Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 10/1 kur. 26-28
  • Kanuni au Kupendwa na Wengi Mwongozo Wako ni Upi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kanuni au Kupendwa na Wengi Mwongozo Wako ni Upi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tamaa ya Kufaana na Wengine
  • Misongo ya Kujipatanisha
  • Umati Waweza Kukosea
  • Kanuni za Biblia Ni Bora Zaidi
  • Wakati Wote Watakapofanya Yaliyo Mema
  • Vijana Wakristo Iweni Imara Katika Imani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Umati Mkubwa Wenye Watu Wengi Sana
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • “Tazama! Umati Mkubwa”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Kumbuka Kanuni za Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 10/1 kur. 26-28

Kanuni au Kupendwa na Wengi Mwongozo Wako ni Upi?

ALIPOKUWA katika darasa la sita Norihito alikuwa akishiriki katika mchezo fulani. Kwa ghafula, alikabiliwa na uamuzi fulani. Wanafunzi wote walihitajiwa kushiriki katika sherehe ya kizalendo. Je! ajiunge na wanafunzi wenzake katika jambo hilo lililoonekana kuwa la kawaida tu?

Norihito alikuwa amejifunza kutoka katika Biblia kwamba ni vibaya kujiunga katika tendo lolote la ibada kwa mungu mwingine ila Yehova. (Kutoka 20:4, 5; Mathayo 4:10) Alijua pia kwamba Wakristo wanapaswa kuendelea kutokuwamo katika shughuli zote za kisiasa za kilimwengu. (Danieli 3:1-30; Yohana 17:16) Kwa hiyo hata ingawa wanafunzi wenzake walimhimiza ajiunge, alisimama imara kwa ujasiri lakini kwa staha. Wewe ungalifanya nini katika hali kama hiyo?

Tamaa ya Kufaana na Wengine

Maandiko huonyesha kwamba wanadamu waliumbwa na Mungu kuwa wenye urafiki, kupatana, na kufurahia kufanya mambo pamoja. Ni jambo la asili kwa mtu kutaka kuwa pamoja na marika wake, kukubaliwa, kufaana nao. Hisia hizo hufanya maisha yafurahishe zaidi na kuchangia amani na upatano katika shughuli zetu na wengine.—Mwanzo 2:18; Zaburi 133:1; 1 Petro 3:8.

Tamaa ya asili ya kufaana na wengine huonekana katika kule kukazia sana kujipatanisha kunakoonwa katika tamaduni nyingine hata leo. Kwa kielelezo, watoto Wajapani, huzoezwa kutoka miaka yao ya mapema zaidi kufahamu na kujipatanisha na kanuni za walio wengi. Urithi wao huwafundisha kwamba mmojapo wajibu wao mkubwa zaidi ni kujipatanisha na jumuiya. “Wajapani wanaelekea zaidi kutenda wakiwa vikundi kuliko watu wa Magharibi,” akasema Edwin Reischauer, aliyekuwa balozi wa U.S. katika Japani na aliye mtazamaji mwangalifu wa tabia za Wajapani. Aliongeza hivi: “Ilihali watu wa Magharibi huenda angalau wakaonyesha nje-nje kuwa wenye kujitegemea na wenye kufuata maoni yao wenyewe, Wajapani walio wengi wataridhika sana kujipatanisha na mambo ya kawaida ya kikundi chao katika mavazi, mwenendo, mtindo wa maisha, na hata fikira.” Hata hivyo, tamaa ya kujipatanisha si ya Wajapani pekee hata kidogo. Ni ya kotekote ulimwenguni.

Misongo ya Kujipatanisha

Hata ingawa ni jambo la kutamanika kwa mtu kujaribu awezavyo kupatana na wengine, kuna hatari ya kujipatanisha na mambo yanayopendwa na wengi bila kufikiri. Kwa nini? Ni kwa sababu mara nyingi mambo yanayopendwa na wengi huwa kinyume cha yale yanayokubalika kwa Mungu. “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu,” Biblia hutuambia. (1 Yohana 5:19) Shetani hutumia kwa hila kila njia awezayo—kupenda vitu vya kimwili, adili za chini, ubaguzi wa rangi, ushupavu wa kidini, utukuzo wa taifa, na kadhalika—kuvuta matungamano ya watu na kuwageuzia mbali na Mungu. Kwa kweli, kujipatanisha na mazoea hayo kungemfanya mtu apingane na Yehova Mungu na makusudi yake. Ndiyo sababu Wakristo wanashauriwa hivi: “Msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”—Warumi 12:2.

Wakiwa wanaishi katika mfumo huu wa mambo, Wakristo wako chini ya msongo wa daima wa kujipatanisha na mambo yanayopendwa na wengi. Vijana hasa ndio huvutwa kwa urahisi katika jambo hili. Tamaa ya kuonekana na kutenda kama wanashule wenzao ni yenye nguvu sana. Ujasiri mwingi wahitajiwa ili waweze kuwaelezea marika wao kwa nini hawashiriki katika utendaji fulani-fulani. Hata hivyo, kushindwa kujitetea kungeweza kumaanisha msiba wa kiroho kwao.—Mithali 24:1, 19, 20.

Watu wazima pia hukabili misongo hiyo kazini mwao. Huenda wakatazamiwa kushiriki katika utendaji fulani-fulani wa kijamii baada ya saa za kazi au katika sikukuu fulani. Kukataa kufanya hivyo huenda kukawafanya waonekane kuwa wenye kujitenga au wasioshirikiana na wengine, hilo likitokeza hali ngumu kazini. Huenda wengine wakahisi ni lazima kufanya kazi muda wa saa nyingi baada ya saa za kazi za kawaida kwa sababu tu wengine wanafanya hivyo na wao pia wanatazamiwa kufanya hivyo. Kulegea katika mambo hayo kungewadhuru kiroho na pia kungewazuia wasitimize wajibu wao mwingine.—1 Wakorintho 15:33; 1 Timotheo 6:6-8.

Misongo ya kujipatanisha ipo penginepo zaidi ya shuleni au kazini. Mama mmoja Mkristo alisimulia kwamba katika pindi moja alisita kumpa mtoto wake nidhamu, hata ingawa ilihitajiwa sana, kwa sababu tu alihisi kwamba wale wake wengine wa nyumbani waliokuwapo hawangekubaliana nayo.—Mithali 29:15, 17.

Umati Waweza Kukosea

Biblia hutupa sisi mashauri mengi ya moja kwa moja kuhusu kufuatana na umati. Kwa kielelezo, taifa la Israeli liliambiwa hivi: “Usiandamane na mkutano [umati, NW] kutenda uovu; wala usitie ushahidi wako katika neno lo lote kwa kugeukia kando na kuandamana na mkutano ili kupotoa hukumu.” (Kutoka 23:2; linganisha Warumi 6:16.) Shauri hilo halikufuatwa sikuzote. Wakati mmoja, muda mfupi baada ya kuondoka Misri, wakati Musa hakuwapo, watu fulani mmoja-mmoja walimvuta Haruni na watu watengeneze ndama wa dhahabu na kumwabudu katika “sikukuu kwa BWANA [Yehova, NW].” Watu walikula na kunywa na kujifurahisha kwa wimbo na ngoma huku wakitoa dhabihu kwa yule ndama wa dhahabu. Viongozi wapatao 3,000 waliuawa kwa sababu ya tendo hilo lisilo la kiadili, la ibada ya sanamu. Lakini wengi wa wale wengine pia walipatwa na pigo kutoka kwa Yehova kwa sababu ya kufuata kwao umati bila kufikiri.—Kutoka 32:1-35.

Mfano mwingine wa kufuatana na umati ili kutenda uovu ulitukia katika karne ya kwanza kuhusiana na kifo cha Yesu Kristo. Wakisadikishwa na viongozi wa kidini wenye wivu, watu wengi walijiunga katika kutaka Yesu auawe. (Marko 15:11) Petro alipoonyesha kosa lao zito katika Pentekoste baada ya ufufuo wa Yesu na kupaa kwake, wengi “wa[li]chomwa mioyo yao,” wakang’amua lile walilokuwa wamefanya kwa kufuatana na umati.—Matendo 2:36, 37.

Kanuni za Biblia Ni Bora Zaidi

Kama vile masimulizi hayo yaonyeshavyo kwa wazi, kufuata mambo yanayopendwa na wengi bila kufikiri kwaweza kuongoza kwenye matokeo mazito. Ni bora zaidi kama nini kuifuata Biblia na kuacha kanuni zayo ziwe mwongozo maishani mwetu! “Kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu,” asema Yehova. (Isaya 55:9) Kwa habari ya adili na mahusiano ya kibinadamu—kwa kweli, katika maamuzi yote ya maishani—imeonyeshwa kwa kurudia-rudia kwamba kufuata njia za Yehova ni bora zaidi ya kufuata mambo yanayopendwa na wengi. Huo ndio ufunguo wa njia ya maisha yenye furaha zaidi na yenye afya bora zaidi.

Kwa kielelezo, chukua ono la Kazuya. Ingawa alikuwa amejifunza Biblia kwa muda fulani, aliendelea kufuata mwendo uliofuatwa na wengi—akijitahidi kuwa tajiri na kufanikiwa. Mara nyingi jitihada zake za kuwapendeza wakubwa wake na kupendwa na wafanyakazi wenzake zilimfanya aende kwenye shamrashamra za kunywa hadi che. Alikuwa mwenye kutaka mambo mengi, mwenye kutokuvumilia, na mwenye kuudhika-udhika. Upesi mtindo-maisha wake wa kupita kiasi uliongoza kwenye ugonjwa wa ghafula, uliomwacha akiwa amepooza kwa sehemu. Alipokuwa akipona kitandani hospitalini, alikuwa na wakati wa kufikiria yale aliyokuwa amejifunza katika Biblia na njia aliyokuwa akiishi maisha yake. Aliamua kwamba huo ulikuwa wakati wa kuanza kutumia yale aliyokuwa amejifunza. Alijiuzulu cheo chake cha umeneja akabadili mashirika yake. Pia alijitahidi sana kuvaa utu wa Kikristo na kurekebisha maoni yake juu ya vitu vya kimwili. Likiwa tokeo, kanuni zake zilibadilika, na afya yake ikaboreka. Hatimaye, aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova akabatizwa.

Ili kufanikiwa katika kufuata mwendo usiofuatwa na wengi, ni lazima mtu ajue kanuni zinazohusika na kusadiki kikamili kwamba zafaa. Yale yaliyompata Masaru yaonyesha hilo kuwa kweli. Alipokuwa katika darasa la sita, shule ya msingi, alipendekezwa na wanadarasa wenzake kuwa mgombea-cheo cha msimamizi wa baraza la wanafunzi. Yeye akumbuka kwa aibu kidogo kwamba kwa sababu ya kutoelewa kikamili kanuni za Biblia zilizohusika, hakuweza kuwaeleza wanadarasa wenzake ni kwa nini hangeweza kugombea cheo cha kisiasa. Kuhofu kwake binadamu kulikuwa kumemzuia asifunue kwamba alikuwa Mkristo. Jambo tu aliloweza kufanya ni kuinamisha kichwa chake na kurudia-rudia kwa machozi, “Siwezi kufanya hivyo.”

Ono hilo lenye kuumiza lilimsababisha achunguze kwa nini Mkristo hajihusishi katika utendaji wa kisiasa. (Linganisha Yohana 6:15.) Baadaye, alipokuwa katika shule ya upili, hali iyo hiyo ilitokea. Hata hivyo, wakati huo alikuwa tayari kumweleza mwalimu wake msimamo wake kwa usadikisho. Mwalimu alikubali elezo lake, kama vile wanadarasa wenzake kadhaa waliomwuliza juu ya itikadi zake zenye kuitegemea Biblia.

Wakati Wote Watakapofanya Yaliyo Mema

Katika ulimwengu mpya unaokuja chini ya utawala wa Kristo, jambo litakalofanywa na wengi litakuwa ndilo jambo jema la kufanya. Mpaka wakati huo, tutalazimika kujilinda dhidi ya hamu ya kujipatanisha na mambo yanayopendwa na wengi. Tunaweza kupata kitia-moyo kutokana na himizo hili la Paulo: “Kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.”—Waebrania 12:1.

Unapokabiliwa na maamuzi na magumu, utafanya nini? Je! utaangukia hofu ya binadamu na kufanya kulingana na mambo yanayopendwa na wengi? Au utageukia Neno la Mungu, Biblia, na kufuata kanuni zalo? Kufuata njia ya pili hakutakunufaisha sasa tu bali pia kutakupa taraja la kuwa miongoni mwa wale “wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.”—Waebrania 6:12.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki