Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
‘Waliendelea Bila Kuacha’
TANGU siku za Yesu Kristo na mitume wake, viongozi wa kidini wamejaribu kutumia kila mbinu katika jitihada zao za kuzuia kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu. Mara nyingi mitume ‘waliamriwa’ kwa nguvu na wenye mamlaka katika Yerusalemu “wasinene kwa jina lake Yesu.” (Matendo 5:27, 28, 40) Hata hivyo, masimulizi ya Biblia yasema kwamba “Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu.”—Matendo 6:7.
Mileani mbili baadaye tungali twapata viongozi wa kidini katika Israeli wanaoshawishi wenye mamlaka kuzuia kazi ya Wakristo wa kweli katika nchi hiyo. Wakiwa chini ya mkazo kutoka kwa vikundi vya kidini vyenye ushupavu, katika Novemba 1987, wenye mamlaka katika Tel Aviv, Israeli, waliwaamuru Mashahidi kukomesha kufanya mikutano ya Kikristo katika Jumba la Ufalme lililokuwa katika ofisi ya tawi ya Watch Tower Society. Amri hiyo ilitekelezwa Oktoba 1989. Kwa utii, Mashahidi walikutana katika majengo yaliyokodiwa katika eneo hilo kwa miaka mitatu huku Jumba lao la Ufalme likibaki karibu bila kutumiwa.
Wakati uo huo, suala hilo lililetwa mbele ya Mahakama Kuu ya Haki ya Israeli. Ofisi ya wakili wa serikali ilipitia hoja zilizotolewa na Mashahidi na kutangaza kwamba haingewezekana kupinga rufani yao kwa sababu ya ubaguzi wa wazi wa kidini uliohusika. Hivyo, wenye mamlaka hawakuwa na la kufanya ila tu kutangua uamuzi wao, na Mashahidi wa Yehova walirudi kwa furaha katika Jumba lao la Ufalme.
Je, kazi ya kuhubiri kweli za Biblia iliathiriwa katika miaka hiyo? La, hasha! Jumba la Ufalme lilipofungwa, kulikuwa na makutaniko mawili katika Tel Aviv na kikundi kingine cha funzo la Biblia katika mji wa Lod ulio karibu. Miaka mitatu baadaye, Jumba la Ufalme lilipofunguliwa tena, Mashahidi wa Yehova walikuwa wameongezeka kufikia makutaniko manne, na kikundi kipya cha funzo la Biblia kilikuwa kikikutania Beersheba.
Ukuzi katika Israeli hautokei tu katika vikundi vikubwa vya lugha, Kiarabu na Kiebrania. Kumekuwa na mmiminiko mkubwa wa wahamiaji kutoka ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, kwa hiyo Mashahidi wa Yehova wasemao Kirusi sasa wana shughuli nyingi za kushiriki nao habari njema. Mikutano fulani katika lugha ya Kirusi hufanywa katika makutaniko matatu; hivi majuzi, zaidi ya watu mia moja walikusanyika katika kusanyiko la Kirusi.
Bila shaka, watu wa kidini wenye ubaguzi wataendelea na vita vyao dhidi ya ibada ya kweli. Lakini wapiga-mbiu wa Ufalme huendelea kuiga Wakristo wa karne ya kwanza ambao, wajapopingwa, “waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya yule Kristo, Yesu.”—Matendo 5:42, NW.