Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 10/1 kur. 5-10
  • “Kwa Kila Jambo Kuna Wakati Uliowekwa”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kwa Kila Jambo Kuna Wakati Uliowekwa”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Wakati wa Kulia na Wakati wa Kucheka”
  • Wenye Furaha Kikweli Hata Ingawa Wanalia!
  • “Wakati wa Kukumbatia, na Wakati wa Kutokumbatia”
  • Ndoa​—Zawadi Kutoka kwa Mungu
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Ndoa—Zawadi Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Ndoa na Kuwa Mzazi Katika Wakati Huu wa Mwisho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Kuwekea Nyumba Yako Msingi Mzuri
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 10/1 kur. 5-10

“Kwa Kila Jambo Kuna Wakati Uliowekwa”

“Kwa kila jambo kuna majira yake [“wakati uliowekwa,” “NW”], na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.”—MHUBIRI 3:1.

1. Wanadamu wasiokamilika wana tatizo gani, nalo limesababisha nini katika hali fulani?

MARA nyingi watu husema, “Laiti ningalifanya jambo hilo mapema zaidi.” Au labda baada ya kujua matokeo ya jambo, “Laiti ningalingoja.” Kusema hivyo hudhihirisha tatizo la wanadamu wasiokamilika la kuamua wakati ufaao wa kufanya mambo fulani. Tatizo hilo limesababisha kuvunjika kwa mahusiano. Limesababisha kukata tamaa na kuvunjika moyo. Na jambo lililo baya zaidi, limedhoofisha imani ya watu wengine katika Yehova na tengenezo lake.

2, 3. (a) Kwa nini kukubali uamuzi wa Yehova kuhusu nyakati zilizowekwa ndiyo hatua ya hekima? (b) Twapaswa kuwa na maoni gani yenye usawaziko kuhusu kutimizwa kwa unabii wa Biblia?

2 Kwa kuwa Yehova ana hekima na ufahamu wa kina ambao wanadamu hawana, akitaka yeye anaweza kujua kimbele matokeo ya kila tendo. Anaweza kujua “mwisho tangu mwanzo.” (Isaya 46:10) Hivyo, anaweza kuchagua bila kukosea wakati ufaao zaidi wa kufanya lolote atakalo. Hivyo, badala ya kutumainia hali yetu yenye kasoro ya kupambanua wakati, ni jambo la hekima kukubali uamuzi wa Yehova kuhusu nyakati zilizowekwa!

3 Kwa mfano, Wakristo wakomavu hungoja kwa uaminifu-mshikamanifu wakati wa Yehova uliowekwa wa kutimizwa kwa unabii mbalimbali wa Biblia. Wao hudumu wakiwa na shughuli nyingi katika utumishi wake, huku wakikumbuka barabara kanuni hii ya andiko la Maombolezo 3:26: “Ni vema mtu autarajie wokovu wa BWANA na kumngojea kwa utulivu.” (Linganisha Habakuki 3:16.) Wakati huohuo, wanasadiki kwamba hukumu ya Yehova iliyotangazwa kutekelezwa, “ijapokawia, . . . haina budi kuja, haitakawia [“haitachelewa,” NW].”—Habakuki 2:3.

4. Andiko la Amosi 3:7 na la Mathayo 24:45 lapaswa kutusaidiaje kumngoja Yehova kwa subira?

4 Kwa upande mwingine, je, tuna sababu ya kukosa subira tukishindwa kuelewa kikamili maandiko fulani ya Biblia au maelezo fulani yatolewayo katika vichapo vya Watch Tower? Kungoja wakati ambao Yehova ameweka ili kubainisha mambo ndiyo hatua ya hekima. “Hakika Bwana MUNGU hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.” (Amosi 3:7) Ni ahadi nzuri kama nini! Ni lazima tung’amue kwamba Yehova hufunua siri zake wakati ambao yeye aona wafaa. Kwa sababu hiyo, Mungu amempa mamlaka “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aandalie watu wake “chakula chao [cha kiroho] kwa wakati ufaao.” (Mathayo 24:45) Hivyo, hatuna sababu ya kuhangaika kupita kiasi, au hata kufadhaika kwamba mambo fulani hayajafafanuliwa kikamili. Badala yake, twaweza kuwa na hakika kwamba tukimngoja Yehova kwa subira, ataandaa, kupitia mtumwa mwaminifu, kile kinachohitajika “kwa wakati ufaao.”

5. Kuna manufaa gani kuchunguza Mhubiri 3:1-8?

5 Mfalme Solomoni mwenye hekima alizungumzia mambo 28, kila moja likiwa na “wakati [wake] uliowekwa.” (Mhubiri 3:1-8, NW) Kuelewa maana na mambo yanayohusishwa na maneno ya Solomoni kutatusaidia kuamua wakati ufaao na usiofaa wa kutenda mambo fulani kulingana na maoni ya Mungu. (Waebrania 5:14) Hilo nalo, litatuwezesha kupatanisha maisha zetu ifaavyo.

“Wakati wa Kulia na Wakati wa Kucheka”

6, 7. (a) Ni nini ambacho hufanya watu wenye kuhangaika leo ‘walie’? (b) Ulimwengu unajaribuje kukinza hali mbaya ambayo inaupata?

6 Ingawa kuna “wakati wa kulia na wakati wa kucheka,” ni nani asiyependelea zaidi wakati wa kucheka? (Mhubiri 3:4) Yasikitisha kusema kwamba twaishi katika ulimwengu ambao hasa hutufanya tulie. Habari zenye kuhuzunisha zimejaa katika vyombo vya habari. Sisi huogopa tusikiapo juu ya vijana wanaowapiga risasi wanafunzi wenzao shuleni, wazazi wanaowatenda vibaya watoto wao, maharamia wanaoua na kulemeza watu wasio na hatia, na ile iitwayo misiba yenye kusababisha vifo vya wanadamu na kuharibu mali. Kwenye televisheni sisi huona watoto wenye njaa, wenye macho yaliyoingia ndani na wakimbizi waliohamishwa kwao wakiwa mwendoni. Maneno kama machinjo ya kikabila, UKIMWI, vita vya kutumia viini hatari, na El Niño, ambayo hapo awali hayakufahamika, sasa yanasababisha hangaiko katika akili zetu na mioyo yetu—kila moja kwa njia tofauti.

7 Hakuna shaka kwamba ulimwengu wa leo umejaa msiba na huzuni. Hata hivyo, biashara za vitumbuizo hutoa kwa ukawaida, kana kwamba kupunguza uzito wa hali zilizopo, vitumbuizo visivyofaa, vyenye uchafu, na mara nyingi vyenye kukosa adili na vyenye jeuri, vinavyokusudiwa kutupotosha tupuuze kuteseka kunakowapata wengine. Lakini hali ya kufanya mizaha ya kipumbavu na kucheka kipuuzi bila kujali, ambayo vitumbuizo hivyo hutokeza, ni tofauti na furaha ya kweli. Ulimwengu wa Shetani hauwezi kabisa kutoa ile furaha ambayo ni tunda la roho ya Mungu.—Wagalatia 5:22, 23; Waefeso 5:3, 4.

8. Je, Wakristo leo wapaswa kutilia maanani kilio au kicheko? Fafanua.

8 Kwa kutambua hali ya kusikitisha ya ulimwengu, twaweza kuelewa kwamba leo si wakati wa kutilia maanani sana kicheko. Si wakati wa kuishi kwa ajili ya tafrija na vitumbuizo tu au wa kutilia maanani “kujifurahisha” kuliko kufuatia mambo ya kiroho. (Linganisha Mhubiri 7:2-4.) “Wale wanaoutumia ulimwengu” wapaswa kuwa “kama wale wasioutumia kwa ukamili,” akasema mtume Paulo. Kwa nini? Kwa sababu “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Wakorintho 7:31) Wakristo wa kweli huishi kila siku wakitambua kikamili uzito wa nyakati tunamoishi.—Wafilipi 4:8.

Wenye Furaha Kikweli Hata Ingawa Wanalia!

9. Ni hali gani yenye kusikitisha iliyokuwako siku za kabla ya Gharika, nayo inamaanisha nini kwetu leo?

9 Watu walioishi wakati wa Gharika ya duniani pote hawakuchukua maisha kwa uzito. Waliendelea na shughuli zao za kila siku, wakakosa kulia juu ya “maovu ya mwanadamu [yaliyokuwa] makubwa duniani,” wakitazama bila kujali huku ‘dunia ikijaa dhuluma.’ (Mwanzo 6:5, 11) Yesu alirejezea hali hiyo yenye kusikitisha, na kutabiri kwamba watu wangekuwa na mtazamo huohuo katika siku yetu. Alionya hivi: “Kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya furiko, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiozwa, hadi siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:38, 39.

10. Waisraeli walioishi katika siku za Hagai walidhihirishaje kwamba walikosa kuelewa wakati wa Yehova uliowekwa?

10 Katika siku za Hagai, yapata miaka 1,850 baada ya Furiko, Waisraeli wengi walidhihirisha hali sawa na hiyo ya kutohangaikia kwa uzito mambo ya kiroho. Wakiwa na shughuli nyingi za kufuatia masilahi ya kibinafsi, walikosa kufahamu kwamba huo ni wakati wa kutanguliza masilahi ya Yehova. Twasoma hivi: “Watu hawa husema, Huu sio wakati utupasao kuja, huu sio wakati wa kujenga nyumba ya BWANA. Ndipo neno la BWANA lilikuja kwa kinywa cha nabii Hagai, kusema, Je! huu ndio wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenye mapambo ya mbao, iwapo nyumba hii inakaa hali ya kuharibika? Basi sasa, BWANA wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu.”—Hagai 1:1-5.

11. Tunaweza kwa kufaa kujiuliza maswali gani?

11 Tukiwa Mashahidi wa Yehova leo, wenye madaraka na mapendeleo mbele za Yehova kama yale ya Waisraeli wa siku ya Hagai, tungefanya vema pia kuzingatia kwa uzito namna tunavyoishi. Je, sisi ‘hulia’ kwa sababu ya hali za ulimwengu na lawama ambayo hizo huliletea jina la Mungu? Je, tunaumia watu wanapodai kwamba hakuna Mungu na kwa madharau kupuuza kanuni zake za uadilifu? Je, sisi hutenda sawa na watu wenye alama ambao Ezekieli aliona katika ono miaka 2,500 iliyopita? Tunasoma hivi kuwahusu: “BWANA akamwambia [mtu mwenye kidau cha wino cha mwandishi], Pita kati ya mji, kati ya Yerusalemu, ukatie alama katika vipaji vya nyuso vya watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika kati yake.”—Ezekieli 9:4.

12. Andiko la Ezekieli 9:5, 6 lina umuhimu gani kwa watu leo?

12 Katika siku yetu, umuhimu wa simulizi hilo hudhihirika tusomapo maagizo waliyopewa wanaume sita wenye silaha za kuangamiza: “Piteni kati ya mji nyuma yake, mkapige; jicho lenu lisiachilie, wala msione huruma; Waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake; lakini msimkaribie mtu ye yote mwenye hiyo alama; tena anzeni katika patakatifu pangu.” (Ezekieli 9:5, 6) Kuokoka kwetu dhiki hiyo kubwa inayokaribia kwa kasi kwategemea kutambua kwamba leo hasa ndio wakati wa kulia.

13, 14. (a) Ni watu wa aina gani ambao Yesu aliwatangaza kuwa wenye furaha? (b) Fafanua ni kwa nini unafikiri ufafanuzi huo unafaa Mashahidi wa Yehova.

13 Bila shaka, furaha ya watumishi wa Yehova haizuiwi na uhakika wa kwamba wao ‘hulia’ kwa sababu ya hali ya mambo ya ulimwengu yenye kusikitisha. Hali ni kinyume kabisa! Wao kwa kweli ndio kikundi cha watu wenye furaha zaidi duniani. Yesu alionyesha jinsi ya kupata furaha aliposema: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho, . . . wale ambao huomboleza, . . . wenye tabia-pole, . . . wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, . . . wenye rehema, . . . wenye kutakata moyoni, . . . wenye kufanya amani, . . . wale ambao wamenyanyaswa kwa ajili ya uadilifu.” (Mathayo 5:3-10) Kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba ufafanuzi huu unawafaa zaidi Mashahidi wa Yehova kwa ujumla, kuliko tengenezo jingine lolote la kidini.

14 Watu wa Yehova wamekuwa na sababu ya “kucheka” hasa tangu kurudishwa kwa ibada ya kweli mwaka wa 1919. Kiroho, walikuwa na furaha kama wale watu waliorudi kutoka Babiloni katika karne ya sita K.W.K.: “BWANA alipowarejeza mateka wa Sayuni, tulikuwa kama waotao ndoto. Ndipo kinywa chetu kilipojaa kicheko, na ulimi wetu kelele za furaha. . . . BWANA alitutendea mambo makuu, tulikuwa tukifurahi.” (Zaburi 126:1-3) Ingawa hivyo, hata wakati wa kicheko cha kiroho Mashahidi wa Yehova hukumbuka kwa hekima uzito wa nyakati. Ulimwengu mpya utakapokuwa halisi nao wakazi wa dunia wawe na “mshiko imara juu ya uhai ulio halisi,” basi wakati utakuwa umefika wa kicheko kuchukua mahali pa kilio kwa umilele.—1 Timotheo 6:19; Ufunuo 21:3, 4.

“Wakati wa Kukumbatia, na Wakati wa Kutokumbatia”

15. Kwa nini Wakristo ni wateuzi katika kuchagua rafiki?

15 Wakristo ni wateuzi kuhusu wale ambao wanachagua wawe rafiki zao. Wao hukumbuka onyo hili la Paulo: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Naye Mfalme Solomoni mwenye hekima alisema: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.”—Mithali 13:20.

16, 17. Mashahidi wa Yehova huuonaje urafiki, kupeana miadi ya kijinsia na ndoa, na kwa nini?

16 Watumishi wa Yehova huwachagua wawe rafiki zao watu ambao vilevile wanampenda Yehova na uadilifu wake. Ingawa wanathamini na kufurahia ushirika wa rafiki zao, wao huepuka kwa hekima maoni yenye uendekevu mwingi ya kupeana miadi ya kijinsia ambayo yameenea sana katika nchi fulani leo. Badala ya kupeana miadi ya kijinsia kama njia ya kujifurahisha isiyodhuru, wao huona kupeana miadi ya kijinsia kuwa hatua nzito kuelekea ndoa ambayo yapaswa kuchukuliwa tu wakati ambapo mtu yuko tayari kimwili, kiakili, na kiroho—na vilevile wakati yuko huru Kimaandiko—kuingia katika uhusiano wa kudumu.—1 Wakorintho 7:36.

17 Huenda wengine wakaona ni jambo la kizamani kuwa na maoni kama hayo kuhusu kupeana miadi ya kijinsia na kuhusu ndoa. Lakini Mashahidi wa Yehova hawaruhusu msongo wa marika uathiri uchaguzi wao wa rafiki au maamuzi yao kuhusu kupeana miadi ya kijinsia na kuhusu ndoa. Wanajua kwamba “hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kwa kazi zayo.” (Mathayo 11:19) Yehova ajua yaliyo bora sikuzote, hivyo wao huchukua kwa uzito shauri lake la kufunga ndoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39; 2 Wakorintho 6:14) Wao huepuka kufunga ndoa haraka-haraka wakiwa na maoni yenye makosa kwamba talaka au mtengano unaruhusiwa ndoa isipofaulu. Wao huchukua wakati kutafuta mwenzi afaaye, wakitambua kwamba mara wawekapo nadhiri za ndoa, sheria hii ya Yehova hutumika: “Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.”—Mathayo 19:6; Marko 10:9.

18. Ni nini kiwezacho kuwa msingi wa ndoa yenye furaha?

18 Ndoa ni kifungo cha maisha kinachohitaji kupangwa kwa uangalifu. Kiakili, mwanamume atajiuliza, ‘Je, kweli yeye ananifaa?’ Lakini, ni muhimu vilevile ajiulize, ‘Je, kweli mimi ninamfaa?’ Je, mimi ni Mkristo mkomavu awezaye kushughulikia mahitaji yake ya kiroho?’ Wanaotazamia kufunga ndoa wana wajibu mbele za Yehova wa kuwa watu wenye nguvu kiroho, wawezao kufanyiza ndoa thabiti istahiliyo kibali cha Mungu. Maelfu ya wenzi Wakristo wanaweza kushuhudia kwamba kwa sababu ya mkazo unaowekwa juu ya kutoa badala ya kupokea, huduma ya wakati wote ni msingi mzuri wa ndoa yenye furaha.

19. Kwa nini Wakristo wengine hubaki waseja?

19 Wakristo wengine ‘huwakumbatii’ kwa kuamua kubaki waseja kwa ajili ya habari njema. (Mhubiri 3:5) Wengine huahirisha ndoa hadi wakati wanapoona kwamba wana sifa za kiroho zinazowawezesha kuvutia mwenzi afaaye. Lakini acheni pia tuwakumbuke Wakristo waseja wanaotamani sana uhusiano wa karibu na manufaa za ndoa na bado wanakosa kupata mwenzi. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hufurahia wanapokataa kuridhiana kanuni za kimungu wanapotaka kufunga ndoa. Sisi pia hufanya vema kuthamini uaminifu-mshikamanifu wao na kuwapa kitia moyo kifaacho wanachohitaji.

20. Kwa nini hata mume na mke ‘wasikumbatiane’ nyakati nyingine?

20 Je, hata mume na mke ‘wasikumbatiane’ nyakati nyingine? Yaonekana hivyo kwa njia fulani, kwa kuwa Paulo alisema: “Nisemalo ni hili, akina ndugu, wakati ubakio umepunguzwa. Tangu sasa acheni wale walio na wake wawe kama kwamba hawana.” (1 Wakorintho 7:29) Kupatana na hayo, ni lazima wakati mwingine madaraka ya kitheokrasi yatangulizwe mbele ya furaha na baraka za ndoa. Maoni yenye usawaziko kuhusu jambo hilo hayatadhoofisha ndoa bali yataiimarisha kwa kuwa yanasaidia kukumbusha mume na mke kwamba ni lazima sikuzote Yehova awe mtegemezaji mkuu wa ndoa yao.—Mhubiri 4:12.

21. Kwa nini hatupaswi kuhukumu mume na mke kwa habari ya kupata watoto?

21 Kwa kuongezea, wengine ambao wameoana wamejizuia kupata watoto ili wawe huru zaidi kuendelea kumtumikia Mungu. Wamejitoa mhanga, naye Yehova atawathawabisha kwa sababu hiyo. Ingawa Biblia inatia watu moyo kubaki waseja kwa ajili ya habari njema, lakini yenyewe haisemi moja kwa moja kwamba watu wasipate watoto kwa ajili ya habari njema. (Mathayo 19:10-12; 1 Wakorintho 7:38; linganisha Mathayo 24:19 na Luka 23:28-30.) Hivyo, mume na mke wapaswa kufanya uamuzi wao wenyewe unaotegemea hali za kibinafsi na dhamiri zao wenyewe. Uamuzi wowote ule ambao mume na mke wanachukua haupaswi kuchambuliwa.

22. Ni jambo gani lililo muhimu kwetu kuamua?

22 Naam, “kwa kila jambo kuna majira yake [“wakati uliowekwa,” NW], na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” Hata kuna “wakati wa vita, na wakati wa amani.” (Mhubiri 3:1, 8) Makala ifuatayo itafafanua kwa nini ni muhimu kuamua huu ni wakati upi kati ya hizo nyakati mbili.

Je, Unaweza Kueleza?

◻ Kwa nini ni muhimu kwetu kujua kwamba “kwa kila jambo kuna wakati uliowekwa”?

◻ Kwa nini leo hasa ni “wakati wa kulia”?

◻ Kwa nini hata ingawa Wakristo ‘wanalia,’ wao wanafurahi kikweli?

◻ Wakristo wengine huonyeshaje kwamba wanaona wakati wa sasa kuwa ‘wa kutokumbatiana’?

[Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Ingawa Wakristo ‘hulia’ kwa sababu ya hali za ulimwengu . . .

. . . wao kwa kweli ndio watu wenye furaha zaidi ulimwenguni

[Picha katika ukurasa wa 8]

Huduma ya wakati wote ni msingi mzuri wa ndoa yenye furaha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki