Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 12/1 kur. 24-28
  • Yehova Amekuwa Kimbilio Langu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Amekuwa Kimbilio Langu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ziara ya Maana
  • Msimamo Wetu kwa Ajili ya Kweli ya Biblia
  • Kuvumilia Upinzani Wenye Nguvu
  • Kupambana na Magonjwa Mabaya
  • Kupainia Ujapokuwa Upinzani
  • Jambo Lililoonwa Lenye Kuthawabisha
  • Yehova Amekuwa Mwema Kwangu
  • Nilipata Utajiri wa Kweli Katika Australia
    Amkeni!—1994
  • Shangwe na Matatizo ya Kuwalea Watoto Wanane Ili Wafuate Njia za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kumtumikia Mungu Nyakati za Magumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 12/1 kur. 24-28

Yehova Amekuwa Kimbilio Langu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA PENELOPE MAKRIS

Mamangu alinisihi sana: “Mwache mumeo; nduguzo watakutafutia aliye bora.” Kwa nini mamangu mwenye upendo atake niikomeshe ndoa yangu? Ni nini kilichokuwa kimemuudhi hivyo?

NILIZALIWA mwaka wa 1897 katika kijiji kidogo cha Ambelos, kwenye kisiwa cha Samos. Familia yetu ilikuwa na washiriki wachaji wa Kanisa Othodoksi la Kigiriki. Baba alikufa muda mfupi kabla ya kuzaliwa kwangu, na ikabidi mama, ndugu zangu watatu, na mimi kujitahidi ili tu kusalimika miongoni mwa umaskini mwingi wa nyakati hizo.

Vita ya Ulimwengu 1 ilianza ghafula mwaka wa 1914, na upesi baadaye kaka zangu wawili wakaamuriwa wajiandikishe jeshini. Lakini ili kuepuka kufanya hivyo, walihamia Marekani, wakituacha mimi na ndugu yangu mwingine nyumbani pamoja na mama. Miaka michache baadaye, mwaka wa 1920, niliolewa na Dimitris, mwalimu kijana katika kijiji chetu.

Ziara ya Maana

Upesi baada ya kuolewa, kaka ya mamangu alikuja kutuzuru kutoka Marekani. Alipata kuleta mojawapo ya mabuku ya Studies in the Scriptures, lililoandikwa na Charles Taze Russell. Kilikuwa kichapo cha Wanafunzi wa Biblia, wanaojulikana sasa kama Mashahidi wa Yehova.

Dimitris alipokifungua hicho kitabu, aliona habari aliyokuwa ametaka kujua juu yayo tangu alipokuwa mtoto, “Inakuwaje kwa mwanadamu anapokufa?” Akiwa katika shule ya sekondari alikuwa amemwuliza mwanatheolojia wa Othodoksi ya Kigiriki kuhusu habari hiyohiyo lakini hakuwa amepokea jibu lenye kuridhisha. Elezo la wazi na lenye kupatana na akili lililoandaliwa katika hicho kichapo lilimpendeza Dimitris sana hivi kwamba alienda moja kwa moja hadi mkahawa wa kijiji, ambako wanaume katika Ugiriki walikuwa na desturi ya kukusanyika. Huko alisimulia mambo aliyokuwa amejifunza kutoka katika Biblia.

Msimamo Wetu kwa Ajili ya Kweli ya Biblia

Kufikia wakati huo—katika miaka ya mapema ya 1920—Ugiriki ilikuwa katikati ya vita nyingine. Dimitris aliandikishwa jeshini akatumwa barani Uturuki, katika Asia Ndogo. Alijeruhiwa akatumwa nyumbani. Baada ya kupona, niliambatana naye hadi Smirna, Asia Ndogo (sasa Izmir, Uturuki). Vita ilipoisha ghafula mwaka wa 1922, ilitubidi tutoroke. Kwa hakika, tuliponyoka chupuchupu hadi Samos, katika mashua iliyoharibika vibaya. Tulipowasili nyumbani, tulipiga magoti na kumshukuru Mungu—Mungu ambaye tulikuwa tungali na ujuzi mchache tu kumhusu.

Upesi Dimitris akapewa mgawo wa kufundisha kwenye shule katika Vathy, mji mkuu wa kisiwa hicho. Aliendelea kusoma fasihi za Wanafunzi wa Biblia, na usiku mmoja wenye mvua nyingi wawili kati yao kutoka kisiwa cha Chios walituzuru. Walikuwa wamerudi kutoka Marekani ili kutumikia wakiwa makolpota, kama vile waeneza-evanjeli wa wakati wote walivyokuwa wakiitwa wakati huo. Tuliwapa makao usiku huo, nao wakatuambia mambo mengi kuhusu makusudi ya Mungu.

Baadaye Dimitris aliniambia hivi: “Penelope, nang’amua kwamba hii ndiyo kweli, na ni lazima niifuate. Hili lamaanisha kwamba inanibidi niache kuimba katika Kanisa Othodoksi la Kigiriki, na kwamba siwezi kuhudhuria kanisa pamoja na watoto wa shule.” Ingawa ujuzi wetu juu ya Yehova ulikuwa mchache, tamaa yetu ya kumtumikia ilikuwa yenye nguvu. Kwa hiyo nilijibu hivi: “Sitakuwa kizuizi kwako. Songa mbele tu.”

Akaendelea kusema kwa kusitasita kidogo: “Ndiyo, lakini mwendo wetu ukidhihirika, nitapoteza kazi yangu.”

“Usiwe na wasiwasi,” nikasema, “kwani watu wote hujiruzuku kwa kazi ya kufundisha? Sisi ni vijana na wenye nguvu, na kwa msaada wa Mungu twaweza kupata kazi nyingine.”

Karibu na wakati huo tulipata kujua kwamba Mwanafunzi mwingine wa Biblia—aliyekuwa kolpota pia—alikuwa amekuja Samos. Tuliposikia kwamba polisi walikuwa wamekataa kumpa ruhusa ya kutoa hotuba ya Biblia ya watu wote, tulienda kumtafuta. Tulimpata katika duka akizungumza na wanatheolojia wawili wa Othodoksi ya Kigiriki. Wakiona aibu kwa sababu ya kutoweza kutetea itikadi zao kwa kutumia Biblia, hao wanatheolojia waliondoka upesi. Mume wangu, akiwa amevutiwa na ujuzi wa huyo kolpota, akauliza: “Ni vipi kwamba waweza kuitumia Biblia kwa urahisi hivyo?”

“Sisi hujifunza Biblia kwa utaratibu,” akajibu. Akiufungua mkoba wake, alitoa kile kitabu cha funzo The Harp of God akatuonyesha jinsi ya kukitumia kitabu hicho katika funzo hilo. Tulikuwa na hamu sana ya kujifunza hivi kwamba mume wangu na mimi, yule kolpota, na wanaume wengine wawili tukaambatana mara moja na mwenye duka hadi nyumbani kwake. Yule kolpota alitolea kila mmoja wetu nakala ya kitabu The Harp of God, nasi tukaanza kujifunza mara hiyohiyo. Tuliendelea na funzo letu hadi kupita sana usiku wa manane, kisha alfajiri ilipokaribia, tukaanza kujifunza nyimbo zilizoimbwa na Wanafunzi wa Biblia.

Tokea wakati huo na kuendelea, nikaanza kujifunza Biblia kwa muda wa saa kadhaa kila siku. Wanafunzi wa Biblia kutoka ng’ambo waliendelea kutupa sisi ugavi wa misaada ya kujifunza Biblia. Katika Januari 1926, nilijiweka wakfu kwa Mungu katika sala, nikiweka nadhiri ya kufanya mapenzi yake bila masharti. Baadaye katika kiangazi hicho mume wangu nami tukaonyesha wakfu wetu kwa ubatizo wa maji. Tulikuwa na tamaa yenye nguvu ya kusema na wengine kuhusu mambo tuliyokuwa tukijifunza, kwa hiyo tukaanza katika huduma ya mlango hadi mlango kwa kutumia ile trakti Message of Hope.

Kuvumilia Upinzani Wenye Nguvu

Siku moja nilialikwa na mwanamke kijana kuhudhuria kawaida ya ibada kwenye kikanisa cha Othodoksi ya Kigiriki. “Nimeacha kumtumikia Mungu katika njia hiyo,” nikaeleza. “Sasa mimi humwabudu kwa roho na kweli, sawa na vile Biblia hufundisha.” (Yohana 4:23, 24) Alipigwa na butaa akaripoti kotekote jambo lililokuwa limetukia, akimhusisha mume wangu pia.

Karibu kila mtu alianza kupinga. Hatukuweza kupata amani popote—wala nyumbani mwetu wala kwenye mikutano tuliyofanya pamoja na wale watu wachache wenye kupendezwa kwenye hicho kisiwa. Kwa kuchochewa na mapadri Waothodoksi, umati ulikusanyika nje ya mahali petu pa kukutania, ukirusha mawe na kututukana kwa sauti kubwa.

Tulipogawanya ile trakti Message of Hope, watoto walikusanyika kutuzunguka wakipaaza sauti “Wamileani” na maneno mengine ya kuvunja heshima. Wafanyakazi wenzi wa mume wangu wakaanza pia kumletea matata. Mwisho-mwisho wa mwaka 1926 alifikishwa mahakamani, akashtakiwa kuwa hafai kuwa mwalimu wa shule ya umma, na kuhukumiwa kifungo cha siku 15 gerezani.

Mama alipopata kujua hilo, alinisihi nimwache mume wangu. “Sikiliza, mamangu mpendwa,” nikajibu, “wajua kadiri nijuavyo jinsi ninavyokupenda na kukustahi. Lakini siwezi kwa vyovyote kukuruhusu utuzuie tusimwabudu Mungu wa kweli, Yehova.” Alirudi kijijini kwake akiwa ametamauka sana.

Katika 1927 kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia lilifanywa Athene, na Yehova akatufungulia njia ya kuhudhuria. Tulisisimuka na kuimarishwa kiroho kwa kukusanyika na waamini wenzetu wengi sana. Tuliporudi Samos, tuligawanya nakala 5,000 za trakti yenye kichwa A Testimony to the Rulers of the World katika miji na vijiji vya kisiwa chetu.

Karibu na wakati huo Dimitris aliachishwa kazi yake ya kufundisha, na kwa sababu ya ubaguzi dhidi yetu, ilikuwa karibu haiwezekani kupata kazi. Lakini kwa kuwa niliweza kushona nguo na Dimitris alikuwa stadi wa kupaka rangi, tuliweza kujiruzuku. Mwaka wa 1928 mume wangu, pamoja na ndugu Wakristo wengine wanne katika Samos, walihukumiwa kifungo cha miezi miwili gerezani kwa sababu ya kuhubiri habari njema. Nikiwa Mwanafunzi wa Biblia pekee aliye huru, niliweza kuwaandalia chakula gerezani.

Kupambana na Magonjwa Mabaya

Wakati mmoja nilipatwa na ugonjwa wa vivimbe vya uti wa mgongo, ugonjwa wenye kudumu usiojulikana wakati huo. Nilipoteza hamu yangu ya kula chakula nikawa na homa kali yenye kuendelea. Matibabu yalihusisha kutiwa ndani ya subu ya mwili ya lipu kutoka shingo yangu hadi mapaja yangu. Ili kukabiliana kifedha, mume wangu aliuza uwanja ili niweze kuendelea na tiba. Kwa kusononeka, nilisali nikimwomba Mungu kila siku anipe nguvu.

Walipokuwa wakinizuru, watu wa ukoo walichochea upinzani sikuzote. Mama alisema tulikuwa tukipatwa na matata hayo yote kwa sababu tulikuwa tumebadili dini yetu. Nikiwa siwezi kujongea, nililowesha mto wangu machozi huku nikimwomba sana Baba yetu wa kimbingu anipe subira na moyo mkuu ili nivumilie.

Kwenye meza yangu kando ya kitanda, niliweka Biblia yangu na ugavi wa vijitabu na trakti kwa ajili ya wageni. Ilikuwa baraka kwamba mikutano ya kutaniko letu dogo ilifanywa nyumbani mwetu; niliweza kupokea kitia-moyo cha kiroho kwa ukawaida. Ilitubidi tuuze uwanja mwingine ili kulipia matibabu kutoka kwa daktari katika Athene.

Upesi baada ya hapo, mwangalizi asafiriye alituzuru. Alisikitika sana kuniona nikiwa katika hali hiyo na Dimitris akiwa bila kazi. Kwa fadhili alitusaidia kufanya mipango ya kuishi Mytilene kwenye kisiwa cha Lesbos. Tulihamia huko mwaka wa 1934, na Dimitris akaweza kupata kazi ya kuajiriwa. Huko tulipata pia ndugu na dada Wakristo wa ajabu walionitunza katika ugonjwa wangu. Polepole, baada ya miaka mitano ya matibabu, nilikuwa nimepona kabisa.

Hata hivyo, mwaka wa 1946, muda mfupi baada ya Vita ya Ulimwengu 2, nilipatwa na maradhi mabaya, wakati huu nilipatwa na vivimbe vya kitambi cha tumbo. Nilikuwa kitandani kwa miezi mitano nikiwa na homa kali na maumivu mabaya. Lakini, kama hapo awali, sikuacha kuwaambia wageni wangu kumhusu Yehova. Hatimaye, nilipata nafuu.

Kupainia Ujapokuwa Upinzani

Upinzani usiokoma ulikuwa fungu la Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki miaka ya baada ya vita. Tulikamatwa mara nyingi sana tulipokuwa tukishiriki katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Mume wangu alitumikia vifungo vya gerezani vilivyojumlika kuwa karibu muda wa mwaka mmoja. Tulipoanza siku yetu ya huduma, kwa kawaida tulipangia kupisha usiku kwenye kituo cha polisi tukiwa tumekamatwa. Hata hivyo Yehova hakutuacha kamwe. Sikuzote aliandaa moyo mkuu na nguvu zilizohitajiwa ili kuvumilia.

Katika miaka ya 1940, nilisoma katika Informant (sasa Huduma ya Ufalme Yetu) kuhusu uandalizi wa upainia wa likizo. Nikaamua kujaribu kushiriki katika sehemu hiyo ya utumishi iliyotaka mtu kutoa muda wa saa 75 kwa mwezi katika huduma. Likiwa tokeo, ziara zangu za kurudia na mafunzo ya Biblia yaliongezeka—kwa muda fulani nilikuwa nikiongoza mafunzo 17 kila juma. Nilianzisha pia njia ya kupelekea watu magazeti kwa ukawaida katika eneo la biashara la Mytilene, nilikopeleka kwa ukawaida nakala zipatazo 300 za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwenye maduka, ofisi, na benki.

Mwangalizi asafiriye alipotumikia kutaniko letu mwaka wa 1964, alisema: “Dada Penelope, niliona kutoka Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri yako kwamba unapata matokeo ya ajabu katika huduma yako. Kwa nini usijaze ombi la upainia wa kawaida?” Nitashukuru sikuzote kwa ajili ya kitia-moyo chake; huduma ya wakati wote imekuwa shangwe yangu kwa miongo zaidi ya mitatu.

Jambo Lililoonwa Lenye Kuthawabisha

Katika Mytilene kuna mtaa wenye idadi kubwa ya watu ulioitwa Langada, walikoishi wakimbizi Wagiriki. Tuliepuka kwenda mlango hadi mlango huko kwa sababu ya upinzani wenye ushupavu tuliokuwa tumekabili. Hata hivyo, mume wangu alipokuwa gerezani, ilinibidi nipitie eneo hilo ili kumtembelea. Siku moja yenye mvua nyingi mwanamke fulani alinialika nyumbani kwake ili kuniuliza ni kwa nini mume wangu alikuwa gerezani. Nilieleza kwamba ilikuwa kwa sababu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kwamba alikuwa akiteseka sawa tu na vile Kristo alivyokuwa ameteseka.

Hatimaye, mwanamke mwingine akapanga nimtembelee nyumbani kwake. Nilipowasili nilipata kwamba alikuwa amealika jumla ya wanawake 12. Nilitazamia uwezekano wa upinzani, kwa hiyo nilisali kwa Mungu anipe hekima na moyo mkuu wa kukabili chochote kile kilichotukia. Hao wanawake walikuwa na maswali mengi, na baadhi yao walizusha vipingamizi, lakini niliweza kuandaa majibu ya Kimaandiko. Niliposimama ili niondoke, mwanamke wa hiyo nyumba aliniomba nirudi tena siku iliyofuata. Nilikubali huo mwaliko kwa furaha. Tulipowasili pamoja na mwandamani fulani siku iliyofuata, tulipata hao wanawake wakingojea tayari.

Baada ya hapo mazungumzo yetu ya Kimaandiko yaliendelea kwa ukawaida, na mafunzo mengi ya Biblia yalianzishwa. Wanawake kadhaa walifanya maendeleo katika ujuzi sahihi, na familia zao pia zilifanya maendeleo. Baadaye kikundi hicho kilifanyiza kiini cha kutaniko jipya la Mashahidi wa Yehova katika Mytilene.

Yehova Amekuwa Mwema Kwangu

Katika miaka ambayo imepita Yehova amebariki jitihada za mume wangu na zangu za kumtumikia Yeye. Wale Mashahidi wachache sana wa Samos katika miaka ya 1920 wameongezeka wakawa makutaniko mawili na kikundi kimoja kukiwa na wahubiri wapatao 130. Na kwenye kisiwa cha Lesbos, kuna makutaniko manne na vikundi vitano vinavyotia ndani wapiga-mbiu 430 wa Ufalme. Mume wangu alipiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kwa bidii hadi kifo chake mwaka wa 1977. Ni pendeleo lililoje kuona wale tuliowasaidia wangali wakiendelea kwa bidii katika huduma! Kwani, pamoja na watoto wao, wajukuu wao, na vitukuu wao, wao wanafanyiza umati mkubwa unaomwabudu Yehova kwa muungano!

Mwendo wangu wa utumishi wa Kikristo, ambao sasa wafikia muda wa miaka mingi kupita 70, haujawa rahisi. Hata hivyo Yehova amekuwa ngome isiyo na kifani. Kwa sababu ya uzee na afya inayozorota, siwezi kuondoka kitandani na siwezi kuhubiri sana. Lakini, kama vile mtunga-zaburi, naweza kumwambia Yehova: “[Ndiwe] kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini.”—Zaburi 91:2.

(Dada Makris alikufa makala hii ilipokuwa ikitayarishwa. Yeye alikuwa na tumaini la kimbingu.)

[Picha katika ukurasa wa 26]

Pamoja na mume wake mwaka wa 1955

[Picha katika ukurasa wa 26]

Dada Makris angalikuwa na umri wa miaka 100 katika Januari 1997

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki