Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 8/1 kur. 26-29
  • Funzo la Familia Ambalo Huleta Shangwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Funzo la Familia Ambalo Huleta Shangwe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Twapaswa Kujifunza Nini?
  • Dumisha Mazingira ya Utulivu
  • Fanya Biblia Ipendeze
  • Saidia Kila Mmoja Kushiriki
  • Wasiliana—Usisumbue!
  • Juhudi Hizo Ni Zenye Kufaa
  • Jifunzeni Neno la Mungu kwa Ukawaida Mkiwa Familia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Ratiba ya Familia—Funzo la Familia
    Huduma ya Ufalme—2005
  • Fanya Bidii ili Kuihifadhi Familia Yako Iingie Ndani ya Ulimwengu Mpya wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Kuongoza Mafunzo ya Biblia ya Familia Yenye Kujaa Maana
    Huduma Yetu ya Ufalme—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 8/1 kur. 26-29

Funzo la Familia Ambalo Huleta Shangwe

“Kwa maarifa [“ujuzi,” “NW”] vyumba vyake hujazwa vitu vyote vya thamani na vya kupendeza,” husema Biblia. (Mithali 24:4) Vitu hivi vya thamani na vya kupendeza si hazina za kimwili tu bali vyatia ndani upendo wa kweli, hofu ya kimungu, na imani yenye nguvu. Sifa kama hizo kwa kweli hutokeza maisha ya familia yenye ubora. (Mithali 15:16, 17; 1 Petro 1:7) Lakini, ili kuzipata, twahitaji kuleta ujuzi wa Mungu katika nyumba zetu.

KICHWA cha familia ana wajibu wa kukazia kikiki ujuzi huu katika washiriki wa familia. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Waefeso 5:25, 26; 6:4) Moja kati ya njia bora zaidi za kufanya hivi ni kupitia funzo la kawaida la familia. Hilo laweza kupendeza washiriki kama nini wakati funzo linapoongozwa katika njia ambayo ni ya kufundisha na pia ya kufurahisha! Hivyo basi, acheni tufikirie baadhi ya mambo muhimu katika kuongoza funzo lenye mafanikio la familia.a

Funzo la familia ni lenye matokeo zaidi linapokuwa la kawaida. Likiachiliwa hadi nafasi ijitokeze yenyewe au kufanywa kwa ghafula, yaelekea halitakuwa na matokeo mazuri. Hivyo ni lazima ‘kununua wakati’ kwa ajili ya funzo. (Waefeso 5:15-17) Kuchagua wakati wa kawaida ambao ni wenye kufaa wote kwaweza kuwa jambo gumu. “Tulikuwa na tatizo katika kudumisha funzo letu la familia kuwa la kawaida,” akiri kichwa kimoja cha familia. “Tulijaribu nyakati tofauti-tofauti hadi hatimaye tukapata wakati fulani jioni kidogo ambao ulitufaa sote. Sasa funzo letu la familia ni la kawaida.”

Baada ya kupata wakati unaofaa, uwe mwangalifu usiruhusu vikengeusha-fikira kuondoa funzo hilo. “Ikiwa wageni wangefika wakati tulipokuwa na funzo,” akumbuka Maria,b ambaye sasa ana umri wa miaka 33, “baba angewakaribisha wangoje hadi funzo lilipoisha. Na kwa habari ya simu, angemwambia tu huyo mtu kwamba angeweza kumpigia simu tena baadaye.”

Hata hivyo, hili halina maana kwamba hakuwezi kuwa na nafasi ya kubadilikana. Dharura au mambo yasiyotazamiwa yaweza kutokea, na yaweza kuwa lazima kufuta au kuahirisha funzo kwa wakati fulani. (Mhubiri 9:11) Hata hivyo uwe mwangalifu sana usiruhusu lolote kati ya mambo hayo livuruge kawaida yenu.—Wafilipi 3:16.

Funzo linapaswa kuchukua muda gani? Robert, ambaye amelea kwa mafanikio binti na mwana, asema: “Kwa kawaida funzo letu lilichukua saa moja. Watoto walipokuwa wachanga, tulijaribu kudumisha upendezi wao wakati wa saa hiyo kwa kuchunguza mambo tofauti-tofauti, kama vile mafungu machache katika makala ya funzo katika Mnara wa Mlinzi, sehemu zilizochaguliwa katika Biblia, na sehemu za vichapo vingine.” Maria akumbuka: “Dada zangu wawili na mimi tulipokuwa wachanga sana, funzo letu lilikuwa la karibu dakika 20 mara mbili au tatu kwa juma. Kadiri tulivyoendelea kukua, funzo letu la familia la kila juma lilidumu kwa saa moja hivi.”

Twapaswa Kujifunza Nini?

Kufikiria swali hili wakati kila mmoja amekaa mezani kwa ajili ya funzo kungetokeza kukatishwa tamaa na kupotezwa kwa wakati wenye thamani wa funzo. Ikiwa ndivyo ilivyokuwa, watoto wasingekuwa na jambo maalumu wanalotazamia kwa hamu na kwa muda mfupi wangepoteza upendezi. Hivyo chagua mapema moja kati ya vichapo vya Sosaiti ili mjifunze.

“Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameandaa vichapo vingi viwezavyo kuchaguliwa. (Mathayo 24:45-47) Labda waweza kuchagua kitabu kimoja ambacho familia haijajifunza bado. Ni jambo lenye kupendeza kama nini kujifunza sehemu zilizochaguliwa kutoka Insight on the Scriptures ikiwa mabuku haya yanapatikana katika lugha yako! Kwa kielelezo, mngeweza kupitia makala juu ya Mlo wa Jioni wa Bwana wakati wa majuma yanayotangulia Ukumbusho. Familia nyingi hufurahia kutayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi la juma hilo. Lakini makala nyingine katika Mnara wa Mlinzi pia huandaa mambo bora kabisa kwa ajili ya funzo. Kichwa cha familia ambaye ajua mahitaji ya kiroho ya familia, yupo katika hali bora kabisa ya kuamua ni kichapo kipi kinachopasa kusomwa.

“Wakati wote tulijifunza kichapo kilichoteuliwa mapema,” akumbuka Maria. “Lakini swali lilipotokea au hali ilipojitokeza shuleni, basi tungebadilika kwenda kwenye habari yenye kufaa.” Mahangaiko ya pekee, kama vile matatizo wanayokabili vijana shuleni, miadi ya kijinsia, utendaji wa baada ya masomo, na kadhalika, hutokea. Hili litokeapo, teua makala au vichapo ambavyo hushughulikia tatizo hilo hasa. Ukiona habari katika toleo la karibuni zaidi la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambayo ungependa kujifunza na familia mara moja, usisite kupanga. Bila shaka, ungependa kuwaarifu washiriki wa familia juu ya mabadiliko hayo kabla ya wakati. Lakini uhakikishe kurudi katika ratiba mara uhitaji huo unapokuwa umeshughulikiwa.

Dumisha Mazingira ya Utulivu

Kujifunza huwa bora zaidi katika mazingira ya amani. (Yakobo 3:18) Hivyo sitawisha mazingira ya kimapumziko, lakini bado yenye staha. Kichwa kimoja cha familia katika Marekani alisema: “Tuwe tunajifunza sebuleni au katika varanda, twajitahidi kukaa karibu-karibu badala ya kukaa mbalimbali katika chumba kikubwa. Kwetu, hili hutokeza hisia changamfu.” Na Maria akumbuka kwa shauku sana: “Dada zangu nami tuliruhusiwa kuchagua mahali katika nyumba ambapo tungependa kuwa na funzo katika juma hilo. Hili lilitufanya tuhisi tumestarehe.” Kumbuka kwamba nuru ya kutosha, mpango wa kuketi wa kufaa, na mazingira yenye uchangamfu na yasiyo na vitu vilivyotapakaa yote huchangia kuwa na utulivu. Kuwa na viburudisho kwa ajili ya familia baada ya funzo pia husaidia kufanya jioni hiyo iwe yenye kupendeza.

Baadhi ya familia hata huchagua kutia ndani familia nyingine katika funzo lao pindi kwa pindi, likifanya funzo liwe la kupendeza zaidi na vilevile kutokeza maelezo tofauti-tofauti. Wapya katika kweli waalikwapo kushiriki katika mpango huu, wao waweza kufaidika kutokana na kuangalia kichwa cha familia mwenye uzoefu akiongoza funzo la familia.

Fanya Biblia Ipendeze

Fanya vipindi vya kujifunza kuwa vyenye kupendeza watoto, nao watavitazamia kwa hamu. Waweza kufanya hivyo kwa kuwatia moyo watoto wadogo wachore picha za mandhari za Biblia. Inapofaa, wafanye watoto waigize matukio ya Biblia na drama. Kwa watoto wachanga si lazima kushikamana na njia ya kawaida ya maswali na majibu. Kusoma au kuwaeleza hadithi za watu katika Biblia ni njia ya kufurahisha ya kukazia kikiki kanuni za kimungu. Robert, aliyetajwa mapema, akumbuka: “Nyakati nyingine tulikuwa tukisoma sehemu za Biblia, tukifanya zamu, tukiiga ‘sauti’ tofauti-tofauti tuliyogawiwa.” Watoto waweza kukaribishwa kuchagua watu ambao wanataka kuwaiga katika usomaji.

Kutumia ramani na chati kutawasaidia watoto wakubwa kupiga picha akilini maeneo na hali za bara ambapo matukio yanayozungumziwa yalitukia. Kwa wazi, kwa ubunifu kidogo, funzo la familia laweza kuwa lenye kupendeza na lenye ubadilifu. Na watoto watafanyiza hamu sana ya Neno la Mungu.—1 Petro 2:2, 3.

Saidia Kila Mmoja Kushiriki

Ili watoto wafurahie funzo, ni lazima wahisi wamehusishwa. Hata hivyo, kufanya watoto wa umri tofauti-tofauti kushiriki kwaweza kuwa jambo gumu. Lakini kanuni moja ya Biblia yasema: “Yeye asimamiaye, acheni afanye hilo katika bidii halisi.” (Waroma 12:8) Kuwa mwenye idili husaidia, kwani idili huambukiza.

Ronald humhusisha binti yake Dina mwenye umri wa miaka mitano kwa kumfanya asome vichwa vidogo katika makala ya kujifunza na kumwomba atoe maelezo juu ya picha. Ukumbusho wa kifo cha Kristo ulipokuwa ukikaribia mwaka uliopita, alikazia vielezi vilivyohusika katika kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi.c Asema: “Hili lilimsaidia kuelewa umuhimu wa tukio hilo.”

Akiwa na binti yake Misha, mwenye umri wa miaka 10, Ronald huchukua hatua ya ziada. “Misha amefanya maendeleo kufikia hatua ya kuelewa si vielezi tu bali pia maana yake,” asema Ronald. “Hivyo tulipokuwa tukijifunza kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!,d tulikazia maana ya vielezi, na hili limemsaidia.”

Watoto waingiapo miaka ya utineja, waalike waonyeshe matumizi ya yale mambo wanayojifunza. Maswali yazukapo wakati wa funzo, toa mgawo wa kufanya uchunguzi. Robert alifanya hivyo wakati mvulana wake Paul, mwenye umri wa miaka 12, alipouliza swali kuhusu klabu iliyoanzishwa shuleni inayohusu mchezo wa Dungeons and Dragons. Paul na wengine katika familia walichunguza habari kwa kutumia Watchtower Publications Index, nao waliipitia wakati wa funzo lao la familia. “Tokeo ni kwamba,” asema Robert, “Paul alifahamu mara moja kwamba huo mchezo haukufaa Wakristo.”

Pia Robert alitoa migawo ya utafiti nyakati nyingine. Mke wake Nancy akumbuka: “Tulipofanya utafiti juu ya mitume wa Yesu, kila mmoja wetu aligawiwa mtume mmoja kila juma. Ilisisimua kama nini kuona watoto wakitoa ripoti zao kwa shauku wakati wa funzo la familia!” Kufanya utafiti wao na kushiriki habari pamoja na familia huwasaidia watoto ‘kukua mbele za BWANA.’—1 Samweli 2:20, 21.

Kuuliza maswali—ya maoni na vilevile ya kuongoza kwenye jibu—pia ni njia nzuri ya kuwafanya watoto wahusike. Mwalimu Stadi, Yesu, aliuliza maswali ya maoni kama vile, “Wewe wafikiri nini?” (Mathayo 17:25) “Yeyote kati yetu alipokuwa na maswali, wazazi wetu hawakutujibu moja kwa moja kamwe,” akumbuka Maria. “Wakati wote waliuliza maswali ya kuongoza, wakitusaidia kufikiri juu ya jambo hilo.”

Wasiliana—Usisumbue!

Shangwe ya funzo la familia inaongezwa ikiwa wote waliopo waweza kuwasilisha maoni yao na hisia zao bila hofu ya kudhihakiwa. Lakini “uwasiliano mzuri wakati wa funzo la familia unawezekana tu ikiwa njia za uwasiliano ziko wazi nyakati nyinginezo,” asema baba mmoja. “Huwezi kujifanya kuwa na uwasiliano mzuri kwa ajili ya funzo tu.” Kwa vyovyote, epuka maelezo yasiyofikiriwa ambayo yanachoma, kama vile, ‘Ni hayo tu? Nilifikiri ni jambo fulani la maana’; ‘Huo ni upumbavu’; ‘Hakuna jambo zuri uwezalo kufanya. Wewe ni mtoto tu.’ (Mithali 12:18) Uwe mwenye huruma na mwenye rehema kwa watoto wako. (Zaburi 103:13; Malaki 3:17) Uwafurahie, na uwaunge mkono wajitahidipo kutumia yale wanayojifunza.—Mithali 29:17.

Mazingira ya funzo la familia yapaswa kuwa yale ambayo yanafanya akili ya mtoto ipokee maagizo. “Uanzapo kuwasahihisha watoto,” aeleza mzazi mmoja aliyefanikiwa mwenye watoto wanne, “wao huwa na uhasama wa kadiri fulani.” Katika mazingira kama hayo, labda hawataelewa habari hiyo. Hivyo epuka kufanya vipindi vya funzo kuwa nyakati za kutia nidhamu na kutoa adhabu. Ikiwa zinahitajika, zitoe baadaye na kwa mtoto hususa.

Juhudi Hizo Ni Zenye Kufaa

Kujenga familia ya kiroho huchukua wakati na jitihada. Lakini mtunga-zaburi atangaza: “Tazama, wana ndio urithi wa BWANA, uzao wa tumbo ni thawabu.” (Zaburi 127:3) Na wazazi wamekabidhiwa daraka la “kuwalea [watoto] katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Hivyo kuza stadi za kuongoza funzo la familia lenye matokeo na lenye kufurahisha. Fanya yote uwezayo ili kuandaa “maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno,” ili kwamba watoto wako waweze “kufikia wokovu.”—1 Petro 2:2; Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

a Ingawa madokezo mengi katika makala hii yanahusu kuwasaidia watoto katika funzo la familia, hayo yatumika pia kwa funzo la familia ambako hakuna watoto.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.

c Kilichapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

d Kilichapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki