Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 10/1 kur. 3-4
  • Kwa Nini Wakati Ni Mchache Sana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Wakati Ni Mchache Sana?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakati kwa Wingi
  • Wakati Wazidi Kuwa Mchache
  • Sio Sisi tu Tulio na Wakati Mchache
  • Kutumia kwa Hekima Wakati Tulio Nao Sasa
  • Yehova Hutujulisha Jinsi ya Kuzihesabu Siku Zetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Tumikia kwa Tumaini la Umilele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Wakati na Umilele Tunajua Nini Hasa Kuzihusu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kutembea Pamoja na Mungu—Tukifikiria Umilele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 10/1 kur. 3-4

Kwa Nini Wakati Ni Mchache Sana?

WAKATI. Huenda ikawa vigumu kwetu kufafanua neno hilo kwa usahihi, lakini twajua kwa hakika kwamba hatuna wakati wa kutosha. Twajua pia kwamba wakati hupita haraka. Kwa kweli, mara nyingi sisi husema kwa kusikitika kwamba, “Wakati huyoyoma tu.”

Hata hivyo, ni dhahiri kwamba maneno ya mshairi Mwingereza, Austin Dobson, yalikuwa sahihi zaidi aliposema hivi mwaka wa 1877: “Wakati hupita, wasema? Ala! Wakati hudumu, sisi hatudumu.” Tangu alipokufa mwaka wa 1921, Dobson ametoweka kwa takriban miaka 80; lakini wakati umedumu tu.

Wakati kwa Wingi

Biblia hutuambia hivi kuhusu Muumba wa wanadamu: “Kabla haijazaliwa milima, wala hujaiumba dunia, na tangu milele hata milele ndiwe Mungu.” (Zaburi 90:2) Au “wewe ndiwe Mungu milele na milele,” kama vile Biblia Habari Njema itafsirivyo mstari huo. Hivyo, wakati utadumu kama Mungu mwenyewe adumuvyo—milele!

Kinyume kabisa na Mungu, aishiye milele na milele, twasoma hivi kuhusu wanadamu: “Maana siku zetu zote zimepita katika hasira yako, tumetowesha miaka yetu kama kite. Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili, maana chapita upesi tukatokomea mara.”—Zaburi 90:9, 10.

Kwa nini wakati ni mfupi sana leo, ilhali Biblia hufundisha waziwazi kwamba Mungu anakusudia mwanadamu aishi milele? (Mwanzo 1:27, 28; Zaburi 37:29) Badala ya kuishi kwa muda usio na kikomo kama vile Mungu alivyokusudia, kwa nini wanadamu, chini ya hali zifaazo kabisa, huishi kwa wastani wa siku zipunguazo 30,000? Kwa nini wanadamu huishi muda mfupi sana? Ni nani au ni nini kinachosababisha hali hii yenye kuhuzunisha? Biblia hutoa majibu yaliyo wazi na yenye kuridhisha.a

Wakati Wazidi Kuwa Mchache

Walio wazee watathibitisha kwamba katika miongo ya majuzi maisha yamekuwa yenye shughuli nyingi sana. Mwandishi mmoja wa habari, Dakt. Sybille Fritsch, alisema kwamba katika miaka 200 iliyopita, muda wa kufanya kazi katika juma umepungua kutoka saa 80 hadi saa 38, “hata hivyo, hilo halijafanya tuache kulalamika.” Yeye alifafanua hivi: “Hakuna wakati; wakati ni wenye thamani; tunauhitaji sana; maisha ni yenye shughuli nyingi.”

Uvumbuzi mpya umetoa fursa na uwezekano mbalimbali wa kufanya mambo ambayo hata hayakupata kuwaziwa na vizazi vya hapo awali. Lakini kadiri uwezekano wa kufanya shughuli mbalimbali unavyokuwa mkubwa zaidi, ndivyo watu wanavyovunjika moyo zaidi kwa kuwa na wakati mchache sana wa kufanya shughuli hizo. Siku hizi, watu katika sehemu nyingi za ulimwengu wana ratiba yenye shughuli nyingi, wakifanya kwa haraka-haraka jambo moja baada ya jingine kabla ya muda kwisha. Lazima Baba aende kazini saa 1:00 asubuhi, Mama apeleke watoto shuleni kufikia saa 2:30 asubuhi, Babu aende kumwona daktari saa 3:40 asubuhi, na ni lazima sote tujitayarishe kwa ajili ya mkutano muhimu saa 1:30 usiku. Katika pilika-pilika za kufanya jambo moja baada ya jingine kabla ya muda kwisha, kunakosa wakati wa kupumzika. Nasi hulalamika juu ya kazi za kila siku zenye kuchosha, au juu ya utendaji mwingi mno.

Sio Sisi tu Tulio na Wakati Mchache

Mpinzani wa Mungu, Shetani Ibilisi, ambaye njama zake zilifupisha muda wa kuishi wa wanadamu, sasa naye ameathiriwa na uovu wake mwenyewe. (Linganisha Wagalatia 6:7, 8.) Likizungumzia kuanzishwa kwa Ufalme wa Kimesiya mbinguni, andiko la Ufunuo 12:12 hutupa sababu ya kuwa na tumaini linaposema: “Kwa ajili ya hili teremeni, nyinyi mbingu nanyi mkaao ndani yazo! Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameteremka kwenu, akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.”

Kwa mujibu wa kronolojia yenye kutegemeka ya Biblia na pia kutimizwa kwa unabii wa Biblia, sasa tunaishi kwenye umalizio wa hicho “kipindi kifupi cha wakati.” Ni shangwe iliyoje kujua kwamba karibuni wakati wote wa Shetani utaisha kabisa! Mara aondolewapo, wanadamu watiifu watarudishwa kwenye ukamilifu, nao wanaweza kufikia uhai udumuo milele ambao Yehova alikusudia wawe nao hapo mwanzoni. (Ufunuo 21:1-4) Hakutakuwa tena tatizo la kutokuwa na wakati.

Je, unaweza kuwazia kitakachomaanishwa na kuwa na uhai udumuo milele—kuishi milele? Hutasumbuliwa tena na mambo ambayo ulilazimika kuacha yakiwa hayajafanywa. Ukitaka wakati zaidi, kuna kesho, au juma lifuatalo, au mwaka ufuatao—kwa kweli, umilele usio na kikomo mbele yako!

Kutumia kwa Hekima Wakati Tulio Nao Sasa

Akijua kwamba wakati wake wa kushawishi wanadamu ni mfupi, Shetani hujaribu kufanya watu wawe na shughuli nyingi sana wasiwe na wakati wa kusikiliza habari njema za Ufalme uliosimamishwa wa Mungu. Hivyo, tunafanya vema kutii shauri hili la kimungu: “Fulizeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia kabisa wakati unaofaa, kwa sababu siku ni za uovu. Kwa ajili ya hili acheni kuwa wenye kukosa akili, bali endeleeni kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.”—Waefeso 5:15-17.

Ni muhimu kama nini kutumia wakati wetu kwa hekima kwa kufanya mambo yaliyo muhimu zaidi badala ya kuutumia vibaya katika shughuli zisizofaa, zisizo na manufaa ya kudumu! Yatupasa kusitawisha mtazamo uleule aliokuwa nao Musa alipomwomba Yehova kwa maneno haya yanayotoka moyoni: “Basi, utujulishe kuzihesabu siku zetu, tujipatie moyo wa hekima.”—Zaburi 90:12.

Ni kweli, katika ulimwengu wa leo kila mtu ana shughuli nyingi. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanakusihi sana utumie kiasi fulani cha wakati wako wenye thamani kujifunza juu ya matakwa ya Mungu ya kupata uhai udumuo milele chini ya utawala wa Ufalme wake. Kutumia muda wa saa moja kila juma kujifunza Biblia kwa ukawaida, “kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini,” huenda kukakuwezesha kuona maneno haya yakitimizwa juu yako mwenyewe: “Jiepue na uovu, utende mema, na kukaa hata milele. Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:27, 29.

[Maelezo ya Chini]

a Ona kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, sura ya 6, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki