Kudhibiti Baa la Ukosefu wa Usawa
Karibuni Muumba ataleta usawa ambao wanadamu wanatamani sana. Hadi wakati huo, tunaweza kuchukua hatua angalau ya kudhibiti baa la ukosefu wa usawa linalotuathiri sisi na familia zetu. Kama vile Nelson Mandela, rais wa zamani wa Afrika Kusini, alivyosema, “kile ambacho hututofautisha na watu wengine ni jinsi tutumiavyo vitu tulivyo navyo, wala si vitu vile tupewavyo.”
HISTORIA yathibitisha maneno yake. Kuna wanaume na wanawake wengi ambao walipata vitu vichache wakati wa kuzaliwa na kwa kuvitumia, wakapata mafanikio mengi yaliyowafanya wawe tofauti na wenzao ambao yaelekea walipata vitu vingi zaidi. Kinyume cha hilo, watu wengine ambao walizaliwa katika hali bora sana wamefuja vitu walivyokuwa navyo, wakashindwa kutumia uwezo wao kikamili.
Tumia Vema Zaidi Vitu Ulivyo Navyo!
Mashahidi wa Yehova wanapendezwa sana kusaidia watu wajue makusudi ya Mungu kupitia funzo la Biblia. Hata hivyo, wanang’amua kwamba ni lazima watu wajue kusoma na kuandika ili wanufaike kikamili na habari ya Biblia. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova wamewafundisha makumi ya maelfu ya watu kusoma na kuandika, kutia ndani watu 23,000 (kufikia miaka ya katikati ya 1990) katika nchi moja tu ya Afrika Magharibi. Likirejezea utumishi wa kijamii wenye kutokeza unaotolewa na Mashahidi wa Yehova, gazeti la San Francisco Examiner lilisema: “Ungeweza kuwachukua wao kuwa raia walio kiolezo kizuri. Wao hulipa kodi kwa bidii ya uendelevu, hutunza wagonjwa, hupambana na kutojua kusoma [na kuandika].”
Kwa kuongezea, kupitia mazoezi yenye kuendelea ya kusema mbele ya watu, Mashahidi wa Yehova wamewazoeza mamia ya maelfu ya watu kuwa wasemaji wanaostahili, wenye uwezo wa kujieleza kwa ufasaha mbele ya watu. Kati ya maelfu hawa kuna wengine ambao wakati mmoja walikuwa na matatizo makubwa ya usemi. Fikiria mwanamume wa Afrika Kusini anayeandika hivi: “Kigugumizi changu kilikuwa kibaya sana hivi kwamba kilinifanya kuwa mndani, kwa kawaida nikitegemea wengine wanisemee. . . . Nilipojiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na kulazimika kusoma Biblia mbele ya wasikilizaji wachache . . . , niligugumiza vibaya sana hivi kwamba nilishindwa kumaliza mgawo katika wakati uliowekwa. Baada ya mkutano, [mshauri] alinitolea kwa fadhili shauri lenye kutumika. Akadokeza kwamba nijizoeze kujisomea kwa sauti kubwa. Nilifanya hivyo, nikitumia wakati siku baada ya siku kusoma Biblia yangu na gazeti la Mnara wa Mlinzi kwa sauti kubwa.” Mwanamume huyu alifanya maendeleo mazuri sana hivi kwamba sasa yeye huwatolea mamia, hata maelfu ya wasikilizaji, hotuba za watu wote.
Kufurahia Usawa Kati ya Akina Ndugu
Hali ya mambo kati ya Mashahidi wa Yehova hutofautiana sana kuhusu elimu, utunzaji wa kiafya, na hali ya kiuchumi na ya kijamii. Tofauti hizo hudhihirisha tu hali zisizokamilika za ulimwengu ambamo wanaishi. Lakini tofauti na vikundi vingine vya kidini, ubaguzi wa kimbari, wa kijamii, na wa kiuchumi karibu umeondolewa kabisa kati yao.
Wametimiza hilo kwa kujitahidi kadiri wawezavyo kujizoeza yale ambayo wamejifunza kutoka katika Biblia. Wao hukubali kwa moyo wote kanuni za Biblia kama: “BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote. Andaeni mambo bora mbele ya macho ya watu wote. Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:17, 18; ona pia 1 Timotheo 6:17-19; Yakobo 2:5, 9.
Kwa kufuata kwa makini kanuni za Biblia zinazoendeleza umoja, Mashahidi wa Yehova hawaruhusu kuwepo kati yao zoea lolote la ukosefu wa usawa, lenye kutegemea tofauti za kimbari, za kijamii, au za kiuchumi. Kwa mfano, tofauti hizo hazina fungu lolote katika kuamua yule atakayepata mapendeleo ya utumishi katika kutaniko la Kikristo. Nyadhifa za madaraka, kama vile ufundishaji na usimamizi, hutolewa kwa kutegemea tu sifa za kiroho.—1 Timotheo 3:1-13; Tito 1:5-9.
Kwa watu ambao wameteseka chini ya ukosefu mbalimbali wa usawa wa ulimwengu wenye ubaguzi, inaburudisha kama nini wakati wengine wanapowatendea kama ndugu na dada wale ambao hali yao ni sawa mbele ya Muumba wao! Martina aweza kuthibitisha jambo hilo. Baada ya babake kuitupa familia yao, yeye alilelewa katika nyumba yenye umaskini, ya mzazi mmoja. Mara nyingi alitendwa kama mtu aliyekataliwa na jamii, akakosa kujitumaini, na kuliona kuwa jambo gumu kupatana na wengine. Alisitawisha mtazamo wa kutojali lolote. Hata hivyo, mambo yalibadilika baada ya kuanza kujifunza Biblia na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Yeye asema: “Bado inanibidi nipambane na mawazo yasiyofaa, lakini sasa ninaweza kukabiliana na tatizo hilo vema zaidi. Sasa ninajistahi zaidi, nami huzungumza kwa uhakika zaidi. Kweli imenifanya nihisi kuwa na daraka. Sasa ninajua Yehova ananipenda na kwamba maisha yana maana.”
Wakiwa kikundi cha Wakristo wa kimataifa, Mashahidi wa Yehova katika nchi zaidi ya 230 hufurahia kadiri fulani ya usawa ambao ni wa kipekee katika ulimwengu wa leo. Je, kuna tengenezo jingine la kidini linaloweza kudai kuwa na usawa huo na kuthibitisha kwa matendo?
Bila shaka, Mashahidi wa Yehova huchukua mambo kihalisi. Wao hukubali bila kusita kwamba kwa kuwa wanatokana na mazingira yasiyokamilika, hawawezi kuondoa kabisa ukosefu wa usawa wa kibinadamu, sawa na vile ilivyo kwa wengine ambao wamejaribu kufanya hivyo katika karne zilizopita—wasifue dafu. Hata hivyo, wao hushangilia kwamba wamefanya mengi kudhibiti baa hili lenye kufisha. Na wakiwa na imani yenye nguvu katika ahadi ya Mungu, wanatazamia kwa hamu ulimwengu mpya wenye uadilifu ambapo ukosefu wa usawa hautakumbukwa milele.
Naam, karibuni wanadamu wote watiifu watarudishiwa usawa “katika adhama na haki” ambao Muumba wao alikusudia wafurahie pale mwanzoni. Ni wazo zuri kama nini! Na wakati huo usawa utakuwa jambo halisi!
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mashahidi wa Yehova hupambana na kutojua kusoma na kuandika kwa kufundisha makumi ya maelfu ya watu kusoma na kuandika
[Picha katika ukurasa wa 8]
Kweli ya Biblia husaidia kuondoa ubaguzi wa kimbari, wa kijamii, na wa kiuchumi