Ukosefu wa Usawa—Je, Mungu Aliukusudia?
Kwa neno moja tu jibu ni la. Acheni tuone ni kwa nini.
MUNGU alikusudia wanadamu wote wawe na fursa sawa za uhai na furaha. Kuhusu kuumbwa kwa mwanadamu, twasoma: “Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kile chenye kutambaa kitambaacho juu ya nchi.” Alipomaliza uumbaji wa kidunia, “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya sita.”—Mwanzo 1:26, 31.
Je, Mungu anaweza kutangaza hali yenye kusikitisha ya ukosefu wa usawa leo kuwa ‘njema sana’? Hata kidogo, kwa kuwa “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Inasemekana kumhusu kwamba ‘hapendelei nyuso za watu’ na kwamba “kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 10:17; 32:4; linganisha Ayubu 34:19.) Naye mtume Petro akamalizia hivi: “Kwa hakika nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.
Kwa kuwa Mungu ni mwenye upendo, asiye na upendeleo, mwenye haki, mnyofu, na mwadilifu, angewezaje kuwa aliwaumba wanadamu wakiwa na ukosefu wa kiasili wa usawa kuhusiana na haki yao ya kuwa na furaha? Kuruhusu ubaguzi uwepo kati ya watu na kuwaweka katika mfumo usio na usawa kungekuwa kinyume kabisa cha utu wake. Alikusudia wote ‘wazaliwe wakiwa huru na sawa katika adhama na haki.’ Hata hivyo, kwa wazi hali ni tofauti leo. Kwa nini?
Kiini cha Ukosefu wa Usawa
Uhakika wa kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa sawa haumaanishi kwamba alikusudia wote wawe sawa katika kila jambo. Wangeweza kutofautiana katika vipawa, mapendezi, na nyutu. Wangeweza kutofautiana pia katika vyeo au viwango vya mamlaka. Kwa mfano, mwanamume na mwanamke si sawa katika kila jambo, lakini Mungu alimwumba mwanamke “awe kikamilisho” cha mwanamume. (Mwanzo 2:18, NW) Ni wazi kwamba wazazi na watoto wanatofautiana katika mamlaka. Hata hivyo, licha ya tofauti hizo, wote—wanaume, wanawake, na watoto—wangelikuwa na fursa sawa za kutosheleza mahitaji ya msingi ya kuwa na furaha. Wote wangelikuwa na adhama na hali sawa mbele za Mungu.
Vivyo hivyo, wana wa roho wa Mungu, walioumbwa kabla ya wanadamu, walipewa migawo na madaraka tofauti-tofauti. (Mwanzo 3:24; 16:7-11; Isaya 6:6; Yuda 9) Hata hivyo, bila kuruka mipaka waliyowekewa, wote waliweza kupata kwa kiwango sawa maandalizi ya Mungu kwa ajili ya uhai na furaha. Hivyo, wakadhihirisha kwa njia iliyo bora kabisa sifa ya Mungu ya kutobagua.
Yasikitisha kwamba, kiumbe mmoja wa roho hakuridhishwa na mpango wa Mungu wa kutobagua. Alitaka zaidi ya yale Mungu aliyompa, akitamani cheo cha juu zaidi, kilichokwezwa zaidi. Kwa kusitawisha tamaa hiyo mbaya, alichukua msimamo wa kushindana na Yehova, ambaye akiwa Muumba anashikilia kwa haki cheo cha juu kupita vyote. Baadaye mwana huyo wa Mungu wa roho, mwenye kuasi, akashawishi wanadamu wamdai Mungu zaidi ya yale Aliyowapa. (Mwanzo 3:1-6; linganisha Isaya 14:12-14.) Hivyo, uandalizi wa Yehova kwa wanadamu wawe na furaha na maisha yenye kupendeza ukaonekana kuyumbayumba. Mwasi huyo wa roho, anayetambulishwa kwenye Ufunuo 20:2 kuwa “Ibilisi na Shetani,” akawa mchochezi mwovu wa ukosefu wa usawa wa kibinadamu.
Je, Hali Zitabadilika Wakati Wowote?
Jibu kwa neno moja tu ni ndiyo!
Lakini ni nani anayeweza kuleta mabadiliko yanayohitajiwa? Viongozi wa kibinadamu wamejitahidi kwa karne nyingi kuleta mabadiliko hayo, bila shaka baadhi yao wakifanya hivyo kwa unyofu wote. Wamekuwa na mafanikio machache, yakifanya watu wengi wafikie mkataa kwamba ni jambo lisilo la busara kutarajia tatizo la ukosefu wa usawa litatuliwe wakati wowote. Hata hivyo, maoni ya Mungu yameandikwa kwenye Isaya 55:10, 11: “Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”
Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova Mungu ametangaza kwamba atatimiza kusudi lake la awali la kuandalia wanadamu wote fursa sawa kwa ajili ya uhai na furaha! Akiwa Mungu wa kweli, amejitwika wajibu wa kutimiza yale ambayo ameahidi. Kwa uzuri, yeye anayo nia na uwezo wa kufanya hivyo. Atatimizaje hayo?
Jibu lategemea Ufalme ambao Yesu Kristo alifundisha wafuasi wake wasali kuuhusu: “Baba yetu uliye katika mbingu, . . . Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:9, 10) Naam, Yehova atatumia Ufalme wa Mungu ‘kuvunja falme hizi zote [zilizopo sasa] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Chini ya utawala wa Ufalme wa kimbingu, jamii mpya ya wanadamu itatokea. Kwa habari hiyo, mtume Yohana aliandika katika Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia, hivi: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali.” (Ufunuo 21:1) Namna zote zenye kuchukiza za ukosefu wa usawa—umaskini, ugonjwa, kutokuwa na ujuzi, ubaguzi, na taabu nyingine za wanadamu zitatoweka kabisa.a
Kwa zaidi ya karne moja, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakikaza fikira za watu kwenye Ufalme huo. (Mathayo 24:14) Kwa kutumia vichapo na kutolea watu msaada kibinafsi, wamejitahidi kusaidia watu wajue kusudi la Mungu kama lilivyoandikwa katika Biblia. Hata hivyo, kazi yao ya ulimwenguni pote huwapa watu tumaini la kuishi kwa usawa na furaha wakati ujao mbali na kuwa na matokeo katika kuzuia baa la ukosefu wa usawa wakati wa sasa. Acheni tuone ni kwa njia gani.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mazungumzo zaidi kuhusu jinsi ambavyo karibuni Ufalme wa Mungu utaleta usawa kwa wote, tafadhali ona sura ya 10 na 11 za kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Mungu alikusudia wanadamu wote wawe na fursa sawa za uhai na furaha