Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Vijana Wamsifu Mungu Katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo
KARNE kadhaa zilizopita, mtunga-zaburi aliwaalika kwa uchangamfu vijana wajiunge katika kumsifu Mfalme wa umilele: “Vijana waume, na wanawali, wazee, na watoto . . . [sifuni] jina la BWANA, maana jina lake peke yake limetukuka.” (Zaburi 148:12, 13) Mambo yaliyoonwa yafuatayo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yakazia pendeleo hilo lisilo na kifani.
• Bwana-kabaila wa painia wa pekee fulani alivutiwa vizuri na mwenendo wa Mashahidi wa Yehova. Hivyo aliwaruhusu Mashahidi wajifunze Biblia na Fifi, binti yake mwenye umri wa miaka mitano. Baada ya kuchunguza kwa makini maendeleo ya Fifi katika kujifunza Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia,a baba yake alimruhusu ahudhurie mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Huko, Fifi mdogo alijifunza nyimbo za Ufalme kutoka katika kitabu cha nyimbo cha Mashahidi. Alipenda hasa wimbo namba 4, wenye kichwa “Ahadi ya Mungu ya Paradiso.”
Siku moja baba ya Fifi aliamua kumpeleka kanisani mwake. Fifi alimshangaza kila mtu kwa kukataa kuimba nyimbo za kanisa. Kwa nini? Kwa sababu alihisi kwamba nyimbo zilizoimbwa kanisani mwa baba yake hazikupatana na yale aliyokuwa amejifunza katika funzo lake la Biblia. Badala yake, aliimba kwa ujasiri wimbo wake wa Ufalme aupendao zaidi.
Baada ya kujaribu mara kadhaa kubadili akili yake bila mafanikio, viongozi wa kanisa waliamua kumtenga Fifi mwenye umri wa miaka mitano! Kujapokuwa kutendwa vibaya huko, baba yake aliendelea kuwa mtulivu. Aliona fahari kwamba Fifi alikuwa amechukua msimamo imara kwa ajili ya yale aliyoamini. Baba na mama ya Fifi wataka aendelee kushirikiana na Mashahidi wa Yehova.
• Mvulana tineja aitwaye Lukodi alipoamua kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, baba yake alipinga sana. Pindi moja Lukodi alipokuwa akijitayarisha kwenda mkutanoni kwenye Jumba la Ufalme, baba yake alimtisha kwa upanga. Pindi nyingine baba ya Lukodi alimpiga kwa fimbo, akisababisha jeraha kubwa mgongoni mwake. Ujapokuwa upinzani huu wenye juhudi nyingi, Lukodi alifuliza kuwa imara katika azimio lake la kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Aliendelea kufanya maendeleo naye akabatizwa. Sasa atumika akiwa painia wa kawaida.
Sona, dada mchanga wa Lukodi, alivutiwa sana na msimamo wa ndugu yake hivi kwamba yeye pia akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, ili kumzuia asijifunze, baba yao alimpeleka Sona katika shule ya kijiji kingine, ambako hakukuwa na Mashahidi. Hata hivyo, Sona alifanya zoea la kusema na wengine juu ya mambo aliyokuwa amejifunza. Tokeo ni kwamba, binamu yake naye akapendezwa.
Mashahidi wa kijiji jirani waliposikia juu ya utendaji wa kuhubiri wa Sona, walimtembelea na kupanga ili awe na funzo la Biblia nyumbani la kawaida. Aliendelea kufanya maendeleo na upesi akajiunga na ndugu yake akiwa Shahidi wa Yehova aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Kwa kuongezea, binamu yake sasa ni mhubiri asiyebatizwa, na funzo la kitabu linaongozwa katika kijiji hicho.
Yapendeza na kuburudisha kama nini vijana wajiungapo katika kulisifu jina la Yehova!
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.