Jinsi ya Kutatua Matatizo kwa Amani
UJEURI wa kibinadamu ni wa zamani kama mwanadamu mwenyewe. Biblia yaonyesha ujeuri ukianzia kwa Kaini, ndugu ya Abeli aliyekuwa mwana mkubwa wa wenzi wawili wa kwanza wa kibinadamu. Mungu alipopendezwa na toleo la Abeli badala ya lile lake, Kaini “alighadhabika sana.” Yeye aliishughulikiaje hali hiyo? “Kaini akamwinukia Abeli nduguye, akamwua.” Baadaye yeye alijipata katika hali yenye matata pamoja na Mungu. (Mwanzo 4:5, 8-12) Ujeuri haukumaliza tatizo la Kaini la kuwa na msimamo mbaya pamoja na Muumba wake.
Twaweza kuepukaje mwendo wa Kaini wa kutumia nguvu za kimwili kutatua matatizo?
Kutoka Ujeuri Hadi Uvumilivu
Fikiria mtu aliyeshuhudia kwa ukubalifu kuuawa kwa Stefano, mfia-imani wa kwanza Mkristo. (Matendo 7:58; 8:1) Mtu huyo, Sauli wa Tarso, hakukubaliana na msimamo wa kidini wa Stefano, naye aliunga mkono uuaji huo wa kijeuri kama njia halali ya kukomesha utendaji wa Stefano. Yakubalika kwamba huenda Sauli hakuwa mjeuri katika pande zote za maisha yake. Hata hivyo, yeye alikuwa tayari kuukubali ujeuri kuwa njia ya kutatua matatizo. Mara baada ya kifo cha Stefano, Sauli “akaanza kushughulikia kutaniko la [Kikristo] kwa njia mbaya kabisa. Akivamia nyumba moja baada ya nyingine na, kukokota nje wanaume na pia wanawake, akawa akiwakabidhi gerezani.”—Matendo 8:3.
Kulingana na msomi wa Biblia Albert Barnes, neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa ‘kushughulikia kwa njia mbaya kabisa’ lina maana ya kuharibu ambako hayawani-mwitu, kama vile simba na mbwa-mwitu wangefanya. “Sauli,” aelezea Barnes, “alikuwa na hasira kali kuelekea kanisa kama hayawani-mwitu—simulizi lenye nguvu, linaloonyesha bidii na kiruu alichokuwa nacho katika kunyanyasa.” Sauli aliposhika njia ya kwenda Damasko ili kuwashika wafuasi zaidi wa Kristo, alikuwa bado “akipumua tisho na uuaji-kimakusudi dhidi ya wanafunzi wa Bwana [Kristo].” Akiwa njiani, alizungumziwa na Yesu aliyefufuliwa, na hili lilimfanya Sauli ageuke na kuwa Mkristo.—Matendo 9:1-19.
Baada ya kugeuka huko, Sauli alishughulika na watu kwa njia tofauti. Tukio lililofanyika miaka 16 hivi baadaye lilionyesha badiliko hilo. Kikundi cha watu kilikuja kwenye kutaniko la nyumbani kwake katika Antiokia, na kuwahimiza Wakristo huko wajipatanishe na Sheria ya Kimusa. ‘Mtengano usio mdogo’ ulitokea. Sauli, kwa wakati huu akijulikana kwa jina Paulo, alihusika katika bishano hilo. Kwa wazi, kulikuwako mabishano makubwa sana. Lakini Paulo hakufanya ujeuri. Badala yake, alikubaliana na uamuzi wa kutaniko wa kuliacha jambo hilo mikononi mwa mitume na wazee wa kutaniko la Yerusalemu.—Matendo 15:1, 2.
Huko Yerusalemu, “bishano kubwa” tena lilitokea katika mkutano wa wazee. Paulo alisubiri hadi “umati mzima ukawa kimya” kisha akaripoti kazi za ajabu za roho ya Mungu miongoni mwa waamini wasiotahiriwa. Baada ya mazungumzo ya Kimaandiko, mitume na wazee wa Yerusalemu ‘walifikia kauli moja,’ kutowaongezea waamini wasiotahiriwa mzigo zaidi wenye kulemea, ila kuwatolea onyo la upole “kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu na damu, na kutokana na vitu vilivyonyongwa na uasherati.” (Matendo 15:3-29) Kwa kweli, Paulo alikuwa amebadilika. Yeye alijifunza kutatua masuala bila ujeuri.
Kukabiliana na Mielekeo Yenye Ujeuri
“Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana,” Paulo akaonya kwa upole baadaye, “bali ahitaji kuwa mwanana kuelekea wote, mwenye sifa za ustahili kufundisha, akifuliza kujizuia mwenyewe chini ya uovu, akiagiza kwa upole wale wasio na mwelekeo ufaao.” (2 Timotheo 2:24, 25) Paulo alimhimiza Timotheo, mwangalizi mchanga, ashughulikie hali zenye kutatiza kwa utulivu. Paulo alikuwa mwenye maoni yaliyofaa. Alijua kwamba hisia zingeweza kuamshwa hata miongoni mwa Wakristo. (Matendo 15:37-41) Akiwa na sababu nzuri, yeye alishauri hivi: “Iweni na hasira ya kisasi, na bado msifanye dhambi; msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Kuzuia hasira pasipo kulipuka kwa kiruu ndiyo njia nzuri ya kushughulika na hisia kama hizo. Lakini hili laweza kutimizwaje?
Leo, si rahisi kudhibiti hasira. “Kuwa mkatili kumeenea sana,” asema Dakt. Deborah Prothrow-Stith, naibu wa mkuu wa Harvard School of Public Health. “Kwa hakika, ule ustadi wa kupatana na wengine—kufanya mashauri ya mapatano, kukubaliana, hisia-mwenzi, msamaha—ni mambo yatumiwayo kuwafafanua watu dhaifu wasiofaa kitu.” Hata hivyo, hizo ni sifa za kiume, nazo ni muhimu katika kudhibiti mielekeo yenye ujeuri ambayo yaweza kufurika ndani yetu.
Alipopata kuwa Mkristo, Paulo alijifunza njia bora ya kushughulika na tofauti ya maoni ya watu wengine. Ilitegemea mafundisho ya Biblia. Akiwa msomi aliyeelimika sana wa dini ya Kiyahudi, Paulo aliyafahamu Maandiko ya Kiebrania. Ni lazima awe aliyajua Maandiko kama vile: “Usimhusudu mtu mwenye jeuri, wala usiichague mojawapo ya njia zake.” “Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa; na mtu aitawalaye roho yake kuliko mtu atekaye mji.” “Asiyetawala roho yake ni mfano wa mji uliobomolewa, usio na kuta.” (Mithali 3:31; 16:32; 25:28) Hata hivyo, kujua hayo hakukumzuia Paulo, kutokuwa mjeuri dhidi ya Wakristo kabla ya kugeuka kwake. (Wagalatia 1:13, 14) Lakini, Paulo akiwa Mkristo, ni nini kilichomsaidia kutatua masuala yenye hisia nzito kwa njia yenye kupatana na akili na kuwavutia watu badala ya kuwa mjeuri?
Paulo alitupa kidokezi aliposema hivi: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Yeye alithamini sana yale ambayo Yesu Kristo alikuwa amefanya kwa ajili yake. (1 Timotheo 1:13, 14) Kristo alikuja kuwa kigezo chake cha kufuata. Alijua namna Yesu alivyoteseka kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi. (Waebrania 2:18; 5:8-10) Paulo angeweza kuthibitisha kwamba unabii wa Isaya juu ya Mesiya ulitimizwa katika Yesu: “Alionewa, lakini alinyenyekea, wala hakufunua kinywa chake; kama mwana-kondoo anyamazavyo mbele yao wakatao manyoya yake; naam, hakufunua kinywa chake.” (Isaya 53:7) Mtume Petro aliandika hivi: “[Yesu] alipokuwa akitukanwa, hakuwa akitukana kwa kurudisha. Alipokuwa akiteseka, hakutisha, lakini alifuliza kujikabidhi mwenyewe kwa yeye ambaye huhukumu kwa uadilifu.”—1 Petro 2:23, 24.
Kuthamini kwa Paulo jinsi Yesu Kristo alivyoshughulika na hali zenye uvutano, kulimsukuma kubadilika. Yeye angeweza kuwatia moyo waamini wenzake hivi: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia.” (Wakolosai 3:13) Kutambua uhitaji wa kutokuwa wajeuri tu hakutoshi. Uthamini wa yale Yehova na Yesu Kristo wametufanyia hutusaidia kuandaa kichocheo kihitajikacho ili kushinda mielekeo yenye ujeuri.
Je, Yawezekana?
Mtu mmoja katika Japani alihitaji kichocheo chenye nguvu kama hicho. Baba yake, aliyekuwa askari mwenye hasira kali, aliitawala familia yake kwa ujeuri. Kwa sababu ya kufanyiwa ujeuri hivyo na kumwona mama yake akiteseka vivyohivyo, mtu huyo alikuza mwelekeo wa ujeuri. Yeye alikuwa akibeba panga mbili za kijeshi zenye urefu tofauti-tofauti alizotumia kutatua matatizo kutia na kuwatisha watu.
Mke wake alipoanza kujifunza Biblia, yeye alikuwa akisikiliza funzo lilipokuwa likiendelea bila kulichukua kwa uzito. Hata hivyo, baada ya yeye kusoma kijitabu kiitwacho Habari Njema Hizi za Ufalme,a alibadilika. Kwa nini? “Niliposoma habari iliyo chini ya vichwa vidogo, ‘Yesu Kristo’ na ‘Ukombozi,’ niliaibika,” yeye aelezea. “Ijapokuwa nilikuwa nikiishi maisha yaliyopotoka, nilipenda kuwa mwenye fadhili kwa wale niliopatana nao vema. Nilifurahia kuwafanya rafiki zangu wafurahi maadamu tu hilo halingeathiri maisha yangu mwenyewe. Bila shaka, Mwana wa Mungu, Yesu, alikuwa tayari kutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu, kutia ndani watu kama mimi. Nilishtuka, kana kwamba nilikuwa nimepigwa kwa rungu.”
Yeye aliacha kushirikiana na rafiki zake wa hapo awali na bila kukawia akajiandikisha kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova. Shule hii huwasaidia waliojiandikisha kujipatia ustadi wa kuwafundisha wengine Biblia. Mwendo huo ulimletea mtu huyu manufaa ya ziada. Yeye akumbuka hivi: “Nilipokuwa mchanga, nilikuwa mwenye vitisho na mjeuri kwa sababu singeweza kueleza hisia zangu kwa wengine. Kadiri nilipojifunza kuwasilisha mawazo yangu kwa wengine, nilianza kusababu nao badala ya kuwa mjeuri.”
Je, yeye amefanya njia ya Kristo ya maisha kuwa yake mwenyewe, kama alivyofanya Paulo? Imani yake ilitahiniwa wakati rafiki yake wa hapo awali, ambaye walikula kiapo cha ushirika naye, alipojaribu kumzuia asiwe Mkristo. “Rafiki” yake alimpiga na kumkufuru Mungu wake Yehova. Mtu huyo aliyekuwa mjeuri hapo awali alijidhibiti na kuomba msamaha kwa kutoweza kwake kutimiza kile kiapo. Kwa kutamaushwa, “ndugu” yake alimwacha peke yake.
Kwa kushinda mielekeo yake yenye ujeuri, mtu huyu aliyekuwa mwenye hasira hapo awali amepata ndugu na dada wengi wa kiroho, ambao wameunganishwa na upendo kwa Mungu na jirani. (Wakolosai 3:14) Kwa hakika, zaidi ya miaka 20 baada ya kuwa Mkristo aliyejiweka wakfu, yeye anatumikia akiwa mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova. Ni furaha iliyoje kwake kuweza kuonyesha kutoka kwa Biblia kwamba watu wenye mielekeo ya kihayawani wanaweza kujifunza kutatua tofauti zao bila ujeuri, sawa tu na alivyojifunza! Na ni pendeleo lililoje kwake kuweza kuelekezea kwenye utimizo mkubwa zaidi wa maneno haya ya kiunabii: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari”!—Isaya 11:9.
Kama mtume Paulo, na mtu huyu aliyekuwa mjeuri hapo awali, wewe pia waweza kujifunza kushughulikia hali zenye kuudhi, kutatua matatizo kwa amani. Mashahidi wa Yehova katika eneo unaloishi watafurahi kukusaidia.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Paulo alikuwa mwenye maoni yaliyofaa. Alijua kwamba hisia zingeweza kuamshwa hata miongoni mwa Wakristo
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kuthamini kile ambacho Mungu ametufanyia huchangia kuwa na mahusiano yenye amaniy