Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 11/1 kur. 8-13
  • Je, Kazi Yako Itastahimili Moto?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Kazi Yako Itastahimili Moto?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuweka Msingi Ufaao
  • Kujenga kwa Vifaa Vifaavyo
  • Je, Kazi Yako Itastahimili Moto?
  • Ni Nani Mwenye Daraka?
  • Kujenga kwa Vitu Visivyoweza Kuchomwa na Moto
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kujenga Nyutu Za Kikristo Katika Watoto Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Kuwasaidia Watu Wamkaribie Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Unapofundisha, Fikia Moyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 11/1 kur. 8-13

Je, Kazi Yako Itastahimili Moto?

“Acheni kila mmoja afulize kuangalia ni jinsi gani anavyojenga juu ya [msingi].”—1 WAKORINTHO 3:10.

1. Wakristo waaminifu wana tumaini gani kuhusu wanaotazamiwa kuwa wanafunzi?

WENZI wa ndoa Wakristo watazama mtoto wao aliyezaliwa karibuni. Mhubiri wa Ufalme aona uso wenye hamu na upendezi wa mwanafunzi wa Biblia. Mzee Mkristo anayefundisha kutoka jukwaani aona kati ya wasikilizaji mtu aliyependezwa karibuni akitafuta kwa bidii maandiko katika Biblia. Watumishi hawa waaminifu wa Yehova wana mioyo iliyojaa tumaini. Kwa kawaida wao hujiuliza, ‘Je, mtu huyu atakuja kumpenda Yehova na kumtumikia—na kudumu akiwa mwaminifu?’ Bila shaka, matokeo kama hayo hayapatikani bila kufanya lolote. Kazi inahitajiwa.

2. Paulo aliwakumbushaje Wakristo Waebrania juu ya umuhimu wa kazi ya kufundisha, na huenda hilo likatuchochea tufanye nini?

2 Mtume Paulo, ambaye mwenyewe alikuwa mwalimu stadi, alikazia umuhimu wa kazi ya kufundisha na kufanya wanafunzi alipoandika hivi: “Mwapaswa kuwa walimu kwa kufikiria wakati.” (Waebrania 5:12) Wakristo aliowaandikia hawakuwa wamefanya maendeleo sana, kwa kufikiria muda ambao walikuwa wamekuwa waamini. Mbali na kutokuwa tayari kufundisha wengine, walihitaji pia kukumbushwa kweli za msingi. Leo, yafaa sisi sote tukadirie mara kwa mara uwezo wetu mbalimbali tukiwa walimu na kuona jinsi tunavyoweza kufanya maendeleo. Uhai wa watu uko hatarini. Tunaweza kufanya nini?

3. (a) Paulo aliulinganisha na nini ule utaratibu wa kumfanya mwanafunzi awe Mkristo? (b) Tuna pendeleo gani kubwa tukiwa wajenzi Wakristo?

3 Katika kielezi chenye maana iliyopanuka, Paulo alifananisha kufanya wanafunzi na utaratibu wa kujenga. Alianza kwa kusema: “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu. Nyinyi watu ni shamba la Mungu lenye kulimwa, jengo la Mungu.” (1 Wakorintho 3:9) Kwa hiyo twashiriki katika kazi ya kujenga inayohusisha watu; tunasaidia kuwajenga wawe wanafunzi wa Kristo. Sisi hufanya hivyo tukiwa wafanyakazi wenzi wa Yule “aliyejenga vitu vyote.” (Waebrania 3:4) Ni pendeleo lililoje! Acheni tuone jinsi shauri lililopuliziwa la Paulo kwa Wakorintho, liwezavyo kutusaidia kuwa stadi zaidi katika kazi yetu. Tutakazia hasa “usanifu [wetu] wa kufundisha.”—2 Timotheo 4:2.

Kuweka Msingi Ufaao

4. (a) Paulo alikuwa na fungu gani katika kazi ya Kikristo ya kujenga? (b) Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yesu na pia wasikilizaji wake walijua umuhimu wa misingi ifaayo?

4 Ikiwa jengo litakuwa imara na lenye kudumu, lahitaji msingi ufaao. Hivyo, Paulo aliandika: “Kulingana na fadhili isiyostahiliwa ya Mungu niliyopewa, kama mwelekezi wa kazi za ufundi mwenye hekima niliweka msingi.” (1 Wakorintho 3:10) Akitumia kielezi sawa na hicho, Yesu Kristo alisimulia juu ya nyumba iliyookoka dhoruba kwa sababu mjenzi wake alikuwa amechagua msingi imara. (Luka 6:47-49) Yesu alijua yote kuhusu umuhimu wa misingi. Alikuwepo Yehova alipoweka msingi wa dunia.a (Mithali 8:29-31) Waliomsikiliza Yesu pia walithamini misingi ifaayo. Nyumba zenye misingi ifaayo pekee ndizo zingeweza kuokoka mafuriko ya ghafula na matetemeko ya dunia ambayo nyakati nyingine yalitokea huko Palestina. Ingawa hivyo, Paulo alikuwa akifikiria msingi upi?

5. Ni nani aliye msingi wa kutaniko la Kikristo, na hilo lilitabiriwaje?

5 Paulo aliandika hivi: “Hakuna mtu awezaye kuweka msingi mwingine wowote zaidi kuliko uliowekwa, ambao ni Yesu Kristo.” (1 Wakorintho 3:11) Hii haikuwa mara ya kwanza ambayo Yesu alilinganishwa na msingi. Kwa kweli, andiko la Isaya 28:16 lilitabiri hivi: “Bwana, MUNGU, asema hivi, Tazama, naweka jiwe katika Sayuni, liwe msingi, jiwe lililojaribiwa, jiwe la pembeni lenye thamani, msingi ulio imara.” Kwa muda mrefu Yehova alikuwa amekusudia Mwana wake awe msingi wa kutaniko la Kikristo.—Zaburi 118:22; Waefeso 2:19-22; 1 Petro 2:4-6.

6. Paulo aliwekaje msingi ufaao katika Wakristo Wakorintho?

6 Ni nini ulio msingi wa Wakristo mmoja-mmoja? Kama Paulo alivyosema, msingi pekee wa Mkristo wa kweli ni ule uliowekwa na Neno la Mungu—Yesu Kristo. Bila shaka Paulo aliweka msingi kama huo. Huko Korintho, ambako falsafa zilistahiwa sana, hakujaribu kuwavutia watu kwa hekima ya kilimwengu. Badala ya hivyo, Paulo alihubiri “Kristo aliyetundikwa mtini,” jambo lililopuuzwa na mataifa kuwa “upumbavu” mkubwa. (1 Wakorintho 1:23) Paulo alifundisha kwamba Yesu ndiye mtu mwenye fungu kubwa zaidi katika makusudi ya Yehova.—2 Wakorintho 1:20; Wakolosai 2:2, 3.

7. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kujirejezea kwa Paulo kuwa “mwelekezi wa kazi za ufundi mwenye hekima”?

7 Paulo alitaja kwamba alifundisha hivyo “kama mwelekezi wa kazi za ufundi mwenye hekima.” Taarifa hiyo haikuwa ya kujisifu. Ilikuwa tu ya kukiri zawadi ya ajabu ambayo Yehova alikuwa amempa—ile ya kupanga na kuelekeza kazi. (1 Wakorintho 12:28) Ni kweli kwamba, leo sisi hatuna zawadi za kimuujiza walizopewa Wakristo wa karne ya kwanza. Nasi huenda tusijione kuwa walimu wenye kipawa. Lakini kwa namna fulani yenye maana, sisi ni wenye kipawa. Ebu fikiria: Yehova hutupa roho yake takatifu itusaidie. (Linganisha Luka 12:11, 12.) Nasi twampenda Yehova na tunao ujuzi wa mafundisho ya msingi ya Neno lake. Kwa kweli hizo ni zawadi za ajabu tuwezazo kutumia kufundisha wengine. Acheni tuazimie kuzitumia ili kuweka msingi ufaao.

8. Tunamwekaje Kristo awe msingi katika wale wanaotazamiwa kuwa wanafunzi?

8 Tunapomweka Kristo awe msingi, hatumwasilishi akiwa mtoto mchanga katika hori, wala akiwa sawa na Yehova katika Utatu. La, maoni hayo yasiyo ya Kimaandiko ndiyo msingi wa Wakristo bandia. Badala ya hivyo, sisi hufundisha kwamba Yesu alikuwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, kwamba alitoa uhai wake mkamilifu kwa niaba yetu, na kwamba leo yeye ni Mfalme aliyewekwa wa Yehova anayetawala mbinguni. (Waroma 5:8; Ufunuo 11:15) Sisi pia hujitahidi kuwachochea wanafunzi wetu wafuate hatua za Yesu na kuiga sifa zake. (1 Petro 2:21) Twataka wachochewe sana na bidii ya Yesu kwa ajili ya huduma, huruma yake kwa watu wa hali ya chini na wenye kuonewa, rehema yake kwa watenda-dhambi waliopondeka kutokana na hatia yao wenyewe, ujasiri wake usioyumbayumba alipokabili majaribu. Kwa kweli, Yesu ni msingi bora kabisa. Lakini ni nini kinachofuata?

Kujenga kwa Vifaa Vifaavyo

9. Ingawa kimsingi Paulo alikuwa mweka-msingi, yeye alikuwa na hangaiko lipi kuhusu wale waliokubali ukweli wa yale aliyofundisha?

9 Paulo aliandika: “Basi yeyote akijenga juu ya huo msingi, dhahabu, fedha, mawe yenye bei, vifaa vya mbao, nyasi kavu, mabua, kazi ya kila mmoja itakuwa dhahiri, kwa maana ile siku itaifichua, kwa sababu itafunuliwa kwa njia ya moto; na moto wenyewe utathibitisha ni ya namna gani kazi ya kila mmoja.” (1 Wakorintho 3:12, 13) Paulo alimaanisha nini? Fikiria hali ya wakati huo. Kimsingi Paulo alikuwa mweka-msingi. Katika safari zake za umishonari, alisafiri kutoka jiji hadi jiji, akihubiria wengi ambao hawakuwa wamesikia kamwe juu ya Kristo. (Waroma 15:20) Watu walipokubali kweli aliyofundisha, makutaniko yalifanyizwa. Paulo aliwajali sana waaminifu hao. (2 Wakorintho 11:28, 29) Hata hivyo, kazi yake ilimtaka aendelee kusafiri. Kwa hiyo, baada ya kutumia miezi 18 akiweka msingi huko Korintho, aliondoka kwenda kuhubiri katika majiji mengine. Hata hivyo, alipendezwa sana na jinsi wengine walivyoendeleza kazi aliyokuwa amefanya huko.—Matendo 18:8-11; 1 Wakorintho 3:6.

10, 11. (a) Paulo alitofautishaje aina mbalimbali za vifaa vya ujenzi? (b) Ni yapi yaliyokuwa majengo halisi ambayo yamkini yalikuweko katika Korintho la kale? (c) Ni majengo ya aina gani ambayo yaelekea zaidi kustahimili moto, nayo yaandaa kielelezo gani chenye funzo kwa wafanya-wanafunzi Wakristo?

10 Yaonekana kwamba watu fulani waliokuwa wakijenga juu ya msingi ambao Paulo alikuwa ameweka huko Korintho hawakuwa wakifanya kazi nzuri. Ili kufichua tatizo hilo, Paulo atofautisha aina mbili za vifaa vya ujenzi: dhahabu, fedha, na mawe yenye bei; halafu vifaa vya mbao, nyasi kavu, na mabua. Jengo laweza kujengwa kwa vifaa bora, vyenye kudumu, visivyoweza kushika moto; au laweza kujengwa haraka-haraka kwa vifaa vya muda visivyoweza kutumika tena, na viwezavyo kushika moto kwa urahisi. Hapana shaka kwamba jiji kubwa kama Korintho lilikuwa na majengo mengi ya aina hizo mbili. Kulikuwa na mahekalu ya kuvutia yaliyojengwa kwa mawe yenye bei, labda sehemu fulani za hayo zikiwa zimefunikwa au kupambwa kwa dhahabu au fedha.b Labda majengo hayo yenye kudumu yalikuwa marefu na yenye fahari kushinda nyumba zilizokuwa karibu, vibanda na viduka vya sokoni vilivyojengwa kwa mbao zisizo laini na kuezekwa kwa nyasi.

11 Ni nini ambacho kingeyapata majengo hayo yakishika moto? Jibu lilikuwa wazi siku ya Paulo kama lilivyo siku yetu. Kwa kweli, huko nyuma mwaka wa 146 K.W.K., jiji la Korintho lilikuwa limeshindwa na kuwashwa moto na Jenerali Mummius wa Roma. Kwa kweli, majengo mengi ya mbao, nyasi kavu, au bua yaliharibiwa kabisa. Vipi majengo imara ya mawe yaliyokuwa yamepambwa kwa fedha na dhahabu? Hapana shaka haya yaliokoka. Huenda ikawa wanafunzi wa Paulo huko Korintho walipitia karibu na majengo hayo kila siku—majengo ya mawe yenye fahari yaliyookoka misiba ambayo zamani ilikuwa imeharibu majengo ya muda yaliyokuwa karibu. Paulo alidhihirisha hoja yake kwa mkazo ulioje! Tunapofundisha twahitaji kujiona kuwa wajenzi. Twataka kutumia vifaa bora zaidi na vyenye kudumu zaidi iwezekanavyo. Kwa njia hiyo, yaelekea zaidi kwamba kazi yetu itadumu. Vifaa hivyo vyenye kudumu ni vipi, na kwa nini ni muhimu kuvitumia?

Je, Kazi Yako Itastahimili Moto?

12. Wakristo Wakorintho walikuwa wakifanyaje kiholela kazi ya kujenga?

12 Kwa wazi, Paulo alihisi kwamba Wakristo katika Korintho walikuwa wakijenga vibaya. Kasoro ilikuwa nini? Kama vile muktadha uonyeshavyo, kutaniko hilo lilikuwa limekumbwa na mgawanyiko, kuvutiwa na watu mashuhuri kujapohatarisha umoja wa kutaniko. Baadhi yao walikuwa wakisema, “Mimi ni wa Paulo,” ilhali wengine walisisitiza, “Mimi ni wa Apolo.” Yaonekana wengine walijivunia mno hekima yao wenyewe. Si ajabu kwamba matokeo yalikuwa hali ya kufikiri kimwili, kutokomaa kiroho, na “wivu na zogo” iliyoenea sana. (1 Wakorintho 1:12; 3:1-4, 18) Bila shaka mitazamo hiyo ilidhihirika katika mafundisho yaliyofanywa kutanikoni na hudumani. Matokeo yalikuwa kwamba kazi yao ya kufanya wanafunzi ilifanywa kiholela, kama kazi ya kujenga iliyofanywa kwa vifaa duni. Haingeokoka “moto.” Paulo alikuwa akizungumzia moto upi?

13. Moto katika kielezi cha Paulo wawakilisha nini, na yawapasa Wakristo wote wajue nini?

13 Kuna moto ambao sisi sote hukabili maishani—majaribu ya imani yetu. (Yohana 15:20; Yakobo 1:2, 3) Kama vile tunavyohitaji kujua leo, Wakristo katika Korintho walihitaji kujua kwamba kila mtu tunayefundisha kweli atajaribiwa. Tukifundisha vibaya, huenda matokeo yakawa yenye kusikitisha. Paulo alionya: “Kazi ya yeyote ambayo ameijenga juu ya huo ikibaki, atapokea thawabu; kazi ya yeyote ikichomwa kabisa, atapata hasara, lakini yeye mwenyewe ataokolewa; lakini, ikiwa ndivyo, itakuwa ni kama kupitia moto.”c—1 Wakorintho 3:14, 15.

14. (a) Huenda wafanya-wanafunzi Wakristo ‘wakapataje hasara,’ hata hivyo huenda wao wakafikiaje wokovu kama kupitia moto? (b) Tunaweza kupunguzaje hatari ya kupata hasara?

14 Ni maneno yenye kuamsha fikira kama nini! Inaweza kuumiza sana kujitahidi kusaidia mtu awe mwanafunzi, kisha kumwona huyo mtu akishindwa na jaribu au mnyanyaso na hatimaye kuacha ile kweli. Paulo anakubaliana na jambo hilo anaposema kwamba sisi hupata hasara katika visa kama hivyo. Jambo hilo linaweza kuwa lenye kuumiza sana hivi kwamba wokovu wetu unafafanuliwa kuwa ‘kama unapitia moto’—kama mtu aliyepoteza kila kitu motoni, naye mwenyewe akaponea chupuchupu. Tunaweza kupunguzaje hatari ya kupata hasara upande wetu? Jenga kwa vifaa vidumuvyo! Tukiwafundisha wanafunzi wetu ili kuwafikia mioyo, tukiwachochea wathamini sifa za Kikristo kama vile hekima, ufahamu, kumhofu Yehova, na imani ya kweli, basi tunajenga kwa vifaa vyenye kudumu, visivyoweza kushika moto. (Zaburi 19:9, 10; Mithali 3:13-15; 1 Petro 1:6, 7) Wanaojipatia sifa hizo wataendelea kufanya mapenzi ya Mungu; nao wana tumaini hakika la kuendelea kuwa hai milele. (1 Yohana 2:17) Ingawa hivyo, tunaweza kutumiaje kielezi hicho cha Paulo kwa njia ifaayo? Fikiria vielelezo kadhaa.

15. Ni katika njia zipi tunaweza kuhakikisha kwamba tunaepuka kufanya kiholela kazi ya kujenga kuhusiana na wanafunzi wetu wa Biblia?

15 Tunapowafundisha wanafunzi wa Biblia, hatupaswi kukuza wanadamu zaidi kushinda Yehova Mungu. Mradi wetu si kuwafundisha kutuona sisi kuwa chanzo kikuu cha hekima. Twataka wamtegemee Yehova, Neno lake, na tengenezo lake ili wapate mwongozo. Ili kufikia mradi huo, hatutajibu maswali yao kwa kutoa maoni yetu tu. Badala ya hivyo, tunawafundisha kutafuta majibu, wakitumia Biblia na vichapo ambavyo “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameandaa. (Mathayo 24:45-47) Kwa sababu sawa na hizo, tunakuwa waangalifu tusiwe wenye kumiliki wanafunzi wetu wa Biblia. Badala ya kuona uchungu wengine wanapoonyesha kupendezwa nao, yatupasa tuwatie wanafunzi wetu moyo ‘wapanuke’ katika shauku zao nyororo na kupata kuwajua na kuwathamini watu wengi iwezekanavyo kutanikoni.—2 Wakorintho 6:12, 13.

16. Wazee wanaweza kujengaje kwa vifaa visivyoweza kushika moto?

16 Wazee Wakristo pia hutimiza fungu muhimu katika kujenga wanafunzi. Wanapofundisha mbele ya kutaniko, wao hujaribu kujenga kwa vifaa visivyoweza kushika moto. Huenda uwezo wao wa kufundisha, uzoefu, na utu wao ukatofautiana sana, lakini hawajinufaishi kwa kutumia tofauti hizi ili wajipatie wafuasi. (Linganisha Matendo 20:29, 30.) Hatujui ni kwa nini hasa wengine katika Korintho walikuwa wakisema, “Mimi ni wa Paulo” au, “Mimi ni wa Apolo.” Lakini twaweza kuwa na hakika kabisa kwamba hakuna yeyote wa wazee hawa waaminifu aliyeendeleza maoni kama hayo yenye kugawanya. Paulo hakufurahishwa na maoni hayo; aliyapinga kwa nguvu. (1 Wakorintho 3:5-7) Vivyo hivyo leo, wazee hukumbuka kwamba wao huchunga “kundi la Mungu.” (1 Petro 5:2) Kundi hilo si la mwanadamu yeyote. Kwa hiyo, wazee husimama imara dhidi ya mwelekeo wowote wa mtu mmoja kutawala ama kundi ama baraza la wazee. Maadamu wazee wanachochewa na tamaa yenye unyenyekevu ya kutumikia kutaniko, kufikia mioyo, na kusaidia kondoo wamtumikie Yehova kwa nafsi yote, wao hujenga kwa vifaa visivyoweza kushika moto.

17. Wazazi Wakristo hujitahidije kujenga kwa vifaa visivyoweza kushika moto?

17 Wazazi Wakristo pia huhangaikia sana jambo hilo. Wana tamaa kubwa kama nini ya kuona watoto wao wakiishi milele! Hiyo ndiyo sababu wao hujitahidi sana ili ‘kukaza kikiki’ kanuni za Neno la Mungu katika mioyo ya watoto wao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7, NW) Wanataka watoto wao wajue kweli, si ikiwa fungu la sheria au mambo ya kukariri tu, bali ikiwa njia ya maisha iliyo kamili, yenye kuthawabisha, na yenye furaha. (1 Timotheo 1:11) Ili kuwajenga watoto wao wawe wanafunzi waaminifu wa Kristo, wazazi wenye upendo hujitahidi kutumia vifaa visivyoweza kushika moto. Kwa subira wao hufanya kazi pamoja na watoto wao, wakiwasaidia waache sifa ambazo Yehova huchukia na kusitawisha zile ambazo yeye hupenda.—Wagalatia 5:22, 23.

Ni Nani Mwenye Daraka?

18. Mwanafunzi anapokataa mafundisho yenye mafaa, kwa nini si lazima kosa liwe la wale wanaojaribu kumfundisha na kumzoeza?

18 Mazungumzo haya huzusha swali muhimu. Ikiwa mtu tunayejitahidi kumsaidia ataacha kweli, je, hilo lamaanisha kwamba sisi kama walimu tumeshindwa—kwamba tulijenga kwa vifaa duni? Si lazima iwe hivyo. Maneno ya Paulo yatukumbusha kwamba ni daraka kubwa kushiriki katika kujenga wanafunzi. Tunahitaji kufanya yote tuwezayo ili kujenga vizuri. Lakini Neno la Mungu halituambii tujitwike daraka hilo lote kisha tulemewe na hatia wakati wale tunaojaribu kusaidia wanapoacha ile kweli. Kuna mambo mengine yanayohusika mbali na kuwajibika kwetu wenyewe tukiwa wajenzi. Kwa kielelezo, ona yale Paulo asemayo kumhusu hata yule mwalimu ambaye amefanya vibaya katika kazi hii ya kujenga: “Atapata hasara, lakini yeye mwenyewe ataokolewa.” (1 Wakorintho 3:15) Ikiwa mwalimu huyo hatimaye aweza kupata wokovu—ilhali utu wa Kikristo aliojaribu kujenga katika mwanafunzi wake waonyeshwa kuwa ‘unachomwa’ katika jaribu kali—je, tutafikia mkataa gani? Bila shaka, Yehova humhesabia mwanafunzi kuwa ndiye kimsingi mwenye daraka kuhusiana na uamuzi wake mwenyewe wa kama atafuata njia ya uaminifu au hatafuata.

19. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

19 Daraka la kibinafsi au la mtu mmoja-mmoja ni jambo lenye umuhimu mkubwa. Huathiri kila mmoja wetu. Biblia husema nini kihususa juu ya jambo hilo? Makala yetu inayofuata itazungumzia hilo.

[Maelezo ya Chini]

a Huenda ‘msingi wa dunia’ ukawa warejezea nguvu za asili zinazoshikilia dunia imara—na sayari zote—mahali pake. Kwa kuongezea, dunia yenyewe imefanyizwa katika njia ya kwamba ‘haitatikisika,’ au kupatwa na uharibifu.—Zaburi 104:5.

b Si lazima ‘mawe hayo yenye bei’ ambayo Paulo alirejezea yawe yalikuwa vito kama vile almasi na yakuti. Yawezekana hayo yalikuwa mawe ya ujenzi yenye bei kama vile marumaru, alabasta, au itale.

c Paulo alishuku kuokoka kwa “kazi” ya mjenzi wala si mjenzi mwenyewe. Tafsiri ya The New English Bible yatafsiri mstari huo hivi: “Jengo la mtu likistahimili, atapokea thawabu; likichomeka, atapata hasara; na bado ataponyoka na uhai wake, kama vile mtu aponyokavyo kutoka motoni.”

Ungejibuje?

◻ Ni nini ulio “msingi” wa Mkristo wa kweli, nao huwekwaje?

◻ Twaweza kujifunza nini kutokana na aina mbalimbali za vifaa vya ujenzi?

◻ “Moto” huwakilisha nini, nao waweza kufanyaje wengine ‘wapate hasara’?

◻ Walimu wa Biblia, wazee, na wazazi waweza kujengaje kwa vifaa visivyoweza kushika moto?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Katika majiji mengi ya kale, majengo ya mawe yasiyoweza kushika moto yalichangamana na ya vifaa duni zaidi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki