayo hayo. Hivyo Yehova aliamsha kumbukumbu letu ili tuweze kugawanya chakula cha kiroho. Tulifanya hivyo kwa kufikia kila ndugu binafsi na kumwimarisha.

Mwaminifu Hadi Kifo

Siku ya Septemba 15, 1939, kikosi chetu cha kazi ngumu kililazimika kiandamane kurudi kambini mapema kuliko kawaida. Nini kingetukia? August Dickmann, mmoja wa ndugu zetu wachanga, alikuwa auwawe hadharani. Wanazi walikuwa na uhakika kwamba hilo lingesadikisha idadi kubwa ya Mashahidi waikane imani yao. Baada ya kuuawa huko, wafungwa wote wengine waliondoshwa. Lakini sisi Mashahidi wa Yehova tulisukumwa-sukumwa nyuma na mbele kwenye uwanja wa gwaride, tukipigwa mateke na kupigwa kwa vijiti mpaka hatukuweza kujimudu tena. Tuliamuriwa tuweke sahihi kwenye hati ya kujulisha kwamba tumeikana imani yetu; kama sivyo, sisi pia tungepigwa risasi.

Kufikia siku iliyofuata, hakuna yeyote aliyekuwa ameweka sahihi. Kwa hakika, mfungwa mpya aliyekuwa ameweka sahihi alipokuwa amewasili, sasa alitangua sahihi yake. Alipendelea zaidi kufa pamoja na ndugu zake kuliko kuacha kambi akiwa msaliti. Miezi iliyofuata, tuliadhibiwa kwa kazi ngumu sana, kutendewa vibaya sikuzote, na kunyimwa chakula. Ndugu zetu zaidi ya mia moja walikufa wakati wa kipupwe kikali cha 1939/40. Walishikilia ukamilifu wao kwa Yehova na kwa Ufalme wake hadi mwisho kabisa.

Kisha Yehova akaandaa msaada wake. Ndugu wengi walihamishwa mahali pengine kufanya kazi katika kambi zilizosimamishwa karibuni, ambapo walipokea chakula zaidi. Isitoshe, kudhulumiwa kulipunguka kwa kadiri fulani. Katika masika ya 1940, nilihamishwa kwenda kwenye kambi ya mateso ya Neuengamme (Nywingame).

Maandalizi ya Kiroho Katika Neuengamme

Nilipowasili, kulikuwako kikundi cha Mashahidi 20, bila Biblia yoyote au vichapo vyovyote. Nilisali kwa Yehova ili anisaidie nitumie yale niliyokuwa nimejifunza katika Sachsenhausen kuimarisha ndugu katika Neuengamme. Kama hatua ya kwanza, nilikumbuka maandiko nikayachagua kuwa maandiko ya kila siku. Halafu maandalizi yakafanywa kwa ajili ya mikutano ambayo katika hiyo niliweza kueleza mawazo kutoka kwa makala za Mnara wa Mlinzi nilizosoma katika Sachsenhausen. Ndugu wapya walipowasili, waliripoti mambo waliyokuwa wamejifunza kutoka kwa Mnara wa Mlinzi ya karibuni.

Kufikia 1943 idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Neuengamme ilikuwa imeongezeka hadi 70. Mashahidi wa Yehova walikuja kupendelewa zaidi kufanya kazi nje ya kambi, kama vile kusafisha baada ya mashambulio ya kutoka angani. Kama tokeo, tuliweza kuleta kambini kwa siri, Biblia, nakala za Mnara wa Mlinzi, na vitabu na broshua nyinginezo za Sosaiti. Pia tulipokea vifurushi kwa posta, vikiwa na fasihi nyingine zaidi na pia divai nyekundu na mkate usiotiwa chachu kwa ajili ya Ukumbusho. Kwa wazi Yehova aliwapofusha wale waliochunguza vifurushi hivyo.

Tukiwa tumetawanyika miongoni mwa majumba tofauti-tofauti, tulifanyiza vikundi saba vya Funzo la Mnara wa Mlinzi, kila kikundi kikiwa na kiongozi na mwingine akiwa badala. Nakala za Mnara wa Mlinzi zilitengenezwa kwa siri katika ofisi ya mkuu wa kambi, ambapo nilifanya kazi kwa muda. Kwa hiyo, kila kikundi cha funzo kilipokea angalau nakala moja nzima kwa ajili ya funzo la kila juma. Hakuna hata mkutano mmoja uliofutwa. Kuongezea hayo, kila asubuhi kwenye uwanja wa gwaride, vikundi vilipata nakala ya andiko la siku, kutia na elezo lililotolewa kutoka kwa Mnara wa Mlinzi.

Wakati mmoja askari wa SS walikuwa na sikukuu, kwa hiyo tuliweza kuwa na mkusanyiko wa nusu-siku na kuzungumzia jinsi ya kuhubiri kambini. Tuligawanya kambi katika maeneo na kujaribu kwa utaratibu kufikia wafungwa na “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Kwa kuwa wafungwa walitoka nchi mbalimbali, tulifanya kadi za ushuhuda za lugha nyingi zilizoeleza kazi yetu na Ufalme. Tulihubiri kwa bidii sana hivi kwamba wafungwa wa kisiasa walilalamika hivi: “Popote uendapo, yale unayosikia ni mazungumzo juu ya Yehova tu!” Ripoti ya utumishi wa shambani ya utendaji wetu hata ilifikia ofisi ya tawi katika Bern, Switzerland.

Mambo yote yalikuwa sawasawa mpaka Gestapo walipofanya uchunguzi wa kambi za mateso zote katika 1944. Bohari yetu ya vichapo katika Neuengamme haikugunduliwa, lakini Karl Schwarzer (Karl Shwartza) na mimi tulipatikana na vitu vichache. Tulihojiwa kwa siku tatu na kupigwa. Jaribu hilo lilipokwisha, sote wawili tulijaa majeraha. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova, tulipona.

Mibaraka ya Kiroho Kwa Wingi

Niliwekwa huru na vikosi vya Muungano katika Mei 1945. Siku baada ya kuwekwa huru, nilianza kuandamana pamoja na kikundi kidogo cha akina ndugu na watu waliopendezwa. Tukiwa tumechoka, tuliketi chini kwenye kisima katika kijiji cha kwanza tulichofika tukanywa maji. Kwa kuhisi burudisho, nilienda kutoka nyumba kwa nyumba nikiwa na Biblia mkononi mwangu. Mwanamke mmoja mchanga aliguswa moyo sana kujua kwamba sisi Mashahidi wa Yehova tulikuwa tumekuwa katika kambi za mateso kwa ajili ya imani yetu. Alitowekea jikoni mwake, akarudi pamoja na maziwa na vipande vya mikate kwa ajili ya kikundi chetu.

Baadaye, tukiwa bado tumevaa mavazi yetu ya kambi, tulitangaza ujumbe wa Ufalme kotekote katika kijiji hicho. Mwana kijiji mwingine alitualika ndani kwa mlo wenye ukarimu. Alituandalia vitu ambavyo tulikuwa tumekosa kwa miaka mingi. Lilikuwa jambo la kutamanisha kama nini! Hata hivyo, hatukulafua chakula tu. Tulisali na kula kwa njia ya upole na yenye adabu nzuri. Hilo liliwavuta wenye kuangalia sana hivi kwamba tulipoanza mkutano baadaye, walisikiza hotuba ya Biblia. Mwanamke mmoja alikubali ujumbe na leo ni dada yetu wa kiroho.

Tuliendelea kuandamana na kuona utunzi wa Yehova katika njia za ajabu. Sasa tukiwa huru, imekuwa hisia yenye utukufu kama nini kuendelea kukionea shangwe chakula chote cha kiroho kinachochapishwa na tengenezo la Yehova na kukishiriki na wengine! Katika miaka ambayo imefuata, tumaini letu kamili katika Yehova limekuwa na thawabu tena na tena.

Kutoka 1945 hadi 1950, nilikuwa na pendeleo la kutumikia katika Betheli ya Magdeburg na kisha, hadi 1955, katika ofisi ya Watch Tower Society katika Berlin. Baadaye, nilitumikia nikiwa mwangalizi asafiriye hadi 1963, wakati mke wangu, Hilde (Hilda), alipotangaza kwamba alikuwa akitazamia kupata mtoto. (Eva, mke wangu wa kwanza, alikuwa amekufa wakati wa kifungo changu, na mimi nikaoa tena katika 1958.) Binti yetu akawa baadaye Shahidi mwenye bidii.

Vipi juu ya watoto kutoka ndoa yangu ya kwanza? Kwa kusikitisha, mwana wangu hakuonyesha upendezi wowote katika kweli. Lakini binti yangu Gisela alionyesha, naye alihudhuria shule ya umisionari ya Gileadi katika 1953. Sasa anatumikia, pamoja na mume wake, kwenye mojawapo Majumba ya Makusanyiko katika Ujerumani. Kwa msaada wa Yehova, nimeweza kukaa katika utumishi wa upainia wa kawaida tangu 1963 na kutumikia ambapo msaada ulihitajiwa kwanza katika Frankfurt na baadaye katika Tübingen.

Mpaka leo ninaendelea kuonea shangwe maandalizi yote yanayofanywa na tengenezo la Yehova kwa ajili ya nyumba yake yenye imani. (1 Timotheo 3:15) Siku hizi, ni rahisi sana kupata chakula cha kiroho, lakini je, huwa tunakithamini sikuzote? Nina uhakika kwamba Yehova ana mibaraka mingi akibani kwa wale wanaomtumaini, wanaobaki washikamanifu, na kula kwenye meza yake.

[Mchoro katika ukurasa wa 26, 27]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

KAMBI YA MATESO YA SAKSENHAUZENI

A. Majumba ya SS

B. Ua la kuitiwa majina

C. Jumba la seli

D. Kifungo cha upekee

E. Kituo cha kuondolea chawa

F. Mahali pa kuulia

G. Chumba cha gesi

[Picha of Ernst and Hilde Wauer katika ukurasa wa 25]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki