Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote—Brazili
BRAZILI ni nchi kubwa mno kwa njia nyingi. Katika ukubwa na wakazi wayo, ndiyo nchi ya tano kwa ukubwa ulimwenguni. Ina eneo la karibu nusu ya eneo la nchi ya Amerika Kusini nayo ina wakazi wengi zaidi kuliko nchi zote za bara hilo zikiunganishwa. Pia Brazili ina msitu mkubwa zaidi ulimwenguni. Kupitia msitu huo kuna mto wenye nguvu zaidi duniani—Amazon.
Brazili ni kubwa mno pia katika maana nyingine. Idadi ya wahubiri wa habari njema ya Ufalme wa Mungu inakaribia 400,000, na mwaka uliopita zaidi ya 1,000,000 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kwa hiyo nchi hii inatokeza hasa kuhusu kazi ya kuhubiri Ufalme. Maono ya juzijuzi yanatoa kielezi juu ya jambo hili.
Kutumikia Mahali Ambako Uhitaji Ni Mkubwa Zaidi
Antonio na mkeye walifanya uamuzi mzito wa kuacha watu wa ukoo wao na kazi thabiti na yenye mshahara mzuri katika São Paulo ili kutumikia mahali ambako uhitaji wa wahubiri wa Ufalme ulikuwa mkubwa zaidi katika mji wa Minas Gerais. Eneo lao lilitia ndani kundi la wafanyakazi wa kiwanda cha sukari. Siku ya kwanza walipotoa ushahidi huko, walianzisha mafunzo ya Biblia tisa. Katika miezi 18, walikuwa wakiongoza zaidi ya mafunzo 40!
Kwanza, mikutano ilifanyiwa ndani ya kiwanda hicho. Walakini, wahubiri wapya walitaka kuona Jumba la Ufalme halisi. Hivyo, basi lilikodishwa kuwapeleka watu 75 kwenye kutaniko lililokuwa karibu zaidi. Kisha mkusanyiko ukafika; 45 wa wanafunzi wapya wa Biblia walihudhuria na walihojiwa. Kumi na watano wao walibatizwa wakati wa tukio hilo. Bila shaka, machozi ya shangwe yalitiririka kwa wingi!
Kampuni hiyohiyo ya basi ilitumiwa kwa safari kama hizo, na wasimamizi walipunguza gharama. Kuonyesha uthamini, Antonio alimpa mwenye kampuni hiyo kichapo cha Biblia. Alikubali kuanza kujifunza Biblia jioni hiyohiyo naye alibatizwa baada ya miezi kadhaa ya funzo lenye bidii. Kwanza, mkeye alikuwa mwenye kupinga funzo hilo, lakini baadaye, mtazamo wake ulibadilika. Leo yeye pia ni Shahidi wa Yehova aliyebatizwa.
Katika Februari 1992 kutaniko lenye wahubiri 22 wenye bidii lilianzishwa. Kufikia 1994 idadi hii ilikuwa imeongezeka hadi 42, kukiwa na mapainia wa kawaida 4, au wahubiri wa wakati wote wa habari njema. Kama tokeo, Antonio amalizia: “Mke wangu na mimi tumeona kwamba ‘tukimjaribu Yehova,’ kama Malaki 3:10 isemavyo, ‘atamwaga baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la.’”
Kutoa Fasihi ya Biblia
Labda sababu nyingine inayofanya kazi ya kuhubiri ichukue hatua kubwa hivi katika Brazili ni kwamba Mashahidi hutoa fasihi ya Biblia kila fursa. Kwa kielelezo, kutaniko moja liliandikia tawi la Watch Tower Society likiomba nakala 250 za kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Kwa nini agizo kubwa hivyo?
Barua hiyo ilieleza hivi: ‘Shule moja mjini imeamua kutumia kitabu hiki kikiwa chombo cha kufundishia katika darasa moja. Uamuzi huo wa wakuu wa shule umetokana na ushahidi wa vivi hivi ambao umefanywa na wazazi wa wanafunzi walio Mashahidi wa Yehova pamoja na mmoja wa wasimamizi wa shule hiyo. Yehova na aendelee kuwabariki watumishi wake wanapotoa mwelekezo bora kwa kutumia kitabu hiki.’ Ndiyo, Yehova na aendelee kubariki maendeleo mazuri ya kazi ya kuhubiri Ufalme katika nchi iliyo kubwa mno ya Brazili.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
HABARI ZA NCHI
Mwaka wa Utumishi wa 1994
KILELE CHA WANAOTOA USHAHIDI: 385,099
UWIANO: Shahidi 1 kwa Watu 404
HUDHURIO LA UKUMBUSHO: 1,018,210
WASTANI WA WAHUBIRI WALIO MAPAINIA: 38,348
WASTANI WA MAFUNZO YA BIBLIA: 461,343
IDADI YA WALIOBATIZWA: 24,634
IDADI YA MAKUTANIKO: 5,928
OFISI YA TAWI: CESÁRIO LANGE
[Picha katika ukurasa wa9]
Gari lenye kikuza sauti lililotumiwa katika São Paulo karibu 1940
[Picha katika ukurasa wa9]
Kutoa ushahidi katika Bustani la Mimea katika Rio de Janeiro
[Picha katika ukurasa wa9]
Ofisi ya tawi katika Cesário Lange