Mawasiliano Yenye Kujenga—Ufunguo wa Kuwa na Ndoa Nzuri
Katika mwaka wa 1778, Robert Barron alibuni kufuli lenye kufungwa kwa nyenzo mbili ambalo laendelea kutegemewa katika utengenezaji wa makufuli ya kisasa. Ubuni wake ulihitaji kutumia ufunguo mmoja, ambao ungeweza kuinua nyenzo hizo mbili kwa pamoja.
VIVYO HIVYO, ndoa yenye mafanikio hutegemea ushirikiano wenye upatano wa mume na mke. Mawasiliano yenye kujenga ni muhimu ili kufungua na kupata shangwe yenye thamani ya ndoa nzuri.
Kile Ambacho Mawasiliano Yenye Kujenga Huhusisha
Mawasiliano yenye kujenga huhusisha nini? Kamusi moja hufafanua mawasiliano kuwa “kutoa au kubadilishana mawazo, maoni, au habari kwa kuongea, kuandika, au kwa ishara.” Kwa hiyo, mawasiliano huhusisha kubadilishana mawazo na hisia za moyoni. Nayo mawasiliano yenye kujenga huhusisha mambo yenye kujenga, yenye kuburudisha, yenye wema wa adili, yenye kusifika, na yenye kuliwaza.—Waefeso 4:29-32; Wafilipi 4:8.
Tumaini, imani, na kuelewana hufanya mawasiliano yenye kujenga yawezekane. Sifa hizi hutokea wakati ndoa inapoonwa kuwa uhusiano wa maisha na kunapokuwa na azimio la kweli la kuifanikisha. Akieleza juu ya uhusiano kama huo, Joseph Addison, mwandishi wa insha wa karne ya 18, aliandika hivi: “Watu wawili ambao wamechaguana kati ya wanadamu wengine wote kwa kusudi la kufarijiana na kutumbuizana, kwa kufanya hivyo, wamejitwika wajibu wa kuwa wachangamfu, wenye fadhili, wenye busara, wenye kusamehe, wenye subira, na wenye shangwe, kuhusiana na udhaifu na kutokamilika mbalimbali kwa mmoja na mwenzake, hadi kifo.” Ni muungano wenye furaha kama nini! Nazo sifa hizo zilizo kama vito zaweza kurembesha ndoa yako, kwa kuwa unaweza kuzipata kupitia mawasiliano yenye kujenga.
Vizuizi vya Mawasiliano Yenye Kujenga
Wenzi walio wengi huanza ndoa wakiwa na matumaini mema, hata kwa msisimko mkubwa. Hata hivyo, kwa wengi msisimko huo hutoweka upesi, nayo matumaini mema hufifia. Huenda hali ya uhakika ikageuka kuwa mchanganyiko wa kukata tamaa, hasira, uhasama, na hata chuki kali. Kisha ndoa inakuwa hali ya kuvumiliana tu “hadi kifo kitakapotutenganisha.” Basi, ni lazima vizuizi fulani viondolewe ili kuboresha au kutegemeza mawasiliano yenye kujenga yanayohitajiwa kwa ndoa nzuri.
Kuhofu jinsi ambayo mwenzi wa ndoa angetenda kuhusiana na habari fulani au tamaa fulani iliyodhihirishwa, kwaweza kuwa kizuizi halisi cha mawasiliano yenye kujenga. Kwa mfano, huenda hofu ya kukataliwa ikazuka baada ya mwenzi mmoja kujua kwamba ameanza kupatwa na ulemavu fulani mbaya. Mtu anawezaje kumweleza mwenzi wake kwamba utaratibu fulani wa matibabu utakaofanywa karibuni utabadili kabisa sura yake au uwezo wake wa kutenda? Katika visa hivyo, mawasiliano ya unyofu na kupangia wakati ujao kwa makini kwahitajiwa hata zaidi. Kumhakikishia mwenzi kwa maneno kwamba ungali unampenda, pamoja na kumtendea kwa wororo mara kwa mara, kungeonyesha upendezi wa kibinafsi ambao ungesaidia kuendeleza ndoa yenye kuridhisha kikweli. Maana ya mithali hii yapaswa kudhihirishwa kabisa katika ndoa: “Rafiki hupenda siku zote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.
Uchungu wa moyo ni kizuizi kingine cha mawasiliano yenye kujenga. Imesemwa kwa kufaa kwamba ndoa yenye furaha ni muungano wa watu wawili wenye sifa nzuri ya kusameheana. Ili wawe na sifa hiyo, wenzi waliooana wangejitahidi kabisa kufuata shauri la mtume Paulo lenye kutumika: “Msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Mawasiliano ya unyenyekevu yanahitajiwa ili kutumia shauri hilo badala ya kuwa wenye hasira au uchungu wa moyo. Wenzi katika ndoa nzuri hawajiachilii washindwe na hasira, ugomvi, na kuweka kinyongo. (Mithali 30:33) Wao hujitahidi kumwiga Mungu, ambaye haweki kinyongo. (Yeremia 3:12) Kwa kweli, wao husameheana kutoka moyoni.— Mathayo 18:35.
Kizuizi dhahiri cha mawasiliano yoyote ni kununia mtu. Huenda kununa huko kukahusisha kuwa na uso mzito, kutweta sana, kutenda mambo shingo upande, au mwenzi mmoja kukataa kuongea. Mwenzi wa ndoa atendaye hivyo anadhihirisha namna fulani ya kuudhika. Lakini kueleza hisia za kibinafsi katika njia iliyo wazi na yenye kupendeza huboresha ndoa kuliko kukaa kimya na kuwa na moyo mzito.
Kutosikiliza kwa makini au kutosikiliza kamwe mwenzi anapozungumza ni kizuizi kingine kipaswacho kushindwa ili kuwe na mawasiliano mazuri katika ukaribu wa ndoa. Labda tumechoka sana au tuna shughuli nyingi tusipate nguvu za kiakili na kihisia-moyo zinazohitajiwa ili kumsikiliza yule mwingine kwa makini. Huenda mabishano yakazuka kuhusu mipango isiyoeleweka vizuri ambayo mwenzi mmoja afikiri ilielezwa vizuri lakini yule mwingine asisitiza kuwa anaisikia kwa mara ya kwanza. Ni wazi kwamba mawasiliano mabaya ndiyo kisababishi cha matatizo hayo.
Jinsi ya Kusitawisha Mawasiliano Yenye Kujenga
Ni muhimu kama nini kutenga wakati kwa ajili ya mawasiliano yenye upendo na yenye kujenga! Watu fulani hutumia wakati mwingi sana wakitazama maisha ya watu wengine katika televisheni hivi kwamba wanakosa kupata wakati kwa ajili ya maisha yao wenyewe. Hivyo, mara nyingi kuzima televisheni ni hatua ya lazima ili kuwa na mawasiliano yenye kujenga.
Hata hivyo, kama vile kuna wakati wa kunena, pia kuna wakati wa kunyamaza. Yule mtu mwenye hekima alisema: “Kwa kila jambo kuna majira yake, . . . Wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena.” Kwa kweli, pia kuna maneno yafaayo kusemwa. “Neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!” yasema mithali. (Mhubiri 3:1, 7; Mithali 15:23) Kwa hiyo, amua wakati ulio mzuri zaidi wa kutoa hoja yako au kueleza mahangaiko yaliyo moyoni mwako. Jiulize hivi: ‘Je, mwenzangu amechoka au amestarehe na kuchangamka kiakili? Je, habari ninayotaka tuzungumzie yaweza kumfanya akasirike? Ni nini ambacho mwenzangu hakupendezwa nacho katika maneno niliyochagua kutumia tulipozungumzia jambo hili mara ya mwisho?’
Ni vema kukumbuka kwamba watu huitikia kwa njia bora zaidi ikiwa wanaweza kuona jinsi ambavyo kuitikia au kukubaliana na ombi fulani kungewanufaisha. Ikiwa mkazo fulani umetokea kati ya wenzi, mmoja wao aweza kuwa na mwelekeo wa kusema, “Jambo fulani limekuwa likinisumbua, nasi tutalitatua sasa hivi!” Bila shaka, maneno hususa yangetegemea hali, lakini ingekuwa afadhali kusema jambo kama hili, “Mpenzi, nimekuwa nikifikiria lile jambo tulilozungumzia mapema kidogo na jinsi mambo yawezavyo kushughulikiwa.” Ni mfikio gani ambao yaelekea zaidi mwenzi wako atathamini?
Naam, jinsi jambo lisemwavyo ni muhimu sana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi.” (Wakolosai 4:6) Jitahidi kuzungumza kwa sauti na kwa maneno yenye kupendeza. Kumbuka kwamba “maneno yapendezayo ni kama sega la asali; ni tamu nafsini, na afya mifupani.”— Mithali 16:24.
Kwa wenzi fulani, kufanya kazi mbalimbali nyumbani wakiwa pamoja kwaweza kuandaa hali nzuri ya kuwasiliana. Kushirikiana huko kwaweza kukuza hali ya ushirikiano huku kukitokeza fursa ya kuwa na mawasiliano yenye kujenga. Kwa wenzi wa ndoa wengine, kuwa pamoja katika hali yenye utulivu bila kujaribu kufanya kazi fulani ni bora na huchangia zaidi kuwepo kwa mawasiliano yenye kujenga.
Tunaweza kujifunza mengi kwa kuzingatia jinsi ambavyo wenzi wa ndoa wanaofaana huwasiliana. Ni nini ambacho kimewafanya wawe hivyo? Yaelekea sana kwamba mawasiliano yao yenye upatano na ya starehe yametokana na jitihada ya kibinafsi, subira, na kufikiriana kwa upendo. Yaonekana kwamba wao wenyewe walikuwa na mengi ya kujifunza, kwa kuwa ndoa nzuri hazitokei tu bila kufanya jitihada yoyote. Hivyo basi, ni muhimu kama nini kufikiria maoni ya mwenzi wako, kuelewa mahitaji yake, na kukomesha kwa neno la busara hali ziwezazo kutokeza mkazo. (Mithali 16:23) Basi, ikiwa umeoa au umeolewa, jitahidi kuwa mwenzi anayependeza kuishi naye na aliye rahisi kuombwa radhi. Kufanya hivyo kutachangia sana uzuri wa ndoa yako.
Yehova Mungu hutaka watu wawe na ndoa zenye furaha na zenye kudumu. (Mwanzo 2:18, 21) Lakini ufunguo wa kufanya hivyo umo mikononi mwa wale waliofunga ndoa. Inahitaji watu wawili wenye kupendana wanaoshirikiana kikweli ili kufungua njia ya kufanikiwa katika ndoa kwa kuwa stadi katika mawasiliano yenye kujenga.
[Picha katika ukurasa wa 22]
Kuzima televisheni huwawezesha mwe na wakati zaidi wa mawasiliano
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mawasiliano yenye kujenga husaidia kuunganisha mioyo katika upendo wenye kudumu