Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 10/1 kur. 29-30
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Habari Zinazolingana
  • Msijifunge Nira Pamoja na Wasioamini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Maswali kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Kudumisha Umoja wa Kikristo Katika Mahusiano ya Kibiashara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 10/1 kur. 29-30

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa kuwa Biblia hutuambia: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini,” je, ingefaa kwa Mkristo kushiriki biashara pamoja na asiyeamini?

Twapata shauri hilo kwenye 2 Wakorintho 6:14-16: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu?”

Hakuna sababu ya kuamini kwamba mtume Paulo alitoa shauri hilo akiwa na nia ya kusitawisha makatazo hususa, kama vile dhidi ya Mkristo kushiriki biashara pamoja na asiyeamini. Lakini, kwa hakika shauri lake lahusiana na hilo, pamoja na sehemu nyingine za maisha.

Paulo aliandika shauri hilo kwa ndugu zake Wakristo katika Korintho la kale. Wakiwa wanaishi katika jiji lililokuwa lenye ufisadi hasa, kila siku walihitaji kukabiliana na hatari za kiadili na za kiroho. Isipokuwa kama wangekuwa waangalifu, kufunuliwa waingiwe na uvutano usiofaa kungedhoofisha polepole azimio lao la kuwa watu walio tofauti, “mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu.”—1 Petro 2:9.

Kabla ya kuandika yale yanayoonekana kwenye 2 Wakorintho 6:14-16, Paulo alikuwa ameshughulikia tatizo zito miongoni mwa ndugu zake Wakorintho. Walikuwa wameruhusu hali ya ukosefu mbaya sana wa adili iweko miongoni mwao, kwa hiyo Paulo aliwaelekeza waondoshe, au kutenga na ushirika, huyo mtenda dhambi asiyetubu. (1 Wakorintho 5:1) Kosa la mtu huyo lilionyesha kwamba mashirika mabaya au kujihusisha sana bila kinga katika hali ya kiadili ya ulimwengu kungeweza kuwaathiri Wakristo.

Wakristo Wakorintho walipaswa kuepuka kushirikiana na yule mtu aliyeondoshwa, lakini je, hilo lilimaanisha kwamba walihitaji kujitenga kabisa na wasioamini? Je! walipaswa kuepuka kabisa kuwasiliana au kushughulika na wasio Wakristo, wakiwa aina fulani ya farakano lenye kujitenga lenyewe, kama vile wale Wayahudi waliohamia Qumran karibu na Bahari ya Chumvi? Acha Paulo ajibu: “Naliwaandikia katika waraka wangu, kwamba msichangamane na wazinzi. Sisemi msichangamane kabisa na wazinzi wa dunia hii . . . maana hapo ingewalazimu kutoka katika dunia.”—1 Wakorintho 5:9, 10.

Maana ya maneno hayo ni wazi. Paulo aling’amua kwamba Wakristo walikuwa wangali kwenye sayari hii, wakiishi miongoni mwa na kuwasiliana karibu kila siku na wasioamini ambao adili zao zilikuwa za chini na ambao viwango vyao vilikuwa tofauti. Kwa kuwa hilo kwa msingi haliwezi kuepukika, Wakristo wapaswa kuwa chonjo kuelekea hatari za kuwasiliana huko.

Sasa ebu tufikirie tena barua ya pili ya Paulo kwa Wakorintho. Alionyesha kwamba Wakristo wapakwa kwa roho wamestahili kuwa wahudumu wa Mungu, mabalozi badala ya Kristo. Aliwaambia wajilinde dhidi ya sababu yoyote ya kukwaza ambayo huenda ikaletea huduma yao sifa mbaya. (2 Wakorintho 4:1–6:3) Paulo aliwahimiza moja kwa moja ndugu zake Wakorintho, waliokuwa kama watoto wake wa kiroho, wapanuke katika shauku zao. (2 Wakorintho 6:13) Baadaye alihimiza hivi: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini.” Ili kukazia jambo hilo, alitumia mfululizo wa mambo yenye kupingana, yasiyohitaji jibu.

Muktadha waonyesha kwamba Paulo hakuwa akikazia eneo hususa maishani, kama vile biashara au kazi ya kuajiriwa, na kutoa kanuni rasmi ya kufuatwa kwa habari hiyo. Badala ya hivyo, alikuwa akiwaandalia ndugu aliowapenda sana, shauri pana, lililo timamu, lenye msaada.

Kwa kielelezo, je, shauri hilo lingehusu katika hali ya Mkristo aliyetaka kuoa au kuolewa? Bila shaka. Katika barua yake ya kwanza, mtume aliwashauri Wakorintho waliotaka kuoa au kuolewa kufanya hivyo “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Alikazia hekima ya maneno hayo kwa yale aliyoandika baadaye, kama ilivyotaarifiwa kwenye 2 Wakorintho 6:14-18. Ikiwa Mkristo angefikiria kuoa au kuolewa na mtu ambaye hakuwa mtumishi wa Yehova na hakuwa mfuasi wa Kristo, yeye angekuwa akifikiria kufungamanishwa pamoja na asiyeamini. (Linganisha Mambo ya Walawi 19:19; Kumbukumbu la Torati 22:10.) Kwa wazi, kutokupatana huko kwa msingi kungeongeza uwezekano wa kuwa na matatizo, kutia na yale ya kiroho. Kwa kielelezo, huenda ikawa mtu huyo asiyeamini anafuatia kwa sasa au atafuatia kwa wakati ujao ibada ya kijimungu bandia. Paulo alisababu hivi: “Pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari?”

Lakini, namna gani sehemu nyingine ya maisha—kushiriki biashara pamoja na asiyeamini? Katika hali nyinginezo huenda Mkristo akahisi kwamba kupata riziki na kutunza familia yake kunahitaji kushiriki biashara na mtu fulani ambaye si Mkristo mwenzake. (1 Timotheo 5:8) Fikiria mambo haya ambayo ni vielelezo tu:

Huenda Mkristo akataka kuanza biashara ya kuuza aina fulani ya bidhaa, lakini njia pekee ingekuwa kukubali kushirikiana na mtu anayeweza kupata mazao au fedha zinazohitajiwa. Mkristo mwingine ataka kufanya ukulima (au kufuga aina fulani ya mifugo); lakini shamba halipatikani, kwa hiyo angelazimika kufanya hivyo pamoja na mtu fulani aliye tayari kumpangisha shamba ili ashiriki faida yoyote inayopatikana. Labda Mkristo mwingine hawezi kufanya biashara ya ufundi wa mabomba ya maji kwa sababu Kaisari hutoa leseni chache tu, nazo zimetwaliwa tayari; njia pekee ingekuwa ajiunge na mtu wa ukoo asiyeamini aliye na leseni.—Marko 12:17.

Hivyo ni vielezi tu. Hatujaribu kuonyesha hali zote zinazowezekana, wala hatutoi taarifa yoyote ya kukubali au kutokubali. Lakini kwa kufikiria vielelezo hivyo, je, huoni ni kwa nini shauri kwenye 2 Wakorintho 6:14-18 halipaswi kupuuzwa?

Mkristo aliyeshiriki biashara pamoja na asiyeamini, awe ni mtu wa ukoo au la, aweza sana kukabili matatizo na vishawishi visivyotazamiwa. Labda yule anayeshiriki naye akata maneno kwamba njia ya kupata faida inayofaa ni kutokuripoti machumo yote au kutokuripoti waajiriwa wote na machumo yao, hata kama hilo lingevunja sheria za serikali. Huenda akawa tayari kumlipa mleta-bidhaa kichini-chini kwa ajili ya bidhaa zisizoonyeshwa katika invoisi rasmi. Je! Mkristo angekuwa na sehemu yoyote katika mambo hayo au ukosefu wa haki wa jinsi hiyo? Na Mkristo angefanya nini wakati ulipofika wa wote wawili kutia sahihi karatasi za kodi au hati nyingine za kisheria kuhusu jinsi wanavyofanya biashara?—Kutoka 23:1; Warumi 13:1, 7.

Au huenda yule mshiriki wa biashara asiyeamini akataka kuweka akibani bidhaa zinazohusiana na sikukuu za kipagani, huenda akapeleka kadi za sikukuu kwa jina la kampuni, na kupamba mahali pa biashara kwa ajili ya sikukuu za kidini. Paulo aliuliza hivi: “Pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai.” Elezo hili lafaa kama nini: “Kwa hiyo, tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema Bwana [Yehova, NW], Msiguse kitu kilicho kichafu, nami nitawakaribisha”! (2 Wakorintho 6:16, 17) Kwa kutumia shauri hilo lenye hekima, Wakristo wengi wamechagua namna za kazi ya kimwili ambazo hazingewaletea matatizo mengi.—Waebrania 13:5, 6, 18.

Kutaniko haliagizwi kulinda au kuchunguza yote ambayo Wakristo wanafanya katika kazi zao za kimwili, wawe ni waajiri-kazi au wenye biashara. Bila shaka, ikiwa ingejulikana kwamba Mkristo ameshiriki katika ukosaji, kama vile kuendeleza ibada bandia au aina fulani ya kusema uwongo au kuiba, kutaniko lingelazimika kuchukua hatua ya kuunga mkono viwango vya Yehova.

Hata hivyo, jambo kuu ni kwamba shauri la Paulo lililopuliziwa, “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini,” laweza kuwasaidia Wakristo waepuke matatizo na hatua yoyote ya hukumu inayohitajiwa. Wakristo wenye hekima watatia maanani shauri hilo na kutokuchagua kuingia katika hali ambamo watakuwa chini ya msongo zaidi wa kuacha kanuni za Biblia. Mtu akihisi kwamba ni lazima ashiriki biashara pamoja na asiyeamini, wengine hawapaswi kuwa wepesi kumhukumu au kumchambua, waking’amua kwamba atalazimika kuchukua daraka la chaguo lake. Kwa msingi, Paulo hakuwa akiweka kanuni rasmi, ya kufuatwa dhidi ya kushiriki biashara pamoja na asiyeamini. Bado, shauri lake halipasi kupuuzwa. Mungu alipulizia shauri hilo akaagiza lirekodiwe katika Biblia kwa manufaa yetu. Tutakuwa wenye hekima tukilitii.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki