Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 7/1 uku. 31
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Habari Zinazolingana
  • Uongozi Timamu kwa Vijana wa Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Kupanda Juu kwa Mbawa Kama Tai
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kitabu Cha Biblia Namba 20—Mithali
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Macho ya Tai
    Amkeni!—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 7/1 uku. 31

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je! mwandikaji wa Mithali 30:19 alihisi kwa kweli kwamba jinsi mwanamume anavyomshawishi msichana kwa hila lilikuwa jambo la “ajabu”?

Hiyo huenda ikawa maana ya Mithali 30:19, ambao kwa kweli si mstari ulio rahisi kuelewa.

Katika kutafuta maana ya mstari huo, hatupaswi kupuuza muktadha. Kabla tu ya fungu hilo, mwandikaji aliyepuliziwa roho aliorodhesha vitu vinne ambavyo kwa njia fulani havishibi kamwe. (Mithali 30:15, 16) Kisha akatokeza orodha hii: “Kuna mambo matatu yaliyo ya ajabu kwangu, naam, kuna manne nisiyoyafahamu. Mwendo wa tai katika hewa; na mwendo wa nyoka juu ya mwamba; mwendo wa merikebu katikati ya bahari; na mwendo wa mtu pamoja na msichana.”—Mithali 30:18, 19.

Ni nini ambacho kingekuwa cha “ajabu” katika mambo hayo manne?

Labda wakihisi kwamba ni lazima neno “ajabu” liwe linadokeza mambo yaliyo chanya au mazuri, wanachuo wengine hueleza kwamba kila moja ya mambo hayo manne huonyesha hekima ya uumbaji wa Mungu: ajabu ya jinsi ndege mkubwa awezavyo kuruka, jinsi nyoka asiye na miguu awezavyo kwenda juu ya mwamba, jinsi merikebu kubwa iwezavyo kuelea baharini yenye msukosuko, na jinsi kijana mwenye nguvu awezavyo kumpenda sana msichana mzuri akamwoe, na kisha wanatokeza mtoto wa ajabu wa kibinadamu. Profesa mmoja aliona jambo jingine lililofanana kati ya mambo hayo manne, kwamba kila moja hufuata njia mpya kila mara—mwendo wa tai, nyoka, na merikebu pasipo kijia na ile hali mpya ya upendo wa wenzi wawili unaositawi.

Hata hivyo, si lazima mambo hayo manne yawe ya “ajabu” kwa maana nzuri, kana kwamba jambo linalofanana kati yayo ni jambo lililo chanya. Mithali 6:16-19 huorodhesha “vitu sita anavyovichukia BWANA [Yehova, NW].” Na kama ilivyoonyeshwa, kabla tu ya mistari inayozungumziwa, Mithali 30:15, 16 huorodhesha vitu (Sheoli, tumbo lisilozaa, nchi isiyoshiba maji, na moto) visivyosema, “Basi!” Kwa hakika hivyo sivyo vitu vya ajabu.

Neno la Kiebrania linalofasiriwa “ajabu” kwenye Mithali 30:18 humaanisha “kutenga, kupambanua; kufanya yenye fahari, -siyo ya kawaida, -a ajabu.” Kitu fulani chaweza kuwa chenye fahari, kisicho cha kawaida, au chenye kustaajabisha bila kuwa kizuri. Danieli 8:23, 24 ilitabiri juu ya mfalme mkali ambaye angeharibu “kiasi cha kustaajabisha” na ‘kuwaangamiza hao walio hodari,’ kutia na watakatifu.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 17:8; 28:59; Zekaria 8:6.

Mstari unaofuata Mithali 30:18, 19 huenda ukaanda kidokezo kuhusu kile ambacho mwandikaji aliona kuwa kigumu kuelewa. Mstari 20 hutaja mwanamke mzinifu ambaye “hula, akapangusa kinywa chake, akasema, Sikufanya uovu.” Labda alikuwa ametenda dhambi kwa usiri na kwa hila, lakini kwa kuwa hakukuwa ushuhuda wowote wa uhalifu wake, angeweza kudai kuwa bila hatia.

Kuna jambo katika orodha hiyo linalofanana na orodha inayotangulia. Tai huruka angani, nyoka hutambaa juu ya mwamba, merikebu hupitia mawimbi—hakuna lolote kati ya mambo hayo linaloacha alama nyuma yalo, na isingekuwa rahisi kufuatia kijia cha lolote kati ya mambo hayo matatu. Ikiwa hilo ndilo jambo linalofanana kati ya mambo hayo matatu, namna gani la nne, “mwendo wa mtu pamoja na msichana”?

Hilo pia laweza kuwa gumu kufuatia. Kijana huenda akatumia ujanja, wororo, na njia za hila ili apate kwa urahisi shauku za bikira asiye na hatia. Kwa sababu hana ujuzi, huenda bikira huyo asitambue hila za kijana huyo. Hata baada ya kushawishwa, huenda asiweze kueleza jinsi kijana huyo alivyomshinda; huenda watazamaji pia wakaona jambo hilo kuwa gumu kueleza. Hata hivyo, wanawake wengi wachanga wamepoteza usafi wao wa kiadili kwa washawishi wenye hila. Ni vigumu kufuatia njia ya wanaume hao wajanja, hata hivyo wao wana mradi fulani, sawa na tai arukaye, nyoka atambaaye, au merikebu baharini. Mradi wa washawishi ni kujifaidi kingono.

Kwa maoni hayo jambo kuu la Mithali 30:18, 19 si juu ya mambo ya kisayansi au ya kimashine katika uumbaji. Badala ya hiyo, fungu hilo latutolea onyo la kiadili, kama vile Mithali 7:1-27 huonya juu ya kuepuka hatari za kahaba mwenye kuvutia kwa kusadikisha. Njia moja ambayo dada Wakristo wanaweza kutii kwa uzito onyo la Mithali 30:18, 19 ni kwa habari ya wanaume wanaodai kupendezwa na kujifunza Biblia. Ikiwa mwanamume mwenye urafiki, hata mfanyakazi mwenzi, aonekana kupendezwa, dada apaswa kumwelekeza kwa ndugu fulani kundini. Ndugu huyo aweza kutosheleza kupendezwa kokote kwa kweli bila hatari za “mtu pamoja na msichana.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki